Maoni ya Biblia
Je, Mashindano Katika Michezo Ni Kosa?
WANAUME wawili wazee-wazee waketi kwenye bustani katika siku yenye jua, wakicheza mchezo wa dama. Karibu na hapo kuna sauti za watoto wanaopiga kelele na kukimbia huku na huku wakicheza mchezo wa kukimbizana na kugusana. Si mbali sana na hapo, kikundi cha vijana kinafurahia mchezo wa mpira wa vikapu. Ndiyo, kutuzunguka kila siku, wachanga kwa wazee hufurahia michezo. Wanaposhiriki, watu wengi hujaribu kucheza vizuri kadiri wawezavyo. Labda wewe hufanya hivyo pia.
Lakini je, ingeweza kusemwa kwamba namna hizo za mashindano ya kirafiki ni mbaya? Wengi wanatambua onyo la mtume Paulo kwenye Wagalatia 5:26 (NW), ambapo alisema kwamba Wakristo hawapaswi “kuchochea mashindano kati ya mtu na mwenzake.” Kulingana na maoni haya, je, lingekuwa jambo lisilofaa kwa Wakristo kushindana katika michezo ya kitafrija?
Kwa ufupi, la. Kwa nini hivyo? Kabla ya kujibu swali hilo, ebu tutazame kifupi historia ya michezo.
Historia ya Michezo
Kushiriki michezoni kulianza huko nyuma katika nyakati za kale na kumekuwa jambo kuu katika historia yote—kutia ndani historia ya watu wa Mungu. Neno “mpira” hata huonekana katika Biblia. Kwenye Isaya 22:18, linapotaja juu ya Yehova Mungu kukataa watu waovu, linasema hivi: “Atakukunja na kukutupa kama mpira.” Mipira fulani ya kisasa—kama vile mipira ya mchezo wa gofu na besiboli—bado hutengenezwa kwa kukunjwa-kunjwa pamoja kwa vitu. Biblia ya King James hutafsiri mstari huo huo hivi: “Yeye . . . atawarusha juu kama mpira.” Ili ulinganifu huu ufae, lazima iwe mipira ilitumiwa na wale waliokuwa wakiishi wakati huo.
Kwa kuongezea, katika Biblia kuna kisa cha mzee wa ukoo Yakobo akishindana mieleka na malaika. Simulizi hili laonekana likidokeza kimbele ustadi uliozoewa kimbele kwa upande wa Yakobo, kwa kuwa mng’ang’ano huo ulikuwa bila mshindi na ulioendelea kwa muda wa saa nyingi. (Mwanzo 32:24-26) Kwa kupendeza, kulingana na wasomi fulani, simulizi hilo huenda likaonyesha kwamba Yakobo alifahamu sheria za mieleka. Yaelekea Waisraeli walijihusisha na kupiga upinde pia—mchezo mwingine uliohitaji mazoezi na ustadi. (1 Samweli 20:20; Maombolezo 3:12) Kukimbia kulikuwa jitihada nyingine ya riadha ambayo kwayo wanaume wa kale walijizoeza.—2 Samweli 18:23-27; 1 Mambo ya Nyakati 12:8.
Michezo iliyohusisha akili—kama vile kunena vitendawili—kwa wazi ilipendwa na wengi na kuheshimiwa sana. Labda kielelezo kilicho wazi zaidi ni kitendawili alichonena Samsoni kwa Wafilisti.—Waamuzi 14:12-18.
Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, michezo nyakati fulani ilitumiwa kama mifano ya maisha ya Kikristo. Mathalani, kwenye 1 Wakorintho 9:24, 25, Paulo ataja mazoezi yenye bidii na yaliyopangwa ya mkimbiaji na kuyatumia kwa kuonyesha uhitaji wa Mkristo wa kujidhibiti na uvumilivu. Pia, ni wazi kwamba Yehova aliweka hali ya kutaka kucheza katika uumbaji wake mwingi, kwa kuwa mwanadamu pamoja na mnyama hupata wakati wa kucheza mara kwa mara.—Ayubu 40:20; Zekaria 8:5; linganisha Waebrania 12:1.
Wakati Mashindano Yanapopita Kiasi
Ni nini basi, alichokuwa akisema mtume Paulo kwa Wakristo wenzake alipowaambia ‘wasichochee mashindano kati ya mmoja na mwenzake’? (Wagalatia 5:26, NW) Jibu lapatikana katika muktadha. Paulo alitanguliza taarifa hii kwa kuwaambia juu ya “kutojisifu bure” au, kama tafsiri nyingine za Biblia zisemavyo, kutokuwa “wenye kiburi,” “wenye majivuno,” “wenye tamaa ya utukufu usio na faida.” Ufuatiaji wa umashuhuri na utukufu ulienea sana miongoni mwa wanariadha katika siku ya Paulo.
Ndivyo ilivyo leo katika ulimwengu uliojaa utukufu wenye majivuno, wanariadha zaidi na zaidi wanageukia kutembea kwa maringo na kuvuta uangalifu kwao wenyewe na stadi zao. Wengine wanapita kiasi hata kufikia kuaibisha wengine. Kudhihaki, kusuta, na kushusha wengine kwa maneno, au kile ambacho wanariadha wengine hukiita “kukejeli,” kunakuwa jambo la kawaida kwa haraka. Yote haya yangekuwa “kuchochea mashindano,” ikiongoza kwa kile alichorejezea Paulo kwenye sehemu ya kumalizia ya Wagalatia 5:26 kuwa—husuda.
Chini ya hali mbaya mno, mashindano yasiyo na usawaziko huongoza kwenye vita na hata kifo. Fikiria kutano kati ya wanaume wa Sauli na wale wa Daudi huko Gibeoni, wakati ambapo Abneri na Yoabu walikubali ‘vijana hao na waondoke na kucheza mbele yao.’ (2 Samweli 2:14-32, Tanakh) Yaelekea simulizi hili larejezea mashindano ya vikundi ya mieleka. Haidhuru mashindano hayo yalikuwa nini, mara hiyo yaligeuka kuwa pigano kali lenye umwagikaji wa damu.
Maoni Yaliyosawazika
Kwetu sisi na kwa wengine, michezo ya kitafrija yapasa kuwa yenye kuburudisha—si yenye kushusha moyo. Hili laweza kufikiwa kwa kuweka mambo katika maoni sawa, tukikumbuka kwamba kustahili kwetu mbele za Mungu na wanadamu wenzetu hakuhusiani kwa vyovyote na stadi zetu katika michezo.
Ungekuwa upumbavu kuruhusu hisia za kuwa bora kuliko wengine kujaa ndani yetu kwa sababu ya uwezo wa kimwili au kiakili. Kwa hiyo, acheni tuepuke mwelekeo usiofaa wa kilimwengu wa kuvuta uangalifu kwetu wenyewe, tusije tukachochea wivu katika wengine, kwa kuwa upendo haujivuni. (1 Wakorintho 13:4; 1 Petro 2:1) Na ingawa ni jambo la kawaida kutarajia msisimko, idili ya ghafula, na kupongezana miongoni mwa wanatimu, hatutaki hisia hizi zipite kiasi na kuwa maonyesho ya kujigamba.
Hatutapima kamwe kustahili kwa wengine kwa uwezo wao katika michezo. Vivyo hivyo, hatungetaka kujifikiria hatuna maana kwa sababu ya ukosefu wa ustadi. Je, hilo lamaanisha kwamba lingekuwa kosa kufunga bao? Si lazima iwe hivyo. Lakini twapaswa kukumbuka jinsi mchezo wowote usivyo na maana—kustahili kwa kweli kwa watu hakutegemei wanafanya vyema kadiri gani. Katika mchezo wa timu wengine hubadilisha kwa ukawaida mchanganyo wa wachezaji katika kila timu ili timu moja isiwe inashinda sikuzote.
Wakristo wanapaswa kukumbuka pia kwamba ingawa michezo inatajwa katika Biblia, inatajwa mara chache tu. Lingekuwa kosa kufikia mkataa kwamba kutajwa tu kwa michezo katika Biblia kunatoa haki kujiingiza moja kwa moja katika michezo yote. (Linganisha 1 Wakorintho 9:26 na Zaburi 11:5.) Pia, Paulo alionelea kwamba “kujizoeza kupata nguvu za kimwili kwafaa kidogo, lakini utauwa [“ujitoaji kimungu,” NW] hufaa kwa mambo yote.”—1 Timotheo 4:8.
Kwa hiyo ikiwekwa mahali pafaapo, michezo inafurahisha na kuburudisha. Biblia hushtumu, si mashindano yote, bali mashindano yanayochochea ubatili, uadui, pupa, wivu, au jeuri.