Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 6/1 kur. 10-17
  • Vijana, Je! Mwenendo Safi Unaosemwa na Biblia Ndiyo Njia Bora?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Vijana, Je! Mwenendo Safi Unaosemwa na Biblia Ndiyo Njia Bora?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MKAZO UPO!
  • NJIA BORA
  • “WAKIJIKOSEA WENYEWE”
  • WAPE WAZAZI MOYO
  • UONGOZE MWIU KAMA MTUMWA
  • UJENGE UHUSIANO WAKO NA MUNGU
  • Je! Ni Busara Kutofanya Ngono Kabla ya Kufunga Ndoa?
    Kupata Faida Zote za Ujana Wako
  • Ngono Kabla ya Ndoa
    Amkeni!—2013
  • Maoni Yako Juu ya Ngono—Yanafanyiza Tofauti Gani?
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Kuna Ubaya Gani Kufanya Ngono Kabla ya Ndoa?
    Amkeni!—2004
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 6/1 kur. 10-17

Vijana, Je! Mwenendo Safi Unaosemwa na Biblia Ndiyo Njia Bora?

“Mimi ni [Yehova], Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kufuata.”​—Isaya 48:17.

1. Kwa sababu gani ujana ni wakati mzuri maishani, walakini wengine wana nia gani?

“SIKU za ujana wetu ni siku za utukufu wetu,” ndivyo alivyoandika mshairi fulani. Vijana wengi wanakubali, kwa maana huo ni wakati wa msisimuko na wa kuwa huru na madaraka mazito ya mtu mzima. Walakini vijana wengi wanatamani kuchukua furaha zote za vijana na za watu wazima. Nia yao yaweza kutajwa kuwa: ‘Hakuna kungojea; ndiyo, tunataka kila furaha mara moja.’

2. (a) Tarakimu za karibuni zinaonyesha nini juu ya vijana na mwenendo safi? (b) Je! unaona maelekeo hayo yanawapata vijana ndani ya kundi la Kikristo?

2 Wakati wa ‘nguvu za ujana’ mmiminiko mkubwa kwenye kila anasa umefanya vijana wengi washiriki katika ngono kabla ya ndoa, inayoitwa uasherati, kuliko wakati mwingine wo wote katika historia ya kisasa.a Mweneo huo wa ngono za ovyo-ovyo umewapata hata vijana fulani ndani ya kundi la Kikristo. Ukiwa Mkristo huenda ukashangaa hivi, ‘Ni nini kinachofanya liwe jambo gumu kwa kijana kuendelea kuwa safi, sana-sana wakati wa hizi “siku za mwisho”?’​—Mhubiri 11:10, NW; 2 Timotheo 3:1-5.

MKAZO UPO!

3, 4. (a) Kwa sababu gani si rahisi kijana aendelee kuwa na adili safi? (b) Watu wa rika moja na uhitaji wa kufahamika vinatokezaje magumu?

3 Wakati wa utineja, kuna tamaa yenye ‘kukamilika’ kwa nyege. Kipindi hicho kinachoitwa “ukamilifu wa ujana” katika Biblia, mara nyingi kinatokeza uvutano wenye nguvu kwa wavulana na wasichana. Kwa hiyo ni jambo la kawaida ikiwa ukiwa kijana, unasumbuliwa na tamaa za ngono. Hata hivyo, tamaa hiyo ya kawaida inazidishwa na tafrija na matangazo ya “siku hizi kupitia njia za kupashia habari, ambayo yanatukuza ngono.​—1 Wakorintho 7:36, NW.

4 Mkazo kutoka vijana wengine unaweza pia kuwa mwingi sana, kama ambavyo msichana wa shule mmoja mchanga Mkristo anavyoeleza, akisema hivi: “Kwa kweli ni vigumu sana kuwa tofauti siku hizi. Wasichana wengine shuleni waliuliza kama nimekwisha kufanya ngono. Nilipowaambia hapana, wote wakaanza kucheka. Kwa kweli nilisikia kama kwamba nataka kulia na kusema nimekwisha kufanya.” Pamoja na hayo, vijana wanahitaji upendo na kufahamika, na huenda mambo hayo yasitolewe nyumbani. Wanathamini mvulana rafiki au msichana rafiki anayewafanya kuwa “wa pekee” na ambaye anasikiliza kwa huruma. Ukaribu huo wa maono ya ndani unaweza kutokeza kufanya ngono. Vijana wengine wanaduwazwa na mmiminiko huo wa maono hayo yote ya ndani. Huenda wakataka kujua hivi, ‘Je! jambo lenye kupendeza sana hivyo laweza kuwa kosa? Je! kufuata mwenendo safi wa Biblia ndiyo njia bora kweli kweli?’

NJIA BORA

5. (a) Isaya 48:17 inatuambia nini juu ya Mungu? (b) Kulingana na 1 Wathesalonike 4:3-8, mapenzi ya Mungu kwetu ni nini juu ya mwenendo safi?

5 Baba yetu wa kimbinguni aliwakumbusha hivi watu wake wateule: “Mimi ni [Yehova], Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kufuata.” (Isaya 48:17) Hiyo ‘njia itupasayo kufuata’ tukiwa na mwenendo safi ni ipi? “Haya ndiyo mapenzi [au, matakwa] ya Mungu . . . mwepukane na uasherati; kila mmoja wenu ajue kuuweza mwili wake katika utakatifu na heshima; si katika hali ya tamaa mbaya [ya ngono] . . . Maana Mungu hakutuitia uchafu, bali tuwe katika utakaso.”​—1 Wathesalonike 4:3-8.

6. (a) Mtume Paulo aliwaamuru nini Wakristo waliotiwa mafuta kuhusu uasherati, na kwa sababu gani? (b) Kwa sababu gani hilo linapasa kuwafanya vijana waufikirie mwendo wao?

6 Mapenzi ya Mungu kuhusu mwenendo safi yako wazi​—‘mwiweze miili yenu’; epukeni uasherati na uchafu. Ninyi vijana ambao mmeweka wakf maisha zenu kwa Mungu mmefanya umoja wa karibu pamoja naye kwa mwendo huo! Lakini mkifanya ngono kabla ya ndoa ingekuwa sawa na kama mmoja wa “washiriki wa Kristo” ambaye ‘ameunganishwa kwa Bwana’ ‘angeungana [kwa njia ya ngono] na malaya.’ ‘Hilo lisitokee kamwe!’ ndivyo alivyokazia Paulo. Kufanya hivyo kungekuwa ni kutusi sana uhusiano huo wenye thamani. Hakuna dhambi nyingine inayofanana na hiyo kabisa, kwa maana ‘yeye anayezoea uasherati anautenda dhambi mwili wake mwenyewe.’ Kwa hakika, dhambi ya namna hiyo inaweza kuharibu uhusiano wa kiroho tulio nao pamoja na Mungu. Haishangazi Paulo alisihi ‘ukimbieni uasherati.’ Ndiyo, ‘kimbieni’! Msingojee-ngojee mwaze au kubishania hilo. Nendeni mbali kabisa iwezekanavyo​—na mfanye hivyo haraka! Lakini namna gani kama mtu ‘hakimbii’ mwenendo wa namna hiyo?​—1 Wakorintho 6:15-18, NW.

“WAKIJIKOSEA WENYEWE”

7-9. (a) 2 Petro 2:9-13 inasema nini juu ya wale wanaojitia katika mwenendo mchafu? (b) Wengine ambao wamejiingiza katika uchafu ‘wamejikoseaje’?

7 Mtume Petro anasema kwamba wale waliomo ndani ya kundi ambao walitukana “watukufu” na kujitia katika mwenendo mchafu mwishowe ‘walijikosea wenyewe kama thawabu ya kutenda mabaya.’ (2 Petro 2:9-13, NW) “Thawabu” hizo za makosa ya kufanya ngono zinafanya mengi zaidi ya kuleta magonjwa ya kisonono na kaswende au mimba haramu. Zinaharibu upendo, heshima na amani ya akili. Kwa mfano, vijana wengine waliopita cheo wakifanya uasherati, walikubali hivi kwa majonzi:

“Jambo hilo lilivunja moyo mno. Hakukuwako maono yo yote ya wema au uchangamfu wa upendo kama ilivyodhaniwa ingekuwa. Mahali pake, kufahamu kikamilifu namna tendo hilo lilivyokuwa baya ndilo jambo lililonipiga kwa nguvu.”

“Nililia usiku wote.”

“Nilijiona kuwa ovyo sana kama mbwa. Haikuridhisha bali iliumiza. Niliacha kujiheshimu mimi mwenyewe pamoja na msichana huyo. Kwa kweli, nilijikuta nikimlaumu kuwa aliruhusu jambo hilo litokee.”

8 Baba yetu wa kimbinguni anatuambia tuepuke uasherati na pia “uchafu.” (1 Wathesalonike 4:7) Ingawa usemi huo unahusu mambo mengi, unaelekeza juu ya mwenendo usiofaa. Kwa mfano, kupiga punyeto, ni zoea ‘chafu’ ambalo vijana wengi wamefanya. Kwa hakika linachochea ‘tamaa ya ngono’ (NW) na linaweza kufanya mtu ajione mwenye hatia sana. Katika visa vingine ambapo mtu hakujitahidi sana kulishinda, kielelezo hicho cha kuwaza kilitokeza matatizo baada ya ndoa. Kijana mmoja alishtuka kuona kwamba baada ya ndoa kawaida yake ya muda mrefu ya kujitosheleza tamaa za ngono ilimfanya asiweze kutoa “haki” ya ndoa. Miezi mingi ya huzuni ilifuata!—1 Wakorintho 7:3.

9 Wenzi wengine wamegusana sehemu za mwili za siri na kuchochea tamaa za ngono. Vilevile huo ni “uchafu” na jambo hilo linaweza kuelekeza kwa urahisi kwenye uasherati, na mara nyingi ndivyo inavyokuwa. Zoea hilo linaweza kumwasha mtu ‘tamaa nyingi za ngono’ (NW) kufikia hatua ya kuwa na msisimuko mwingi wa kiwazimu. Kijana mmoja mwanamume alikubali hivi: “Unajiona mwenyewe kama mnyama mwenye tamaa za kinyama, jambo ambalo linaharibu maono ya ndani.” Mwenendo wa namna hiyo umetokeza kuvunjika kwa uchumbab na mara nyingi umetokeza matatizo kwa wale waliooa au kuolewa baadaye. “Tulifanya karibu kila kitu kinachofikisha kwenye uasherati na karibu sana tungeufanya kabla hatujafunga ndoa,” ndivyo walivyokiri wenzi vijana. “Ingawa tulipata msaada kutoka kwa wazee, mambo hayakupata kuwa sawa tena. Imekuwa vigumu kuheshimiana tena kama tulivyofanya wakati mmoja.”

10. Kwa sababu gani “uchafu” unaumiza watu ambao hawajafunga ndoa?

10 Mtu ambaye hajaoa anapoanza kushiriki mazoea ya ngono ‘yenye kulevya’ ambayo ni haki ya kitanda cha ndoa tu, yeye anaweza kudanganyika afunge ndoa na mtu asiye na sifa zinazotakwa kwa mume mwema au mke mwema. Ngono inaelekea kuficha tofauti kubwa ambazo zinatokea baada ya ndoa na kutokeza matatizo. Haishangazi kwamba uchunguzi mmoja ulifunua kwamba kati ya arusi 265 ambazo katika hizo bibi-arusi alikuwa mwenye mimba, baada ya miaka mitano ni wenzi 15 peke yao waliokuwa wangali pamoja! Uchunguzi mwingine unaonyesha kwamba mtu akishiriki ngono kabla ya ndoa, yeye ana maelekeo mara mbili zaidi ya wengine ya kufanya uzinzi. Kwa hiyo ninyi ndugu na dada vijana, msidanganywe na “maneno matupu” ya watu wanaosema kwamba kufanya ngono kabla ya ndoa kunatokeza ndoa yenye furaha zaidi. (Waefeso 5:6, NW) Wengine hata wanadai utakuwa mgonjwa usipofanya ngono unapobalehe. Huo ni uongo. Hakuna ugonjwa wo wote ambao madaktari wamehusianisha na usafi. Kwa kusikitisha, watu wengine ambao wamefuata tamaa nyingi mbaya badala ya upendo, wamesikitika maisha yao yote baada ya hapo!

11, 12. (a) Yehova anatoaje adhabu ya uasherati? (b) Ayubu anasema nini juu ya wale wanaomwonyesha Mungu ugumu? (c) Sasa tutazungumza juu ya ulizo gani?

11 Usisahau kamwe kwamba “[Yehova] ndiye alipizaye kisasi cha haya yote [uasherati na uchafu].” (1 Wathesalonike 4:6) Adhabu hiyo inaweza kuwa dhamiri yenye kuumiza, adabu kutoka kwa wazee wa kundi, au kuvuna matokeo ya yale unayopanda. Bila shaka, tukitubu, Yehova anatusamehe mara moja na kufunika dhambi zetu kabisa. Walakini wengine ni wagumu na wanakataa kuzitii sheria za Mungu. “Ni nani aliyejifanya mgumu juu yake [Mungu] akafanikiwa?” ndivyo Ayubu alivyouliza. (Ayubu 9:4) Hakuna ye yote! Inamsikitisha Yehova kuona ‘ugumu’ huo. Inasikitisha wazee wenye kuhangaikia ambao wameona vijana wetu wengi wakipatwa na maumizo hayo yaliyotangulia kutajwa. Waangalizi hao wanatambua kwamba hakuna ye yote anayeweza kuvunja sheria za Mungu na kanuni ‘afanikiwe.’ Ni kama kijana mmoja Mkristo aliyetubu juu ya uasherati alivyowaambia wazee wake wa kundi: “Laiti ningaliweza kumwambia kila kijana aliye katika Kweli, ‘Usifanye hivyo!’ Huenda Yehova akakusamehe makosa yako lakini huenda wewe usijisamehe kamwe. Kumbukumbu mbaya hizo zitakusumbua-sumbua. Jambo hilo halistahili.” Wazee wanajiunga na Yehova kusihi hivi: “Laiti ungalisikiliza amri zangu!”​—Isaya 48:18.

12 Lakini kijana Mkristo anawezaje kufuata amri za Yehova na kuepuka mitego mingi na vishawishi vyenye hila vya uasherati?

WAPE WAZAZI MOYO

13. Vijana wenye wazazi watawa wanawezaje kutumia Mithali 23:26, kuwe na matokeo gani?

13 “Mwanangu, nipe moyo wako; macho yako yapendezwe na njia zangu.” (Mithali 23:26) Ombi hilo linataka zaidi ya utii wa vivi hivi tu. Lazima kijana aufungue moyo wake na kuwaeleza wazazi siri zake. Hata hivyo, ukiwa kijana, huenda ukawa na maoni kwamba Baba au Mama yako Mkristo hafahamu kabisa maono yako ya ndani. Msichana mmoja Mkristo aliyekuwa na tatizo la kupiga punyeto (kusugua kiungo cha uzazi) akawa anahitaji msaada aliona hivyo. Yeye alikuwa na wasiwasi wa kuzungumza na mamaye. Mamaye angeitikiaje? Je! yeye angefahamu? “Basi, nilipozungumza naye juu ya jambo hilo, yeye alisikiliza naye hakunilaumu,” ndivyo tineja huyo alivyosema. “Yeye aliweka mkono wake kunizunguka, akaniambia ananipenda na angenisaidia kushinda tatizo hilo. Tulizungumza juu ya hilo kwa unyofu na tulipomaliza alinishikilia mikononi mwake na tukatoa sala pamoja. Tangu wakati huo ninaweza kuzungumza naye juu ya lo lote.”

14. Vijana Wakristo wanapaswa kuzionaje sheria za wazazi wao watawa?

14 Ndiyo, vijana wamekuta msaada ukiwa tayari kwa kuwaeleza wazazi wao Wakristo siri zao. Wanapata ‘kupendezwa’ na njia za wazazi wao watawa na wanaziona amri zao na adabu wanayotoa kama “mikufu” yenye thamani wala si ‘mnyororo’ unaowazuia ‘wasijifurahishe.’ (Mithali 1:8, 9) Je! kweli wewe unasema kwa unyofu na wazazi wako? Au wewe ni kama kijana yule aliyekubali hivi: “Ninapokuwa karibu na wazazi wangu ninatenda kama wanavyotaka nitende, bali ninapokuwa mbali, ndipo ninapotenda kama ninavyotaka”? Kwa kuwakaribia wazazi wanaomwogopa Mungu, unaweza kusaidiwa uepuke maumivu mengi yasiyo ya lazima. Wale ambao huenda wasiwe na wazazi Wakristo wanaweza kuwafikia Wakristo waliokomaa​—wanaume na wanawake​—pamoja na wazee kundini. Tafuta msaada wao wanaoutoa kwa kupenda.​—Tito 2:3, 4; Yakobo 5:14, 15.

UONGOZE MWIU KAMA MTUMWA

15. Mtume Paulo anasimuliaje mwendo wake katika 1 Wakorintho 9:27, na kijana anawezaje kutenda kwa njia kama hiyo?

15 Mtume Paulo alisema hivi: “Naupiga-piga ngumi mwili wangu na kuufanya kama mtumwa [wala sio, ‘unaonifanya kuwa mtumwa’], ili nikiisha kuhubiri wengine, mimi mwenyewe nisije nikakataliwa kwa njia fulani.” (1 Wakorintho 9:27, NW) Paulo hakujiachilia ‘kizembe’ tu. Vivyo hivyo, pia, badala ya kuruhusu tamaa zenu za mwili ziwatawale, tangulieni kuona hali ambazo zinaweza kuamsha, tamaa za ngono na kuziepuka kwa makusudi. Kwa mfano, unajua itakavyokuwa kwa tamaa zako za mwili ukisoma vitabu na kutazama vipindi vya televisheni na sinema zinazotukuza ngono. Kwa hiyo epuka vitu hivyo kama kwamba ni ugonjwa mbaya sana! Matembezi ya wavulana na wasichana (mahali yanapokubaliwa na ujamii) mnapokuwa hamko tayari kufanya ndoa, namna fulani za dansi, karamu zisizoongozwa kwa usafi na mahali ambapo wanaume na wanawake wanacheza wawili wawili, yote hayo yanatokeza ‘tamaa mbaya ya ngono’ (NW). Kwa hiyo epukeni mambo hayo na “kufisha viungo vyenu . . . [kwa habari ya] uasherati uchafu, tamaa mbaya [ya uasherati].”​—Wakolosai 3:5.

16. Wenzi Wakristo wanapofanya matembezi na kujitayarishia ndoa wanapaswa kujihadhari na mambo gani?

16 Sanasana msichana na mvulana wanapofanya matembezi na kujitayarisha kufanya ndoa wanahitaji kujihadhari. Kuwa peke yao katika motokaa, nyumba (pengine mtu anayeishi peke yake mbali na nyumbani), au katika sehemu zilizo peke yake nje ya nyumba zaweza kushawishi wenzi wakaribiane kupita kiasi. Kijana mmoja mwenye umri wa miaka 17 alisema hivi kwa unyofu: “Mtu ye yote anaweza kusema, ‘tunajua wakati wa kuacha.’ Ni kweli, huenda mtu akajua wakati wa kuacha, walakini ni wangapi wanaofanya hivyo? Ni afadhali kuepuka hali hiyo. Mwe na wengine pamoja nanyi.” Ndiyo, mtu wa kuwaangalia anaweza kuwapa nguvu ya zaida ya kutawala kabisa tamaa za ngono ndani ya miili yenu mnapokuwa pamoja. Vilevile, ‘wekeni mipaka’ ya maneno ya mapenzi mnayoweza kusema. Ifuateni mipaka hiyo.

17. Je! ni jambo la maana kujihadhari na mashirika yetu? Kwa sababu gani?

17 Mwili unapotamani sana kuwa karibu na wale wenye mwenendo mchafu, uondoe mbali na ushirika huo. “Itenge njia yako mbali naye [mwanamke mwasherati], wala usiukaribie mlango wa nyumba yake,” ndivyo Biblia inavyopendekeza. (Mithali 5:8) Bila shaka, wanapokuwa shuleni, vijana wanaingizwa kwenye ushirika na watu wengi wenye mwenendo mchafu. Walakini je! mnafanya urafiki nao? Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 18 alitaja maoni ya wengi aliposema hivi: “Wale unaoshirikiana nao wanaweza kugeuza sana mwenendo wako mwema. Baada ya kuyasikiliza mazungumzo yao juu ya ngono, unakuwa mtafiti. Unataka kujua jinsi ngono ilivyo. Je! ni nzuri kama wanavyosema. Ninajua hayo ni kweli kwa sababu ninalea mtoto nikiwa peke yangu kwa ajili ya mambo ayo hayo.”​—Mithali 13:20.

18. Mkristo kijana anapodhihakiwa kwa sababu ya kuwa na adili safi, anapaswa kutafakari maulizo gani?

18 Maandiko yanaonyesha kwamba watu wengine wenye mwenendo mchafu wangejipenyeza ndani ya kundi la Kikristo. Kwa hiyo, jiangalie. Ukisadiki wo wote huenda wakawa wa namna hiyo, waelekeze kwa wazee ili wapate msaada wa kiroho. Kwa njia hiyo utakuwa unawaonyesha upendo wa kweli na pengine pia kuwalinda wengine kundini. Ni kweli kwamba huenda watu wengine wa ulimwengu wenye mwenendo mchafu wakakufanyia dhihaka kwa ajili ya msimamo wako safi. Lakini, fikiri tu! Je! unapaswa kuruhusu watu ambao ni “watumwa wa uovu”​—ndiyo, watumwa wa tamaa za ngono zao wenyewe​—wakufanye uone haya? (2 Petro 2:19, NW) Ni nani mwenye kujiweza kwingi zaidi​—yule mwanamke (au mwanamume) mwasherati na mwenye mwenendo mchafu ‘anayefuata wapenzi wake’ wenye tamaa ya ngono, au yule bikira safi anayeweza kusema juu ya anavyojiweza na kuwa na mwenendo safi, ‘Mimi ni ukuta’? (Wimbo Ulio Bora 8:10; linganisha Hosea 2:7) Ni nani kati yenu aliye na maelekeo zaidi ya kupoteza hali ya kujiheshimu na ‘kuwapa wengine heshima yake’?​—Mithali 5:9; Yuda 4, 8-13.

19. (a) Ni nani ‘aliyeufanya mwili kama mtumwa’​—mvulana na msichana wanaosimuliwa katika Wimbo Ulio Bora, au Amnoni? (b) Matokeo yalikuwa nini?

19 Kwa kuuongoza mwili wako, kuutawala, utaweza kuikumbuka miaka ya nyuma bila masikitiko yo yote. Ebu wazia furaha ya yule msichana mchanga Mshulami na mpenzi wake mchungaji walipoungana mwishowe katika ndoa. Kwa msaada wa wengine, na kwa jitihada zao wenyewe, walishinda tamaa yao ya mwili wakaendelea kuwa safi. Ingawa walikuwa wamesemezana maneno ya mapenzi, hawakuwa wamefuata mwenendo mchafu kabla hawajafanya arusi, kwa njia hiyo wapunguze furaha ambayo wangekuwa nayo baada ya kufaana katika ndoa. Hao ni tofauti kama nini na Amnoni mwenye tamaa za ngono ambaye hakuweza kungojea na ambaye ‘mwili wake ulimfanya awe mtumwa’ mpaka akafanya uasherati!—Wimbo Ulio Bora 2:16; 4:16; 5:1; 2 Samweli 13:1, 2, 10-16.

UJENGE UHUSIANO WAKO NA MUNGU

20. (a) Kwaweza kutokea nini mtu asipokuwa na uhusiano wa kibinafsi na Mungu? (b) Ni nini kilichokuwa kimekosekana katika watu wenye kufuata mwenendo mchafu wanaosimuliwa na Paulo katika Warumi sura ya 1?

20 “Sikujenga kamwe uhusiano wa kibinafsi na Yehova,” ndivyo alivyokiri msichana mwenye umri wa miaka 22 aliyelelewa tangu utoto katika nyumba ya Kikristo. “Mungu hakuwa mtu halisi kwangu. Nafikiri hiyo ndiyo sababu sikusumbuliwa nilipofanya uasherati.” Hali yake ilikuwa sawa na ile ya watu wenye mwenendo mchafu wanaosimuliwa na Paulo. Wao ‘walimjua Mungu’; ‘walijua vizuri kamili amri yake yenye haki,’ walakini walikosa “maarifa sahihi.”c (Warumi 1:21, 28, 32, NW) Hayo “maarifa na ufahamiano wenye kina zaidi na wa ukaribu zaidi,”d maarifa ya kibinafsi, ambayo yalipasa kuwa yamesitawishwa, yalikuwa yamekosekana. Je! wewe ukiwa kijana, una “maarifa sahihi” hayo ya kibinafsi? Unahitaji kujifunza Neno la Mungu kibinafsi na kwa ukawaida ili uthamini sifa za Mungu. Kumbuka namna “maarifa sahihi” hayo yalivyotia nguvu Wakristo wa kwanza. (Ona ukurasa 8.) Walakini kunatakiwa mengi zaidi ya maarifa tu ya kitabuni.

21, 22. Ni nini kitakachojenga uhusiano wa kibinafsi wenye nguvu pamoja na Mungu?

21 Sala za kutoka moyoni zinajenga ukaribu na Mungu. Msichana mmoja Mkristo kijana, aliyenaswa na uasherati lakini baadaye akafanya maendeleo, alisema:

“Njia pekee ya kuendeleza uhusiano huo wa kibinafsi ni sala, si zile za desturi bali zile zinazotoka moyoni kabisa. Ninapomwambia Yehova yale ninayoona moyoni na kuwa na upashanaji habari huo wa kawaida, ninatambua kwamba yeye ni Mtu halisi na anapendezwa na maisha yangu. Uhusiano wangu pamoja naye ndilo jambo la maana zaidi ulimwenguni.”

22 Je! sala zako ni za bidii hivyo? Je! unatenda kwa kupatana nazo? Vilevile, kwa kuwa ‘mfanya kazi pamoja na Mungu,’ na kushiriki kazi ya kuhubiri, mapendezi na makusudi yako yatakuwa sawa na ya Mungu. Kama ilivyo, jambo hilo litajenga ukaribu na Yehova. Kumbuka, ni wewe tu unayeweza kujenga uhusiano huo wa kibinafsi pamoja na Mungu.​—1 Wakorintho 3:9.

23. (a) Je! kushindana na mwenendo mchafu kutaendelea milele? (b) Kwa sababu gani unapaswa kuwa na nia ya kutia jitihada yo yote ili kumpendeza Yehova

23 Ni kweli kwamba vijana wanakazwa leo. Kuwa mwaminifu ni pigano la kila siku. Hata hivyo, mara ukiisha kuupita “ukamilifu wa ujana,” vita hiyo inaweza kuwa rahisi zaidi. Hata hivyo, pigano hilo halitaendelea milele. Karibuni Shetani, mchochezi mkuu wa mtindo huo wa mwenendo mchafu, ataharibiwa. Katika taratibu mpya ya Mungu inayokaribia sana, kutakuwako mazingira yenye haki ambayo yatafanya mwendo wetu uwe rahisi zaidi. Tafakari juu ya baraka za hiyo taratibu mpya. Hakika unakubaliana na mawazo ya mwanamke mmoja kijana, aliyesema hivi: “Ninafikiri juu ya kila kitu ambacho Yehova amenifanyia na kuniahidi. Yeye hajaniacha. Yeye amenibariki katika njia nyingi sana. Ninajua yeye anataka nipate yaliyo bora peke yake, nami ninataka kumpendeza. Uzima wa milele unafanya jitihada yo yote kwa ajili ya Yehova istahili.”​—Warumi 16:20; 2 Petro 3:13.

[Maelezo ya Chini]

a Ona tarakimu zenye kushtua katika ukurasa wa 6.

b Zoea la kugusa sehemu za siri za mwili kwa tamaa ya kufanya ngono, lasemekana, na wengine wenye maarifa, kuwa kisababishaji kimoja kikuu cha kuvunjika kwa uchumba. Uchunguzi unaonyesha kwamba angaa mmoja kati ya kila uchumba tatu mwishowe hauwi ndoa.

c Katika mstari wa 21 Paulo anatumia neno la Kigiriki gnoʹsis, ambapo katika mstari wa 28 yeye anatumia e·piʹgno·sis, ambayo ni namna yenye mkazo zaidi ya neno hilo. Linaonyesha maarifa ya undani zaidi na makamilifu zaidi.

d Mwanachuo Mgiriki Dakt. Richard C. Trench katika kitabu Synonyms of the New Testament.

Kwa kujikumbusha, wewe unaweza kujibu maulizo haya?

■ Ni nini mapenzi ya Mungu kwa Wakristo kuhusu mwenendo safi?

■ Kwa sababu gani “uchafu” unaotokana na ngono isiyo halali unaumiza watu ambao hawajafunga ndoa?

■ Vijana Wakristo wanapaswa kuonaje msaada wenye msingi wa Biblia unaotolewa na wazazi wao watawa?

■ Wenzi Wakristo wanapaswa kujihadhari na nini wanapojitayarisha kufanya ndoa?

■ Uhusiano wa kibinafsi wenye nguvu pamoja na Yehova Mungu unaweza kusitawishwaje?

[Picha katika ukurasa wa 13]

Uasherati unaumiza kwa sababu ya dhamiri iliyoharibiwa na kupoteza heshima

MWENENDO MCHAFU

HESHIMA ILIYOPOTEZWA

[Picha katika ukurasa wa 15]

Uhusiano wa kibinafsi pamoja na Mungu, unaositawishwa kupitia sala, unakuwa ni ulinzi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki