Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 8/15 kur. 21-26
  • Zoeza Mtoto Wako Asitawishe Utawa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Zoeza Mtoto Wako Asitawishe Utawa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Upashanaji Habari wa Kutoka Moyoni
  • Kazia Chakula cha Kiroho
  • “Kufanya Yehova Awe Halisi”
  • Uhitaji wa Nidhamu ya Upendo
  • Taabu Inapoingia
  • Kazi Ngumu—Lakini Inastahili!
  • Wazazi, Fikieni Moyo wa Mtoto Wenu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Zoeza Mtoto Wako Tangu Utoto Mchanga Sana
    Siri ya Furaha ya Familia
  • Kulea Watoto tangu Uchanga
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
  • Ubora wa Kutia Adabu katika Upendo
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 8/15 kur. 21-26

Zoeza Mtoto Wako Asitawishe Utawa

“Mzoeze mvulana kulingana na njia inayomfaa; hata anapokuwa mzee hataiacha.”​—MITHALI 22:6, New World Translation.

1. Ni nini kinachopasa kufikiwa ili kumzoeza mtoto kwa mafanikio, na kwa sababu gani?

MTUMBUIZAJI mmoja wa sarakasi akijaribu kumfundisha mwanaye ufundi wa pembea aliona anatatizwa kuviruka vyuma. “Kama utautupa tu moyo wako juu ya vyuma,” mwanamke huyo akapendekeza, “mwili wako wote utafuata.” Hali moja na hiyo, wale ‘wanaozoeza’ mtoto wao asitawishe utawa ni lazima wauguse moyo. Hilo ni jambo gumu wakati wa miaka ya utineja (ujana). Mithali 4:23.

2. Ni kwa sababu gani miaka ya ujana ni migumu, na wazazi wanaweza kusaidiaje?

2 “Kwa miaka mingi halikuwa jambo gumu kujua yaliyokuwa yakiendelea ndani ndani ya wavulana wangu,” akasema baba mmoja Mkristo katika Ujeremani. “Lakini hilo lilibadilika kama umeme mara tu walipobalehe.” Wakati huo wa kubadilika kuwa mtu mzima, tamaa nyingi mpya na zenye kusisimua, zikichochewa na mwili na mabadiliko ya mwili na ya hormoni, zinageuza moyo wa kijana. Hata hivyo mara nyingi miaka hiyo inaharibiwa na makosa yenye maumivu. Hata Ayubu mwaminifu alihuzunishwa na kufikiria “matokeo ya makosa ya ujana [wake].” (Ayubu, 13:26, NW) Mikazo ya maono ya ndani inaweza kutokeza “uzito katika moyo” wa kijana. Andiko la Mithali 12:25 linasema kwamba hilo linaweza kusababisha moyo ya mtu uiname; bali neno jema huufurahisha.’ Unaweza kumsaidiaje mtoto wako kuwe upashanaji mzuri wa habari wakati wa miaka hiyo ya hatari?

Upashanaji Habari wa Kutoka Moyoni

3, 4. (a) Njia za kushauri ambazo Elihu alitumia, na zile za “marafiki” watatu wa Ayubu zilitofautianaje? (b) Ni nini kitazuia upashanaji habari wa kutoka moyoni?

3 Fikiria tofauti ya njia ya kushauri ya Elihu na ile ya “marafiki” watatu wa Ayubu. Kufanya hivyo kutaonyesha wazi ni nini yatafanyiza upashanaji habari uwepo na yale ambayo yatauzuia. Elihu alikuwa msikilizaji mzuri. Ingawa wale wengine walibaki wakiwa wanajikweza, wasikubali kamwe udhaifu wao wenyewe wa kibinadamu, yeye alisema: “Tazama, mimi ni mbele ya Mungu kama ulivyo wewe; mimi nami nilifinyangwa katika udongo.” Alimsihi Ayubu ‘ajibu,’ aseme yaliyokuwa moyoni mwake, wala asihofu. (Ayubu 33:5-7) Kwa upande mwingine, wale “marafiki” watatu walijionyesha wanamsikitikia Ayubu na kumfariji, lakini walisikiliza wakiwa wamekwisha kuamua mambo. “Sikieni sasa basi hoja zangu, mkayasikie mashindano ya midomo yangu,” akasihi Ayubu bila matokeo yo yote. (Ayubu 13:6) Ndiyo, njia waliyotumia ilikuwa imetokeza kizuizi.

4 Asipokuwa mwangalifu, mzazi anaweza kutokeza vizuizi vya namna hiyo bila kujua. Kwa hiyo msikilize mtoto wako. (Mithali 18:13) Fikiria kwa uangalifu jinsi jibu lako litakavyochukuliwa. “Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga; bali ulimi wa mwenye [hekima] ni afya.” (Mithali 12:18) Ni kweli, nyakati nyingine nia na/au maneno ya kijana huenda yakaudhi. Lakini kumbuka, sababu ya “maneno makali” hayo yaweza kuwa moyo uliojaa mvurugo. Kwa kufikiri tumia ulimi wako uponye.​—Ayubu 6:2, 3.

5. (a) Ni nini kitasaidia mzazi ayatoe nje makusudio ya moyo wa mtoto? (b) Kurejezea vitabu vya Sosaiti vya miaka iliyopita kunaweza kusaidiaje?

5 Kusikiliza kwa makini ambako kunatia ndani maswali ya busara, kutasaidia kumfanya mtoto atoe ya moyoni na kufanya iwe rahisi zaidi kwake kuzungumza juu ya jambo linalomsumbua. (Mithali 20:5) “Nyakati nyingi mwana wangu angeanzisha mazungumzo wakati ulioelekea kuwa usiofaa na kusema kifupi tu, labda juu ya kisa fulani shuleni,” akasema mama mmoja wa kijana wa miaka 18. “Lakini ilikuwa juu yangu ‘kuyatoa’ yaliyokuwa moyoni mwake kwa fadhili nikitumia maswali kama, ‘Halafu ikawaje?’ Au, ‘Ulionaje juu ya hilo?’ Au, ‘Ulifanya nini au ulisema nini?’ Alikuwa akitaka hivyo, naye alieleza wazi tatizo lake. Lakini hiyo ilichukua wakati mwingi!” Tumia wakati huo pamoja na mtoto wako! Labda wakati wa safari ndefu ya kutembea kwa miguu au mnapostarehe pamoja, yajue yaliyomo akilini mwake. Wazazi wengi wameona kwamba, kwa kurejezea habari zilizotolewa miaka iliyopita katika vichapo vya Sosaiti walisaidiwa wawaelewe vizuri zaidi vijana wao na kuwa na msingi wa mazungumzo ya maana pamoja nao. Kwa sababu hiyo, mazungumzo ya kutoka moyoni yameongezeka kati ya washiriki wa jamaa. Lakini, mengi zaidi ya upashanaji mzuri wa habari yanahitajiwa ili kusitawisha utawa.

Kazia Chakula cha Kiroho

6, 7. Mama yake Timotheo alitimiza nini, na wazazi wanaweza kufuataje mfano wake?

6 Mama yake Timotheo hakukaa tu bila kufundisha mambo ya kiroho yaliyomaanisha uzima kwa mwanaye. Juu yake iliandikwa hivi: “Tangu utoto umeyajua maandiko matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate wokovu.” (2 Timotheo 3:15) Hali moja leo, wazazi wale ambao watoto wao wanasitawisha utawa wanahangaikia sana chakula cha kiroho cha watoto wao. Wanawafundisha kufanya funzo la kibinafsi tangu umri mchanga.

7 Je! umehakikisha kwamba mtoto wako ana vitabu vyake vya Biblia na anajitayarisha kwa ajili ya mikutano ya kundi? Je! unamtia moyo sana aweke ratiba ya wakati wa kuchimbua hazina za Neno la Mungu? (Mithali 2:1-5; 1 Yohana 2:14) Mnapokuwa kwenye mikutano, je, unaketi pamoja naye ili uhimize akili yake​—na moyo​—visitange-tange? Je! yeye anasihiwa ashiriki? (Waebrania l0:23-25) Je! wewe unadumisha funzo la jamaa la kawaida linalotoa maarifa yanayohusu mahitaji hasa ya mtoto wako? Fikiria maswali hayo.​—Mithali 24:5.

“Kufanya Yehova Awe Halisi”

8. Ni wapi ambapo andiko la Kumbukumbu la Torati linaonyesha utawa unapasa kuanza, na wazazi wanakufuatishaje hilo kwa mtoto leo?

8 Hata hivyo, kujaza tu akili na mambo ya hakika kwaweza kuacha moyo na dhamiri vikiwa havijaguswa. Ili kusitawisha dhamiri njema, ni lazima mtoto wako aone kwamba Yehova ni mwenye nguvu na mwenye kupendezwa sana na yeye na mambo anayofanya. Lakini kwanza ni lazima kumpenda Yehova kujae moyo wako mwenyewe kisha kukusukume wewe useme kwa ukawaida juu ya ulinzi wake wa upendo na ukuu wake. Ni lazima upende ukweli na kuishi kupatana nao. Alipoulizwa jinsi watoto wake, wote wawili wakiwa ni waevanjeli wa wakati wote, walivyositawisha upendo mwingi kwa ajili ya Mungu, mama mmoja katika Uingereza alieleza hivi: “Kwa kusema nao juu ya jinsi Yehova alivyo halisi. Yeye amenisaidia sana hata sikuwa na jingine ila kufanya Yehova awe halisi kwao. Kila jambo linamtegemea yeye.” Zoeza mtoto wako, pia, kuzungumza na Yehova “kwa sala zote na maombi [asali] kila wakati katika [roho].” (Waefeso 6:18) Mruhusu mtoto asikie sala zako za bidii, za kutoka moyoni na kuzungumza naye mambo yaliyomo katika sala zake mwenyewe.​—Kumbukumbu la Torati 11:1, 2, 18, 19; Mithali 20:7.

9. Wazazi wanaweza kutumiaje mifano halisi maishani wazoeze dhamiri ya mtoto?

9 Dhamiri ya kijana inaweza kuvutwa kwa nguvu sana na mifano halisi ya maisha. (Linganisha 1 Wakorintho 8:10.) Pindi kwa pindi huenda ukasikia juu ya watu mmoja mmoja wanaoteseka kwa sababu ya kuvunja sheria za Mungu. Kwa njia ya kutoshtaki, zungumza mifano hiyo pamoja na mtoto wako, kwa njia hiyo umsaidie kuthamini maneno ya Paulo: “Huwezi kumpumbaza Mungu. Cho chote unachopanda utakivuna.” (Wagalatia 6:7, Beck) Kuhusu mfano unaofaa, zungumzeni masimulizi yenye kugusa moyo ya Injili juu ya maisha ya Yesu. Utakuwa ukimsaidia mtoto wako kuwa na “akili ya Kristo.” (1 Wakorintho 2:16, NW) Lakini ni lazima uyafanye masimulizi hayo yawe yenye uhai! Mtie moyo mtoto apige picha akilini tamasha zenye kutazamisha na kufikiria njia ya ustadi ambayo Yesu alitumia ashughulikie mambo. Chagua habari katika vichapo vyenye msingi wa Biblia vinavyoeleza kirefu maisha ya Yesu na sifa za kibinafsi, na kuongeza namna tofauti tofauti, uzitumie pindi kwa pindi kwenye funzo la jamaa yenu.a

10. Unaweza kumsaidiaje mtoto wako ‘aujue upendo wake Kristo’?

10 Pia ni lazima mtoto wako ajitahidi kufuata mfano wa Kristo. Ndipo tu kwa mambo halisi kijana ataweza “kuujua upendo wake Kristo, upitao ufahamu.” (Waefeso 3:19) Kwa hiyo, mtie moyo afuate zaidi mfano wa Yesu wa kuchukia uovu, kupenda kwake watu, bidii yake kwa ajili ya ibada ya Babaye, rehema na moyo mkarimu wake, na nia yake ya kuvumilia dhihaka. (Waebrania 1:9; Marko 6:34; Yohana 4:34; Luka 23:34; 1 Petro 2:23) Sifu kwa uchangamfu mtoto wako anapoitikia. Ni lazima aone kwamba, ingawa sisi si wakamilifu, kwa kadiri tunavyofuata karibu-karibu sana kielelezo cha Bwana ndivyo tunavyokuwa wenye furaha zaidi na ndivyo dhamiri zetu zinavyokuwa chonjo zaidi. Pia tunamkaribia Mungu zaidi, kwa kuwa Yesu anaonyesha utu wa Babaye. (Yohana 14:6-10) Sikuzote mkumbushe mtoto wako ubora wa uhusiano huo. Ni kama mama mmoja Mkristo mwenye watoto wanne ambaye amefanikiwa alivyosema: “Mume wangu haachi kamwe siku moja ipite bila kuweka mkono wake juu ya kila mmoja na kuwaambia jinsi anavyowapenda sana na kwamba anajua Yehova anajivunia mwenendo wao. ‘Yehova anawapenda ninyi,’ ndivyo anavyosema. ‘Msimvunje moyo.’​—Mithali 27:11.

Uhitaji wa Nidhamu ya Upendo

11. Ni kwa sababu gani kila mtoto anahitaji nidhamu?

11 Ajapofundishwa na Mungu “tokea ujana [wake],” bado Daudi alisihi, “Usiyakumbuke makosa ya ujana wangu, wala maasi yangu.” (Zaburi 71:5, 17; 25:7) Ndiyo, kila mtoto “amefungiwa ujinga ndani ya moyo.’ Lakini “fimbo ya adhabu [nidhamu] itaufukuzia mbali.” (Mithali 22:15) “Fimbo” hiyo ya mamlaka ya kimzazi mara nyingi yaweza kuwa neno la kusahihisha au kizuizi imara. Kwa hiyo moyo wenye hila wa mtoto wako unapotamani kufanya jambo lenye kudhuru, kuna uhitaji wa kuwa imara kukataa!—Yeremia 17:9; Mithali 29:17, 19, 21.

12, 13. Unaweza kufanyaje nidhamu iwe na matokeo?

12 Katika kutoa nidhamu, hasa wakati wa kutoa adhabu, fuata kielelezo cha Yehova ambaye ‘anasahihisha kulingana na yaliyo sawa.’ Andiko la Isaya 28:26-29 (NW) linaonyesha kwamba yeye ni kama mkulima anayetumia ufahamu kuamua ni chombo gani atatumia ili apure kwa njia yenye matokeo aina tofauti tofauti za nafaka na ni kwa muda gani atapura, wala si ‘kuikanyaga-kanyaga bila kukoma.’ Kwa hiyo jiulize: Je! kizuizi hicho ni cha kadiri nikifikiria umri wa mtoto wangu na maendeleo yake kuelekea kukomaa? Je! adhabu hiyo inapatana na uzito wa kosa na inafaa wala haitolewi tu kwa sababu ya jinsi ninavyojisikia wakati huo tu? Na je, mtoto anajua ni kwa sababu gani hasa anaadhibiwa?​—Ayubu 6:24.

13 Vizuizi visivyo vya kadiri au visivyopatana na nidhamu vitaudhi au kumchokoza mtoto.b (Waefeso 6:4; Wakolosai 3:21) Hata hivyo uthabiti wa upendo utamlinda mtoto wako na hali ambazo zinaweza kuharibu mafundisho yote mema ambayo umeweka moyoni mwake. Hasa hilo ni la maana kuhusu washiriki wake. (Mithali 13:20; 28:7) Lakini iweje baada ya jitihada yote mtoto wako akiingia taabani kweli kweli?

Taabu Inapoingia

14. Ni kwa sababu gani mzazi hapaswi kukata tamaa haraka na kuacha kuzoeza mtoto anapoingia katika taabu kubwa?

14 Hali Ya kukata tamaa yenye maumivu imewafanya wazazi wengine wafanye haraka na kumwacha tu mtoto anayekosa. Ingawa Yehova alitoa adhabu na karipio linalofaa, yeye hakukata tamaa haraka na kuliacha tu taifa la kale la Israeli ambalo wakati mmoja lilikuwa kama ‘mwana’ kwake. (Hosea 11:1; 2 Mambo ya Nyakati 36:15, 16; Zaburi 78:37, Nehemia 9:16, 17) Sawa na ambavyo walimu wa kuzoeza wa kale walivyoweza kufunga vidonda na kutengeneza mifupa iliyovunjika mwanariadha alipoumia, wazazi wanapaswa kujitahidi ‘kunyoosha mikono inayolegea-legea, ili kilicho na kilema kisiteguke bali badala yake kiponywe.’​—Waebrania 12:12, 13, NW.

15. Mzazi anaweza kutumiaje andiko la Wagalatia 6:1 katika kumrudisha mtoto aliyekosa?

15 Kunyoosha mtoto ambaye ni “kiwete” kiroho na kuzuia hali yake isiharibike zaidi kunataka kurekebisha kufikiri kwa mtoto. Hata ingawa mtu [au mtoto] achukua hatua fulani ya uwongo kabla ya yeye kuijua,” akashauri Paulo, “ninyi mlio na sifa za kiroho jaribuni kumrekebisha upya mtu huyo katika roho ya upole.” (Wagalatia 6:1, NW) Neno la kigiriki linalotafsiriwa ‘rekebisha’ lilikuwa usemi wa kitiba uliotumiwa wakati wa Paulo kuhusu ‘kutengeneza mifupa iliyovunjika.’ Bila shaka tendo hilo lenye uchungu lilitaka ufundi mwingi sana ili kuzuia mfupa uliovunjika usiwe kasoro ya maisha yote. Neno ilo hilo linatafsiriwa ‘kutengeneza’ (nyavu). (Marko 1:19; 1 Wathesalonike 3:10) Ili “kutengeneza” moyo wa kijana, jitahidi kumfikia kwa “ustadi wa kufundisha.” Badala ya kupigana kwa maneno, fuata pendekezo la maana sana la Biblia: “Kuwa mwanana . . . mvumilivu [chini ya uovu]; [ukiwaonya] kwa upole wale washindanao [nawe], ili kama ikiwezekana, Mungu awape kutubu.”​—2 Timotheo 2:24-26; 3:16; 4:2.

16. (a) Ni marekebisho gani ambayo huenda ikawa lazima kuyafanya ili kumpata tena mtoto aliyekosa? (b) Ni jambo gani analopaswa kuelezwa wazi mtoto?

16 Ili kurekebisha mawazo yenye makosa ya mtoto inataka mzazi azidishe jitihada zake za kuzoeza. Huenda mzazi akahitaji kufanya marekebisho katika mtindo wake wa maisha ili atoe uangalifu unaotakwa. Katika mfano unaoonyesha jitihada inayofaa ya kumpata tena “mwenye dhambi mmoja,” Yesu anasimulia mwanamke aliyeacha karibu kila kitu ili apate sarafu yake ya fedha iliyokuwa imepotea. (Luka 15:7-10) Mtoto aliyezoezwa katika kicho cha Mungu anaweza kukazwa sana na hisia za kutofaa na hatia wakati dhambi yake inapojulikana, kwa hiyo huenda mzazi akahitaji kumthibitishia mtoto upendo wake. Msaidie mtoto huyo aone kwamba ni mwenendo wake unaochukiwa, si yeye mwenyewe, na kwamba mwenendo huo unaweza kusahihishwa.​—Yuda 23.

17, 18. (a) Baba mmoja alimrudishaje mwana wake? (b) Ni jambo gani ambalo kwa kawaida linaleta mafanikio?

17 Baba mmoja, ambaye mwanaye alitiwa nidhamu na kundi kwa ajili ya mwenendo usio wa adili, alianza kutembea safari ndefu pamoja na mwanaye mara kadha kwa juma moja, wakizungumza kirefu na kwa starehe. Pia alichagua vichapo vyenye msingi wa Biblia vilivyoshughulika na mahitaji ya mwanaye hasa. Baba huyo alijifunza vichapo hivyo pamoja naye, zaidi ya kumtia moyo mvulana huyo ashiriki funzo ambalo baba huyo aliongoza pamoja na jamaa yote. Mzazi huyo alirekebisha kazi yake ya kuwa mzee wa kundi ili aangalie kikamili mahitaji ya mwanaye ya kimoyo na ya kiakili. Mvulana huyo alirudishwa.

18 Hata hivyo, nyakati nyingine mwana au binti aweza kuwa mwasi kabisa, hata ‘adharau utii.’c (Mithali 30:17) Kwa furaha, hali hizo zinazopita kiasi ni chache kati ya watu wa Mungu. Inatia moyo kama nini kujua kwamba, ijapokuwa hawaachilii mwenendo wenye kosa, katika hali zilizo nyingi matokeo yanakuwa mazuri wakati wazazi wanapoendelea kuzoeza mtoto bila kukata tamaa haraka, bali kwa subira wanajaribu kuufikia moyo wake!

Kazi Ngumu—Lakini Inastahili!

19. Unaweza kufuataje mfano wa Mariamu katika kutunza jamaa yako?

19 Kulea watoto, hasa katika hizi “siku za mwisho,” ni kazi kubwa kweli kweli. Wazazi wanaochukua daraka hilo kwa uzito wanapaswa kusifiwa! Daima changanua mambo ya maana zaidi. Usiruhusu kamwe hangaiko la kuwapa wapendwa wako “vitu vingi” vya kimwili likuzuie usitumie nafasi za kiroho pamoja nao. Kumbuka, Yesu alimwambia Martha kwamba “kinatakiwa kitu kimoja tu.” Ndiyo, chakula kisicho na vitu vingi kilikuwa kinatosha. Uwe kama Mariamu, aliyefurahia, wakati wenye kupendeza wa kiroho pamoja na Yesu. Chagua “fungu lililo jema” kwa ajili ya jamaa yako kwa kushiriki katika utendaji wa kiroho mkiwa jamaa.​—Luka 10:38-;

20. Ni thawabu gani zinazongojea wazazi Wakristo wenye kufanikiwa?

20 Miaka fulani baada ya kufanikiwa kusaidia watoto wake sita wampende Yehova ,mama mmoja aliye mzazi alipokea kadi kutoka kwa mmoja wao. Kwa sehemu ilisema hivi “Mama, nakupenda sana sana, zaidi ya kiasi ambacho hutaweza kujua wakati wo wote. Asante kwa kunipa mwelekezo na uongozi... Ulinipa tumaini bora zaidi ulimwenguni na hilo ni ukweli. Asante kwa kuokoa uhai wangu.” Jinsi mama huyo alivyofurahi! Ni kama Mithali 23:24, 25 (Today’s English Version) inavyosema: “Unaweza kujivunia mwana[au binti] mwenye hekima. Acha baba na mama yako wajivunie wewe; mpe mama yako furaha hiyo.” Kwa msaada wa Yehova, furaha hiyo na iwe yako!

[Maelezo ya Chini]

a Ili upate muhtasari wa maisha ya kidunia ya Yesu, ona makala “Ushike Sana Uzima Ulio Kweli Kweli,” katika toleo la Julai 1,1973 la Mnara wa Mlinzi. Makala “Iweni Wanafunzi wa Kweli wa Kristo,” katika toleo la Desemba 1, 1977 la Mnara wa Mlinzi, inazungumza nyingi za sifa zake binafsi, na pia ndivyo kinavyofanya kitabu Aid to Bible Understanding (kilichochapishwa na Sosaiti yetu), kurasa 927-932.

b Uchunguzi unaohusu vijana 417 uliochapishwa katika gazeti Adolescence ulimalizia hivi: “Nyumba yenye vizuizi vingi sana inaongoza kwenye kukata tamaa halafu kwenye ugomvi, nayo nyumba yenye kuendekeza sana inaongoza kwenye kukatisha tamaa, kwa kutokujua matazamio ya wazazi ni nini, jambo ambalo kisha linaongoza kwenye ugomvi, kwa kutafuta viwango.”

c Ona “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) wa Mei 1, 1960, kurasa 287,

Unasemaje?

◻ Mzazi anaweza kufanyaje ili upashanaji habari wa kutoka moyoni pamoja na mtoto uwe bora zaidi?

◻ Ni nini kitakachomsaidia mtoto asitawishe dhamiri njema?

◻ Ni nini kitakachofanya nidhamu iwe na matokeo?

◻ Mtoto mwenye kukosa anaweza kurudishwaje?

[Picha katika ukurasa wa 22]

Kusikiliza kwa makini, hata isipokufaa, kutatia moyo kuwe upashanaji habari wa kutoka moyoni

[Picha katika ukurasa wa 24]

Ni jambo la kushindaniwa kweli kweli kumhakikishia mtoto kuwa unampenda na kuufikia moyo wake anapokuwa amefanya kosa zito

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki