Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 10/15 kur. 473-475
  • Manabii Walikuwa na Kazi Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Manabii Walikuwa na Kazi Gani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • HAWAKUWA WATANGAZA MISIBA TU
  • UNABII WA LEO
  • Siku ya Yehova—Ujumbe Muhimu
    Izingatie Siku ya Yehova Maishani
  • Manabii wa Uwongo
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Watumishi wa Yehova Wana Tumaini la Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Kitabu Cha Biblia Namba 33—Mika
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 10/15 kur. 473-475

Manabii Walikuwa na Kazi Gani?

WAKATI manabii Waebrania wa nyakati za kale wanapotajwa, wewe unafikiria nini? Je! unawafikiria kuwa watu waliotabiri habari za wakati uliokuwa ukija? Au, unawafikiria kuwa watu waliohimiza wenzao wafanye mapenzi ya Mungu?

Bila shaka, manabii Waebrania wa kale walitabiri matukio fulani. Lakini kazi yao haikuwa kutabiri tu. Hiyo ni wazi kutokana na neno la Kiebrania linalomaanisha nabii, na·viʼʹ. Neno hilo likiwa peke yake halimaanishi kutabiri. Na·viʼʹ lamaanisha ‘mtu anayemimina maneno kwa wingi’ au ‘mtu ambaye usemi wake unatiririka.’ Matumizi halisi ya neno hilo yaonyesha kwamba manabii wa kweli walikuwa wanenaji wa Mungu waliokuwa na ujumbe wake wenye kufurahisha. Twaweza kufahamu vizuri zaidi agizo ambalo manabii wa Mungu walikuwa nalo tukilinganisha mwenendo wao na ule wa waliojidai kwa uongo kuwa manabii.

Kwa mfano, fikiria hali iliyokuwako wakati wa nabii Mwebrania Mika. Adili za watu zilikuwa zimeharibika sana katika Israeli na Yuda. Viongozi walikuwa wakionea watu, hasa maskini na wenye shida. Waamuzi na makuhani walikuwa na pupa nyingi sana ya pesa. Siku hizo zilikuwa za kumwaga damu na kufanya upotovu wa kila aina. Mtu asingeweza kutumaini hata rafikize wala washiriki wa jamaa yake mwenyewe.

Hakika, huo ulikuwa wakati wa kufunua makosa ya Waisraeli na kuwasihi wabadili njia zao. Je! hivyo ndivyo walivyokuwa wakifanya wenye kujidai kwa uongo kuwa manabii? Sivyo. Katika Mika 3:5 manabii hao wanasemekana kwamba walipotosha Waisraeli, kwamba walikuwa watu “waumao kwa meno yao, na kulia, Amani; na mtu awaye yote asiyetia kitu vinywani mwao, wao humwandalia vita [takatifu, New English Bible].” Kwa hiyo manabii hao wa uongo walitoa ujumbe wao wakitegemea malipo. Maadamu walipata thawabu yao, walikuwa na nia ya kuahidia hata watu wenye adili mbovu ufanisi. Manabii hao wa uongo hawakutia watu moyo hata kidogo waache njia zao mbovu. Kwa hiyo, watu walijiona kuwa wenye usalama, wakaendelea na njia zao za kuvunja sheria. Lakini manabii hao wa uongo walipokosa kupewa kitu na mtu, walifanya haraka ‘kuomba ghadhabu ya Bwana’ imshukie mtu huyo.

Lakini, manabii wa kweli wa Yehova hawakutafuta faida zao wenyewe. Walifahamu kwamba walikuwa wamewekwa na Mungu, na kwa hiyo hawakujaribu kupendeza wanadamu. Akitofautisha mwendo wake mwenyewe na ule wa manabii wa uongo, Mika alisema hivi: “Mimi, hakika nimejaa nguvu kwa roho ya [Yehova]; nimejaa hukumu na uwezo; nimhubiri Yakobo kosa lake, na Israeli dhambi yake.” (Mik. 3:8) Mika alitumia ushujaa kufunua dhambi za Waisraeli, yaani, ibada yao ya sanamu, mazoea ya kupunja, kuonea watu bila rehema na kufanya udhalimu. Vilevile alitabiri kufikilizwa kwa hukumu ya Mungu juu ya Yuda na Israeli. Alitabiri uharibifu uliokuwa ukiujia Samaria, mji mkuu wa ufalme wa makabila kumi, na Yerusalemu, mji mkuu wa ufalme wa makabila mawili.

Unabii mbalimbali uliohusu hukumu iliyokuwa ikija juu ya Samaria na Yerusalemu ulikuwa na makusudi mawili. Kwa upande mmoja, ulirudia kutia mkazo juu ya ubaya ambao watu walikuwa wakifanya. Kwa upande mwingine, ulitia Waisraeli moyo watubu, wapate kurehemiwa na Mungu. Yeremia 18:7-10 yaonyesha kwamba unabii mbalimbali uliohusu msiba uliwapa watu nafasi ya kutubu pia. Hapo twasoma yafuatayo juu ya maneno ya Yehova ya hukumu na baraka: “Wakati wo wote nitakapotoa habari za taifa, na habari za ufalme, kuung’oa, na kuuvunja, na kuuangamiza; ikiwa taifa lile nililolitaja litageuka, na kuacha maovu yake; nitaghairi, nisitende mabaya yale niliyoazimia kuwatenda. Na wakati wo wote nitakapotoa habari za taifa, na habari za ufalme, kuujenga na kuupanda; ikiwa watatenda maovu mbele za macho yangu, wasiitii sauti yangu, basi nitaghairi, nisitende mema yale niliyoazimia kuwatendea.”

HAWAKUWA WATANGAZA MISIBA TU

Kwa kuwa manabii wa Mungu walikuwa na daraka la kuhimiza watu waache njia zao mbaya, je! hiyo yamaanisha kwamba walitabiri habari za misiba na huzuni tu? Sivyo, mara nyingi matangazo yao yalihusu ujumbe wenye kufurahisha wa tumaini. Ingawa Waisraeli kwa ujumla hawakutaka kusikiliza tangazo la hukumu ya Yehova iliyokuwa ikija, watu mmoja mmoja wangeweza kuhakikisha kwamba hawakukubaliana na jeuri na uvunjaji wa sheria uliokuwako wakati huo. Wao wangefurahia kuona udhalimu ukiondolewa wakati hukumu ingefikilizwa juu ya waovu.

Zaidi ya hilo, kwa sababu Yehova ni Mungu mwenye haki na rehema, watu wenye nia nzuri wangeweza kuwa na matumaini kwamba asingeendelea kuchukizwa milele. Jambo hilo limekaziwa katika Maombolezo 3:31, 32: “Bwana hatamtupa mtu hata milele. Maana ajapomhuzunisha atamrehemu.”

Kupatana na rehema yake na fadhili zake za upendo, Yehova Mungu aliongoza manabii wake watolee watu tumaini. Kwa mfano, Mika alitabiri kwamba Waisraeli wangerudishwa katika nchi yao baada ya kuachwa ukiwa. Mika alitaja neno hili la Yehova: “Hakika nitakukusanya, Ee Yakobo, nyote pia; bila shaka nitawakusanya waliobaki wa Israeli; nitawaweka pamoja kama kondoo wa Bozra; kama kundi la kondoo kati ya malisho yao; watafanya mvumo kwa wingi wa watu.” (Mik. 2:12) Kwa hiyo, baada ya Waisraeli kuuona ukiwa, wenye kutubu wangeweza kufarijiwa na tumaini hilo la kurudishwa.

Basi, manabii walitumikia hasa kama wajumbe wa Yehova kwa Waisraeli. Walitaka sana kusaidia wananchi wenzao wafuate mwendo uliokubaliwa na Mungu na kuepuka msiba. Waliokataa kufanya mapenzi ya Mungu peke yao ndio waliowatangazia msiba. Lakini manabii walipelekea wenye nia nzuri ujumbe wa ukombozi na tumaini. Ezekieli 33:11 yaonyesha habari kuu inayotajwa katika unabii mbalimbali: “Kama mimi niishivyo, asema Bwana [Yehova], sikufurahii kufa kwake mtu mwovu; bali aghairi mtu mwovu, na kuiacha njia yake mbaya, akaishi. Ghairini, ghairini, mkaache njia zenu mbaya; mbona mnataka kufa, Enyi nyumba ya Israeli?”

UNABII WA LEO

Ujumbe mkubwa wa manabii Waebrania wa kale unahusu siku hizi pia. Kama zamani, Yehova Mungu hakubali uvunjaji wa sheria, jeuri, udhalimu wala uonezi unaoendelea kuongezeka katika sehemu mbalimbali za dunia. Katika Neno lake, Yehova Mungu ametangaza kwamba atakomesha uovu wote. Biblia yasema: “Ghadhabu ya Mungu imedhihirishwa kutoka mbinguni juu ya uasi wote na uovu wa wanadamu waipingao kweli kwa uovu.” (Rum. 1:18) Lakini, kabla siku hiyo ya ghadhabu haijaja, watu wana nafasi ya kubadili njia zao, wajitayarishe kuokolewa ikiwa hukumu hiyo itafikilizwa wakiwa hai. Tena, watakaookoka uharibifu huo watakuwa na tumaini zuri sana la kupata uzima wa milele katika taratibu mpya yenye haki. (2 Pet. 3:9, 13) Habari nzuri sana tulizo nazo leo ni kwamba tumaini hilo linakaribia sana kutimizwa.

Je! hizo si habari zinazopaswa kutangazwa leo? Lakini ni nani anayepaswa kuwa akizitangaza? Je! wewe usingetazamia wenye kufanya hivyo wawe watu wanaoenenda sawasawa na manabii Waebrania wa kale? Wanapaswa kuwa watu wanaofuata kanuni zenye haki za Neno la Mungu na kuhimiza wengine wafanye ivyo hivyo. Inawapasa wawe wakitoa onyo kwamba waovu watauawa na kuonyesha watu kwamba kutakuwa na taratibu mpya yenye haki itakayokuwa na mambo matukufu.

Kutokana na mambo ambayo umeona, je! makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yanajitahidi kweli kweli kusaidia watu wabadili njia zao? Au, badala yake umeona viongozi wa dini wakiachilia mara nyingi makosa ya namna zote yafanywe na wanakanisa maadamu viongozi hao wanapokea mshahara wao?

Namna gani jamii inayoitwa Mashahidi wa Yehova wa Kikristo? Watu wengi wamepata kufahamu kwamba pana tofauti kubwa kati ya Mashahidi wa Yehova na makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Wameona kwamba Mashahidi wanasisitiza wale wanaoshirikiana sana nao waishi kupatana na Biblia. Je! wewe pia umeona hivyo juu ya Mashahidi wa Yehova? Ikiwa umeona, je! unashiriki kusaidia wengine waishi kupatana na njia za Mungu?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki