Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 6/22 kur. 6-9
  • Je, Ulimwengu Ulitokea Wenyewe Tu, Au Uliumbwa?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Ulimwengu Ulitokea Wenyewe Tu, Au Uliumbwa?
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Pande Mbili za Suala Hilo”
  • Mwanzo Wenye Utaratibu
  • Kwa Nini Wengine Hawataki Kuamini
  • Jinsi Vyombo vya Angani Viwezavyo Kusafiri
  • Ulimwengu Uliumbwa na Nani?
  • Je, Kweli Ulimwengu Ulikuwa na Mwanzo?
    Amkeni!—1999
  • Ulimwengu Wetu Ulitokeaje?—Ubishi Uliopo
    Je, Kuna Muumba Anayekujali?
  • Ulimwengu Wetu Wenye Kustaajabisha—Je, Ulitokea kwa Nasibu?
    Amkeni!—2000
  • ‘Kitu Fulani Kinakosekana’—Kipi?
    Amkeni!—1996
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 6/22 kur. 6-9

Je, Ulimwengu Ulitokea Wenyewe Tu, Au Uliumbwa?

WANASAYANSI wengi hawapendi wazo la kwamba ulimwengu uliumbwa na Muumba mwenye akili. Basi wao hukisia-kisia kwamba ulimwengu ulitokea wenyewe tu kwa njia fulani. Lakini hakuna mtu ambaye ameweza kueleza jinsi ambavyo ulimwengu ungetokea wenyewe.

Kwa kweli, ni kama vile gazeti Scientific American lilivyotaarifu katika toleo la Januari 1999: “Nadharia ya mlipuko mkubwa haielezi jinsi ulimwengu ulivyoanza.” Gazeti hilo likaendelea kusema: “Nadharia nyingine inayofafanua nyakati za mapema hata zaidi itahitajiwa ili kufafanua uumbaji wa awali wa ulimwengu.”

Lakini, je, wewe unaona kama ni jambo lenye kupatana na akili kwamba kwa njia fulani ulimwengu ulijiumba wenyewe? Mwanafizikia Charles H. Townes alisema hivi: “Ni kweli kwamba wanafizikia hutumaini kuchunguza ‘mlipuko mkubwa,’ na labda kueleza kwamba ulimwengu ulitokana na aina fulani ya mabadiliko, tukisema kwa mfano. Lakini, mabadiliko ya nini na mabadiliko hayo yalianzaje kuwapo? Kwa maoni yangu, sikuzote swali la mwanzo huonekana kama halijibiwi tukilichunguza kwa maoni ya kisayansi pekee.”

Sasa imekubalika kwamba pindi moja ulimwengu haukuwapo na kwamba kwa njia fulani ukapata kuwapo. Je, mambo ambayo yamejulikana kuhusu kanuni zinazoongoza ulimwengu yanaweza kutusaidia kuelewa jinsi ulimwengu ungalipata kutokea?

“Pande Mbili za Suala Hilo”

Jambo hilo limetajwa kuhusu nishati na mata. “Mata ni aina mojawapo tu ya nishati,” Scientific American lilisema. Uhusiano huu uliopo baina ya mata na nishati ulionyeshwa na hesabu maarufu ya Einstein ya E=mc2 (nishati inatoshana na masi × mwendo wa nuru maradufu). Hesabu hiyo inafunua kwamba masi, au mata, kidogo tu ina nishati nyingi ajabu. “Inaonyesha,” asema profesa wa chuo kikuu Timothy Ferris, “kwa nini bomu linalotoshana na chungwa linaweza kuangamiza jiji lote.”

Tukitazama upande mwingine wa suala hilo—kulingana na nadharia ya Einstein, nishati vilevile inaweza kugeuzwa kuwa mata. Kufanyizwa kwa ulimwengu halisi huenda kulihusu kitu ambacho mtaalamu mmoja wa ulimwengu anakiita “mgeuzo mkuu ajabu wa mata kuwa nishati ambao umepata kutokea.”

Lakini, mata na nishati zilizohitajika kufanya “mgeuzo” huo zilitoka wapi? Sayansi haina jibu lenye kuridhisha. Kwa kupendeza, Biblia yasema hivi kuhusu Mungu: “Kwa sababu ya wingi wa nishati zenye nguvu, na vilevile akiwa na nguvu nyingi, hakuna hata moja ya [magimba ya kimbingu] linalokosekana.” (Isaya 40:26, NW) Hata Mungu awe alitumia njia gani kuumba ulimwengu, kwa wazi yeye ana nishati na uwezo wa kufanya hivyo.

Je, uthibitisho wa kisayansi waandaa msingi wa kuamini kwamba Mtu Mwenye Akili Zaidi ndiye aliyeumba ulimwengu wetu? Kutazama jinsi ulimwengu ulivyoanza kunaweza kutujibu.

Mwanzo Wenye Utaratibu

Ebu fikiria jambo hili: Kugeuzwa kiholela kwa mata iwe nishati katika mlipuko wa bomu la nyuklia husababisha mvurugo, kama ilivyoonekana nchini Japani wakati Hiroshima na sehemu kubwa ya Nagasaki ilipoharibiwa vibaya na mabomu kama haya mwaka wa 1945. Lakini, mbali na kuwa mvurugo, ulimwengu una upatano na ni maridadi! Fikiria vilevile dunia hii ya ajabu ikiwa na aina nyingi zenye kushangaza za viumbe. Kwa wazi, haingeweza kutokea bila mwongozo na udhibiti wa mtu fulani mwenye akili!

Gazeti Newsweek la Novemba 9, 1998, lilitaja kifupi mambo yanayotokezwa na ugunduzi huo kuhusu uumbaji wa ulimwengu. Lilisema kwamba mambo ya hakika “yalidokeza kwamba mata na mwendo zilitokea kama vile tu [kitabu cha] Mwanzo [katika Biblia] kinavyodokeza, pasipo kitu, katika mlipuko mkubwa ajabu wa nuru na nishati.” Ebu ona sababu ambazo Newsweek lilitoa kwa kulinganisha mwanzo wa ulimwengu na ufafanuzi wa Biblia wa tukio hilo.

“Kani zilizoachiliwa zilikuwa—na bado zingali—zimesawazika kwa njia ya kustaajabisha (kimwujiza?): Kama ule Mlipuko Mkubwa ungalikuwa mdogo tu kuliko ulivyokuwa, ulimwengu ungepanuka polepole zaidi kuliko unavyopanuka, na upesi (kwa milioni chache za miaka, au dakika chache—upesi) ungekuwa umeporomoka. Ikiwa ule mlipuko ungalikuwa wenye nguvu kidogo kuliko ulivyokuwa, ulimwengu ungalitawanyika na kuwa umajimaji ambao haungeweza kutokeza nyota. Uwezekano wa kwamba ulimwengu ulianza wenyewe ni kidogo mno kiasi ambacho hata hatuwezi kuwazia. Uwiano wa mata na nishati kwa kulinganisha na ukubwa wa anga wakati wa Mlipuko Mkubwa ni lazima uwe ulikuwa sahihi kufikia sehemu moja kwa kuodrilioni moja [1 ikifuatwa na sifuri 15] ya asilimia 1.”

Gazeti Newsweek lilipendekeza kwamba ni kama kulikuwa na “Mpimaji’ wa ulimwengu, likisema: “Punguza kwa sehemu moja tu (ona juu, sehemu moja kwa kuodrilioni moja ya asilimia 1), . . . na matokeo hayawi tu mvurugo bali kutotenda kabisa kwa mata na nishati na kuwapo kwa barafu. Basi, ni nini—au nani?—aliye Mpimaji huyo mkuu?”

Mtaalamu wa fizikia ya anga Alan Lightman alikiri kwamba wanasayansi “wanashangaa kwamba ulimwengu uliumbwa kwa utaratibu wa hali ya juu sana.” Yeye aliongezea kusema kwamba “nadharia yoyote ile ya kweli kuhusu ulimwengu ni lazima ieleze ni kwa nini mata na nishati hazijaacha kutenda”—kwa nini ulimwengu haujavurugika.

Kwa Nini Wengine Hawataki Kuamini

Je, wewe ungekubali kwamba “utaratibu wa hali ya juu sana” wadokeza kwamba kuna Mratibu? Watu wengi hukubali. Lakini watu ambao wanadai kwamba hawaamini kama kuna Mungu wanapinga. Kwa nini? Eti kwa sababu ya imani! Kama Profesa Ferris alivyoandika, “kwa kusema kweli, kutoamini kama kuna Mungu ni itikadi tu nyingine.” Na ni afadhali, yeye akadai, “kutomhusisha Mungu kabisa kwenye suala la ulimwengu.”

Hivyo ndivyo watu wengi wanavyofanya—lakini kwa ugumu sana. Kwa mfano, baada ya George Greenstein, ambaye ni profesa wa elimu ya nyota, kuona vitu ambavyo angeweza kuvifikiria kuwa uthibitisho wa uumbaji wa ulimwengu, aliandika: “Nikasadiki kwamba ‘nasibu’ hizo hazingetokea peke yake.” Hata hivyo, Greenstein asisitiza: “Si Mungu aliyezitokeza.” Basi, wanasayansi fulani hukataa kusababu kuzuri ili wahifadhi itikadi walizoshikilia tangu zamani.

Lakini, “imani” ya mwanafizikia mashuhuri Fred Hoyle kwa kweli ilitikiswa baadaye maishani mwake. Katika miaka ya 1980, yeye alikiri hivi: “Kwa kutumia akili, mambo ya hakika yaonyesha kwamba mtu mwenye akili sana ameongoza fizikia, na vilevile kemia na biolojia, na kwamba hakuna kani zisizoongozwa katika mambo ya asili. Tarakimu zinazohusu mambo hayo ya hakika zaonekana kuwa kubwa sana hivi kwamba hakuna shaka yoyote kufikia uamuzi wa kwamba kuna mtu mwenye akili zaidi.”

Kwa kupendeza, wakati uchunguzi wa kisasa wa sayansi ulipokuwa ukianza tu, Sir Isaac Newton, alifikia uamuzi kama huo. Yeye alisukumwa kuandika hivi baada ya kufanya ugunduzi wake: “Mfumo huu maridadi kabisa wa jua, sayari na nyota-mikia, ungeweza kutokezwa tu na kusudi na udhibiti wa Mtu mwenye akili na mwenye nguvu nyingi sana.”

Ebu fikiria mojawapo ya matokeo ya ugunduzi wa kanuni za mwendo uliofanywa na Newton na Johannes Kepler.

Jinsi Vyombo vya Angani Viwezavyo Kusafiri

Kepler alifafanua kanuni za mwendo wa sayari mapema katika miaka ya 1600, na The World Book Encyclopedia kilisema kwamba kanuni hizo “hutumiwa kujua mzunguko wa setilaiti zilizowekwa na wanadamu angani na kupanga njia ambazo vyombo vya angani vitafuata.” Mwaka wa 1687, Newton alichapisha kanuni zake mashuhuri za mwendo, na kanuni hizo, “kama ile ya Kepler ndizo msingi wa kupangia safari za angani,” kikasema kitabu hicho. Kwa nini iwe hivyo?

Kwa sababu kwa kutumia kanuni hizo, wanadamu wanaweza kupiga hesabu na kujua gimba fulani la angani litakuwa wapi wakati fulani. Hesabu kama hizo zinawezekana kwa sababu ya miendo ya daima na isiyokosea ya magimba ya angani, kutia ndani mwezi na dunia. Kwa mfano, mwezi huzunguka dunia kwenye mzingo wake kwa wastani wa kilometa 3,700 kwa saa, ukimaliza mwendo huo kwa muda unaopungua kidogo tu mwezi mmoja bila kukosea hata kidogo. Dunia huzunguka jua kila mwaka kwa mwendo wa kilometa 107,200  kwa saa, bila kuchelewa hata kidogo.

Basi, wanapoongoza safari za kwenda kwenye mwezi, wanadamu duniani hulenga vyombo vya angani vielekee maelfu ya kilometa mbele ya mwezi unaozunguka. Kwa kufanya hesabu mbalimbali wao wanajua mahali barabara ambapo mwezi utakuwa wakati fulani. Na chombo hicho kikiongozwa vizuri na kutiwa nguvu, kitafika hapo pia, na hivyo basi kiweze kutua kwenye mwezi.

Ni nini kinachofanya iwezekane kujua miendo ya magimba ya angani? Mwanaanga wa kwanza wa Marekani kuzunguka dunia, John Glenn, alipaza sauti akisema hivi kuhusu utaratibu ulioko kwenye ulimwengu: “Je, huu ungetukia tu wenyewe? . . . Siwezi kuamini.” Kisha akaongezea kusema: “Uwezo fulani uliweka vitu hivi vyote vizunguke na unavidumisha huko.”

Mwanasayansi wa anga Dakt. Wernher von Braun, akishangazwa na kanuni zinazoongoza ulimwengu, alisema: “Vyombo vya angani vyenye watu . . . vimetuonyesha kidogo tu ukubwa wa kustaajabisha wa anga. Mtazamo huo mdogo tu wa mafumbo makubwa ya ulimwengu wathibitisha tu itikadi yetu kwa muumba wake.”

Mwanafizikia mashuhuri P. A. M. Dirac, aliyekuwa profesa wa hisabati kwenye Chuo Kikuu cha Cambridge, alisema: “Labda mtu angeweza kusimulia hali hiyo kwa kusema kwamba Mungu ndiye mhisabati mwenye utaratibu ulio bora sana, Naye alitumia hisabati za juu sana katika kuumba ulimwengu mzima.”

Ni nani huyo Mtaalamu wa Hisabati, ambaye ana Akili Nyingi Sana, na ambaye amesababisha maajabu ya uumbaji?

Ulimwengu Uliumbwa na Nani?

Tukisafiri mahali ambapo hatupajui kisha tupate nyumba nzuri sana yenye nyasi zilizokatwa vizuri na bustani zenye kupendeza hatuwezi kusema nyumba hiyo ilitokea yenyewe tu. Huo ni uamuzi usiopatana na akili kabisa. Ni lazima mjenzi stadi na mtunza-bustani stadi waliifanyia kazi.

Vivyo hivyo, ulimwengu wetu mtukufu, ambao ni tata zaidi, kwa wazi uliumbwa na Muumba. Katika Biblia, yeye yuatambulisha jina lake akisema: “Mimi ni BWANA [“Yehova,” NW]; ndilo jina langu.” (Isaya 42:8) Watu wanaothamini kazi za Mungu wamerekodiwa katika Biblia wakisema: “Wewe wastahili, Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako na vikaumbwa.”—Ufunuo 4:11.

Mbali na kufunulia wanadamu jina lake binafsi alilojipa mwenyewe, kupitia Neno lake lililoandikwa, Yehova vilevile amefunua kusudi lake la kutayarisha dunia ili ikaliwe na watu. Na Yesu Kristo, Mwana mwenyewe wa Mungu, alithibitisha kwamba Neno la Mungu laweza kutegemewa aliposema: “Neno lako ni kweli.”—Yohana 17:17.

Muda usio mrefu uliopita gazeti moja la kisayansi lilisema hivi: “Tofauti na vizazi vyote vilivyotangulia, twajua jinsi tulivyopata kuwapo. Lakini, kama ilivyo na vizazi vyote vilivyotangulia, bado hatujui ni kwa nini tupo.” Lakini, swali hilo, Kwa nini?, lina jibu—Neno la Mungu laandaa jibu hilo. Tafadhali chunguza jibu hilo katika makala ifuatayo.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Wakati wa mlipuko wa bomu la atomu huko Hiroshima, mata kidogo tu iliachilia nishati nyingi ajabu

[Hisani]

Hiroshima Peace and Culture Foundation from material returned by the United States Armed Forces Institute of Pathology

USAF photo

[Picha katika ukurasa wa 7]

Nishati iligeuka ikawa makundi ya nyota yenye utaratibu na yenye kustaajabisha sana

[Hisani]

Courtesy of Anglo-Australian Observatory, photograph by David Malin

[Picha katika ukurasa wa 9]

Ni kanuni zipi zinazofanya iwezekane kutua kwenye mwezi?

[Picha katika ukurasa wa 9]

“Uwezo fulani uliweka vitu hivi vyote vizunguke na unavidumisha huko.” —John Glenn

[Hisani]

[Picha katika ukurasa wa 9]

NASA photo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki