Ulimwengu Wote Mzima Wenye Kutisha
‘Kitu Fulani Kinakosekana’—Kipi?
BAADA ya kuangaza macho kwenye nyota wakati wa usiku uliotakata, wenye giza, twarudi ndani ya nyumba, tukihisi baridi na macho yakiwa yanapepesa-pepesa, akili zetu zikitatanishwa na umaridadi mwingi na maswali chungu nzima. Kwa nini ulimwengu wote mzima upo? Huo ulitoka wapi? Huo waelekea wapi? Haya ndiyo maswali ambayo wengi hujaribu kujibu.
Baada ya miaka mitano ya kufanya utafiti katika taaluma ya anga, ambayo ilimchukua kwenye makongamano ya kisayansi na vituo vya utafiti tufeni pote, mwandikaji wa sayansi Dennis Overbye alifafanua mazungumzo yake pamoja na mwanafizikia maarufu sana ulimwenguni Stephen Hawking hivi: “Hatimaye kile nilichotaka kujua kutoka kwa Hawking ni kile ambacho sikuzote nilitaka kujua kutoka kwa Hawking: Mahali ambapo sisi huenda tunapokufa.”
Ingawa maneno hayo ni ya kukejeli, maneno haya hufunua mengi kuhusu enzi yetu. Maswali hayawi mengi sana kuhusu nyota zenyewe na nadharia na maoni yenye kupingana ya wanaanga ambao huzichungua. Watu leo bado wana tamaa ya kupata majibu ya maswali ya msingi ambayo yamesumbua wanadamu kwa mileani nyingi: Kwa nini tuko hapa? Je, kuna Mungu? Sisi huenda wapi tunapokufa? Majibu ya maswali haya yako wapi? Je, yatapatikana katika nyota?
Mwandikaji mwingine wa sayansi, John Boslough, alionelea kwamba kwa kuwa watu wameacha dini, wanasayansi kama wanaanga wamekuja kuwa “makuhani kamili wa enzi ya kilimwengu. Wanasayansi, na si viongozi wa kidini, ndio ambao wangefunua siri zote za ulimwengu wote mzima hatua kwa hatua, si kwa mfanyizo wa ghafula wa kiroho bali katika aina ya milinganyo iliyofichika kwa wote isipokuwa kwa wateule.” Lakini je, watafunua siri zote za ulimwengu wote mzima na kujibu maswali yote ambayo yamesumbua wanadamu kwa enzi nyingi?
Wanaanga wanafunua nini sasa? Wengi huunga mkono ile fasiri ya “theolojia” ya mshindo mkubwa, ambayo imekuwa dini ya kilimwengu ya wakati wetu, hata wanapobishana daima juu ya vijambo. “Hata hivyo,” Boslough akaonelea, “katika muktadha wa uchunguzi mpya na wenye kujipinga, nadharia ya mshindo mkubwa inaanza kuonekana kwa ubayana zaidi kuwa yafanana sana na ufafanuzi sahili ambao inatafuta kupatanisha maelezo ya uumbaji. Kufikia mapema katika miaka ya 1990 nadharia ya mshindo mkubwa ilikuwa . . . ikiendelea kushindwa kujibu mengi ya maswali ya msingi.” Yeye aliongezea kwamba “wananadharia wengi wametoa hoja kwamba hiyo haitaweza hata kudumu hadi mwishoni mwa miaka ya 1990.”
Labda baadhi ya makisio ya sasa ya kianga yatakuja kuwa sahihi, labda sivyo—kama vile labda kuna sayari hasa zinazoibuka katika kilimia cha Orioni nebula, labda sivyo. Ukweli usiobishaniwa ni kwamba hakuna yeyote katika dunia hii kwa hakika anajua. Lakini kuna nadharia nyingi zinatokezwa, lakini watazamaji wenye unyoofu warudia ule uchunguzi wenye saburi wa Margaret Geller kwamba licha ya mazungumzo ya kijuu-juu, kitu fulani cha kimsingi chaonekana kinakosekana katika uelewevu wa sasa wa wanaanga.
Wakosekana—Ule Utayari wa Kukubali Mambo ya Hakika
Wanasayansi wengi—na hawa watia ndani wanaanga wengi—hupendelea nadharia ya mageuzi. Wao huona vigumu kukubali mazungumzo yanayoupa fungu weledi na kusudi katika uumbaji, nao hunyarafika Mungu atajwapo kuwa Muumba. Wao hukataa hata kutafakari uzushi kama huo. Zaburi 10:4 husema kwa kukashifu kuhusu mtu mwenye kujitutumua ambaye ‘hatafuti, jumla ya mawazo yake ni, hakuna Mungu.’ Mungu wake aliyejiumbia ni Nasibu. Lakini ujuzi unapoongezeka na nasibu na pia sadfa kuporomoka kwa uthibitisho wenye kuongezeka, wanasayansi huanza kugeukia zaidi na zaidi miiko yao kama weledi na usanii. Ebu fikiria vielelezo vifuatavyo:
“Kijenzi fulani kwa wazi kimekuwa kikikosa katika machunguo ya kianga. Chimbuko la Ulimwengu Wote Mzima, kama vile suluhisho la kyubu ya Rubik, chahitaji weledi fulani,” akaandika mwastrofizikia Fred Hoyle katika kitabu chake The Intelligent Universe, ukurasa 189.
“Kadiri ninavyochungua ulimwengu wote mzima na kuchunguza vijambo vidogo-vidogo vya ufundi wao, ndivyo ninavyopata uthibitisho zaidi kwamba ulimwengu wote mzima kwa njia fulani lazima ulijua kuhusu kuja kuwapo kwetu.”—Disturbing the Universe, kilichoandikwa na Freeman Dyson, ukurasa 250.
“Ni sehemu zipi za Ulimwengu Wote Mzima zilizokuwa muhimu katika kutokea kwa viumbe kama sisi, na je, ilikuwa ni kupitia sadfa, au kupitia sababu isiyojulikana, kwamba Ulimwengu Wote Mzima wetu una sehemu hizi? . . . Je, kuna mipangilio fulani ya kina zaidi ambayo huhakikisha kwamba Ulimwengu Wote Mzima uliumbwa kwa ajili ya jamii ya kibinadamu?”—Cosmic Coincidences, kilichoandikwa na John Gribbin na Martin Rees, kurasa 14, 4.
Fred Hoyle pia aeleza juu ya tabia hizi kwenye ukurasa 220 wa kitabu chake kilichonukuliwa hapo juu: “Tabia hizo zaonekana kuingiliana na ulimwengu wa asili kama mfanyizo wa aksidenti zenye kufurahisha. Lakini kuna nyingi ya hizi sadfa zinazohusu maisha zenye kuhitaji maelezo fulani ili kuzifafanua.”
“Si kwamba tu mwanadamu amebadilishwa ili kufaa ulimwengu wote mzima. Ulimwengu mzima umebadilishwa ili kufaa mwanadamu. Ebu wazia ulimwengu wote mzima ambao katika huo moja au nyingineyo ya vima visivyobadilika vya msingi vya fizikia vyabadilishwa kwa asilimia ndogo kwa njia moja au nyingine? Mwanadamu hangeweza kamwe kuishi ndani ya ulimwengu wote mzima kama huo. Hicho ndicho kiini hasa cha kanuni ya mahusiano ya kuishi kwa binadamu. Kulingana na kanuni hii, kisababishi chenye kupatia uhai ni chimbuko la utaratibu mzima na usanii wa ulimwengu.”—The Anthropic Cosmological Principle, kilichoandikwa na John Barrow na Frank Tipler, ukurasa 7.
Mungu, Usanii, na Vima Visivyobadilika vya Fizikia
Ni vipi baadhi ya vima hivi visivyobadilika vya msingi vya fizikia ambavyo ni vya lazima ili uhai uwepo katika ulimwengu wote mzima? Ripoti fulani katika The Orange County Register la Januari 8, 1995, iliorodhesha vichache vya vima hivi visivyobadilika. Hiyo ilikazia jinsi sehemu hizi lazima ziwe zina upatano kabisa, ikitaarifu hivi: “Vile viwango vya kikiasi vya vima vingi vya kimaumbile visivyobadilika vinavyoainisha ulimwengu wote mzima—kwa kielelezo, badiliko la elektroni, au udumifu wa kasimwelekeo ya nuru, au uwiano wa nyezo za kani za msingi katika asili—kwa kushangaza vyapatana mno, nyingine kwa desimali 120. Ukuaji wa ulimwengu wote mzima wenye kutegemeza uhai kwa kuzidi umekuwa mnyetivu kwa vima hivyo mahususi. Badiliko lolote dogo—kuondoa sehemu moja ya bilioni ya sekunde hapa, kuongeza sehemu moja ya bilioni kumi ya meta moja pale—na ulimwengu wote mzima utakuwa mfu na mnyaufu.”
Mwandikaji wa ripoti hii kisha alitaja kile ambacho kwa ukawaida huwa hakitajwi: “Yaonekana ni kusababu kunakofaa zaidi kudhania kwamba mwelekeo fulani usiojulikana watenda katika ukuaji wa ulimwengu wote mzima, labda katika utendaji wa uwezo fulani wenye weledi na ambao uliupatanisha ulimwengu wote mzima kwa kutayarisha kuwasili kwetu.”
George Greenstein, profesa wa astronomia na taaluma ya anga, alitoa orodha ndefu zaidi ya vima hivi visivyobadilika vya kimaumbile katika kitabu chake The Symbiotic Universe. Miongoni mwa vilivyoorodheshwa mlikuwa na vima visivyobadilika vinavyopatana sana hivi kwamba ikiwa vingekuwa na kasoro ndogo sana, hakungekuwa na atomu, hakungekuwa na nyota, hakungekuwa na ulimwengu wote mzima. Vijambo vidogo-vidogo vya mahusiano haya vimeorodheshwa katika sanduku lililoambatanishwa. Ni lazima viwepo kwa ajili ya kuwezesha uhai wa kimaumbile. Vijambo hivyo ni tata na huenda visieleweke kwa wasomaji wote, lakini vyatambulika, pamoja na vinginevyo vingi, kwa wanafizikia wa anga waliozoezwa katika taaluma hizi.
Kadiri orodha hii ilivyoendelea kuwa ndefu, Greenstein alishindwa. Yeye alisema “Lo! Sadfa nyingi mno! Kadiri ninavyosoma zaidi, ndivyo ninavyosadikishwa zaidi ‘sadfa’ kama hizo katu hazingeweza kutokea kwa nasibu. Lakini kadiri usadikisho huu ulivyokua, ndivyo jambo fulani jingine lilivyokua pia. Hata sasa ni vigumu kueleza ‘jambo hili fulani’ kwa maneno. Hilo lilikuwa kutamauka kwingi, na nyakati nyingine kulikuwa kwa kiasili. Ningeshtuka kihalisi kwa kukosa utulivu. . . . Je, yawezekana kwamba kwa ghafula, bila ya kunuia, kiaksidenti tumepata ithibati ya kuwapo kwa Kiumbe Kikuu Kuliko Vyote? Je, alikuwa Mungu ambaye alichukua hatua na kwa kufanya uandalizi akapanga ulimwengu wote mzima kwa faida yetu?”
Akiwa ametamaushwa na kutishwa na hilo wazo, Greenstein mara moja alilitupilia mbali wazo hilo, na kushikilia imani ya dini ya kisayansi, na kupiga mbiu hivi: “Si Mungu.” Hii siyo sababu yenye kufaa—hilo wazo lilikuwa chungu sana hivi kwamba hangeweza kulistahimili!
Uhitaji wa Kiasili wa Binadamu
Hakuna lolote la maoni haya ambalo ni la kukashifu kazi ngumu ya unyoofu wa moyo ya wanasayansi, kutia ndani wanaanga. Hasa Mashahidi wa Yehova huthamini uvumbuzi wao mwingi kuhusu uumbaji ambao hufunua uwezo na hekima na upendo wa Mungu wa kweli, Yehova. Warumi 1:20 hutangaza hivi: “Kwa sababu mambo yake yasiyoonekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana, na kufahamika kwa kazi zake; yaani, uweza wake wa milele na Uungu wake; hata wasiwe na udhuru.”
Ule uchunguzi na kazi ngumu ya wanasayansi ni itikio la kiasili la binadamu kwa uhitaji ambao ni wa msingi kwa wanadamu kama vile uhitaji wa chakula, makao, na mavazi. Ni ule uhitaji wa kujua majibu kwa maswali fulani kuhusu wakati ujao na kusudi la uhai. Mungu ‘ameweka umilele katika mioyo ya wanadamu; hata hivyo hawawezi kuvumbua kile ambacho Mungu amefanya tangu mwanzo hadi mwisho.’—Mhubiri 3:11, The Holy Bible—New International Version.
Hii si habari mbaya sana vile. Hiyo humaanisha kwamba wanadamu hawatajua mambo yote kamwe, lakini hawatakosa mambo mapya ya kujifunza: “Niliiona kazi yote ya Mungu, ya kuwa haitafutikani na mwanadamu kazi inayofanyika chini ya jua; kwa sababu mwanadamu na akijisumbua kadiri awezavyo kuitafuta, hata hivyo hataiona; naam, zaidi ya hayo, mwenye hekima ajapodhania ya kuwa ataijua, lakini yeye hataweza kuiona.”—Mhubiri 8:17.
Wanasayansi wengine hupinga kwamba kumfanya Mungu kuwa “suluhisho” kwa tatizo fulani humaliza ile ari ya kufanya utafiti wa ziada. Hata hivyo, mtu ambaye hutambua Mungu kuwa Muumba wa mbingu na dunia ana vijambo vingi zaidi vidogo-vidogo vyenye kuvutia vya kuvumbua na mafumbo yenye kuvutia ambayo aweza kupekua. Ni kana kwamba ana idhini rasmi ya kuendelea na safari yenye kufurahisha ya kuvumbua na kujifunza!
Ni nani anayeweza kukinza mwaliko wa Isaya 40:26? “Inueni macho yenu juu, mkaone.” Tumeinua macho yetu juu katika kurasa hizi chache, na kile tumeona ni ‘kitu fulani kimekosa’ ambacho kiliwaponyoka wanaanga. Pia tumepata majibu ya msingi ya maswali hayo yenye kujirudia ambayo yamesumbua akili ya mwanadamu katika enzi zote.
Majibu Yapatikana Katika Kitabu Fulani
Sikuzote majibu yamekuwapo, lakini kama vile wanadini wa siku ya Yesu, watu wengi wamefunga macho yao, wameziba masikio yao, na kufanya mioyo yao kuwa migumu kwa majibu ambayo hayakupatana na nadharia zao za kibinadamu au mtindo-maisha wao waliouchagua. (Mathayo 13:14, 15) Yehova ametueleza ulimwengu wote mzima ulikotoka, na jinsi dunia ilitokea, na wale ambao wataishi juu yake. Yeye ametuambia kwamba wakazi wa kibinadamu wa dunia ni lazima wailime na kutunza kwa upendo mimea na wanyama wanaoishiriki pamoja nao. Yeye pia ametueleza kile kinachotukia watu wanapokufa, kwamba wanaweza kuishi tena, na kile wapaswacho kufanya ili kuishi kwenye dunia milele.
Ikiwa unapendezwa kupata majibu yakitolewa kwa lugha ya Neno la Mungu lililopuliziwa, Biblia, tafadhali soma maandiko yafuatayo: Mwanzo 1:1, 26-28; 2:15; Mithali 12:10; Mathayo 10:29; Isaya 11:6-9; 45:18; Mwanzo 3:19; Zaburi 146:4; Mhubiri 9:5; Matendo 24:15; Yohana 5:28, 29; 17:3; Zaburi 37:10, 11; Ufunuo 21:3-5.
Kwa nini usisome maandiko haya pamoja na familia yako au pamoja na jirani au pamoja na kikundi cha marafiki katika nyumba yako jioni moja? Uwe na uhakika yatatokeza mazungumzo yenye kuarifu na kupendeza!
Je, unasisimuliwa na mafumbo ya ulimwengu wote mzima na kuchochewa moyoni na umaridadi wao? Kwa nini usijifunze ili umjue vizuri zaidi Mmoja aliyeuumba? Mbingu ambazo haziwezi kusema hazina upendezi wowote katika udadisi na mshangao wetu, lakini Yehova Mungu, Muumba wazo, pia ni Muumba wetu, naye hujali wenye upole ambao wanapendezwa kujifunza kumhusu na uumbaji wake. Mwaliko sasa unatolewa duniani pote: “Njoo! Naye asikiaye na aseme, Njoo! Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.”—Ufunuo 22:17.
Huu ni mwaliko wenye kuchangamsha moyo kama nini kutoka kwa Yehova! Badala ya kutokea kwa mlipuko usio wa kiakili, wenye kukosa kusudi, ulimwengu wote mzima uliumbwa na Mungu mwenye weledi usio na mwisho na kusudi halisi ambaye alikufikiria wewe tangu mwanzoni. Akiba zake za nishati zisizo na mipaka zimedhibitiwa kwa umakini na sikuzote zapatikana ili kutegemeza watumishi wake. (Isaya 40:28-31) Kwa kumjua thawabu yako itakuwa bila mipaka kama ulimwengu wote mzima wenyewe, ambao ni wenye madaha!
“Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, na anga laitangaza kazi ya mikono yake.”—Zaburi 19:1.
[Sanduku katika ukurasa wa13]
Orodha ya Baadhi ya Vima Visivyobadilika Ambavyo Ni vya Lazima kwa Kuwapo kwa Uhai
Nishati za elektroni na protoni ni lazima zilingane na ziwe kinyume; nutroni ni lazima ipite uzani wa protoni kwa asilimia ndogo sana; ulingano lazima uwepo kati ya halijoto ya jua na ufyonzaji wa klorofili kabla ya usanidimwanga kuweza kutukia; ikiwa kani yenye nguvu ingekuwa dhaifu kidogo, jua halingeweza kutokeza nishati kupitia kwa utendanaji wa nyukilia, lakini ingalikuwa yenye nguvu zaidi kidogo tu, fueli inayohitajiwa ili kutokeza nishati ingekosa usawaziko sana; bila udukiziwimbi aina mbili uliotengwa baina ya kiini katika vitovu vya nyota kubwa mno nyekundu, hakuna elementi yoyote isipokuwa heli ambayo ingeweza kufanyizwa; nafasi ingekuwa imepungua mipanuko mitatu, na miunganishio ya mtiririko wa damu na mfumo wa neva haingekuwapo; na ikiwa nafasi ingezidi mipanuko mitatu, sayari hazingeweza kuzunguka jua kwa usawaziko.—The Symbiotic Universe, kurasa 256-257.
[Sanduku katika ukurasa wa14]
Je, Kuna Yeyote Aliyepata Kuona Uzito Wangu Unaokosekana?
Galaksi ya Andromeda, kama vile galaksi zote za mviringo, huzunguka kwa madaha angani kana kwamba ni tufani kubwa mno. Waastronomia wanaweza kuhesabu kima cha kuzunguka cha magalaksi mengi kutokana na spektra ya nuru, na wafanyapo hivyo, wao huvumbua kitu fulani chenye kutatanisha. Vima vya kuzunguka huonekana kutowezekana! Galaksi zote za mviringo huonekana kuzunguka kwa kasi mno. Hizo hutenda kana kwamba nyota zinazoonekana za galaksi zimefunganywa katika mvururo-nuru mkubwa zaidi wa mata nyeusi, isiyoonekana kwa darubiniupeo. “Hatujui mifanyizo ya hiyo mata nyeusi,” akakiri mwastronomia James Kaler. Wanasayansi wa anga hukadiria kwamba asilimia 90 ya uzito huo unaokosekana haujulikani ulipo. Wao wana hamu sana ya kuupata, ama katika mfanyizo wa neutrino kubwa ama aina ya mata isiyojulikana lakini iliyo nyingi mno.
Ukiuona uzito unaokosekana, mjulishe mara moja mwanaanga wa mahali penu!