Yale Ambayo Vijana Wanahitaji kutoka kwa Wazazi Wao
KILA mtu mzima alikuwa kijana wakati mmoja. Kila mzazi wa kijana alikuwa kijana yeye mwenyewe wakati mmoja. Kwa hiyo watu wazima wanapaswa kufahamu matatizo pamoja na mambo yanayowakatiza vijana tamaa. Walakini mara nyingi sana wazazi hawakumbuki matatizo waliyokuwa nayo walipokuwa vijana nao wanashindwa kuwatendea watoto wao vijana kwa njia yenye ufahamu. Babu mmoja anakumbuka maono haya yake:
“Nilipokuwa mtoto niliona kwamba mara nyingi adabu ya jamaa ilikuwa kali na isiyo ya haki. Nakumbuka nilikuwa nikiwaza kwamba nitakapokuwa mtu mzima na kuwa na watoto, nitawaadibisha kwa njia ya upendo, niwasikilize na kuwapa sababu ya mambo. “Nilipofikia wakati huo maishani mwangu, nilipata kuona kwamba mikazo ya kulea jamaa ilikuwa mikubwa sana. Kufanya kazi saa nyingi kulinizuia nisiwe na muda mwingi wa kuwaona watoto wangu. Nilipokuwa pamoja nao nilikuwa nikikasirika upesi na kukosa ustahimilivu.
“Miaka ya kukua kwa watoto inapita kwa haraka sana. Sasa mimi ni babu, nami nina maoni tofauti kabisa na yale niliyokuwa nayo nilipokuwa mzazi. Ninapata wakati wa kucheza na kufurahia wajukuu wangu, nikitaka mara nyingi kuwatetea wanapoingia matatani, nikiona kama kwamba wazazi wao ni wakali kupita kiasi na kwamba hawawafahamu. Mara nyingi nawaza hivi: Laiti sisi wazazi tungeonyesha ustahimilivu na ufahamu kama wa akina babu na nyanya.”
Mara nyingi wazazi wanasahau kwamba kwa kawaida kijana anadai haki yake kama mtu binafsi aliye na mahitaji yake binafsi. Wanakosa kufahamu, nayo magumu hutokea. Mhudumu ambaye amechunguza habari za vijana anaripoti kwamba aliwauliza vijana wengi ulizo hili: “Ni jambo gani moja ambalo ungetaka zaidi kutoka kwa wazazi wako kuliko mengine yote?” Karibu wote walikuwa wakisema:
“KUFAHAMIKA”
Msichana wa miaka 15 alionyesha tamaa hii, akisema hivi: “Mimi nina wazazi wazuri, lakini ningependa wafahamu kwamba mimi si mtoto mdogo sasa. Wananitendea kama kwamba mimi ni mtoto wa darasa la tatu. Laiti wangalinifahamu na kunitumaini.” Yeye alitaka sheria fulani zibadilishwe kwa kukubali umri wake.
Kule kutaka sana kuwa na uhuru zaidi ni sehemu ya kawaida ya kukua kuwa mtu mzima—uhakika ambao wazazi wengi hawaukubali. Mtoto wao amekuwa akiwategemea nao walifurahia jambo hilo. Sasa mtoto wao kijana anabadili roho ya kuwategemea kabisa na kuwa na roho ya kutaka kujitegemea zaidi na zaidi. Kubadili maoni namna hiyo si jambo baya. Vijana wengine wanaanza kusitawisha maoni kama ya mtu mzima wakiwa na umri mdogo kwa kulinganisha. Mfano wa Biblia ni ule wa Mfalme Yosia. “Naye akali mchanga [miaka 15,] alianza kumtafuta Mungu wa Daudi.” Akiwa na umri wa miaka 25 alichukua hatua yenye kuonyesha kwamba alichukia ibada ya uongo iliyokuwa imesitawishwa na baba yake. Kijana huyu alikuwa na uhuru wa kutenda kwa hiari yake. Je! maoni na tendo lake yalikuwa mabaya kwa sababu tu yeye alikuwa bado mchanga? Hapana. (2 Nya. 34:1-8) Vilevile, kijana Daudi alikuwa na maoni mazuri alipouliza juu ya kupigana na Goliathi, yajapokuwa yalifahamika vibaya na nduguye mkubwa.—1 Sam. 17:26-28.
Hata hivyo, kwa kuwa kijana bado hajakuwa mtu mzima, tamaa zake zote si za hekima. Yeye anahitaji wakati wa kucheza. Wazazi wake wanahitaji kufahamu kwamba yeye bado ana nguvu za kufanya mambo wakati wazazi wake wanapenda kupumzika. Vijana wanahitaji ushirika. Wazazi wakikosa kutoa ushirika unaofaa, vijana watatafuta ushirika wao wenyewe nao huenda wakapata ule wasioukubali wazazi.
Vijana wengi wanafurahia kuwa na karamu. Kwa sababu ya mwenendo unaokuwako katika nyingine za karamu hizo, huenda wazazi wasitake vijana wao wazishiriki. Walakini, kuwakataza kabisa wasishiriki katika karamu kwaweza kuwavunja moyo na kuwashushe vijana moyo. (Kol. 3:21) Wazazi wakipanga kuwe na karamu, wana haki ya kuchagua wale watakaoalikwa na kusimamia utendaji na kuepuka matatizo. Vijana wanaposhiriki kuipanga, itafanikiwa hata zaidi.
Kijana anapofanya kosa na kupatwa na magumu, sana sana huo ndio wakati ambao kijana anahitaji sana kufahamika. Wazazi watafanya vizuri wakikumbuka wakati wa ujana wao na kukumbuka makosa waliyofanya kwa sababu ya kutokuwa na ujuzi mwingi. Wakifanya hivyo, itakuwa rahisi zaidi kushinda jaribu la kutenda au kulaumu kupita kiasi. Ikiwa wanataka kijana wao awajie anapokuwa na magumu, lazima wamsaidie kijana awatumaini kwa namna wanavyomtendea anapofanya makosa madogo.
Kosa linapokuwa la kutenda bila kufikiri, inawapasa wazazi waonyeshe fadhili nyingi pamoja na huruma. Kila jitihada inapaswa ifanywe katika kueleza kosa lilikuwa nini na namna ya kuepuka kulirudia. Walakini kijana huyo hapaswi kuambiwa kwamba yeye ni mbaya.
Lakini inawapasa wazazi wafanye nini ikiwa kijana wao anajiingiza katika matatizo mazito yanayohusu kupokea adhabu shuleni, au kuingia matatani na polisi, au yanayohusu dawa za kulevya, au uasherati? Wazazi wanaweza kutumaini kwamba mazoezi waliyotangulia kutoa yatazuia jambo kama hilo. Walakini namna gani kama likitukia? Huo ndio wakati ambao kijana anahitaji sana uongozi wenye hekima pamoja na msaada.
Tatizo kama hilo linakuwa lenye kujaribu sana wazazi. Mara nyingi wanauliza hivi: “Tulikosea wapi?” Mara nyingi wanatoa vitisho au kumlaumu vikali mtoto huyo mpotovu, jambo ambalo laelekea kumkasirisha na kumpa moyo mgumu wa kuendelea na mwendo huo wake. Yehova alikuwa na ufahamu naye alikuwa tayari kusamehe watu wake walipoacha kufuata yaliyo mema. Yeye alichukua hatua ya kwanza kupashana habari pamoja nao akajitolea awasaidie, ijapokuwa dhambi zao zilikuwa nzito sana. “Haya, njoni, tusemezane,” akasema Yehova. “Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji.”—Isa. 1:18.
Wakati ujao wa kijana huyo utategemea namna anavyotendewa wakati huu wenye hatari. Usiseme wala kufanya. jambo litakalofanya iwe vigumu kwake kukurudia, kama vile yule “mwana mpotovu” alivyomrudia baba yake. Haiwapasi wazazi kukata tamaa juu ya watoto Wao kamwe maadamu watoto wako chini ya uangalizi wao. Onyesha uvumilivu. Warehemu. Mwige Yehova katika kuonyesha sifa hizi.—Yak. 2:13; 2 Pet. 3:9, 15; Luka 15:11-24.
KUTENDEWA KAMA MTU BINAFSI
Uhitaji mkubwa wa vijana ni kutendewa kama mtu binafsi. Charles R. Foster anasema hivi katika kitabu chake Psychology for Life Today:
“Inakubaliwa kwamba mwanadamu anataka zaidi ya kula na kulala tu. Anataka kukubaliwa kama mtu, naye anataka kujisikia kwamba anafanikiwa.”
“Bila shaka mtu anajisikia vizuri zaidi naye anafanya kazi vizuri zaidi akifanikiwa kutimiza jambo fulani na ikiwa anajisikia kwamba sehemu yake ulimwenguni ni yenye maana. Wengi wa wanafunzi wa tabia za kijamii wanaona kwamba kila mwanadamu ana uwezo fulani usiotumiwa bado—kwamba kila mtu ana jambo fulani analoweza kufanya vizuri, ikiwa tu tungeweza kujua jambo hilo ni jambo gani.”
Kila kijana anahitaji kufikiriwa kuwa tofauti kabisa na mtu mwingine ye yote. Wazazi wanajifunza kwamba hakuna watoto wawili wanaofanana. Mazoezi na adabu inayoleta matokeo katika mtoto mmoja huenda isiwe na matokeo juu ya mwingine. Sana sana ndivyo ilivyo wanapokuwa vijana.
Kwa hiyo, si vizuri kulinganisha mtoto mmoja na mwingine. Kazi ya mtu ikilinganishwa na kazi bora zaidi ya mtu mwingine, kunakuwa na chuki, haitii moyo. (Linganisha 2 Wakorintho 10:12) Kijana anataka kukubaliwa kwa vile yeye alivyo, na kwa yale anayoweza kufanya kama mtu binafsi. Anataka apendwe na wazazi wake kwa vile yeye mwenyewe alivyo, na kutendewa kwa fadhili za kibinadamu. Kwa upande mwingine, yeye hataki kuzuiwa asiendelee, au kutendewa kama mtoto milele.
KUWA NA MAONGOZI YANAYOPATANA
Uhitaji mwingine wa kijana ni kupata uongozi imara na unaopatana. Akizungumza juu ya jambo hili, Mkuu wa jeshi la baharini James F. Calvert, ambaye ni msimamizi wa Shule ya jeshi la baharini la U.S. na ni baba ya watoto watatu, alisema hivi karibuni, kama ilivyoripotiwa katika The Detroit News:
“Watoto wa leo wanajifunza zaidi kutoka kwa television kuliko yale watakayojifunza kutoka kwetu. Mtoto wa kawaida wa miaka 15 anatumia dakika 20 kila siku akisoma na saa mbili akitazama television.”
Baada ya kutoa maelezo juu ya kushindwa kwa wazazi kutia ndani ya watoto wao ‘daraka la kazi na kujivunia jamaa,’ aliendelea kusema hivi: “Pasipo adabu hakuwezi kuwa na heshima ya msingi.” Calvert alifananisha adabu ya kibinadamu na ganda la yai. “Linapokuwa kamili,” alisema, “ni lenye nguvu na linapendeza. Likivunjika kidogo, upesi linavunjika-vunjika.
“Huenda vijana wasiombe adabu, walakini wanaihitaji sana sana. Wazazi wakitumia mamlaka yao watoto wanajisikia salama.”
Kijana anahitaji usalama wa adabu inayopatana. Huenda asikubali mara moja uhitaji wo vizuizi pamoja na amri fulani, walakini atakubali upesi kwamba inawapasa wazazi wake wawe na amri zinazopatana. Anataka kujua yale anayokubaliwa au asiyokubaliwa kufanya. Anakata tamaa ikiwa amri hizo zinabadilishwa siku baada ya siku kulingana na namna mzazi “anavyojisikia” wakati huo. Yesu alisema: “Maneno yenu yawe Ndiyo ndiyo; Siyo, siyo.”—Mt. 5:37.
Amri na vizuizi vyaweza kufananishwa na mipaka. Kijana anahitaji mipaka inayoonyeshwa waziwazi; kisha anataka kutumainiwa na kuwa na uhuru ndani ya mipaka hiyo. Baba mmoja alifananisha uhakika huu na jambo lililoonwa na jamaa yake kwa habari ya nyumba waliyokodisha:
“Lilikuwa eneo lenye miti. Mojawapo la maulizo tuliyouliza ni mahali ilipokuwa mipaka. Tulitaka kujua, Ni jambo gani tunaloruhusiwa kufanya katika eneo hilo? Lingekuwa jambo la lazima kujua hili ili tupate kufurahia kuishi humo. Waweza kuwazia namna ambavyo lingekuwa jambo lenye kuvunja moyo na kukatisha tamaa ikiwa mwenye sehemu hiyo angebadilisha vizuizi kila juma. Kanuni iyo hiyo inatumika kwa habari ya vizuizi wanavyowekewa vijana. Amri zenyewe zaweza kuwa zenye kiasi na zenye kupatana. Kisha uwatumaini na kuwapa uhuru ndani ya mipaka hiyo.”
Amri hizo hazipaswi kuwa ngumu kupita kiasi. Jambo la pekee laweza kuwa sababu ya kutosha kufikiria ombi la pekee.
SAIDIA KATIKA KUWEKA MIRADI MAISHANI
Uhitaji wa uongozi unatia ndani kusaidia katika kuweka miradi maishani, kuchagua kazi na kupata elimu ya kilimwengu inayohitajiwa. Kila mtu anapaswa kujisikia kwamba anafaa na kwamba yale anayofanya yanafaa. Inampasa ajiheshimu na kujionea fahari kama mtu bi nafsi.
Wazazi wanaonyesha kwamba wanahangaikia kijana wao wanapomsaidia kuchagua kazi inayomfaa. ‘‘Karama” zake pamoja na uwezo wake wa kufanya mambo au mambo anayopendelea yanapaswa kufikiriwa. (Linganisha Warumi 12:6.)ʼ Anapaswa kusaidiwa kuweka miradi inayoweza kufikiwa. Si kila mtu anayeweza kufikia cheo chenye sifa. Miradi inaweza kutimizwa kikweli kwa kuweka miradi ya juu zaidi kadiri kila mradi mdogo unavyotimizwa.
Kuna daraka zito la kutoa elimu ambayo itawatayarisha vijana kukabili magumu ya maisha ya mtu mzima. Vijana wanapaswa kuzoezwa na kuwa na ujuzi katika kazi fulani ili waweze kujilisha. (1 Tim. 5:8; Mit. 31:10, 19, 20) Ijapokuwa Yesu ndiye aliyetazamiwa kuwa Kristo, Yusufu baba yake mlezi alimfundisha kazi hata kwamba alikuja kujulikana kama “mwana wa seremala” na “seremala.” (Mt. 13:55; Marko 6:3) Mtume Paulo alijilisha mwenyewe pamoja na wale waliokuwa naye kwa kufanya kazi yake ya kutengeneza hema. —Matendo 18:1-4; 20:33, 34.
Katika kujitayarisha ili kukabili magumu ya maisha ya mtu mzima na kukubali madaraka ya mtu mzima, vijana wanahitaji kusaidiwa na wazazi wao, na kutiwa moyo ili wasishindwe maishani. Mara nyingi wanahitaji kusaidiwa wanapofanya masomo wanayopewa shuleni ya kufanyia nyumbani. Mara nyingine huenda wakajisikia kushindwa. Nyakati kama hizo, wazazi wanaweza kuwa chanzo cha kutia moyo kwa kufahamu mambo yanayokatiza tamaa na kuyazungumza waziwazi pamoja nao. Ikiwa mzazi anasaidia mara kwa mara na masomo magumu ambayo kijana amepewa shuleni afanyie nyumbani, yeye anaweza kufahamu vizuri zaidi mambo yenye kukatisha tamaa ambayo kijana hukabiliana nayo anapokuwa akifanya masomo ambayo amepewa shuleni afanyie nyumbani naye mzazi atakuwa katika hali nzuri ya kutoa mashauri yanayofaa. Mara nyingine kijana anatiwa moyo na kusaidiwa ashinde hali ngumu kwa sababu tu mzazi mwenye kufahamu amechukua wakati wa kuzungumza naye juu ya hali hiyo.
KUJISIKIA KUWA UNAHITAJIWA
Labda tamaa kubwa kupita zote ni ile ya kujisikia kuwa unahitajiwa. Kwa sababu hiyo, mara kwa mara watoto wanawauliza wazazi wao kama wao ni wazazi wao halisi au ni wazazi walezi tu, au kama wazazi wao walipanga kuwa nao na kama walitaka kuwa nao. Wanataka kuhakikishiwa kwamba wazazi wao wanawapenda. Sisi sote tunatamani sana kuwa na usalama wa kujua kwamba tunahitajiwa. Ikiwa wazazi watakubali mahitaji ya vijana wao na kuyatosheleza. kwa ufahamu, hali ya jamaa itakuwa yenye furaha zaidi.