Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 3/1 kur. 107-112
  • Vijana Wanataka Nini Maishani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Vijana Wanataka Nini Maishani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUIPATA FURAHA AMBAYO VIJANA WANATAKA
  • MAONI YA KIASI JUU YA MICHEZO
  • MAONI YA KIASI JUU YA PESA NA NGONO
  • KUPATA YALIYO BORA MAISHANI
  • Michezo na Tafrija
    Kupata Faida Zote za Ujana Wako
  • Je! Ni Busara Kutofanya Ngono Kabla ya Kufunga Ndoa?
    Kupata Faida Zote za Ujana Wako
  • Kuweka Michezo Mahali Payo Panapofaa
    Amkeni!—1992
  • Vijana—Mnafuatia Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 3/1 kur. 107-112

Vijana Wanataka Nini Maishani?

“Zikimbie tamaa za ujanani; ukafuate haki, na imani, na upendo, na amani.”​—2 Tim. 2:22.

1-3. (a) Vijana wanasema wanataka nini hasa maishani? (b) Ni kusudi gani zuri zaidi ambalo mtu aweza kuwa nalo, na Biblia yaonyeshaje hivyo? (c) Kwa sababu gani si vibaya kutaka kuwa mwenye furaha?

VIJANA, MWATAKA nini maishani? Vijana wengi waliulizwa ulizo hilo karibuni. Nasi tuangaliapo sana majibu yao, twadhani twajua vile ambavyo wewe ungalijibu ulizo hilo.

2 Kwa ufupi, vijana wanasema kwamba wanataka furaha na raha. Kijana mmoja wa miaka minane alisema hivi: “Mimi nataka kuwa mwenye furaha. Tena nataka starehe​—mavazi mazuri, nyumba nzuri, muziki mzuri na chakula kizuri, na kujiona kwamba ninafanya kajambo kenye maana.” Ingawa vijana wengi walitaka pia vitu hivyo, wao walisema walitaka kumtumikia Mungu wao Yehova, na kupata uzima wa milele katika taratibu yake mpya ya mambo, kwa sababu ya kuzoezwa Kikristo. (1 Yohana 2:17; 2 Pet. 3:13) Kwa kweli, huwezi kuwa na kusudi zuri kuliko hilo, kwa sababu thawabu ambazo Mungu atawapa watumishi wake waaminifu zinapita sana kitu cho chote unachoweza kujipatia maishani.​—Zab. 37:4; 145:16.

3 Kwa hiyo, si vibaya kwa vijana kutaka furaha, na kutaka kujifurahisha. Biblia yamtaja Yehova kama “Mungu mwenye furaha,” na kwa hiyo yeye ataka watu wake wawe wenye furaha pia. (1 Tim. 1:11, NW) Kwa hiyo, lisiwe jambo la kushangaza kwamba Neno la Mungu linataja vijana kama wakipata raha kutokana na utendaji wanaofanya. Kwa mfano, wakati Biblia inaposimulia watu wa Mungu waliobarikiwa, inasema hivi: “Na hizo njia za mji zitajaa wavulana, na wasichana, wakicheza katika njia zake.” Vilevile, inasema kwamba kuna “wakati wa kucheza dansi.”​—Zek. 8:5; Mhu. 3:4, New English Bible.

KUIPATA FURAHA AMBAYO VIJANA WANATAKA

4. (a) Vijana wengi wanataka kazi za namna gani? (b) Kwa sababu gani vijana Wakristo wanajua kwa ujumla kwamba kutafuta kazi hizo kunaleta matatizo?

4 Vijana wengi leo wanafurahia michezo sana, na wanaamini kwamba wakijitafutia kazi ya kila siku inayohusu michezo watafurahi kweli kweli. Kijana Mkristo wa miaka kumi na minne alisema hivi: “Mimi napendezwa sana na michezo, hasa mchezo wa mpira uitwao basketball. Nataka kumtumikia Yehova, lakini natamani pia siku moja kuwa mcheza mpira huo katika timu mashuhuri.” Bila shaka maelfu ya vijana wa Kikristo wana tamaa izo hizo. Au, pengine wanaona kwamba mradi wao wa kupata furaha unaweza kutimizwa wakijitafutia kazi nyingine, kama kupiga muziki au kufanya machezo ya sinema. Kutokana na mambo ambayo wamejifunza katika Neno la Mungu, wanajua kwamba yawapasa watake kumtumikia Yehova, na kusaidia wengine wapate uzima, katika taratibu mpya Yake. Lakini vijana wengi wanaona kwamba mambo hayo ni ndoto tu kwao.

5, 6. (a) Ni mambo gani mengine ambayo vijana wanasema wanataka maishani? (b) Ni nini kimefanya vijana watake mambo hayo?

5 Kukusanya pesa nyingi sana ni kwa maana kwa watu wengi leo. Kwa hiyo tusishangae kujua kwamba vijana wengi walisema mradi wao maishani ni kuwa matajiri. Vilevile, vijana wamezungukwa na mambo mengi yanayoamsha nyege zao. Ukweli ni kwamba, sikuzote imekuwa kawaida ya vijana kupendezwa na wenzao, wa kiume au wa kike. Hivyo jibu la msichana mmoja Mkristo wa mji wa New York linafahamika: Alisema, “Jambo kubwa ambalo ningependa maishani ni kuolewa.” Vijana wengi Wakristo wanasema wanataka kuoa au kuolewa wakati fulani na kuwa na maisha mazuri ya jamaa.

6 Lakini maoni ya vijana wa ulimwengu yako tofauti sana na hayo. Kwa mfano, mvulana wa miaka kumi na tisa alisema hivi: “Mimi nataka wanawake wengi.” Naye msichana wa miaka kumi na saba aliitikia hivi: “Mimi nataka kuishi kwa raha nisisumbukie lo lote. Na lo lote ni kutia na ugonjwa unaosababishwa na maisha ya uzembe. Labda hili halipendezi wengine, lakini huu ndio wakati wanapopaswa kukua. Ndoa inakugandamiza. Mimi nataka niishi kidogo.”

7, 8. (a) Kwa sababu gani bila shaka ni vibaya kufanya uasherati? (b) Ni katika njia zipi vijana wengi wanahitaji msaada?

7 Naam, vijana wengi wanaona kwamba mapesa mengi na kufanya ngono na wenzi wengi ndiko kutakakowafurahisha zaidi maishani. Lakini, ni wazi kwamba kuna kasoro katika kuwaza kwao. Ebu angalia ni matatizo makubwa namna gani yametokana na uasherati​—kuenea sana kwa magonjwa ya kisonono na kaswende, kuwako kwa mamilioni ya watoto wa haramu na kutoa mimba, maumivu ya kichwa na kuvurugika akilini. Si ajabu kwamba katika United States kujiua kumekuwa sababu kubwa ya pili ya mauti miongoni mwa vijana, na miaka ya karibuni kumepanda kufikia 250 kwa mia!

8 Ni wazi kwamba vijana wengi wanaume na wanawake wanahitaji uongozi na usimamizi bora. Wanahitaji kusaidiwa wakuze maoni yatakayowatayarisha wapate furaha na uradhi wa kudumu maishani. Wanahitaji kuelekezwa kwa Muumba wao, Yehova Mungu, ili watambue kwamba Yeye yuko kweli. (Ebr. 11:6) Wanahitaji kuona hekima na kufaa kwa sheria zake, jinsi ambavyo zinawafaidi ‘wakizikimbia tamaa za ujanani’ ili waweze kuwa na manufaa kwa Mungu. (2 Tim. 2:20-22) Wanahitaji kujifunza kwamba kusudi lake ni kuharibu taratibu hii potovu na kuibadilisha na taratibu mpya atakayoifanya mwenyewe. Wanahitaji kusaidiwa waishi kwa ajili ya taratibu mpya hiyo, waishi sasa kwa njia ambayo wanaweza kuhakikisha wanastahili kuishi milele. Hilo ndilo jambo litakalowaletea furaha kweli kweli.​—Mit. 3:13-18.

MAONI YA KIASI JUU YA MICHEZO

9-12. (a) 1 Timotheo 4:7, 8 inatusaidiaje tuwe na maoni ya kiasi juu ya michezo? (b) Ni faida gani zinazopatikana katika michezo, lakini kuna hatari gani za kujitia michezoni kupita kiasi? (c) Kwa sababu gani utawa na kumtumikia Mungu kwapaswa kuwa kwa maana zaidi katika maisha zetu? (Zab. 36:9; Ebr. 6:10; Yak. 1:12)

9 Neno la Mungu linaweza kusaidia vijana wawe na maoni ya kiasi juu ya michezo. Kwa mfano, linatoa shauri jema hili: “Kujizoeza kupata nguvu za mwili kwafaa kidogo, lakini utauwa hufaa kwa mambo yote; yaani, unayo ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye.” (1 Tim. 4:7, 8) Kwa hiyo Biblia yaonyesha kwamba “kujizoeza kupata nguvu za mwili,” kama katika michezo, kunafaa. Kunaweza kutusaidia kusawazisha mwili, kuufanya uwe wenye kukunjika vyepesi, kwaweza kujenga misuli yetu na kutupa nguvu. Lakini angalia onyo linalotolewa, “kujizoeza kupata nguvu za mwili kwafaa kidogo.” Inaweza kuwaje ukipuza shauri hilo la Biblia na kujishughulisha sana na michezo?

10 Kwanza, ukilipuza unaweza kujitia sana michezoni, badala ya kuifanya kama tafrija. Alipokuwa akionyesha matokeo ya kushughulika kupita kiasi na michezo ya kushindana, mchunguzi wa akili mwenye kushughulika na michezo, Bruce Ogilvie, alisema hivi: “Wakati mmoja nilihoji wachezaji wasio na ujuzi katika kambi 10 kubwa za mchezo wa baseball na 87 kati ya mia walisema kama wangalijua wasingalicheza mchezo huo kwa sababu walidhani ungewafurahisha lakini haikuwa hivyo.” Vilevile, michezo mingine, kama mpira wa miguu, inaweza kuwa hatari, hasa wakati mwili wako unapoendelea kukua. Jambo ambalo limefanya michezo fulani iwe hatari sana ni kushindana kupita kiasi, na mara nyingi watu hutiwa moyo wawe na nia hiyo ya kujitahidi wasishindwe hata iweje.

11 Jambo jingine unalopaswa kufikiria pia ni mashirika utakayokuwa nayo michezoni. Kwa mfano, wakati wachezaji wanapoingia katika chumba cha kuvalia au kuvulia mavazi yao kabla au baada ya michezo, mazungumzo yanayoendeshwa humo huwa ya uasherati mara nyingi. Kuna faida gani kujiingiza katika jambo linaloweza kukuharibia kwa vyepesi kanuni zako za adili na uhusiano wako na Muumba wako? Wakati kijana mmoja anayejipatia mshahara kwa kucheza mpira wa miguu katika kikoa kiitwacho Oakland Raiders cha U.S.A. alipoanza kuthamini mafundisho ya Neno la Mungu, aliamua kuacha kazi hiyo ya mpira yenye pesa nyingi. Wajumbe wa kikoa hicho walimtembelea wajaribu kubadili nia yake. Yeye alisema, “Niliwaambia matokeo ya kushirikiana nao yalikuwa nini​—kutumia dawa za kulevya, kuishi maisha mapotovu, kuwa na nia ya kiburi na majivuno. Niliwaeleza kwamba maisha hayo yote yaliyohusu kujipatia mshahara kwa kucheza mpira wa miguu yangeniharibia maisha ya Kikristo ambayo sasa nilitaka kuishi.”

12 Kwa hiyo michezo ni kama mambo mengine yanayokuwa mazuri yakifanywa kiasi​—yasipotawala maisha yako kiasi cha kufunika mambo yaliyo ya maana zaidi, au yasipokutia katika hali zenye madhara. Unaweza kusisimuka sana unapocheza mchezo wa haraka na mwili unapoonyesha ufundi wake. Lakini michezo peke yake haileti furaha yenye kudumu. Haitoi “ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye,” kama utawa. Naam, ukifanya kumtumikia Baba yako wa mbinguni, Yehova Mungu, kuwe ndilo jambo la maana zaidi maishani mwako, utapata furaha na uradhi wa kweli​—milele.

MAONI YA KIASI JUU YA PESA NA NGONO

13, 14. (a) Kwa sababu gani, kulingana na 1 Timotheo 6:9, 10, Luka 12:16-21 na Mhubiri 5:10, si hekima kuwa na kusudi la kujikusanyia mali nyingi za kimwili? (b) Kulingana na 1 Timotheo 6:11, 12, yatupasa kufuatia nini, na kwa sababu gani?

13 Mahali pengi leo mtu anahitaji pesa ndipo aweze kula, kununua mavazi, kuwa na nyumba. Kwa hiyo ni lazima tujitahidi kuchuma pesa. Hata hivyo si hekima kukusudia kukusanya mali tu maishani. Kufanya hivyo hakuleti furaha. Neno la Mungu linasema kweli: “Hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu. Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi.”​—1 Tim. 6:9, 10.

14 Magonjwa, wasiwasi, kukosa usingizi siku nyingi na kuharibika kwa maisha ya jamaa ni kati ya matatizo yanayopata watu wengi ambao kusudi lao maishani ni kujikusanyia mapesa mengi sana. Hata, mtu awezapo kujikusanyia utajiri mwingi sana, kwa kawaida inaonekana kwamba kufanya hivyo hakumletei furaha. (Mhu; 5:10) Kwa hiyo onyesha kwamba una hekima. Uwe na maoni ya kiasi juu ya pesa maoni ya kimungu. Utii onyo la upole la Biblia: “Uyakimbie mambo hayo; ukafuate haki, utauwa, imani, upendo, saburi, upole. Piga vita vile vizuri vya imani; shika uzima ule wa milele.”​—1 Tim. 6:11, 12, 17-19; 2 Tim. 2:22.

15, 16. (a) Biblia inaelezaje wazi mambo ya ngono? (b) Kwa sababu gani Biblia imeleta faida kwa kuzungumza mambo ya ngono waziwazi hivyo?

15 Bila shaka, ili mtu apate uzima wa milele, yampasa awe na maoni ya kiasi na ya kimungu juu ya ngono pia, si pesa peke yake. Biblia yazungumza waziwazi habari ya ngono, bila kuficha. Ukweli ni kwamba, Biblia ni kitabu kinachozungumza habari za watu hasa, nayo ngono ni sehemu kubwa ya maisha ya watu. Kwa hiyo Neno la Mungu linaeleza furaha inayotokana na ndoa yenye kuheshimika. (Mwa. 26:8; Mit. 5:15-20; 1 Kor. 7:1-5) Lakini inaeleza pia matumizi mabaya ya ngono. Kwa mfano, fikiria yaliyomo katika kitabu cha Biblia cha Mwanzo. Kinaeleza vile wanaume wa Sodoma walivyowakia wanaume wenzao tamaa, vile Lutu alivyolala na binti zake akiwa mlevi, vile Dina, binti ya Yakobo, alivyoingiliwa kwa nguvu, vile Yuda alivyofanya ngono na mke wa mwana wake akidhani ni malaya, na vile mke wa Potifa alivyojaribu kumshawishi Yusufu wafanye ngono.​—Mwa. 19:4, 5, 30-38; 34:1, 2; 38:12-26; 39:7-16.

16 Watu wengine wamelaumu Biblia kwa sababu inaeleza maisha yalivyo hasa, kwa sababu inaeleza wazi ubaya ambao watu walifanya. Hata hivyo Biblia haielezi hivyo kwa kusudi la kuamsha nyege za watu, wala kuwatia moyo wafanye mabaya. Bali, kwa kawaida inaonyesha matokeo mabaya ya kufuata mwendo mbaya. Vilevile, masimulizi hayo yameandikwa ili tuweze kujifunza masomo yenye maana. Kwa mfano, fikiria yaliyotukia nyumbani kwa Mfalme Daudi.

17, 18. (a) Twajifunza nini kutokana na yaliyotukia kati ya Amnoni na Tamari, kama yanavyoelezwa katika 2 Samweli 13:1-33? (b) Vijana wa kisasa wamepatwa na matokeo gani yanayofanana na hayo kwa sababu ya uasherati?

17 Mwana mkubwa zaidi wa Daudi, Amnoni, alizidi kumtamani Tamari, dada mzazi mmoja naye, aliyekuwa mrembo. Alijigonjweza, akatumia ujanja hata Tamari akawa ndiye mwenye kumletea chakula wakati ambao hakukuwa na mtu mwingine karibu. Ndipo “akamkamata, akamwambia, Njoo ulale nami, ndugu yangu.” Tamari alipinga sana, lakini Amnoni akakataa kumsikiliza akamlazimisha Tamari alale naye. Je! Amnoni alipata alichokuwa akitamani? Habari inasimulia matokeo: “Amnoni akamchukia machukio makuu sana; . . . machukio aliyomchukia yakawa makuu kuliko yale mapenzi aliyokuwa amempenda kwanza. Amnoni akamwambia, Ondoka nenda zako.”​—2 Sam. 13:1-33.

18 Ni wazi kwamba, Amnoni hakupata raha wala dada mzazi mmoja naye hakuipata wakati Amnoni alipotosheleza nyege zake za zinaa ya maharimu. Ndivyo inavyokuwa mara nyingi watu wanapofanya uasherati. Gazeti Journal of the American Medical Association lilimripoti kijana mmoja aliyefanya uasherati na wasichana wengi wapotevu akiungama hivi: “Nimejua kwamba hiyo haikuniletea furaha.” Vilevile, kijana mwingine aliyekuwa katika shule ya wavulana na wasichana alieleza yafuatayo kuhusu uasherati aliofanya, huku machozi yakimtoka: “Hakika haukufaa​—hakukuwa na raha wakati huo, nimekuwa na wasiwasi tangu wakati huo.”

19. (a) Kwa sababu gani kufuata adili ya mambo ya ngono kunafaa? (b) Ni nini kinachoweza kukusaidia ujiepushe na uasherati, kama inavyoonyeshwa na maandiko kama Waefeso 5:3-5 na Wafilipi 4:8?

19 Tunakuwa wenye hekima sana tutiipo amri ya Biblia: “Ukimbieni uasherati”! Kwa kweli, “zikimbie tamaa za ujanani,” zinazoweza kukufanya uwe na matata maishani. (1 Kor. 6:18, NW; 2 Tim. 2:22) Kufuata adili ya ngono kunafaa kwa sababu wanaofanya hivyo wataelekea zaidi kufanikiwa katika ndoa. Kwa upande mwingine, ule uitwao “uhuru” wa kufanya ngono hufanya ngono yenyewe iwe ovyo na ya kuchukiza, badala ya kuifanya iwe yenye raha na safi. Kwa hiyo ili ujiepushe na uasherati, jiepushe na mambo yanayoelekeza huko: mazungumzo ambayo saa zote yanahusu wavulana au wasichana, vilevile kusoma vitabu au kutazama picha zinazoamsha nyege. Elekeza akili yako, macho yako na ulimi wako kwenye mambo yaliyo safi, mambo yanayofaa, ujitahidi kufikia miradi inayofaa na yenye kuleta faida za kudumu.​—Efe. 5:3-5; Flp. 4:8.

KUPATA YALIYO BORA MAISHANI

20, 21. Unaonyeshaje wazi kile unachotaka kweli kweli maishani?

20 Kwa hiyo, WATAKA nini maishani? Huenda ukajisikia kwamba wataka kumpendeza Yehova na kujitayarisha kuishi katika taratibu mpya yake, kama vijana wengi Mashahidi walioulizwa ulizo hilo. Hilo ni kusudi jema, nalo ni jema kuliko makusudi mengine yote! Inafaa sana kuwa na kusudi hilo. Lakini ulizo ni hili bado: “Mambo unayofanya yanapatana na unayosema?”

21 Huenda mtu akasema kwamba ataka kuwa mganga hodari maishani. Lakini namna gani ikiwa mtu huyo hajitahidi sana shuleni, au namna gani ikiwa hasomi mambo yanayoweza kumjulisha jinsi mwili wa kibinadamu ulivyo na unavyofanya kazi? Pengine ungetia shaka kama mtu huyo kweli ataka kuwa mganga. Vivyo hivyo, wewe unajibu ulizo, “Wataka nini maishani?”, kwa jinsi unavyoishi. Hiyo inakumbusha mtu ule usemi usemao, ‘Vitendo vina nguvu zaidi kuliko maneno.’ Huenda mtu akasema ataka kumpendeza Yehova Mungu na kupata uzima wa milele, lakini mtu huyo asipojitahidi kumsikiliza Mungu kwa kujifunza au kulitii Neno Lake, ni wazi kwamba amepungukiwa.

22. (a) Unaweza kufanya nini ujisaidie kutia nguvu tamaa yako kumtumikia Yehova? (b) Unawezaje kuwa “chombo cha kupata heshima,” kama inavyoeleza 2 Timotheo 2:20-22?

22 Unaweza kufanya nini ukiona kwamba wewe ni mmoja wa wanaosema wanataka kumtumikia Yehova Mungu, lakini hujitahidi upaswavyo umtumikie? Hatua moja uwezayo kuchukua ni hii: Kisome kitabu kipya kilichochapwa na Watchtower Bible and Tract Society, Your Youth​—Getting the Best out of It. Jitahidi kweli kweli uanze kutumia mashauri ya Maandiko yaliyomo, yanayofaa. Vilevile, ikiwezekana, mwombe baba au mama yako ajifunze kitabu hicho nawe. Kufanya hivyo kutakuweka katika njia ya kupata upendeleo wa Yehova. Kutakusaidia ‘uzikimbie tamaa za ujanani,’ na kuwa “chombo” kimfaacho Mungu.​—2 Tim. 2:20-22.

23, 24. (a) Njia ya kupata yaliyo bora ni nini, kama inavyoonyeshwa katika Mithali 4:20-23? (b) Ijapokuwa wako maadui wanaotupinga, kwa sababu gani twaweza kuwa na hakika kwamba twaweza kupata yaliyo bora maishani sasa na milele?

23 Yampasa kila mmoja wetu ajue kwamba njia ya kupata yaliyo bora maishani ni kumtegemea Baba yetu wa mbinguni, Yehova Mungu. Hata wazazi wako wawe walikupa mwanzo mzuri au mbaya namna gani, hata uwe na akili na mwili mzuri namna gani, siku zote itakupasa kufahamu kwamba unahitaji uongozi wa Yehova. Yeye aliongoza maneno yafuatayo yaandikwe kwa ajili ya vijana kama wewe mwenyewe: “Sikiliza maneno yangu; tega sikio lako, uzisikie kauli zangu. Zisiondoke machoni pako; uzihifadhi ndani ya moyo wako. Maana ni uhai kwa wale wazipatao, na afya ya mwili wao wote. Linda moyo wako kuliko yote uyalindayo; maana ndiko zitokako chemchemi za uzima.”​—Mit. 4:20-23.

24 Naam, kadiri ambavyo unazidi kumtegemea Yehova Mungu na Neno lake upate uongozi, ndivyo njia ya uzima itakavyozidi kuwa laini kwako. Ni kweli kwamba mambo hayatakuwa rahisi maadamu tumo katika ulimwengu huu, na maadamu mungu wake yuko, Shetani Ibilisi, anayejaribu kutuondoa kwa Yehova. (1 Kor. 4:4; Efe. 6:12; 1 Pet. 5:8, 9) Lakini simama imara! Uwe na hakika! Ukishikilia uamuzi wako wa kumtumikia Yehova Mungu, yeye na majeshi yake yote ya mbinguni watakusaidia. Watakusaidia upate yaliyo bora katika ujana wako sasa, na uzima wa milele katika taratibu mpya yenye haki ya Mungu ambayo inakaribia sana.​—Zab. 34:7.

​—Kutoka The Watchtower, Oct. 15, 1976.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki