Wakati Shauri la Mungu Linapokosa Kufuatwa
Shahidi mmoja mwanamke kijana akiwa mwenye umri wa miaka 20 na kitu anaeleza juu ya matokeo ya kukosa kwake kufuata shauri la Mungu. Anaandika hivi:
“Nilifanya kosa baya sana miaka kadha iliyopita. Nilifanya uasherati na mwanamume mmoja kijana asiyebatizwa ambaye alikuwa akijifunza Biblia wakati huo. Nilikuwa nimebatizwa. Nilikuwa nataka anipende. Mahali pake, sote wawili tulivunja sheria ya Yehova. . . .
“Sasa maisha yangu ni mfululizo wa kusema ‘afadhali ningefanya ivi na hivi.’ Kama ningekuwa kijana mwenye kumpenda Yehova ningekuwa na nguvu zaidi. Afadhali ningekaza fikira zaidi kwenye matakwa ya Mungu. Afadhali ningefikiria uzito wa matendo yangu nilipofanya kosa. Sasa nalazimika kuvuna niliyopanda. . . . Usiku mwingi nisiolala usingizi, vipindi vya kumwaga machozi ya kukata tamaa ni sehemu ya bei ninayolazimika kulipa kwa ajili ya kukosa kumtii Yehova. . . .
“Afadhali vijana wangekubali kwamba wazee na Yehova wanawapenda nao hawataki kuona wakiumia. Matakwa ya Mungu ni ya kutuletea furaha tu. Mara tu unapofanya kosa hakuna kurudi nyuma ulifute. Sikuzote lazima tuendelee kumtumaini Yehova na kuazimia kushikamana na kanuni zake za haki na upendo. Furaha yetu tukiwa vijana inahusika. Sikuzote lazima tufikirie wakati ujao; uhusiano wetu pamoja na Yehova. Ili kufanya hivyo lazima tuchague miendo yetu kwa hekima sasa, kulingana na kanuni za Kimaandiko. Ni somo ambalo nimejifunza, kwa kusikitisha, kwa njia ya taabu. Natumaini wengine wataepuka kutenda kosa lo lote, wakimtumaini Yehova.
“Nampenda Yehova kweli kweli. Inanisikitisha kwamba nilikosa kumtii. Walakini nimeazimia kukazana kusonga mbele, kufanya kazi kwa bidii, kusitawisha uhusiano wenye nguvu na wenye kuendelea pamoja na Yehova. Natazamia sana wakati ambapo zawadi ambayo Yehova atawapa raia zake washikamanifu, taratibu mpya yenye kujaa uadilifu, itakapopatikana na kufurahiwa na wote. Ndipo tu nitakaposahau uchungu wa moyoni na maumivu ambayo yameletwa na dhambi yangu.”