Nguvu Zinazotegemeza Ulimwengu—Je! Ni Nguvu Isiyofahamika au ni Mtu Halisi?
SAFARI za mwezini na uchunguzi wa kisayansi wa namna nyingi umeongeza sana maarifa yetu ya ulimwengu wote ulio mkubwa sana. Ukubwa wake wenye kutia woga na utaratibu ni mambo yanayokuwa wazi zaidi na zaidi. Kwa watu wengi, kuwapo kwa ulimwengu pasipo namna fulani ya nguvu yenye kuongoza ni jambo lisilo la akili. Ingawa mamilioni wamepoteza imani katika makanisa, mafundisho ya kidini na dini kwa ujumla, wangali wanamwamini “Mungu.”
Walakini neno “Mungu” lamaanisha nini kwako? Nguvu isiyojulikana? Akili fulani isiyofahamika vizuri? Mtu asiye na jina ambaye yuko mbali sana, asiyeelezeka?
Au, je! kwako wewe, “Mungu” anamaanisha mtu wa kibinafsi sana, aliye karibu na apendwaye kama baba mwenye upendo? Kwa wale wanaoweka imani yao katika sayansi na ufundi, hilo huenda likaonekana kuwa jambo la upumbavu. Walakini fikiria jambo hili:
UWEZO WA KUFANYA MAMBO WA SAYANSI NA UFUNDI NI WA KIASI TU
Kwa habari ya uvumbuzi na maarifa yenye kuongezeka, tunaishi katika karne yenye kusisimua. Mambo ambayo wanadamu wametimiza ni yenye kutokeza. Watu wenye karama wameipatia jamii ya kibinadamu vitu vingi vya ajabu vilivyovumbuliwa ambavyo vimeongeza utendaji na maarifa ya wanadamu.
Hata hivyo wanasayansi, wakiwa na maarifa yaliyoongezeka na ufundi wao mkubwa, ndio wa kwanza kukubali kwamba hawawezi kutokeza hata chembe moja yenye uhai. Kitu cha kawaida kama vile unyasi unazidi sana uwezo wa wanasayansi kufanyiza.
Katika kujaribu kueleza mambo ya ajabu yanayowazunguka, waandikaji wengine hutumia semi kama vile “Mama Asili alifanyiza hiki,” au, “Mageuzi yalifanya hicho,” kama kwamba vitu hivyo ni watu wenye akili. Lakini je! haiko wazi kabisa kwamba nguvu isiyo na akili haiwezi kuwa ndiyo iliyotokeza namna mbalimbali za vitu vilivyo hai vyenye kustaajabisha. Wala nguvu hiyo isiyo na akili haingetokeza hekima na uwezo usiopimika unaoonyeshwa katika ulimwengu wote ulio mkubwa mno?
MAKAO YA MWENYE AKILI AU ROHO
Tunapoingia katika makao ya mwenye akili au roho na kutafuta kufahamu chanzo cha sifa kama vile hekima, haki ya hukumu, rehema, fadhili na kweli, twaweza kupata wapi majibu yenye kutegemeka ya maulizo yetu? Je! mwanadamu ye yote anaweza kueleza kazi na chanzo cha kitu cha ajabu kinachotenda cha utu wa ndani wa mtu kinachomwambia anapotenda kosa—dhamiri ya kibinadamu? Wanyama hawana dhamiri. Lakini hata watu wasiostaarabika, wasio na elimu wanayo. Kama alivyoeleza wakati mmoja mwandikaji Mkristo wa zamani Paulo: “Wanaonyesha kazi ya sheria iliyoandikwa mioyoni mwao, dhamiri yao ikiwashuhudia humo ndani, na mafikira yao yenyewe kwa yenyewe yakiwashtaki au sivyo yakiwaruhusu.” (Rum. 2:15, American Standard Version) Mambo hayo hayawezi kufahamika kwa uwezo wa kibinadamu. Na, hata hivyo, je! mambo ya akili na ya kiroho yaliyotimizwa na wanadamu si ya maana zaidi sana kuliko uwezo wake wa kimwili?
Wanyama wengi wana uwezo mkubwa wa kimwili kuliko wanadamu. Ndovu (tembo) ni wenye nguvu zaidi, tai wanaweza kuona mbali zaidi, swala wanaweza kukimbia mbio zaidi, popo wanaweza kusikia vizuri zaidi, mbwa wananusa vizuri zaidi. Walakini ni mnyama gani anayeweza kubuni vitu vipya? Ni kweli kwamba ndege wanaweza kufanyiza viota, beavers (wanyama wadogo wa jamii ya panya) wanaweza kufanyiza maboma ya maji, buibui wanaweza kutanda utando. Lakini viumbe hao hufanyiza kitu kile kile pasipo badiliko katika kiolezo kile. Hakuna anayeweza kupiga ramani ya kitu kipya na kukikuza.
Tofauti kabisa na hayo, wanadamu wanaweza kuwaza juu ya jambo fulani, kupiga ramani na kufanyiza vitu vya namna nyingi mbalimbali. Awe ni mwanamke anayefuma fulana au mafundi wanaounda chombo cha angani kiende mwezini na kurudi, viwavyo vyote, wanadamu hufurahia kufanyiza vitu. Ni sehemu ya maumbile ya wanadamu. Wakiwa na uwezo wa akili na tabia unaozidi sana sana ule wa wanyama na uwezo wa asili wa kufanyiza vitu, wanadamu ni sura isiyokamilika ya Aliye Mkuu Zaidi, aliyefanya mwanadamu kwa mfano Wake.—Mwa. 1:26.
Sasa fikiria sifa nyingine ya wanadamu wasiyokuwa nayo wanyama—tamaa yake ya kuabudu. Ni jambo la hakika lisiloweza kukanushika lililo wazi katika vizazi na mataifa yote kwamba, wanadamu wana tamaa nyingi ya asili ya kuabudu uwezo usioonekana.
Wanafilosofia wa kisasa wanaweza kukana jambo hilo, wakisema, “Tumekwisha endelea kupita jambo hilo.” ‘Kuendelea’ kufika kwenye kitu gani? Kwenye ulimwengu unaotumbukia kutoka kwa hatari moja kwenda kwa nyingine na unaoogopa sana kupatwa na msiba wa ulimwenguni pote. Sababu gani? Kwa sababu watu wengi sana wameabudu “miungu” ya ufundi mawazo mbalimbali huku wakikataa hekima ya Aliye Mkuu Zaidi.—Yer. 8:9.
Hivyo, watu wengi leo, wajapokuwa wamepoteza imani katika makanisa na dini, wanakubaliana na maneno kutoka katika kitabu kinachosomwa sana na kinachoheshimiwa kuliko kingine cho chote kilichopata kuwapo, Biblia, ambayo inasema juu ya Aliye Mkuu Zaidi hivi: “Sifa zake zisizoonekana, yaani, uwezo na uungu wake wa milele, vimekuwa vikionekana, tangu ulimwengu ulipoanza, kwa jicho la akili, kupitia kwa vitu vilivyofanywa.”—Rum. 1:20, The New English Bible.
WANASAYANSI WAMESAIDIA SANA
Kadiri wanasayansi wanavyochunguza zaidi na zaidi ulimwengu wote ulio mkubwa mno, chembe iliyo ndogo zaidi na namna zote za vitu vilivyo hai, ndivyo uchunguzi wao unavyozidi kufunua uzuri, upatano na kutofahamika kwa vitu hivyo. Ukubwa usiopimika wa ulimwengu wote na jinsi ilivyo vigumu kuufahamu ni jambo linalotatiza sana akili za wanadamu. Walakini hakuna jambo linalotokea pasipo chanzo. Katika uzuri wote huo, wonyesho huo wa ajabu wa hekima na uwezo mwingi sana, je! wewe ‘huoni’ kwa “jicho la akili” “sifa zisizoonekana” za Muumba Mkuu? Bila shaka, ulimwengu wote ulio mkubwa mno unaongozwa kwa sheria zisizobadilika. Je! jambo hilo halithibitishi kuwapo kwa Mtoa Sheria Mkuu Zaidi? Hali na vitu vingi visivyoheshabika duniani kwa wazi vilifanywa ili vifae kabisa mahitaji ya wanadamu. Na mambo mengi hayo lazima yawe na CHANZO chake, Mpaji mkuu na Mtoaji-Uzima.
Wanasayansi wengine wanasema nini juu ya jambo hilo?
Frank Allen, mtaalamu wa elimu ya viumbe na nguvu, alieleza hivi: “Matayarisho ya dunia kwa ajili ya uhai ni mengi sana hata haiwezi kuwa yalijitokeza yenyewe.”
Mwalimu wa chuo kikuu wa hesabu katika Chuo Kikuu cha Cambridge, P. Dirac, aliandika hivi katika gazeti Scientific American: “Mungu ni mtaalamu wa hesabu mkuu zaidi, Naye alitumia hesabu ngumu sana katika kuumba ulimwengu wote.”
Bwana Isaac Newton, anayeelezwa na wanahistoria wengi wa sayansi kuwa “mwanasayansi mkubwa zaidi kuliko wote ambao ulimwengu umepata kuona,” aliandika hivi katika kitabu chake kinachojulikana sana Principia: “Utaratibu huu mzuri sana wa jua, sayari, na nyota zenye mkia, ungeweza kutokana tu na shauri na milki ya Mtu mwenye akili na mwenye nguvu. . . . Mungu Mkuu Zaidi ni Mtu anayeishi milele, hana mwisho, mkamilifu kabisa.”
Pengine unakubaliana na Bwana Isaac Newton. Vilevile, pengine wewe hufurahia fahari ya nyota, uangavu wa jua, uzuri wenye utulivu wa mwezi, kuburudisha kwa mvua, fahari ya milima, hali yenye kubadilika wakati wote ya mawingu na bahari, maua mbalimbali yenye kustaajabisha, miti, wadudu, ndege na wanyama, kicheko cha watoto, fadhili za rafiki na upendo wa mwenzi. Na ndani kabisa ya moyo wako unafahamu kwamba vyote hivyo vilitolewa na MTU halisi—Mjenzi mkuu wa ulimwengu wote ulio mkubwa mno.—Ebr. 3:4.
Basi, ni jambo la akili linalopatana na mambo yote ya hakika na kuwaza kote kwamba Aliye Mkuu Zaidi bila shaka ni MTU HALISI. Ikiwa ndivyo, je! yeye ana jina? Ikiwa ndivyo, JINA hilo ni jina gani?