Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w80 6/15 kur. 3-8
  • Kumfurahia “Mungu wa Tumaini”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kumfurahia “Mungu wa Tumaini”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UHITAJI WA TUMAMINI LENYE UZIMA
  • TUMAINI KATIKA “UZAO”
  • MSINGI UNAOFAA WA TUMAINI LA UZIMA WA MILELE
  • TUMAINI LA SERIKALI YENYE HAKI
  • Furahia Tumaini Lisilokatisha Tamaa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2023
  • Mtumaini Yehova na Uwe Hodari
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Tumaini Katika Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Kushangilia Katika Tumaini Letu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
w80 6/15 kur. 3-8

Kumfurahia “Mungu wa Tumaini”

“Wewe u tumaini langu, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, uhakika wangu tangu ujana wangu.”​—Zab. 71:5, NW.

1, 2. (a) Tuna ushuhuda gani wa Kimaandiko wa kwamba Mungu hutujali sisi? Furaha yetu yaweza kukamilishwaje?

JE! NYAKATI nyingine wewe unatua na kuufikiria uhusiano wako wenye thamani pamoja na Mungu? Namna inavyosisimua kufahamu kwamba Mungu hutujali! Kweli, kwa maoni ya Yehova mataifa ni kama tone tu la maji kutoka katika ndoo. Kwa hiyo, kama mtu mmoja, kwa hakika twaonekana kuwa wadogo sana kwake. Hata hivyo, Yesu Kristo anatuhakikishia hivi: “Je! mashomoro wawili hawauzwi kwa senti moja? Wala hata mmoja haanguki chini asipojua Baba yenu; lakini ninyi, hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope basi; bora ninyi kuliko mashomoro wengi.”​—Mt. 10:29-31; Isa. 40:15.

2 Iwapo Mungu huona shomoro akianguka, basi sisi wanadamu alioumba kwa mfano wake anatuhurumia kama nini! (Mwa. 1:26) Kwa kweli, Mungu wetu anastaajabisha sana katika hekima na uwezo wake wa kuumba, walakini yeye ni mwenye ubora mwingi hata zaidi katika kuliangalia kusudi la haki la wale wanaoonewa na katika kuonyesha upendo mwingi kwa wanadamu. (Zab. 33:4, 5) Kwa hakika ni pendeleo kwamba sisi twaweza kuingia katika upendo wake na kukaa katika huo, kwa kupatana na uhakikisho wa Yesu: “Mkizishika amri zangu, mtakaa katika pendo langu; kama vile mimi nilivyozishika amri za Baba yangu na kukaa katika pendo lake.” Naye Yesu akaongeza hivi: “Hayo nimewaambia, ili furaha yangu iwe ndani yenu, na furaha yenu itimizwe.”​—Yohana 15:10, 11.

3. Sababu gani Daudi alikuwa na uhakika kamili katika Yehova, nasi pia sababu gani?

3 Katika nyakati hizi zenye hatari, twaweza kufurahi pia kwamba Mungu wetu atupendaye anatoa tumaini. Inaonekana kwamba Daudi aliiandika Zaburi ya 71 baada ya kupatwa na majaribu makali, na humo anamtukuza Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova kuwa tumaini na uhakika wake tangu ujana. Kwa mfano, alipokuwa analikabili jitu lenye kujikokota Goliathi, Daudi alitangaza hivi: “[Yehova] aliyeniokoa na makucha ya simba, na makucha ya dubu, ataniokoa na mkono wa Mfilisti huyu.” Yehova alifanya hivyo! (1 Sam. 17:37, 45-50) Na mpaka siku hii Yehova anaendelea kutegemeza mabaki watiwa mafuta wa mashahidi wake ambao, wakiwa na tumaini lenye nguvu, wamemtumikia kwa uaminifu ‘tangu ujana wao.’

UHITAJI WA TUMAMINI LENYE UZIMA

4. Sababu gani mambo “yaliyotangulia kuandikwa” ni chanzo cha tumaini?

4 Ahadi za kufikia wakati mrefu za Yehova kama vile zilivyoandikwa katika Neno lake, kweli kweli ni chanzo cha tumaini lenye uhakika kwa wakati ujao. Kama asemavyo mtume Paulo: “Kwa kuwa yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi; ili kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini.” (Rum. 15:4) Hakika, tunahitaji kuwa na tumaini. Walakini mambo “yaliyotangulia kuandikwa” yanatoaje sababu ya tumaini? Kwanza kabisa, sababu gani uhitaji wa tumaini ukatokea?

5. (a) Uhitaji wa tumaini ulitokeaje? (b) Sababu gani wazazi wetu wa kwanza walijiletea adhabu ya kifo kwa haki, na sababu gani sisi twatiwa ndani?

5 Mambo “yaliyotangulia kuandikwa” yanasimulia waziwazi namna Mungu alivyowaumba wazazi wetu wa kwanza na kuwaweka katika paradiso ya furaha, wakiwa na taraja la kuishi milele na kuijaza dunia kwa wanadamu wenye upendo, wenye furaha ambao hawangekufa kamwe. (Mwa. 1:26-28; 2:7-9, 18-25) Lakini, Adamu na Hawa walipoteza pendeleo hilo. Sababu gani? Ilikuwa kwa sababu wali-fanya dhambi, wakakosa shabaha ya utii mkamilifu kwa Baba yao, Yehova Mungu. Kwa haki, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova aliwahukumia wenzi hao wawili kifo. Walikuwa wamekuwa wenye kujitakia yao wenyewe, wenye kujitegemea, na hawakuwa na pahali tena kati ya viumbe washikamanifu wa Yehova. Na zaidi ya hayo, walipasisha adhabu ya kifo si juu yao wenyewe tu bali pia juu ya mabilioni ya watoto ambao wangezaliwa na wazazi hao wenye dhambi. Kama vile atuambiavyo Paulo: “Kwa hiyo, kama kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.”​—Rum. 5:12.

6. Viumbe vilitiwa utumwani kwa msingi wa tumaini gani?

6 Hata hivyo, Paulo anaendelea kusema kwamba, ingawa “viumbe vyote pia vilitiishwa chini ya ubatili,” ilikuwa juu ya msingi wa “tumaini.” Tumaini gani? Kwani, si tumaini lenye uzima ambalo kwalo ‘vingewekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata viingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu,’ kama vile tu wazazi wetu wa kwanza walivyofurahia uhuru huo katika paradiso ya Edeni? Lingetia ndani tumaini la uzima wa milele. Ni Mungu tu ambaye angeweza kutoa tumaini kama hilo.​—Rum. 8:20, 21; Yohana 17:3.

TUMAINI KATIKA “UZAO”

7. “Uzao” wa ahadi hiyo unatambulishwaje?

7 Mapema katika mambo “yaliyotangulia kuandikwa” twasoma ahadi ya Mungu kwamba “uzao” wa tengenezo lake lililo kama mke mbinguni ‘utajeruhi [nyoka] kichwani,’ yaani, kumharibu Shetani, pamoja na uzao wake wote. (Mwa. 3:14, 15) Walakini ni nani “uzao” huo? Baadaye yeye anazungumzwa kuwa pia “uzao” wa rafiki ya Mungu Ibrahimu, uzao ambao kupitia kwao “mataifa yote ya dunia watajibarikia.” Mtume Paulo anatambulisha “uzao” huo, akisema hivi: “Basi ahadi zilinenwa kwa Ibrahimu na kwa mzao wake. . . . Kwa mzao wako, yaani Kristo.”​—Mwa. 22:18; Gal. 3:16.

8. (a) Mwendo wa maisha ya Yesu duniani ulitabiriwaje muda mrefu kabla? (b) Upendo wa Mungu kwa wanadamu ulionyeshwaje?

8 Mambo “yaliyotangulia kuandikwa” yaliutabiri mwendo wa maisha ya Kristo Yesu wakati angekuwa duniani. Kama vile Isaya alivyotabiri zaidi ya miaka 700 kabla, Yesu alidharauliwa, akaonwa kuwa si kitu, akaonewa na ‘kupelekwa kama kondoo machinjoni.’ Kwa kupatana na mapenzi ya Baba yake, “alimwaga nafsi yake” katika kifo, kusudi kwamba aweze kukomboa “watu wengi” kutoka katika utumwa wa dhambi. (Isa. 53:3-12) Yehova alimfufua kutoka kwa wafu na kumweka awe ‘Wakili Mkuu wa uzima’ katika mbingu, “ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” Mungu ametoa mpango huo kwa sababu Yeye “aliupenda ulimwengu [wa wanadamu]” sana. (Yohana 3:15, 16; Matendo 3:15, NW) Jambo hilo limetoa tumaini zuri sana kama nini!—Yohana 5:24-29.

MSINGI UNAOFAA WA TUMAINI LA UZIMA WA MILELE

9. (a) Ni jambo gani linalohakikisha tumaini letu? (b) Tumaini letu lapaswa kuwa na matokeo gani yetu?

9 Tumaini letu lenye msingi mzuri linahakikishwa na jina lenyewe la Mungu wetu, Yehova. Jina hilo linamaanisha “Yeye Hufanya Iwe,” kuonyesha kwamba yeye hufanya mambo fulani yatokee katika kutimiza makusudi yake. Yeye ndiye Mungu yule “asiyeweza kusema uongo” na ambaye anatoa msingi wa “tumaini . . . aliuahidi tangu milele.” (Tito 1:2) Tumaini hilo linamaanisha nini kwako? Je! unaliona kama watu wa Jumuiya ya Wakristo wanavyoiona dini yao—kama desturi ambayo wanaitolea utumishi wa mdomo tu? Au je! ndani ndani ya moyo wako, umekwisha kuweka wakf mwili wako wote, uhai wako wote, kwa “Mungu wa tumaini”? (Rum. 15:13) Je! tumaini hilo limekuwa lenye nguvu sana kwako kwamba tayari linaonekana kama jambo lililotokea? Ikiwa ndivyo, basi limekuwa imani yako—imani ambayo itakuwa yenye uzima kwa matendo mazuri katika kuwatolea wengine ushuhuda juu ya tumaini lako.​—Ebr. 11:1; Yak. 2:17.

10. (a) Ni jambo gani linaloongezea nguvu tumaini letu? (b) Sababu gani Wakristo waliotiwa mafuta wanapaswa kulifurahia tumaini lao sasa?

10 Kama vile Bwana Mwenye Enzi Kuu wetu Yehova anavyoishi milele, ndivyo na ahadi zake zinavyotoa msingi wa “tumaini lenye uzima.” Naye Mwana wake aliyefufuliwa, Yesu Kristo, “kwa kuwa akaa milele,” anaongezea tumaini hilo nguvu, kwa kuwa “aweza kuwaokoa kabisa wao wamjiao Mungu kwa yeye; maana yu hai sikuzote ili awaombee.” (Ebr. 7:24, 25) Hivyo, mtume Petro aliandikia Wakristo watiwa mafuta hivi: “Ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kwa rehema zake nyingi alituzaa mara ya pili ili tupate tumaini lenye uzima kwa kufufuka kwake Yesu Kristo katika wafu; tupate na urithi usioharibika, usio na uchafu, usionyauka, uliotunzwa mbinguni kwa ajili yenu. Nanyi mnalindwa na nguvu za Mungu kwa njia ya imani hata mpate wokovu ulio tayari kufunuliwa wakati wa mwisho. Mnafurahi sana [katika hilo].” (1 Pet. 1:3-6) Kwa kuwa sasa tumefikia “wakati wa mwisho,” kuna sababu yenye nguvu kwa Wakristo waliotiwa mafuta kufurahi katika tumaini hilo.

11. (a) “Mkutano mkubwa” pia una ‘tumaini gani lenye uzima?’ (b) Kuna msingi gani imara kwa tumaini hilo?

11 Walakini, namna gani juu ya “mkutano mkubwa, . . . wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha,” unaotazamia uzima wa milele katika dunia iliyo paradiso? Lao, pia, ni “tumaini lenye uzima,” kwa kuwa ahadi waliyopewa ni hii: “Hawataona njaa tena, wala hawataona kiu tena, wala jua halitawapiga, wala hari iliyo yote. Kwa maana huyo Mwana-Kondoo, aliye katikati ya kiti cha enzi [cha Mungu], atawachunga, naye atawaongoza kwenye chemchemi za maji yenye uhai, na Mungu atayafuta machozi yote katika macho yao.” (Ufu. 7:9, 16, 17) Wale wanaotumainia “habari njema” hizo hawatakatishwa tamaa, kwa kuwa msingi wake wote ni Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho. Akitaja maneno ya Isaya 40:8, mtume Petro alisema hivi juu ya “neno la Mungu anayeishi na anayedumu: “‘Miili yote ni kama nyasi, na utukufu wayo yote ni kama kuchanua kwa nyasi; nyasi hunyauka, nalo ua linaanguka, bali usemi wa Yehova hudumu milele.’ Naam, huo ndio ‘usemi,’ ambao umetangazwa kwenu kama habari njema.”​—1 Pet. 1:23-25, NW.

12. Mungu ni mkarimu kadiri gani katika kutoa uzima wa milele?

12 Akijieleza kuwa ndiye mchungaji mwema ambaye “huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo,” Yesu alisema hivi, “Mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele.” (Yohana 10:10, 11) Ukarimu huo hauonyeshwi “kundi dogo” peke yake, ambao watakuwa warithi-washirika na Kristo mbinguni. (Luka 12:32) Sivyo, kabisa, kwa kuwa Yesu alisema hivi: “Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja. Nami nawapa uzima wa milele.” (Yohana 10:16, 28) Pamoja na “mkutano mkubwa” unaotazamia kupita ile “dhiki kubwa” wakiwa hai, kutakuwako watumishi waaminifu wa nyakati za kabla ya Ukristo na mabilioni ya wafu wengine wa kibinadamu ambao watafufuliwa duniani wakiwa na mataraja ya uzima wa milele. (Mt. 24:21; Ebr. 11:35; Ufu. 20:12) Mungu wetu ni mkarimu kama nini kwa kutoa mpango huo wa uzima!

13. Upendo wa Mungu kwa wanadamu unaonyeshwaje, nalo hilo lapaswa kuwa na matokeo gani kwetu?

13 Ukarimu wa Yehova katika kuonyesha upendo wake kwa wanadamu unaonyeshwa vilevile katika maneno ya Yesu ya mapema zaidi: “Mungu aliupenda ulimwengu [wa wanadamu], hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu [kwa hukumu mbaya] bali ulimwengu uokolewe katika yeye. Amwaminiye yeye hahukumiwi.” (Yohana 3:16-18) Kwa kuwa Yehova na Mwanawe ni wakarimu sana, je! sisi hatupaswi kuwa wakarimu, vilevile, katika kujulisha wengine “habari njema” hizi za utukufu?

14. (a) Sababu gani mataifa ‘hayana tumaini?’ (b) Tunaonyeshaje imani na “tumaini lenye uzima” letu?

14 Kwa kufanya jambo hilo, tunashiriki katika “matendo mema, ambayo tokea awali Mungu aliyatengeneza ili tuenende nayo.” Sisi hatuko kama wale ambao Paulo anasimulia kuwa “wageni wasio wa maagano ya ahadi ile” na wasio na “tumaini” na bila “Mungu duniani.” Hatuenendi tena “kama mataifa waenendavyo, katika ubatili wa nia zao; ambao akili zao zimetiwa giza, nao wamefarikishwa na uzima wa Mungu, kwa sababu ya ujinga uliomo ndani yao, kwa sababu ya ugumu wa mioyo yao.” (Efe. 2:10, 12; 4:17, 18) Hasha, kwa kuwa sasa twaenenda na Mungu, nayo “matendo mema” yetu, ambayo yanatia ndani kuhubiri na kufundisha “habari njema,” yanaonyesha imani yetu na “tumaini lenye uzima” lijaalo sana na kufurika mioyoni mwetu.​—Mt. 4:17; 5:16; 9:35; 24:14.

TUMAINI LA SERIKALI YENYE HAKI

15. (a) Sababu gani serikali nzuri ni ya lazima ili tuwe na “tumaini lenye uzima”? (b) Isaya aliandika unabii gani wenye kutia moyo kwa habari ya jambo hilo?

15 Tumaini letu lenye uzima linatia ndani zaidi ya taraja la uzima wa milele. Fikiria: Je! ingefurahisha kuishi milele chini ya serikali za kibinadamu zenye ukatili na zenye kuonea, kama zile ambazo zimetawala wakati mwingi katika historia yote? Wengine wangependelea kufa kuliko utumwa wa namna hiyo. Inafurahisha kwamba tumaini lenye uzima la watu wa Mungu linatia ndani tumaini la serikali yenye haki, Ufalme ambao Wakristo wameomba kwa muda mrefu, na ambao utalitakasa jina la Yehova na kufanyiza mapenzi yake “hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mt. 6:9, 10) Katika matayarisho yake ya muda mrefu ya ufalme huo, Yehova alimtumia Mfalme Daudi wa Israeli kumfananisha Kristo Yesu katika daraka Lake kama Mfalme. Nabii Isaya alimsimulia Huyo kuwa “Mfalme wa amani,” kwa kusema hivi: “Maongeo ya enzi yake na amani hayatakuwa na mwisho kamwe, katika kiti cha enzi cha Daudi na ufalme wake; kuuthibitisha na kuutegemeza kwa hukumu na kwa haki, tangu sasa na hata milele. Wivu wa [Yehova] wa majeshi ndio utakaotenda hayo.”​—Isa. 9:6, 7.

16. Gabrieli na mtunga zaburi walitoa uhakikisho gani kuhusiana na Ufalme?

16 Zaidi ya miaka 1,000 baadaye, malaika Gabrieli alimtokea bikira, Mariamu, akamwambia hivi: “Umepata neema kwa Mungu. Tazama, utachukua mimba na kuzaa mtoto mwanamume; na jina lake utamwita Yesu. Huyo atakuwa mkuu, ataitwa Mwana wa Aliye juu, na [Yehova] Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi, baba yake, . . . na ufalme wake utakuwa hauna mwisho.” (Luka 1:30-33) Kwa hiyo huyu “Mwana wa Aliye juu” anatoa si njia ya wokovu kuingia kwenye uzima wa milele peke yake bali vilevile baraka kupitia kwa ufalme wake. Serikali hiyo itatawala wanadamu wote katika haki na kuletea raia zake duniani pote amani kwa wingi.​—Zab. 72:1-8.

17. Sababu gani, basi, twapaswa ‘kuzidi katika tumaini,’ nasi twaweza kulionyeshaje tumaini hilo?

17 Akitaja tena mambo “yaliyotangulia kuandikwa,” mtume Paulo anaandika hivi: “Na tena Isaya anena, Litakuwako shina la Yese [baba ya Daudi], naye aondokeaye kuwatawala Mataifa; ndiye Mataifa watakayemtumaini. Basi Mungu wa tumaini na awajaze ninyi furaha yote na amani katika kuamini, mpate kuzidi sana kuwa na tumaini, katika nguvu za [roho takatifu].” (Rum. 15:12, 13) Hakika, kutumaini kwetu ufalme wa Mungu kupitia kwa Kristo ni chanzo cha furaha na amani ya moyoni, na tuzidipo katika tumaini hilo, twatiwa moyo tuwatangazie wengine tumaini hilo, kwa nguvu tunazopewa na roho ya Mungu.​—Zek. 4:6; Isa. 40:28-31.

18. Isaya anatoa maono gani ya kimbele kuhusiana na Ufalme?

18 Kwa kuzungumza juu ya “shina la Yese,” Paulo alikuwa akitaja maneno ya Isaya sura ya 11, ambayo yanatoa maono haya ya kimbele ya utawala wa Kristo wa Ufalme: “Na roho ya [Yehova itakaa] juu yake, roho ya hekima na ufahamu, roho ya shauri na uweza, roho ya maarifa na ya kumcha [Yehova]; na furaha yake itakuwa katika kumcha [Yehova]; wala hatahukumu kwa kuyafuata ayaonayo kwa macho yake, wala hataonya kwa kuyafuata ayasikiayo kwa masikio yake; bali kwa haki atawahukumu maskini, naye atawaonya wanyenyekevu wa dunia kwa adili.” Baada ya kuisimulia hali ya amani ya paradiso ya kiroho ambayo watu wa Mungu wanafurahia hata leo, kama kwamba wanyama-mwitu wa dunia wamekwisha tiisha, unabii huo unatangaza hivi: “Dunia itajawa na kumjua [Yehova], kama vile maji yanavyoifunika bahari.” Tumaini tukufu kama nini! Si ajabu kwamba wengi kutoka kwa mataifa wanageukia “shina la Yese” kwa kutaka kujua, Yesu aliyetawazwa, ambaye ‘anasimama kama ishara kwa kabila za watu.’​—Mist. 1-10.

19. Sababu gani, sana sana sasa, twapaswa kulifurahia tumaini?

19 Tangu mwaka wenye matukio wa 1914, wanadamu wamekuwa wakiishi katika ‘mwisho wa taratibu ya mambo.’ “Mwana wa Adamu” amekwisha kufika, na malaika wote pamoja naye, kwa kusudi la kuketi juu ya kiti chake cha enzi cha kimbinguni chenye utukufu. Ameyakusanya mataifa kwa ajili ya kuhukumiwa na kuwabagua watu “kama vile mchungaji abaguavyo kondoo na mbuzi.” Kwa mataifa na “mbuzi” huu ni wakati wa taabu isiyo na tumaini, walakini kwa wanadamu watiifu wenye mfano wa kondoo huu ni wakati wa ‘kusimama [wima] na kuinua vichwa vyao juu, kwa maana ukombozi wao umekaribia.”—Mt. 24:3-8, NW; 25:31-34; Luka 21:26-28, HNWW.

20. Ni kwa kufanya nini sasa tutaweza kuvumilia katika tumaini hilo?

20 Hata hivyo, uvumilivu unahitajiwa kusudi tupate kuona kutimizwa kwa tumaini hilo. Kadiri hizi “siku za mwisho” zinavyokaribia kumalizika, twapaswa kuyaona mambo kama vile Yesu, kama vile Paulo alivyoonya: “Mungu aliye msingi wa saburi na faraja yote, awajalieni ninyi kuwa na msimamo mmoja kufuatana na mfano wake Kristo Yesu, ili ninyi nyote, kwa nia moja na sauti moja, mumtukuze Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo.” (Rom. 15:5, 6, HNWW) Basi, na tuendelee “na msimamo mmoja” “na sauti moja,” tukitumikia kwa uvumilivu, tunapozihubiri habari njema hizi za Ufalme “kwa ushuhuda kwa mataifa yote,” tukiwa na hakika kwamba “ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mt. 24:13, NW) Ndiyo, na tuweke uhakika wetu imara katika Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, “Mungu wa tumaini.”

[Picha katika ukurasa wa 5]

“Kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote.”​—Rum. 5:12

“Mungu aliupenda ulimwengu hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki