Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g92 7/8 kur. 14-16
  • Kuweka Michezo Mahali Payo Panapofaa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuweka Michezo Mahali Payo Panapofaa
  • Amkeni!—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Namna Gani Mashindano?
  • Mwelekeo kwa Wanariadha
  • Jinsi Michezo Ilivyo na Faida
  • Je, Nijiunge na Michezo ya Timu?
    Amkeni!—1996
  • Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Michezo?
    Vijana Huuliza
  • Ujitoaji Kimungu Una Faida Kuliko Mazoezi ya Kimwili
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2019
  • Je, Mashindano Katika Michezo Ni Kosa?
    Amkeni!—1995
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1992
g92 7/8 kur. 14-16

Kuweka Michezo Mahali Payo Panapofaa

WATU wanapocheza michezo wanayopendelea zaidi, wanahisi wakiwa wenye furaha wakati miili yao inapoitikia na kufanya mambo ya ustadi au ya uvumilivu. Mungu alituumba tuonee shangwe utendaji wa kimwili. Labda watu wengi hata zaidi hufurahia kuwatazama wengine wakicheza. Kwa hivyo michezo huwa kama mambo mengi yaliyo mazuri inapowekwa mahali payo panapofaa.

Ili kutoa kielezi: Watu wanapoenda kwenye ufuo wa bahari kufurahia jua, hutukia nini wakikaa sana kwa jua? Wanapata mchomo wa jua wenye maumivu ambao huharibu wakati huo mzuri na hata waweza kuwa hatari sana. Ndivyo ilivyo na michezo. Ikifanywa kwa kiasi ni mizuri, lakini ikipita kiasi yaweza kudhuru.

Michezo yaweza kuwa kiburudisho kizuri chenye kuchangamsha, lakini haipasi kuwa ndio mambo yote. Huwa haileti uradhi wa kweli au furaha ya kudumu. Kwa kusikitisha nyakati nyingine huwa lazima kuwe majuto ili mtu ang’amue hilo. “Tuzo na medali zangu zote si kitu,” akaeleza Mary Wazeter, mwanariadha wa kike aliyeruka kutoka kwa daraja na kupooza.

“Nimejifunza mambo mengi hakika kuhusu maisha,” mwanamke huyo akaripoti. “Jambo moja ni kwamba uradhi wa kweli haupatikani kwa njia ambazo watu wengi hujitahidi kufikia ukamilifu na utimizo. Uradhi wangu haukutokana na kuwa mwanafunzi hodari sana, mkimbiaji wa mashindano wa kitaifa wala kwa kuwa mwenye umbo la kuvutia.”

Akiyaweka mambo kwa njia ya mkato zaidi, msosholojia John Whitworth alisema: “Mchezo unapokwisha, kile unachobakia nacho ni orodha tu ya tarakimu. Mambo yote huonekana yakiwa bila msingi wowote. Hata hivyo, nafikiri hilo lafaa katika jamii yetu.” Umaana usiofaa ambao huambatanishwa na michezo leo hufanya mambo mengine yote yakose umaana wayo.

Baada ya Henry Carr kushinda katika mbio fupi za meta 200 katika Olimpiki ya 1964, yeye alieleza: “Nilipokuwa nikirudi kwa gari kuelekea kwenye Vijiji vya Olimpiki, nikaitazama medali yangu ya dhahabu kwa makini zaidi kwa mara ya kwanza. . . . Nikajiuliza: ‘Yaani nimekuwa nikijitahidi kwa miaka hii yote ili tu nipate hii?’ Nilighadhabika, badala ya kuwa mwenye furaha. Nilishuka moyo sana.” Baada ya Marlon Starling kushinda katika shindano la uzani wa welter (kilo 61-66.6) la Shirika la Ngumi Ulimwenguni katika 1987, yeye alihisi vivyo hivyo. “Ubingwa huo,” yeye akasema, “haulingani na mtoto wangu kusema, ‘Ninakupenda baba.’”

Kwa hiyo mtu aweza kujifunza somo la maana: Kazi yenye matokeo, familia, na hasa ibada kwa Mungu yapasa kutangulizwa ifaavyo. Biblia ni sahihi inaposema: “Kujizoeza kupata nguvu za mwili [ambako michezo huandaa] kwafaa kidogo.” (1 Timotheo 4:8) Hilo laonyesha mahali panapofaa pa michezo katika maisha zetu. Papasa pawe mahali pa pili. Kwa sababu michezo yaweza kuvutia sana, mtu apaswa awe mwangalifu kwamba mambo yaliyo ya maana zaidi hayapuuzwi.

Kwa hiyo, kwa hekima, uwe mwepesi wa kuitikia ikiwa washiriki wa familia wanalalamika kwamba unatumia wakati mwingi zaidi kuzungumzia, kutazama, au kucheza michezo. Mwanamke mmoja ambaye mume wake alifanya marekebisho katika maelekezo yake ya fikira kwa michezo, alisema hivi kwa kushukuru: “Yeye sasa hutumia wakati mwingi zaidi pamoja na watoto na mimi. Nyakati nyingine familia yetu hutazama mchezo kwenye televisheni, lakini jioni nyingi sisi hutembea pamoja na kuzungumza juu ya matukio ya siku hiyo. Hilo ni jambo zuri na hutusaidia tuendelee kuwa wenye furaha.”

Kwa kufikiria matatizo yanayoweza kutokea, mbona usikabili swali hili kwa unyofu: Je! yawezekana kuwa ninatumia wakati mwingi zaidi na mwelekezo wa fikira katika michezo kuliko ninavyopaswa? Bado, kuna pande nyingi katika jambo hili la kuweka michezo katika mahali payo panapofaa.

Namna Gani Mashindano?

Ili michezo iwe yenye faida badala ya kuwa yenye kuumiza, mtazamo ufaao kuelekea mashindano ni wa maana. “Makocha, walimu wa mazoezi ya viungo vya mwili, wazazi, na vijana wenyewe wamekazania sana kushinda hivi kwamba wanasahau kile kinachomaanishwa na michezo [kwa vijana],” akalalamika tabibu mmoja wa timu ya magongo. Yeye alisema kwamba, kusudi la michezo lapasa kuwa “kukuza ushirikiano na nidhamu, kuwa na afya njema, na, la maana zaidi ya yote, kufurahia.”

Hata hivyo, kwa kusikitisha, mkazo uliotiliwa ili kushinda umeharibu furaha ya wengi. Msaikolojia wa michezo Bruce Ogilvie alisema: “Wakati mmoja niliwahoji wachezaji wapya wasio na ujuzi katika kambi 10 kubwa za mashindano ya besiboli na asilimia 87 kati yao walisema kwamba ni afadhali kama hawangecheza katika Mashindano Madogo ya besiboli kwani yaliondoa shangwe ya mchezo ambao ulikuwa wenye kufurahisha.” Tatizo linalohusiana na hilo ni kwamba mashindano ya kupita kiasi hutokeza hesabu kubwa ya majeraha.

Biblia hutoa miongozo, ikisema: “Acheni sisi tusiwe wenye ubinafsi, kuchochea shindano la mmoja na mwingine, kuhasidi mmoja na mwingine.” (Wagalatia 5:26, NW) Kulingana na kamusi ya Kigiriki-Kiingereza, neno la Kigiriki hapa linalofasiriwa “kuchochea shindano” humaanisha “kuamsha,” “kutoa ushindani ili kupigana vita au kupambana na mwingine.” Hivyo An American Translation inaifasiri: “Tusishindane na wengine katika ubatili wetu.” Na kielezi-chini katika New World Translation chatoa elezo la ziada: “Kuongozana kwenye vita vya kukata maneno.”

Basi, ni wazi kwamba kuchochea ushindani si jambo la hekima. Hakufanyizi uhusiano mzuri. Ukilazimishwa ushindane kisha ushindwe, na mshindi ajisifu kwa kukushinda, ono hilo laweza kukuaibisha sana. Mwelekeo wa mashindano yenye bidii si wa upendo. (Mathayo 22:39) Kwa wakati ule ule, ikiwa mashindano yanafanywa kwa njia ya kirafiki, na kwa ukunjufu, inaweza kufanya mchezo upendeze na uchangamshe.

Huenda wengine wakatafuta njia za kucheza michezo kwa njia itakayoondoa mashindano. “Mimi huamini sana michezo kwa ajili yayo yenyewe hadi kufikia umri wa 13 au 14,” kocha mmoja wa soka Mwingereza akasema. Yeye alipendekeza kutoweka rekodi za matokeo ya timu mbalimbali wala kadiri wanavyofanya kwenye ligi—“hakuna kupanda, hakuna fainali.” Ndiyo, mkazo unaotiwa sana wa kushinda wapasa kupunguzwa ifaavyo au uondolewe kabisa.

Mwelekeo kwa Wanariadha

Kuweka michezo mahali payo panapofaa kwatia ndani mwelekeo wetu kwa wanariadha wanaojulikana sana, wenye ujuzi mwingi. Inaeleweka kwamba huenda tukavutiwa na uwezo wao wa riadha na matendo yao ya ajabu. Lakini je! wanapaswa kupewa heshima kuu? Vijana mara nyingi huweka picha za wanariadha kama hao vyumbani mwao. Kwa kweli je! mambo yaliyotimizwa na watu hao yanawafanya wastahili kupewa heshima? Haipasi kuwa hivyo.

Hapo mbeleni mchezaji mpya katika timu ya mashindano ya Ligi Kuu ya Kitaifa ya Soka alistahi wengi wa wachezaji wenzake. Lakini yeye alisema kwamba mwenendo na mwelekeo wao, “uliondolea mbali kabisa hisi zote na heshima niliyokuwa nayo kuwaelekea.” Yeye alieleza: “Kwa mfano, wao wangesema: ‘Ah, niliwapata wasichana watano wiki jana, bila kuhesabu mke wangu.’ Na ningemtazama mtu huyo na kufikiri: ‘Yaani huyu ndiye yule niliyeheshimu sana.’”

Kwa kweli, haifai kumpa binadamu yeyote heshima kuu, na hasa hilo lingekuwa hivyo kwa wale wanaofanya vema katika utendaji ambao Biblia husema una faida kidogo au wa kadiri tu. Watumishi wa Mungu wanahimizwa ‘Waikimbie ibada ya sanamu.’—1 Wakorintho 10:14.

Jinsi Michezo Ilivyo na Faida

Kama tulivyoona, Biblia husema kwamba mazoezi ya kimwili, kama yale yafanywayo katika michezo, ‘yafaa kidogo.’ (1 Timotheo 4:8) Hilo lawezekana katika njia zipi? Wewe waweza kufaidikaje kutokana na michezo?

Galen, daktari Mgiriki wa karne ya pili, ambaye alikuwa daktari wa kibinafsi wa mmaliki wa Roma Marcus Aurelius, alikazia umaana wa mazoezi kwa afya ya kawaida. Naye alipendekeza michezo ya mpira, kwa sababu hiyo huzoeza mwili mzima kwa njia ya kiasili. Michezo ya mpira hufurahisha kwa kawaida, kwa hiyo mtu ataelekea kucheza michezo hiyo ambayo yeye hufurahia kuliko aina nyingine ya mazoezi.

Wengi huona kwamba mazoezi yapatikanayo kwa michezo huwapa hisi ya afya njema. Baada ya mazoezi au mchezo wenye kusisimua, wao huhisi wamepata nguvu mpya na kuburudishwa. Na hilo halipasi kuwa jambo la kushangaza, kwani, kama vile Dakt. Dorothy Harris anavyosema, “mazoezi ndio dawa ya asili iliyo bora zaidi.”

Mazoezi ya mwili, kama yale yanayoandaliwa na mazoezi ya viungo vya mwili ya kutia nguvu na uzuri, kukimbia polepole, na michezo, kwa kawaida yanatambuliwa leo kuwa ya maana kwa afya njema. “Watu wenye afya njema hufanya kazi zao za kawaida kwa wepesi bila kuchoka na bado wanakuwa na nishati kwa mapendezi mengine,” chasema The World Book Encyclopedia. “Wao pia wanaweza kukinza vizuri zaidi matokeo ya kuzeeka kuliko wale wasio na afya njema.”

Hata hivyo, bila kujali jinsi michezo inavyoweza kumfanya mtu awe mwenye afya njema, faida hiyo ni ya kadiri tu. Kuzeeka na kufa hakuwezi kushindwa kwa jitihada za kibinadamu. Na bado, baada ya kusema kwamba “Kujizoeza kupata nguvu za mwili kwafaa kidogo,” Biblia husema: “Utauwa hufaa kwa mambo yote, yaani, unayo ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye.”—1 Timotheo 4:8.

Ni Yehova Mungu pekee, aliye Muumba wetu, awezaye kutupa uhai. Hivyo, hakuna kitu kilicho cha maana zaidi kuliko “utauwa [ujitoaji kimungu, NW],” yaani, uchaji, ibada, na utumishi kwa Mungu. Kwa hiyo wale wanaozoea utauwa watatanguliza kufanya mapenzi ya Mungu kwanza. Watajitoa wenyewe katika utumishi wa Mungu, wakitumia ujana wao kama vile ambavyo Yesu Kristo alivyofanya, wakiwaambia wengine juu ya mambo mazuri kuhusu Mungu na Ufalme wake.

Naam, kwa kuweka mapenzi ya Mungu kwanza, wanadamu waweza kupata upendeleo wake na kupata uhai milele katika ulimwengu wake mpya wenye haki. Huko Mungu mwenye furaha, Yehova, atawapa furaha na uradhi wa kweli wenye kudumu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki