Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g96 3/22 kur. 21-23
  • Je, Nijiunge na Michezo ya Timu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Nijiunge na Michezo ya Timu?
  • Amkeni!—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Shinda kwa Vyovyote?
  • Kuvunja Maadili
  • Mazoezi ya Kimwili au Maumizo ya Kimwili?
  • Mambo Mengine ya Kufikiriwa
  • Kufanya Uamuzi Wenye Hekima
  • Michezo ya Timu—Je, Yanifaa?
    Amkeni!—1996
  • Kuweka Michezo Mahali Payo Panapofaa
    Amkeni!—1992
  • Wimbi Jipya la Jeuri Kwenye Michezo ya Watoto
    Amkeni!—2002
  • Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Michezo?
    Vijana Huuliza
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1996
g96 3/22 kur. 21-23

Vijana Huuliza . . .

Je, Nijiunge na Michezo ya Timu?

“NI NINI cha pekee sana kuhusu kuwa kwenye timu?” ikauliza makala katika gazeti Seventeen. Ikijibu makala hiyo ilisema: “Unafanya kazi pamoja kuelekea mradi uleule, hivyo unakuwa karibu sana. Pia unajifunza kushughulika na watu, kama vile jinsi ya kutatua matatizo pamoja na kikundi, jinsi ya kunyumbulika na kuwa mwenye ufikirio, na jinsi ya kupatana.”

Hivyo, kucheza michezo iliyopangwa kwaonekana kuwa na manufaa, ni yenye kufurahisha na yenye kuzoeza.a Wengine hata hudai kwamba kucheza michezo ya timu husaidia mtu kukuza utu. Ligi moja ya mpira wa besiboli ya vijana inatumia usemi huu wa shime “Utu, Ushujaa, Uaminifu-Mshikamanifu.”

Tatizo ni kwamba, michezo ya timu haifikii sikuzote makusudio hayo mazuri. Kitabu Kidsports chasema: “Katika visa fulani vijana wanaovutiwa vyepesi hujifunza kuapa, kudanganya, kupigana, kuogopesha, na kuumiza wengine.”

Shinda kwa Vyovyote?

Makala katika Seventeen yakubali hivi: “Kuna upande usiofaa wa michezo, wakati watu wanapokazia sana kushinda.” Hili lapingana moja kwa moja na maneno ya Biblia: “Sisi na tusiwe wenye majisifu, wenye kuchochea shindano juu ya mtu na mwenzake, tukihusudiana.” (Wagalatia 5:26, NW) Ingawa mashindano machache ya kirafiki yaweza kufanya mchezo upendeze na kufurahisha, roho ya kushindana kupita kiasi yaweza kutokeza uadui—na kuondoa ile furaha ya kucheza.

Jon, aliyekuwa mchezaji wa mpira wa miguu katika shule ya sekondari, akumbuka: “Tulikuwa na kocha aliyekuwa shupavu kabisa; sikuzote akitupigia mayowe na makelele . . . Niliogopa sana kwenda kwenye mazoezi. . . . Nilihisi kana kwamba nilikuwa katika kambi ya mateso.” Ingawa si makocha wote wanaowatumia wengine vibaya, wengi wao hutia mkazo mwingi sana katika kushinda. Mwandishi mmoja alifikia mkataa huu: “Wachezaji wengi . . . hufikia wakati ambapo ile furaha ya kushinda inalemewa na mzigo mkubwa usiovumilika wa kutaka kushinda.” Tokeo laweza kuwa nini?

Science News liliripoti juu ya uchunguzi uliofunua kwamba kati ya wachezaji wa mpira wa miguu na mpira wa vikapu katika vyuo, “asilimia 12 iliripoti kuwa na matatizo katika angalau maeneo mawili kati ya matano: mkazo wa kiakili, mkazo wa kimwili, ugumu wa kuepuka madawa au vileo, kutendwa vibaya kimwili na kiakili, na matokeo ya chini sana ya kimasomo.” Juu ya jambo hilohilo, kitabu On the Mark charipoti: “Karibu kila mmoja anayehusishwa katika timu ya michezo hukubali kwamba kuna tatizo kubwa la matumizi mabaya ya madawa kwenye michezo katika viwango vyote.”

Kuvunja Maadili

Ule mkazo wa kushinda waweza pia kumfanya mchezaji mchanga kuvunja viwango vizuri vya usawa na ufuatiaji wa haki. Kitabu Your Child in Sports chaonelea: “Katika ulimwengu wa kisasa wa michezo, kushinda si jambo zuri tu; hilo ndilo jambo linalokubalika. Kushindwa si jambo baya tu, bali halikubaliki.”

Uhalisi mwingine usiopendeza ni: Makocha huwaweka wachezaji wao chini ya mkazo mkubwa wa kuwaumiza wapinzani wao. Makala katika Psychology Today ilisema: “Ili ufaulu katika michezo, lazima uwe katili kabisa. Au hilo ndilo waaminilo wachezaji wengi, makocha na mashabiki wa michezo.” Mchezaji mmoja wa kulipwa wa mpira wa miguu aeleza utu wake wa kila siku kuwa “mwenye sauti pole, mwenye ufikirio na mwenye urafiki.” Lakini kwenye uwanja wa michezo anakuwa mtu aliye tofauti kabisa. Akieleza juu ya utu wake kwenye uwanja, yeye asema: “Wakati huo mimi huwa katili kabisa. . . . Sipendezi wala sina fadhili. Sina staha kamwe kwa yule ninayekusudia kuzaba makonde.” Makocha mara nyingi hutia moyo kuwa na mwelekeo huo.

Biblia huwatia moyo Wakristo: “Jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu.” (Wakolosai 3:12) Je, ungeweza kukuza sifa hizo ikiwa kila siku ungekuwa unapokea vichochezi ili uumize, uponde, na kulemaza wapinzani wako? Robert mwenye umri wa miaka 16 akubali hivi: “Nimecheza michezo iliyopangwa. Hujali ni nani unayeumiza maadamu tu ushinde.” Sasa kwa kuwa yeye ni Mkristo aliyebatizwa, maoni yake yamebadilika. Yeye asema: “Singeweza kamwe kurudia hilo.”

Mazoezi ya Kimwili au Maumizo ya Kimwili?

Zisizopasa kupuuzwa, pia, ni hatari za kimwili. Kwa kweli, michezo huambatana na hatari hata inapochezwa pamoja na marafiki ili kujifurahisha tu. Lakini hatari hizo zinaongezeka sana wakati vijana wanapozoezwa ili wacheze kwa kiwango kinachokaribia kile cha wachezaji wa kulipwa.

Kitabu Your Child in Sports chaonelea: “Wachezaji wa kulipwa wanaweza kuumia. Lakini watu wazima wakomavu walio tayari kuumia ni stadi sana, wakakamavu kimwili, nao hulipwa fedha nyingi kwa kufanya hivyo. Zaidi ya hayo, kwa kawaida wao hupata mazoezi ya aina nzuri zaidi sana, yenye ustadi zaidi sana, vifaa bora zaidi sana, na utunzi wa kitiba wa hali ya juu sana. . . . Watoto wa shule hawana yote hayo.” Wakristo waambiwa ‘waitoe miili yao iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu.’ (Warumi 12:1) Je, haikupasi kufikiri kwa uangalifu kama ni jambo la busara kuutumikisha mwili wako chini ya hatari zisizo za lazima au zisizo za kiakili?

Mambo Mengine ya Kufikiriwa

Hata wakati ambapo hatari za kiafya zionekanapo kuwa ndogo, michezo ya timu bado hupoteza wakati mwingi. Vipindi vya mazoezi havipunguzi tu wakati wa maisha yako ya kustarehe na watu bali pia vyaweza kuchukua sehemu kubwa ya wakati upaswao kuweka kando kwa ajili ya kujifunza na kufanya mgawo wa masomo ya nyumbani. Science News liliripoti kwamba wachezaji kwenye vyuo walielekea kuwa na “maksi za chini zaidi kidogo” kuliko wanafunzi wengine ambao walijihusisha na utendaji mwingine mbalimbali baada ya masomo. Lenye umaana hata zaidi, waweza kuona kwamba kucheza kwenye timu hufanya iwe vigumu kufuatia yale ambayo Biblia huita “mambo yaliyo ya maana zaidi”—mapendezi ya kiroho. (Wafilipi 1:10, NW) Jiulize, ‘Je, kujiunga na timu kutanitaka nikose mikutano ya Kikristo, au kutazuia kushiriki kwangu katika kazi ya kuhubiri?’

Chunguza vizuri, pia, yale matokeo yawezayo kutokana na kutumia saa nyingi sana pamoja na vijana na watu wazima wasio na maoni kama yako kuhusu maadili, uneni msafi, au ushindani. Usisahau, Biblia husema kwamba “mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.” (1 Wakorintho 15:33, NW) Fikiria, kwa kielelezo, makala katika ukurasa wa matukio ya pekee katika The New York Times: “Chumba cha kubadilishia nguo cha wachezaji . . . ni mahali ambamo wanaume huzungumza juu ya miili ya wanawake kwa kutumia maneno yaliyo wazi sana ya kingono, ambamo wao hujivunia ‘kufaulu kufanya ngono’ na kufanya mzaha juu ya wanavyowashinda wanawake.” Wewe ungeendeleaje kiroho ikiwa ungechagua kuwa katika mazingira kama hayo?—Linganisha Yakobo 3:18.

Kufanya Uamuzi Wenye Hekima

Je, umekuwa ukifikiria kujiunga na timu ya michezo? Basi huenda mambo yaliyotangulia yatakusaidia kuhesabu gharama ya kufanya hivyo. Fikiria dhamiri za wengine unapofanya uamuzi wako. (1 Wakorintho 10:24, 29, 32) Bila shaka, hakuna sheria za moja kwa moja ziwezazo kuwekwa, kwa kuwa hali hutofautiana toka sehemu moja ya ulimwengu hadi nyingine. Katika maeneo mengine huenda wanafunzi wakatakwa washiriki katika michezo. Lakini ukiwa na shaka, zungumza na wazazi wako au Mkristo mkomavu.

Vijana wengi Wakristo wamefanya uamuzi mgumu wa kutocheza michezo ya timu. Hilo haliwi rahisi ikiwa wewe ni mkakamavu nawe huifurahia michezo kikweli! Mkazo kutoka kwa walimu, makocha, na wazazi waweza kuongeza fadhaiko. Kijana Jimmy akubali hivi: “Naliona kuwa pigano la kibinafsi kutocheza. Baba yangu asiye mwamini alikuwa mchezaji mashuhuri katika siku zake za shule ya sekondari. Nyakati nyingine inakuwa vigumu sana kwangu kutojiunga na timu fulani.” Hata hivyo, utegemezo wa wazazi waamini na Wakristo wakomavu katika kutaniko waweza kukusaidia sana kushikamana na azimio lako. Asema Jimmy: “Namshukuru mama yangu. Nyakati nyingine nashuka moyo kwa sababu ya kukazwa nicheze. Lakini sikuzote yeye yuko ili kunikumbusha miradi yangu halisi maishani.”

Huenda michezo ya timu yaweza kufundisha wachezaji jinsi ya kushirikiana na kutatua matatizo. Lakini kuna fursa nyingi za kujifunza mambo hayo ndani ya kutaniko la Kikristo. (Linganisha Waefeso 4:16.) Michezo ya timu yaweza pia kufurahisha, lakini si lazima uwe katika timu ili uifurahie. Michezo fulani yaweza kufurahiwa pamoja na marafiki Wakristo katika uwanja nyuma ya nyumba fulani au kwenye bustani ya tafrija. Matembezi ya familia nje yaweza kuandaa fursa zaidi za michezo mizuri. “Ni afadhali zaidi kucheza na wengine kutoka kutaniko lako,” asema Greg mwenye miaka 16. “Ni kwa kusudi la kufurahia tu, nawe unakuwa pamoja na rafiki zako!”

Ni kweli kwamba, kucheza tu na rafiki zako kwenye uwanja wa nyumba huenda kusikupe kamwe ule msisimuko wa kuwa katika timu inayoshinda. Usisahau kamwe, hata hivyo, kwamba hata yawe ya kiwango cha juu namna gani “mazoezi ya kimwili ni yenye manufaa kidogo [tu]; lakini ujitoaji kimungu ni wenye manufaa kwa mambo yote.” (1 Timotheo 4:8, NW) Kuza ujitoaji kimungu, nawe utakuwa mshindi kwelikweli machoni pa Mungu!

[Maelezo ya Chini]

a Ona “Vijana Huuliza . . . Michezo ya Timu—Je, Yanifaa?” katika toleo letu la Februari 22, 1996.

[Blabu katika ukurasa wa 22]

“Tulikuwa na kocha aliyekuwa shupavu kabisa; sikuzote akitupigia mayowe na makelele . . . Niliogopa sana kwenda kwenye mazoezi”

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mara nyingi sana, makocha hutilia mkazo kushinda—hata ikiwa itamaanisha kuwaumiza wengine

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki