Wakati Ujao Kwa Washikamanifu wa Mungu
“Yehova ni mwenye haki; yeye anapenda matendo ya haki. Wanyofu ndio Watakaouona uso wake.” Maneno hayo ya Mfalme Daudi yanapatikana katika Zaburi ya 11, mstari wa 7, NW. Na leo, ni wakati ujao wenye utukufu kama nini unaowangojea wale wanaofanya matendo matakatifu katika utumishi wa Mungu! Ufunuo sura ya 7 unawaeleza “mkutano mkubwa . . . watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha,” unaookoka vita ya mwisho ya Har–Magedoni. Mungu atanda “hema” yake juu yao, akiwavuta watumishi hao walio wakf kwenye uhusiano wa karibu sana pamoja naye.—Ufu. 7:9-17.
Mungu wetu mwenye upendo hataki sisi tuharibiwe pamoja na waovu katika siku Yake ya kisasi. Yeye anataka tupate wokovu. Na ili atutie moyo katika jambo hilo, yeye anatoa katika Biblia njozi tukufu ya kiunabii ya “mbingu mpya na dunia mpya.” Hiyo dunia mpya itakuwa jamii imara ya kibinadamu, iliyounganishwa kwa upendo wa kimungu chini ya “mbingu mpya” ambazo washiriki wake ni Kristo Yesu na watawala wenzake 144,000. Watiwa mafuta hao wote watakuwa wamekwisha kujionyesha wenyewe kuwa washikamanifu kwa Mungu wakiwa hapa duniani, nao watakuwa wamekwisha fufuliwa watawale pamoja na Kristo katika ufalme wake wa kimbinguni. Mabilioni ya wanadamu wataliona kuwa jambo rahisi kuwatumaini kabisa watawala hao waliojaribiwa.—Ufu. 14:1, 4, 5; 20:6; 21:1, 2.
Je! tulisema mabilioni ya wanadamu hapa duniani chini ya utawala wa Ufalme? Ndiyo, mabilioni! Kwa kuwa huo ndio utakaokuwa wakati mzuri sana wa kufufuliwa kwa wafu waingie kwenye paradiso ya kidunia. (Luka 23:43, ZSB) Itakuwa furaha kuu kama nini kati ya hao waliofufuliwa kuweza kufunguliwa wasiwe tena mateka wa mauti! Machozi, kuomboleza, kilio, maumivu—hata kifo kilichorithiwa—yote hayo hayatakuwapo tena.—Ufu. 20:11-14; 21:3, 4.
Katika hiyo taratibu mpya, macho ya vipofu yatafumbuliwa yafurahie kuona uumbaji wa Mungu wenye kupendeza sana. Masikio ya viziwi yatazibuliwa yapate kusikiliza muziki wenye kupendeza zaidi kuliko muziki wo wote uliopata kutungwa na wanadamu. Waandikaji wa nyimbo wenyewe watakuwa wakamilifu, nazo nyimbo zao zitamtukuza Yehova na mambo ambayo ametimiza. Ulimi wa bubu utafunguliwa, upate kushiriki katika mazungumzo yenye kufurahisha na katika kusifu Yehova. Vilema watakimbia tena, nayo afya nzuri sana itakuwa ndiyo fungu la wanadamu wote. Baraka hizi zote, na nyingine nyingi, zitawamiminikia wanadamu.—Linganisha Isaya 35:1-6.
Katika taratibu mpya ya Mungu, hakutakuwako wanasiasa wapotovu wenye kuonea, hayatakuwako majeshi yenye kuua na kulemaza, hawatakuwako watu wachoyo wenye kujitakia faida kwa kupandisha sana bei ya mafuta na bidhaa nyinginezo. Madhehebu elfu-elfu ya dini ya Kibabeli hayatakuwapo tena yakiwavuruga watu, wala kumwaga damu isiyo na hatia katika vita vya kidini. Badala yake, wanadamu wote wataungana katika ibada moja ya kweli ya Mungu wetu mwenye upendo, anayetangaza hivi kutoka kiti chake cha enzi cha kimbinguni: “Tazama, nayafanya yote kuwa mapya.”—Ufu. 21:5.
Acheni wote wanaotazamia mbele kwenye mpango huo bora sana wa Yehova washiriki katika kutimiza unabii huu: “Washikamanifu wako watakubariki. Watasema juu ya utukufu wa ufalme wako.”—Zab. 145:10, 11, NW.