Jitihada Zake Zilibarikiwa
Yehova Mungu huwabariki wale wanaojitahidi wenyewe katika utumishi wake wajapokuwa na magumu kama vile afya mbaya. Mwanamke mmoja katika Barbados anaandika hivi:
“Asubuhi moja ya Jumapili wakati nilipokuwa sina uchangamfu sana na nikawa nimeshuka moyo kidogo, bado nilijitahidi kushiriki katika utumishi wa nyumba kwa nyumba. Watu wengi ambao nilitembelea asubuhi hiyo walionyesha [kutopendezwa]. Hilo likanifanya nijisikie kushuka moyo zaidi. Hata hivyo, niliamua kwamba ningetembelea [nyumba] nyingine moja kabla ya kuondoka. Ziara hiyo ya mwisho ilipata kuwa nzuri kuliko vile nilivyotazamia, kwa kuwa baadaye nilipata kujua kwamba mwanamke niliyetembelea alikuwa akijisikia kama vile mimi nilivyokuwa nikijisikia. Yeye alikuwa ndipo tu ametoka hospitalini naye alisema kwamba alikuwa akifanya kazi zake za nyumbani lakini ‘akilia na kuomba kwamba Mungu amtumie mtu wa kumfariji.’”
Shahidi huyo aliweza kumpa mwanamke huyo ujumbe wenye kufariji wa ahadi ya Mungu ya taratibu mpya ya mambo isiyo na magonjwa, kilio na hata kifo. (Ufu. 21:4) Jambo hilo likaongoza kwenye funzo la kawaida la Biblia. Baada ya juma tatu tu, mwanamke huyo akawa akihudhuria mikutano ya Kikristo. Upesi akaanza kushiriki “habari njema” pamoja na wengine.
“Nina furaha kuripoti kwamba sasa mwanamke huyo ni dada yangu wa kiroho,” anaandika Shahidi huyo. “Alibatizwa katika ‘Tumaini Lenye Uzima’ Kusanyiko la Wilaya. Namshukuru sana Yehova kwamba roho yake, na pengine malaika, walinisaidia nistahimili asubuhi ya Jumapili hiyo yajapokuwa maono yangu ya mwilini, kwa kuwa si kwamba tu mtu huyo mwenye kupendezwa alifaidika bali [pia] jambo hilo nililoliona limekuwa chanzo cha uthibitisho kwangu wa maneno ya mtume Paulo, ‘niwapo dhaifu ndipo nilipo na nguvu.’” 1 Kor. 12:10.