Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 6/1 kur. 17-24
  • Wazazi, Fikieni Moyo wa Mtoto Wenu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wazazi, Fikieni Moyo wa Mtoto Wenu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • TEKA MASHAURI KUTOKA MOYONI
  • UAGIZE MOYO
  • ADABU INAUSAFISHA MOYO
  • MSAIDIENI MTOTO AJENGE UHUSIANO NA MUNGU
  • WANAHITAJI MSAADA UNAOPITA ULE WA KAWAIDA
  • Zoeza Mtoto Wako Asitawishe Utawa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Zoeza Mtoto Wako Tangu Utoto Mchanga Sana
    Siri ya Furaha ya Familia
  • Kulea Watoto tangu Uchanga
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
  • Jinsi ya Kuwalinda Watoto Wako
    Amkeni!—2007
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 6/1 kur. 17-24

Wazazi, Fikieni Moyo wa Mtoto Wenu

“Mwanangu, kama moyo wako una hekima, moyo wangu utafurahi.”​—Mithali 23:15.

1, 2. (a) Tamaa ya wazazi Wakristo ni nini, walakini baba mmoja alikuwa na maoni gani? (b) Katika kumzoeza mtoto, ni nini kinachohitaji kufikiwa, na kwa sababu gani?

WAZAZI Wakristo wanatamani sana kuwalinda watoto wao kutokana na mitego ya adili yenye kuharibu. Bila shaka wewe, ukiwa mzazi, una wasiwasi ule ule kama wa baba mmoja Mkristo mwenye matineja wanne aliyeandika hivi: “Adili ambazo vijana wetu wanakabili zinaendelea kuwa mbaya zaidi, na nyakati nyingine ni vigumu kukabili kila njia mpya ambayo ulimwengu unafuata. Sala yangu ya wakati wote ni kwamba niweze kuwasaidia. Ninawapenda sana sana.”

2 Hata hivyo, ni kwa nini nyakati nyingine, hata baada ya kupelekwa kwenye mikutano ya kidini na kufundishwa adili za Biblia, huenda bado mtoto akajiingiza kwenye mwenendo mchafu wa ngono? Ingawa mafunzo ya akilini ni ya maana, moyo unafanya sehemu ya maana kubwa sana, sanasana kuhusu adili. Mzazi anaweza kufanya nini ili aufikie moyo wa mtoto ili uwe na ‘hekima’?​—Mithali 4:23; 23:15.

TEKA MASHAURI KUTOKA MOYONI

3. Mithali 20:5 inamaanisha nini, na hiyo inahitaji wazazi wachukue hatua gani?

3 Kabla hujaweza kuufikia moyo, ni lazima upate kujua, kwa kadiri fulani, yaliyomo moyoni. “Mashauri [kusudi la halisi la mtu au makusudi yaliyotia mizizi ndani sanaa] ya moyoni ni kama kilindi; lakini mtu mwenye ufahamu atayateka.” (Mithali 20:5) Maono ya kweli ndani ya moyo wa mtoto ni kama maji yaliyomo ndani ya kisima chenye kina kirefu. Katika nyakati za kuandikwa kwa Biblia, visima fulani vilikuwa na vina vya mita 30, na iliwapasa watu watelemke kwa ngazi ili ‘wakayateke’ maji hayo. Ilikuwa kazi ngumu kweli kweli! ‘Kuteka’ makusudi ya mtoto wako kwaweza kuwa kugumu namna iyo hiyo. Kufanya hivyo kunahitaji kujiweka katika hali ya mtoto na kuchunguza mambo kwa uangalifu mwingi. Huenda kukahitaji matumizi ya ustadi ya maulizo, subira​—nyakati nyingine uwe na nia ya kuzungumza na mtoto kwa saa nyingi kabla maono yake ya kweli hayajajitokeza wazi. Kwa kumkumbusha mtoto kwamba wewe ulipitia kipindi icho hicho, na kwamba wewe pia hujakamilika, na kwa kutokeza nafasi ili kwamba mtoto awe na wewe mkiwa peke yenu nyakati nyingi, utafanya iwe rahisi kwake kusema yaliyomo moyoni mwake.​—Ayubu 33:5-7.

4. Kulingana na Mithali 12:18, ni namna gani ya usemi inayoweza kuharibu upashanaji wa habari?

4 Hata hivyo neno ‘lisilofikiriwa’ au usemi waweza kuharibu sana. Wengine wanasema bila kufikiri, “kama kuchoma kwa upanga.” Maneno yao yanaumiza na kutenganisha. Kwa hiyo jitahidi uwe na “roho ya utulivu” unaposikiliza kweli kweli. Pengine unaweza kukumbuka wakati mtu alipokukatisha kwa sauti kubwa ulipokuwa ukisema au akakufanyia dhihaka kwa ajili ya maono yako. Pengine alisema hivi, ‘Unajua zaidi ya hayo!’ Je! ulitaka tena kumweleza mtu huyo siri zako?​—Mithali 12:18; 17:27.

5. (a) Tineja anahitaji namna gani ya mashauri? (b) Je! wazazi walio wengi wanatoa mashauri hayo?

5 Mtoto anapofika miaka ya utineja, tamaa zake za ngono zinakuwa kali sana. Kijana huyo anahitaji kuzungumza na mtu anayeweza kumweleza yanayoupata mwili wake na anayeweza kujibu orodha ndefu ya maulizo ya kibinafsi yasiyopasa kuchukuliwa vyepesi. Hata hivyo katika uchunguzi uliofanywa wa wazazi 1,400 wenye watoto waliobalehe, asilimia 92 hawakuzungumza kamwe na watoto wao juu ya tabia ya ngono. Namna wazazi hao walivyolelewa, desturi za nchi, au sadikisho la kwamba mazungumzo hayo si ya lazima, nyakati nyingine mambo hayo yanawazuia hata wazazi Wakristo wasitoe uangalizi huo wenye ufahamu. Mazungumzo ya namna hiyo ni ya maana kadiri gani?

6, 7. Ni jambo la maana kadiri gani kwamba wazazi wazungumze juu ya tabia ya ngono pamoja na watoto wao?

6 Baada ya kuhoji jamaa fulani, mzee mmoja Mkristo alikata maneno hivi: “Inavutia kuona namna kielelezo fulani kinavyofuatwa. Matokeo yalikuwa mazuri kwa wazazi waliohangaikia mambo ya ngono mapema na wakajitahidi kuendelea kupashana habari kwa urafiki na watoto wao. Kwa wale ambao, kwa sababu yo yote ile, hawakushughulika na tatizo hilo mapema, matokeo wakati mwingi yalikuwa mabaya.”

7 Faida zinazopatikana kutokana na mazungumzo hayo ni nyingi. Kwanza, yanaweza kukinga akili ya mtoto na habari chafu ya uongo ambayo atasikia baadaye. Pili, yanaweza kutokeza heshima kwa wazazi na hali ya kuwatumaini na kuweka msingi wa kupashana habari ambao utaendelea hata wakati wa kubalehe. Na tatu, yanaweza kufanya iwe rahisi zaidi kwa mtoto wako kuzungumza nawe mambo ya kindani kabisa. Hata hivyo, wazazi wengi wangetaka kujua namna ya kufanya mazungumzo hayo yenye kutokeza haya.

UAGIZE MOYO

8. Mazungumzo juu ya ngono yanapasa kuanza mapema kadiri gani?

8 Thamani ya kuanza kumwagiza mtoto akiwa mwenye umri mdogo ni kubwa sana. Hesabu fulani ya watoto wenye umri wa miaka 10 na 11 wamepata mimba. Wachunguzi wengine wanasihi kwamba upashanaji wa habari juu ya ngono unapasa kuimarishwa kabisa kabla mtoto hajafikia miaka sita. Kama sivyo huenda jambo hilo lisitimizwe kamwe. Mara nyingi, kujibu kwa unyofu na bila aibu maulizo ambayo mtoto mchanga anauliza juu ya jambo hilo kwatosha.b Hata hivyo, tineja anahitaji maagizo juu ya namna ya kuzuia tamaa hizo. Ili kuufikia moyo lazima maagizo hayo yatolewe kwa namna ya msaada wa kirafiki, wala si kama shtaka.

9. Mzazi anapaswa kujaribu kutia nini ndani ya moyo wa mtoto, na kwa sababu gani?

9 Yesu alisema: “Mtu mwema katika hazina njema ya moyo wake hutoa yaliyo mema.” (Luka 6:45) Kwa hiyo, ili kuufikia moyo wa mtoto wako inataka uingize katika moyo huo mchanga mambo ya thamani​—mambo ambayo yeye ataitikia kwa maono ya ndani na kuyatunza. Kwa sababu gani? Ili hayo “yaliyo mema” yatoke ndani ya moyo huo.​—Mathayo 12:34, 35

10, 11. Kutokana na mifano katika kitabu cha Mithali ni mambo gani tunayoweza kujifunza juu ya namna ya kufikia moyo wa mtoto wako wakati wa mazungumzo ya mwenendo safi wa ngono?

10 Maagizo yanayotolewa juu ya habari hiyo katika Mithali yanawapa wazazi mfano mzuri. Yanazungumza juu ya tabia ya ngono kwa unyofu lakini bado kwa njia ya heshima. Angalia namna mazungumzo hayo yalivyo yenye kiasi katika sura ya tano. Mshauri au mzazi huyo anazungumza namna mambo yalivyo kuhusu furaha ya ngono na sanasana juu ya uhitaji wa mwenendo msafi kuhusu ngono. Inaelekea midomo ya malaya ‘inadondoza asali’ anapotafuta kumtongoza mwanamume. Ai, lakini matokeo ya baadaye ni ‘machungu kuliko pakanga’ na ‘makali kama upanga wa makali kuwili’! (Mistari 3, 4) Kisha mshauri huyo wa Kibiblia anataja sehemu ya kuzungumzwa kwa uangalifu kwa kumwonyesha mwanamume huyo kijana namna anavyoweza kupoteza “heshima” yake kwa mwenendo wa jinsi hiyo. (Mstari 9) Hata hivyo, hayo si mazungumzo ya kwamba ‘ngono zote ni dhambi.’ Yeye anatoa maelezo mazuri kama nini juu ya ngono ndani ya kifungo cha ndoa.​—Mistari 15-19.

11 Mzazi huyo hamshtaki wala kumshusha mwanamume huyo kijana. Katika Mithali sura ya saba, yeye anasimulia mambo mengine yaliyoonwa na kutumia semi zenye kutaja mambo moja kwa moja. (Mithali 7:6, 7, 13, 17, 18) Mshauri huyo anatumia mifano iliyo wazi kabisa​—mwanamume mwenye tamaa za ngono anayetongozwa na malaya anafananishwa na ng’ombe anayekwenda machinjoni, na ‘mshale unaochoma maini yake.’ (Mithali 7:22, 23) Kijana angewezaje kusahau masimulizi kama hayo! Mfano huo wa kuonya ukiwekwa moyoni utamsaidia kijana akabiliane na kishawishi. Mzazi huyo hakusema tu kwamba mwenendo mchafu wa ngono ni kosa, lakini alieleza sababu gani hivyo, kwa kueleza matokeo na kuonyesha namna kijana huyo angalivyoweza kujikuta humo kwa urahisi.

12, 13. (a) Ni zipi baadhi ya pindi ambazo mzazi anaweza kuzungumza juu ya tabia ya ngono pamoja na mtoto wake? (b) Je! umepata kuona nyakati nyingine zinazofaa kufanya hivyo? (c) Ili mtoto awe na mwenendo safi, je! inatosha tu kutia mashauri mazuri moyoni mwake?

12 Wazazi wengi Wakristo wamekuwa na mazungumzo kama hayo. Wameyafanya pindi nyingi wakati ambapo habari hiyo ingeweza kuzungumzwa kwa njia ya kawaida na inayofaa. Baadhi ya nafasi hizo zilikuwa wakati wa matembezi marefu, wakati wa kuzungumza juu ya kisa fulani kinachoonyesha thamani ya adili zinazofaa, baada ya habari hiyo kuzungumzwa wakati wa mikutano ya kundi, au wakati mazungumzo ya kiroho ya jamaa zao wenyewe yalipokuwa yanaihusu habari hiyo. Wengine wametumia kitabu Kupata Faida Zote za Ujana Wakoc ili kuwasaidia. Mazungumzo ya namna hiyo sikuzote hayakuwa rahisi, walakini upendo wa kweli kwa mtoto uliwachochea wazazi hao. Ni kama ambavyo mama mmoja mwenye watoto watano alivyokubali: “Nilijilazimisha nizungumze juu ya jambo hilo mpaka mwishowe nikawa najiona nastarehe, na mtoto mwenyewe pia.” Usiache mtoto wako apate maumivu mengi ya moyoni kwa sababu ya kukosa “mafundisho mazuri” juu ya sehemu hii yenye kutaka uangalifu mwingi sana.​—Mithali 4:2.

13 Hata hivyo, yajapokuwa mafundisho yote mazuri yanayoweza kutiwa ndani ya moyo wa mtoto, vilevile ujinga umetia mizizi sana moyoni kwa sababu ya hali ya dhambi iliyorithiwa.​—Zaburi 51:5.

ADABU INAUSAFISHA MOYO

14. Adabu ni nini, na kwa sababu gani ni ya maana sana?

14 Ni nini kinachoweza kuondoa ujinga ndani ya moyo mchanga huo? ‘Fimbo ya adabu,’ kulingana na Mithali 22:15. Adabu ni mazoezi yanayofinyanga au kusahihisha. Ni uthabiti wenye ufahamu; kwa hiyo haibembelezi wala ‘kuudhi’ mtoto kwa vizuizi visivyo na kiasi. (Waefeso 6:4) Adabu ni ya lazima wakati mtoto wako anapovutiwa na wengine ambao si aina yake. Kukubali mvulana na msichana washinde pamoja inapokuwa wote wawili ni wachanga mno kuweza kufunga ndoa ni kualika msiba.

15. (a) Ni hali gani inayohangaisha wazazi wengi? (b) Ndugu za mwanamwali Mshulami walifanya nini wakati yeye na rafikiye mvulana walipotaka kwenda pamoja wakiwa peke yao?

15 Walakini wazazi wengi wanauliza hivi, ‘Unaweza kufanya nini wanapotaka kuwa pamoja?’ Kwa wazi chini ya uongozi au kwa ukubali wa wazazi wao, wakati ndugu za mwanamwali Mshulami walipogundua kwamba yule kijana mchungaji alitaka kwenda na dada yao kwenye matembezi wakiwa peke yao katika sehemu moja ya mlimani iliyo peke yake, wao walikomesha jambo hilo! Walimpa msichana huyo kazi ya kuumaliza wakati wake na ya kuwatenganisha wao wawili. Ingawa walikuwa wanamtumaini, walikuwa wanajua nguvu nyingi ya kishawishi. Je! jambo hilo liliharibu maisha ya msichana huyo? Tofauti na hilo, liliwasaidia wote wawili waendelee kuwa na adili safi mpaka walipooana baadaye.​—Wimbo Ulio Bora 1:6; 2:8-15.

16. Wazazi wengine wamefanya nini ili kulinda mioyo ya watoto wao?

16 Uthabiti kama huo, pamoja na kumpa mtoto huyo utendaji wa kushughulisha akili yake, ni mambo yanayohitajiwa leo. Kwa habari hiyo, lazima wazazi watumie ufahamu wa kweli na hekima ya kimungu. (Mithali 24:3) Ni vigumu sana kwa wazazi kuzuia maono ya ndani ya mtoto akiisha kuguswa moyoni. Kabla ya kuruhusu mtoto wao afanye matembezi ya mvulana na msichana (mahali ambapo jambo hilo linakubaliwa na ujamii), wazazi Wakristo wangepaswa kufikiria umri wa mtoto, kiwango cha kukomaa kwa maono ya ndani na maendeleo ya kiroho, ni nani ambaye mtoto huyo anataka kutembea naye na utendaji wao utakuwa nini. Mama mmoja ambaye binti yake wa miaka 19 alitengwa na ushirika kwa ajili ya uasherati aliulizwa ni nini aliona angalipaswa kufanya kwa njia tofauti katika kumlea mtoto huyo wake. Yeye alijibu hivi: “Singalimruhusu kamwe ajishirikishe na wavulana katika uhusiano wa kimapenzi alipokuwa katika miaka yake ya mapema ya utineja. Singaliwaza kwamba yeye alikuwa imara sana kwamba yeye angeweza kushughulikia tatizo lake.”

17, 18. (a) Je! mvulana na msichana wanaotaka kufunga ndoa wachukie wakati mzazi au mtu mwingine anayewekwa na mzazi anapotenda kama mwangalizi wao? (b) Mwanamume mmoja kijana alijifunza nini kwa njia yenye kuhuzunisha?

17 Wazazi wengine wameketi pamoja na mvulana na msichana hao wachanga na kuwaeleza ni kwa sababu gani hawawezi kukubali wafanye matembezi yao. Kwa kuzungumza jambo hilo pamoja na wazazi wa yule mtoto mwingine, tegemezo zaidi huenda likatolewa. Mzazi mmoja Mkristo mwenye watoto wanne alisema hivi: “Wazazi fulani wanafikiri kwamba uhusiano wa wavulana wachanga na wasichana wachanga ni wenye kupendeza na wanautia moyo, pamoja na kuruhusu vikundi-vikundi vya matineja waende kutembea pasipo usimamizi wa mtu mzima. Tunaloona ni kutembea wawili wawili, uasherati na ndoa za mapema. Tunawatia moyo watoto wetu wasitawishe mapendezi na utendaji mwingineo wa kutumia mwili kama vile kuendesha baisikeli, mambo wanayoweza kufanya wakiwa. peke yao, wakiwa na jamaa, au pamoja na wengine wa aina yao.”

18 Hata mvulana na msichana wanapokuwa wenye umri mkubwa kutosha kuweza kuchumbiana, wasaidie kwa kupanga awepo mtu wa kuwaangalia. Wenzi Wakristo waliokuwa wameposana na ambao karibuni wangeoana waliacha kujihadhari wakajiingiza katika “uchafu.” (Wagalatia 5:19) Kwa kukumbuka yaliyotokea, mwanamume huyo kijana alikubali hivi: “Wakati mwingi tulikuwa na mtu wa kutuangalia. Nyakati hatukuangaliwa tulikosa.” Vijana wengine waliwashukuru wazazi wao baadaye kwa kuwa thabiti na kuongoza tafrija yao, kwa maana waliendelea kuwa wenye adili safi wakafunga ndoa pasipo masikitiko wala kumbukumbu mbaya. Ikiwa makusudi ya mtoto wako ni yenye heshima, yeye hatachukizwa na adabu yako ya kimungu, kwa maana hiyo ndiyo “njia ya uzima.”​—Mithali 6:23.

MSAIDIENI MTOTO AJENGE UHUSIANO NA MUNGU

19. (a) Ulinzi mkubwa zaidi wa mtoto wako juu ya mwenendo mchafu ni nini, na nini kitakachomsaidia ausitawishe? (b) Wazazi wanaweza kuuliza nini juu ya mfano wao wenyewe?

19 Ulinzi mkubwa zaidi kutokana na mwenendo mchafu ni mtoto wenu kusitawisha uhusiano wa kibinafsi wa karibu pamoja na Yehova. Ingawa hilo ni jambo ambalo mtoto mwenyewe anapaswa kufanya, mzazi anaweza kusaidia. Kwanza kabisa, mfano wako mwenyewe wa kujitoa utatoa kielelezo chenye nguvu cha kuigwa. Wale waliokuwa Wakristo katika Thesalonike ya karne ya kwanza waliona Paulo na wenzi wake walikuwa “watu wa aina gani” na ‘wakawa waigaji,’ wakasitawisha ‘sadikisho lenye nguvu’ kama lao. (1 Wathesalonike 1:4-6, NW) Watoto wako wanakuona wewe kuwa ‘mtu wa aina gani’? Je! wanaona ‘sadikisho lako lenye nguvu,’ na kukuona ukijenga maisha yako yote juu ya kujitoa kwako kwa Mungu na kujinyima kwa ajili ya ibada yake? Je! wanaona ukichukizwa sana na mwenendo mchafu kwa wewe kutokufurahishwa na mambo yaliyopotoka kiadili? Je! wanaona mfano wa upendo katika njia ile unayomtendea mwenzi wako au unaposhughulika na wengine? Je! wanakusikia ukisema juu ya Yehova katika njia inayoonyesha wazi kwamba yeye ni halisi kwako? Mfano wa namna hiyo utakuwa kichocheo kwa mtoto wako ajinyime ili afuate sheria ya Yehova. Mtoto wako ataona kwamba kufanya hivyo ni jambo la maana.

20. Ni nini kinachoweza kuharibu matokeo ya kazi yako nzuri ya kulea watoto?

20 Vilevile, kwa kulinda sana ushirika wa watoto wako na kuwachagulia washiriki wenye kuonyesha ‘sadikisho lenye nguvu,’ utatia nguvu jitihada zao. Washiriki wabaya wanaweza kuharibu kazi yako haraka sana​—hata ikiwa wao wanapatikana ndani ya kundi la Kikristo. Washiriki hao wabaya wanaweza kuharibu hali ya kiroho ya mtoto wako na kutokeza pengo la kutokupashana habari kati ya watoto na wazazi.​—Mithali 13:20; Yuda 3, 4, 12, 16, 19.

21. (a) Kulingana na 1 Yohana 2:14, ni nini kinachotoa nguvu za kiroho, na jambo hilo linawapa wazazi daraka gani? (b) Una mapendekezo gani ya kutoa ili mafunzo hayo yaendelee kuwa ya kawaida na yenye kupendeza?

21 Ukiwa mzazi, unapaswa kusadikishwa na nguvu za Neno la Mungu, Biblia. Mtume Yohana alisema kwamba “vijana” wenye nguvu za kiroho katika kundi aliloliandikia walikuwa ‘wamemshinda yule mwovu’ kwa sababu ‘neno la Mungu lilikuwa limeendelea kuwa ndani yao.’ (1 Yohana 2:14) Kwa hiyo, pamoja na kusitawisha roho ya ukaribu ya jamaa na kuweka mfano mzuri, wazazi watawa wanapaswa kupanga kujifunza Neno la Mungu kwa ukawaida na jamaa ili ujumbe walo uingie ndani kabisa katika moyo wa mtoto. Mume na mke mmoja walitazama kwa uchungu wawili kati ya watoto wao watatu wakigeuka wakawa wabaya wakati wa miaka yao ya utineja. Baba huyo ambaye alikuwa amewalea katika nyumba ya Kikristo tangu utoto, alikubali hivi: “Kama ningalipata nafasi ya kurudia jambo hilo tena, kungalikuwako funzo la Biblia la jamaa lenye ukawaida zaidi. Funzo letu halikuwa na mradi. Ninajua funzo la kawaida lingalituvuta pamoja tuwe kama jamaa zaidi kwa njia ya kiroho.” Wazazi wakitayarisha vizuri, wakiepuka kuongoza funzo kwa njia ile ile ya kufuata tu utaratibu uliowekwa, bila kubadilikana bali wakiliongoza kwa njia inayofaa mahitaji ya mtoto, mazungumzo hayo yatatazamiwa kwa shauku nayo yataivuta jamaa pamoja kiroho. Jambo hilo si rahisi kwa sababu linachukua muda mwingi wa wazazi, lakini jambo la maana zaidi ya urefu wa mazungumzo hayo ni ubora wa wakati wanaoutumia pamoja. Zaidi ya hayo, watoto wanahitaji kufunzwa mazoea mazuri ya kujifunza kibinafsi wakiwa peke yao.​—Kumbukumbu la Torati 6:4-9.

22. Unawezaje kumfunza mtoto wako atoe sala zenye maana?

22 Kama inavyoonyeshwa na jambo lililoonwa katika ukurasa wa 16, sala ya kutoka moyoni ya urafiki wa karibu sana inajenga uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Msaidieni mtoto wenu ajifunze juu ya uhitaji wa kusali na namna ya ‘kuufunua moyo’ wake kwa Yehova. (Zaburi 62:8) Acheni mtoto wenu azisikie sala zenu za kutoka moyoni. Kwa kumweleza namna Yehova amejibu sala zenu na kwa kumtia moyo mtoto atazamie sali zake mwenyewe zijibiwe, mtoto huyo atatambua kwamba sala zina nguvu.

23, 24. (a) Kwa sababu gani mtoto anapaswa kufunzwa kumwogopa Yehova? (b) Wazazi wanapaswa kufanya kazi kwa ukawaida na nani katika huduma ya shambani, na kwa sababu gani?

23 “Urafiki wa karibu zaidi na Yehova ni wa wale wanaomwogopa yeye,” ndivyo alivyoandika Mfalme Daudi. (Zaburi 25:14, NW) Ili mtoto wenu asitawishe kweli kweli uhusiano wa karibu zaidi na Mungu, lazima awe na woga unaofaa wa matokeo yenye kutisha sana ya kumchukiza “Mungu aliye hai.” (Waebrania 10:31; Mithali 8:13) Ni kweli kwamba lazima mtoto huyo ampende Yehova na kuthamini sana fadhili za upendo na wema Wake, lakini vilevile lazima aheshimu kwa uzito uwezo wa Yehova wa kuadhibu au kuruhusu mtu ‘avune alichopanda.’ (Wagalatia 6:7) Ikiwa ‘woga’ huo unaofaa unasitawishwa tangu umri mchanga, mtoto huyo atasitawisha dhamiri nzuri. Mahali pa kufikiri, ‘Ni sawa, mradi sikamatwi,’ yeye atakuwa na maoni kama ya Yusufu, ambaye alipinga kishawishi cha kufanya uasherati na kusema: “Nifanyeje ubaya huu mkubwa nikamkose Mungu?”​—Mwanzo 39:7-9.

24 Kwa kufanya kazi pamoja katika huduma ya Kikristo, mtamsaidia mtoto wenu asitawishe kupendezwa kule kule kwa upole na watu aliko nako Yehova. Kwa kadiri mtoto huyo anavyokuza kuthamini kwake, moyo wake utaona namna unavyoweza ‘kutajirisha wengi’ kwa kuwafundisha “habari njema” zinazoweza kutokeza mabadiliko yenye faida katika maisha yao. Huduma hiyo vilevile ni msaada mzuri wa kusitawisha uhusiano wa karibu sana Mungu.​—2 Wakorintho 6:10.

WANAHITAJI MSAADA UNAOPITA ULE WA KAWAIDA

25, 26. (a) Kwa sababu gani msaada ‘unaopita ule wa kawaida’ unahitajiwa na wazazi? (b) Msaada huo unatoka wapi? (c) Baba mmoja alifanya nini alipofikiri mtoto wake alikuwa ‘akipotea,’ naye alitambua nini baadaye?

25 “Si rahisi kuwa mzazi wa matineja,” ndivyo alivyosema baba moja Mkristo aliyetaja juu ya hangaiko lake juu ya binti yake wa miaka 16 ambaye amejitenga peke yake na anayekazwa sana na wavulana shuleni. “Mara nyingi ninatoa sala peke yangu na vilevile nikiwa naye​—lakini bado nina wasiwasi.” Kweli kweli, yeye aliona uhitaji wa msaada wa kimungu ambao ungempa yeye na bintiye “uwezo unaozidi ule wa kawaida.”​—2 Wakorintho 4:7, NW.

26 Nyakati nyingine huenda wazazi wakajiona hoi inapoonekana kwamba jitihada zao zote zinashindwa. Walakini usiache! Kwa sababu ya maelekeo ya kupotoka ya mvulana wake, baba mmoja Mkristo alikubali kwamba ilipofikia hatua fulani alikuwa na maoni ‘amempoteza’ mwanaye, ambaye alikuwa amemlea katika mafundisho ya Ukristo tangu utoto. “Nilipiga magoti na nikatoa sala mpaka machozi yakatiririka juu ya uso wangu, na nikamsihi Yehova anisaidie,” ndivyo alivyosema baba yake. “Yehova alijibu sala hizo na polepole mvulana huyo akaanza kubadilika kuwa mzuri. Hakika nilimkaribia zaidi Yehova nilipouona mkono wake ukitenda katika jamaa yangu.” Ndiyo, mtumaini Yehova atoe msaada; mtegemee. Toa sala pamoja na watoto wako na uwaombee. Uone mkono wa Yehova ukitenda kazi katika jamaa yako.​—1 Wathesalonike 5:17.

27. (a) Ni nani anayepaswa kuiandika sheria ya Mungu juu ya moyo wa mtoto? (b) Ninyi wazazi mnaonaje mtoto wenu anapoonyesha kwamba moyo wake ‘umekuwa na hekima’?

27 Tambua kwamba mwishowe mtoto lazima aziandike sheria za Yehova juu ya moyo wake mwenyewe. (Linganisha Mithali 3:1-4.) Walakini fanya yote uwezayo ukiwa mzazi uufikie moyo wa mtoto wako. Ni thawabu kama nini kumwona mtoto huyo akibaki mshikamanifu kwa ile kweli! Ni sababu kubwa kama nini ya ‘kuufurahisha moyo wako’ watoto wako wakionyesha kwamba mioyo yao ‘imekuwa na hekima’! (Mithali 23:15) Utakuwa kama mtume Yohana ambaye angeweza kusema hivi juu ya watoto wake wa kiroho: “Sina furaha iliyo kuu kuliko hii, kusikia ya kwamba watoto wangu wanakwenda katika kweli.”​—3 Yohana 4.​—Kutoka The Watchtower, Novemba 1, 1981.

[Maelezo ya Chini]

a Nyakati nyingine “Shauri,” maana yake ni kusudi.​—Ona Isaya 29:15; 46:10.

b Kwa mapendekezo halisi juu ya mazungumzo ya namna hiyo, ona kitabu Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha, kur. 122-124, pamoja na makala “Baba Aongea na Watoto Wake wa Kiume,” na “Mama Aongea na Binti Zake,” zilizotokea katika Amkeni! ya Machi 1977 na Aprili 1977.

c Kilichochapishwa na Sosaiti.

Kwa kujikumbusha wewe unaweza kuyajibu maulizo haya?

■ Katika kuwazoeza watoto, kwa sababu gani ni jambo la lazima kufikia moyo?

■ Kwa sababu gani wazazi wanapaswa kuzungumza mambo yanayohusu ngono pamoja na watoto wao?

■ Ulinzi mkubwa wa mtoto juu ya mwenendo mchafu wa ngono ni nini? na ni nini kitakachosaidia kusitawisha ulinzi huo?

■ Mtoto anawezaje kufunzwa atoe sala zenye maana?

■ Kwa sababu gani wazazi Wakristo wanapaswa kufanya kazi kwa ukawaida pamoja na watoto wao katika huduma ya shamani?

[Blabu katika ukurasa wa 19]

‘Wazazi wangu hawakuzungumza waziwazi pamoja na mimi habari za ngono. Kulikuwako mambo mengi sana niliyotaka kujua. Nikawa mtafiti sana, mjinga na asiye na ulinzi.’​—Msichana mmoja wa miaka 15

[Picha katika ukurasa wa 20]

Kupashana habari kati ya mzazi na mtoto ni kwa maana sana

[Picha katika ukurasa wa 21]

Kwa kutumia vifaa vya kujifunza Biblia, mzazi anaweza kutoa mashauri juu ya ngono

[Picha katika ukurasa wa 22]

Kushiriki pamoja katika huduma ya shambani kunamsaidia mtoto wako akue kiroho

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki