Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 1/1 uku. 23
  • Historia ya Kisasa ya Mashahidi wa Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Historia ya Kisasa ya Mashahidi wa Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • KUENDESHA KAZI BAADA YA MKATABA WA KUACHA VITA
  • NJIA NYINGINE ZA KUGAWA
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 1/1 uku. 23

Historia ya Kisasa ya Mashahidi wa Yehova

(Inaendelezwa)

KUENDESHA KAZI BAADA YA MKATABA WA KUACHA VITA

Baada ya kutiwa sahihi kwa mkataba wa kuacha vita katika Juni, raia wengi wa Ufaransa waliokuwa wamekimbia majeshi ya Hitler walirudi manyumbani mwao. Ndugu Geiger alirudi Paris (mji mkuu wa Ufaransa). Aliishi pamoja na mkewe na mwanawe katika chumba cha orofani, naye alifanya kazi ya kimwili katika kampuni ya uhandisi wakati wa mchana, hali akitumia jioni na mwisho wa juma kuongoza kazi ya kutoa ushuhuda na kutembelea akina ndugu. Akieleza juu ya kuendesha kazi ya siri-siri katika upande wa kaskazini wa Ufaransa katika Septemba 1940, Ndugu Geiger aliandika hivi:

“Barua zote zilifunguliwa na askari wa Gestapo. Kwa hiyo lilikuwa jambo la lazima kutembelea kila kikundi na kila ndugu aliye peke yake wewe mwenyewe. Akina ndugu walikutana pamoja katika vikundi vidogo kwa ajili ya mafunzo yao ya ‘Mnara wa Mlinzi’ na mikutano ya utumishi. Waliendelea kuhubiri habari njema nyumba kwa nyumba wakiwa Biblia peke yake. Walipokuta watu wenye kupendezwa, walirudi wakiwa na vitabu na kuongoza mafunzo.”

Katika Paris, vitabu vilikuwa vimefichwa wakati wa marufuku navyo vilikuwa vimewekwa akiba katika sehemu mbalimbali.

Gazeti Mnara wa Mlinzi lilipelekwaje kisiri mpaka kwa Ndugu Geiger na Delannoy katika Paris? Chombo ambacho Yehova alitumia kutimiza jambo hilo alikuwa ndugu mmoja mnyenyekevu na mwenye kiasi, Henri Germouty. Anasimulia hivi:

‘Mji wa Moulins ulikuwa katika mstari uliogawanya kati ya eneo lenye kukaliwa na majeshi yenye kuteka na lile lisilokaliwa nayo. Mstari huo wenye kugawanya ulikuwa unalindwa na walinzi Wajeremani ambao walikuwa wakimpiga risasi mtu ye yote aliyejaribu kupita bila ruhusa. Walakini katikati sehemu hii mstari wenye kugawanya ulipita katikati ya mji, ambapo dada Mpolandi alikuwa akiishi naye alizungumza Kijeremani. Nilikuwa nikizuru nyumbani mwake, kisha alikuwa akiondoka nyumbani mbele yangu na kuvuta fikira za mlinzi huyo huku mimi nikipita mstari huo.

Kisha nilikuwa nikipanda gari-moshi, walakini kabla haijafika Paris abiria wote walikuwa wakipekuliwa, wanaume wakipekuliwa na wanaume na wanawake na wanawake. Lakini nilikuwa najua ni katika sehemu gani walikuwa wanaanza kufanya upekuzi huo, kwa hiyo kabla hatujafika hapo nilikuwa nikiruka kutoka katika gari-moshi katika mahali lilipokuwa likipunguza mwendo. Nilikuwa nikisafiri usiku na baada ya kuruka kutoka gari-moshi nilikuwa nikijificha mpaka kupambazuke na kisha kumaliza safari hiyo kwa kutembea.”

Mara tu lilipofika Paris, gazeti Mnara wa Mlinzi lilitafsiriwa, kisha Dada Gendreau alikuwa akichapa stenseli ili kwamba hati iweze kunakliwa kwa mashine ya kunakili. Kisha nakala zilikuwa zinapelekwa kwa akina ndugu katika majimbo. Ndugu Samuel Nongaillard anaeleza namna gazeti hilo lilivyokuwa likipelekwa kisiri mpaka kaskazini ya Ufaransa:

“Wakati wo wote ilipowezekana, ndugu mmoja kutoka Paris alikuwa akipanda gari-moshi mpaka mji wa Peronne, ambako mstari wenye kugawanya kati ya sehemu mbili za kijeshi za Wajeremani ulipitia. Ndugu mwingine alikuwa akisafiri mpaka kwenye mji huu kutoka kaskazini nayo magazeti yalikuwa yakipokezanwa kati yao juu ya jukwaa la kituo cha Peronne.”

Kwa kawaida, karatasi zikiwa zimepunguka nazo njia za kusafiria zikiwa zenye hatari sana, haikuwezekana kunakili kwa mashine ya kunakili na kutuma nakala ya Mnara wa Mlinzi kwa kila mhubiri. Ndugu waliokuwa wakitumika kama matarishi, wakiwa wanahatirisha maisha zao, wangeweza kuficha mwilini mwao nakala moja au mbili. Hiyo ilimaanisha kwamba wakati nakala moja ya makala ya Mnara wa Mlinzi ilipofika sehemu fulani, kunakili kwingi kulifanywa ili kwamba kila kikundi kidogo cha wahubiri kipate angaa nakala moja yenye chakula cha kiroho chenye maana. Dada Dina Fenouil, ambaye wakati huo alikuwa akiishi katika eneo la Lyons, aeleza hivi:

“Nilikuwa nimepewa mgawo na kuchapa nakala 10 za ‘Mnara wa Mlinzi.’ Niliweza kuchapa nakala tano wakati mmoja, hiyo ilimaanisha kuchapa kila ‘Mnara wa Mlinzi’ mmoja mara mbili. Kwa kuwa kila toleo lilikuwa na kurasa 14 zenye nafasi iliyo kati ya mstari iliyo kati ya mstari mmoja na mwingine [inayolingana na ya gazeti hili], nililazimika kuchapa kurasa 28 kila wakati mmoja. Mara baada ya kumaliza kuchapa toleo moja lile lingine lilikuwa limekwisha fika. Nilifanya hivyo muda wote wa vita. Kila kikundi kilikuwa na nakala moja ya makala ya ‘Mnara wa Mlinzi.’”

Lenye kuonyesha hatari ambayo ilikabiliwa mara nyingi katika kufikisha hati hizi kwa akina ndugu ni jambo lililoonwa na Ndugu Stanis Sikora, aliyekuwa anasimamia kikundi cha ndugu wenye kuzungumza lugha ya Kipolandi katika Saint-Denis, kiunga cha mji kaskazini mwa Paris, Yeye anasimulia hivi:

“Asubuhi moja nilikuwa napeleka nakala ya ‘Mnara wa Mlinzi’ iliyoandikwa kwa mkono kwenye kikundi kingine nilipoona kikundi cha askari Wajeremani wakiwa mbele ambao walikuwa wakimsimamisha kila mtu na kumpekua. Nikaendelea kupanda juu ya baisikeli yangu nami nikaamua kuendelea kuiendesha polepole na kupita. Nikafika kilipokuwa kikundi cha kwanza cha askari nao hawakufanya lo lote kunisimamisha. Nikaendelea kuiendesha pole-pole nao askari waliokuwa kwenye kizuiaji wakaniacha nipite. Nikaendelea kuienedesha kwa mwendo uo huo hata nilipoweza kuingia katika barabara nyingine, na kisha nikaiendesha mbio kweli kweli! Yehova hulinda kazi yake.”

NJIA NYINGINE ZA KUGAWA

Wajeremani walipoteka sehemu iliyobaki ya Ufaransa katika Novemba 1942 Mnara wa Mlinzi wa Kiingereza ukawa haupokewi katika Ufaransa wala Uswisi. Hata hivyo, afisi ya Uswisi ilifaulu kupata nakala ya Mnara wa Mlinzi katika lugha ya Kiswedi. Dada Alice Berner alijifunza haraka Kiswedi cha kutosha kuweza kutafsiri makala ya Mnara wa Mlinzi katika Kijeremani. Tafsiri hizo za Kijeremani zilifikishwa Ufaransa nazo zikatafsiriwa katika Kifaransa.

Kutoka kitabu cha Mwaka cha 1980

(Habari hii itaendelezwa katika toleo linalofuata)

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki