Historia ys Kisasa ya Mashahidi wa Yehovah (Ufaransa)
(Imeendelezwa)
Some portions of the yb article were not translated
BAADA YA Petain kutia sahihi mkataba wa amani pamoja na Ujeremani katika Juni 1940, Alsace-Lorraine ilishikamanishwa na Ujeremani. Haikuonwa kuwa “eneo lenye kukaliwa na majeshi yenye kuteka,” bali mahali pake, ilionwa kuwa sehemu ya nchi ya Ujeremani. Hiyo maana yake ilikuwa kwamba mpaka wa kweli uliwekwa kati ya Alsace-Lorraine na sehemu nyingine iliyobaki ya Ufaransa. Kwa hiyo akina ndugu katika Alsace-Lorraine walitenganishwa kabisa na afisi iliyokuwa ikifanya kazi kisiri-siri katika Paris. Walipewaje chakula cha kiroho wakati wa vita?
Wakati Wanazi walipotwaa Alsace, akina ndugu huko walikuwa wakipokea nakala za Mnara wa Mlinzi katika milima ya Vosges ambayo ilitenganisha Ufaransa na AIsace-Lorraine. Waliyafikishaje magazeti kwenye milima hiyo? Ndugu Zingle kutoka Mulhouse, ambaye alikuwa bingwa wa kupanda milima, alienda kuishi huko Saint-Maurice katika Ufaransa yenye kukaliwa na Wajeremani. Alikuwa akipokea Mnara wa Mlinzi wa Kifaransa, ambao alikuwa akipanda nao kwenye kijia cha mlimani Jumapili ya kwanza ya kila mwezi. Alipitia njia yenye mwinuko mkubwa sana yenye miamba ili asikutane na walinzi wo wote wa mpaka. Kwenye upande wa Alsace, akina ndugu wakiwa wamevalia kama watembezi walikuwa wakipanda milima hiyo kuchukua Mnara wa Mlinzi. Kisha gazeti hilo lilitafsiriwa kwenye lugha ya Kijeremani na ndugu wa huko, ambao walifanya kazi hiyo kwa siri sana. Baadaye nakala zilinakiliwa na Ndugu Marcel Graff kwa ajili ya ndugu katika Alsace, nakala fulani zilifika hata kwenye kambi za mateso za Kijeremani mwishowe.
Ingawa kijia hicho cha mlimani kilikuwa cha kufikisha Mnara wa Mlinzi katika Alsace kutoka Ufaransa, baadaye wakati wa vita vitabu ambavyo ndugu Wafaransa hawakuwa navyo vilifikishwa kupitia kwa njia iyo hiyo kutoka Ujeremani mpaka Ufaransa. Hata hivyo, nyakati zote mambo hayakwenda kama ilivyo tazamiwa. Ndugu Marcel Graff anasimulia hivi:
“Siku moja tuliondoka baada ya kupambazuka pamoja na wake zetu ili tupande kwenye milima hiyo. Hali ya hewa ilikuwa nzuri sana. Walakini tulipofika juu, mwendo mfupi kutoka mpakani, ghafula tulisikia, ‘Heil Hitler!’ Alikuwa mlinzi wa mpaka Mjeremani, ambaye aliuliza hivi: ‘Mnaelekea wapi?’
“Nikajibu hivi: ‘Tunatembea tu kwenye milima.’
“Alitutazama kwa kushuku na kusema hivi: ‘Je! hamjui kwamba mu karibu sana na mpaka?’
“‘Kweli?’ tukajibu, tukitenda kama wasiojua.
“Akaongeza hivi kwa haraka: ‘Iwapo mna nia ya kwenda upande mwingine wa Ufaransa, nawaonya kwamba bunduki zetu zimejaa risasi za kweli!’
“Tukaendelea kutembea kuelekea upande wa kisehemu kilichochaguliwa. Mara tu tulipokuwa mahali tusipoweza kuonekana na mlinzi huyo wa mpakani, tulimkuta Ndugu Zingle na mkewe wakitungoja. Tulisalimiana kwa furaha, tukasemezana kifupi na vilevile tukapeana vitabu tulivyokuwa tumebeba. Kisha, baada ya sala, tukaachana.”
Hakika ndugu na dada hao waliotumika kama matarishi walionyesha ujasiri mwingi na upendo mwingi kwa Yehova. Ndivyo pia na wale waliohusika na kunakili vitabu ili vipate kugawa kwa ndugu. Jambo hilo lilifanywa chini ya hali gani?
KUTAYARISHA VITABU VIPATE KUGAWANYWA
Ndugu Adolphe Koehl alikuwa na duka la kunyolea lililokuwa katika barabara kuu ya Mulhouse, katika Alsace, karibu na kituo kikuu. Duka hilo lilikuwa chini ya orofa tano za jumba moja, naye pamoja na Ndugu Graff kila mmoja alikuwa na vyumba katika jengo hilo juu ya duka hilo. Kazi ya kunakili ilifanywa juu ya orofa, huku askari na polisi wakinyolewa na Ndugu Koehl upande wa chini wa orofa! Nyakati nyingine waliponyoka kidogo sana, kama ambavyo Ndugu Graff anavyosimulia:
“Nakumbuka wakati Wanazi walipotwaa radio za wale wote waliokataa ‘kushirikiana’ nao. Nilikuwa nimeuza kisanduku cha barafu cha zamani kwa mtu aliyekuwa akituletea maziwa, naye akasema angerudi aje kukichukua kesho yake. Asubuhi iliyofuata nilikuwa nikisoma nikisahihisha stenseli fulani huku mke wangu akishughulika jikoni. Ghafula mlango ulibishwa hodi. Kwa kuwa tulikuwa tunamtazamia mtu aliyekuwa akituletea maziwa, mke wangu alifungua mlango. ‘Polisi!’ mmoja wa wanaume hao akasema. ‘Mna radio nasi tutaitwaa.’
“Baada ya kugutuka kumtoka mke wangu, alisema hivi kwa sauti kubwa: ‘Fanya haraka!’ Kisha akawaambia polisi hao watatu kwamba nilikuwa mgonjwa na ningevaa nguo haraka iwezekanavyo. Jambo hilo lilinipa wakati wa kukusanya stenseli zangu na kuziweka chini ya kitanda. Nilikuwa nimemaliza kufanya hivyo walipomsukuma mke wangu kando na kuingia chumbani, wakisema ‘Heil Hitler!’ Walipokwenda zao pamoja na radio yetu, tulijawa furaha sana na kumshukuru Yehova Mungu kwa kutulinda kwa mara nyingine.
Siku moja, mwanamume mmoja Gestapo aliyekuwa rafiki, ambaye alikuja kwa ukawaida kwenye duka la kunyolea la Ndugu Koehl apate kunyolewa nywele, alimwuliza hivi ghafula: ‘Herr Koehl, je! ungali unajifunza Biblia?’ Lakini kabla hajajibu, mwanamume huyo Gestapo alimwonya ajihadhari sana kwa kuwa alikuwa anaangaliwa. Alimshauri Ndugu Koehl kwamba kama alikuwa angali na vitabu vyo vyote vilivyopigwa marufuku aviondoe haraka.
Akitenda kulingana na onyo hilo, Ndugu Koehl aling’oa sakafu ya vigae ya duka la kunyolea na kuficha Minara ya Mlinzi chini ya sakafu. Wanazi waliokuwa wanakuja kunyolewa hawakutambua hata kidogo kwamba walikuwa wanatembea centimetres chache juu ya akiba ya magazeti ya Mnara wa Mlinzi yaliyopigwa marufuku! Walakini wakati ukaja nafasi yote iliyokuwa chini ya sakafu ilipokwisha. Vipi sasa?
Ndugu Koehl alikuwa na wazo zuri sana: Dirisha la duka hilo lingekuwa mahali pazuri pa kuficha vitu. Kwa hiyo stenseli zilifichwa nyuma ya kuta za upande za dirisha la duka, nayo Minara ya Mlinzi ilifichwa ndani ya karatasi ngumu za kutangaza bidhaa zilizokuwa zikionyeshwa kwenye dirisha la duka hilo. Kwa hiyo, muda mrefu wa sehemu kubwa ya vita, Wanazi walitazama kwenye dirisha hilo la duka pasipo kujua kwamba karatasi hizo ngumu za kutangaza bidhaa zilikuwa na magazeti ya Mnara wo Mlinzi yaliyopigwa marufuku!
MATARISHI WALIOLIPA KWA MAISHA YAO
Ingawa Ndugu Graff na Koehl walifaulu kuwaepa Gestapo, ndugu wengineo hawakupatwa na mambo mazuri. Katika mwaka 1943 akina ndugu katika Mulhouse walikuwa wakipata nakala za Mnara wa Mlinzi kwa ukawaida kutoka Ujeremani, zikiwa zinaletwa na ndugu wawili kutoka Freiburg im Breisgau. Ghafula, hakuna Minara ya Mlinzi iliyopatikana kutoka upande huo. Ndugu Marcel Graff alisafiri mpaka kwenye mji huo wa Kijeremani, naye akapata kujua kwamba matarishi hao wawili Wajeremani walikuwa wamekamatwa na Gestapo na kukatwa vichwa kwa shoka. Tangu wakati huo kuendelea akina ndugu katika Mulhouse, ambao vilevile walikuwa wakipokea nakala za Mnara wa Mlinzi kutoka Ufaransa, walitengeneza nakala za ziada za Mnara wa Mlinzi wa Kijeremani na kuzipeleka Ujeremani. Kwa hiyo, wakati chanzo kimoja cha chakula cha kiroho kilipofungwa, kingine kilifunguliwa, na ikawa hivyo muda wote wa vita.
Ndugu Jacgues Danner anasimulia hivi:
“Mikutano ilikuwa ikifanywa kila juma, siku tofauti tofauti, nyakati tofauti na katika sehemu tofauti. Ikitegemea kipindi cha mwaka, tulikuwa tunakutana msituni, nyasi za malishoni au katika nyumba, mara nyingi tukiwa tumezunguka meza iliyowekwa tayari kutumiwa kwa kunywa kahawa, nao akina dada wakiwa na nyuzi zilizofumwa kama udhuru. Gestapo hawakutufumania wakati wo wote, wakati wa mikutano hiyo. Akina ndugu walikubali daraka lao nalo hudhurio la mikutano lilikuwa zuri. Wakati mikutano ilipofanyiwa nyumbani mwangu, tulikuwa tunamwacha mtoto wetu mdogo kabisa uwanjani [wa nyumba], nao polisi wakija alikuwa akilia hivi ‘Mama,’ nao waliokuwapo walikuwa wakitokea kupitia kwa shamba la nyumba.”
WATOTO WAJARIBIWA
Ni mambo gani yaliyowapata watoto wakati wa siku hizo mbaya sana za mateso? Je! wangetazamiwa waendelee kuwa waaminifu chini ya majaribu makali ambayo Wanazi waliwaletea?
Mwanzoni mwa kila kipindi cha shule, wimbo wa taifa wa Ujeremani uliimbwa, sala ilitolewa kwa ajili ya Fuhrer (kiongozi) nao watoto walitakiwa waseme ‘Heil Hitler! (wokovu watokana na Hitler) mkono wao wa kuume ukiwa umenyoshwa kuelekea juu. Walakini watoto wa Mashahidi, kama vile Ruth Danner mwenye umri wa miaka minane, walikataa. Yeye alipelekwa mbele ya mwalimu mkuu na waalimu wengine wote na kuhojiwa, walakini alikataa kuwasaliti wazazi wake. Ndugu Jacques Danner anaeleza hivi: “Kila siku, kabla hajaenda shuleni, tulisema sala pamoja nasi tukamshauri amwombe Yehova roho yake na msaada wake mara moja kabla hajahojiwa.” Baadaye Ruth alihamishwa pamoja na wazazi wake na kufungiwa katika kambi sita tofauti za Kijeremani. Baada ya vita, alikuwa painia na kuhitimu katika darasa la 21 la shule ya misionari ya Gileadi katika Amerika.
Vilevile, binti ya Ndugu Arnold, Simone, alifukuzwa katika shule ya masomo ya juu kwa sababu alikataa kusema ‘Heil Hitler!’ Alipelekwa kwenye shule nyingine, ambapo muda si muda aliingia taabani kwa mara nyingine kwa sababu watoto walitakiwa walete shuleni kila juma kipande cha chuma cha zamani kipate kutumiwa kutengeneza silaha. Mwishowe alihukumiwa mbele ya mahakma ya vijana na kupelekwa kwenye shule ya kufundishia tabia katika Constance, Ujeremani, ambapo alipewa mafundisho ya Nazi kwa miezi 22. Walakini aliendeleza ukamilifu! Baadaye, yeye pia alipainia, akahitimu katika Gileadi, na kutumikia kama misionari katika Afrika na kuolewa na Max Liebster, ambaye wakati huo alikuwa mshiriki wa jamaa ya Betheli ya Brooklyn.
WASIOKUWAMO MPAKA KUFA
Katika Agosti 1942, vijana katika Alsace-Lorraine waliitiwa utumishi katika majeshi ya Hitler. Mashahidi wengine, kutia ndani Ndugu Freyermuth, Hofer na Sutter, walilipia kutokuwamo kwao kwa maisha yao. Saa chache kabla hajakatwa kichwa kwa shoka katika jela ya Torgau, Ujeremani, Marcel Sutter mwenye umri wa miaka 23 aliandika barua ifuatayo:
“Wazazi na dada zangu wapendwa sana,
“Mpokeapo barua hii, sitakuwa hai tena. Ni saa chache tu zinazonitenganisha na kifo changu. Nawaomba kwamba mwe na nguvu na wajasiri; msilie, kwa kuwa nimeshinda. Nimeumaliza mwendo na kuendeleza imani. Yehova Mungu anisaidie mpaka mwisho. Ni kipindi kifupi tu kinachotutenganisha na ufalme wa Bwana yetu Yesu Kristo. Karibuni tutaonana tena katika ulimwengu mzuri zaidi wenye amani na haki. Nafurahi ninapowazia siku hiyo, kwa kuwa wakati huo hakutakuwako kupiga kite tena. Litakuwa jambo zuri kama nini! Natamani amani. Wakati wa saa hizi chache una uchungu kidogo ninapowaza sitaweza kuwapiga za mwisho nimekuwa nikiwafikiria nao moyo wangu busu ya kwa heri. Walakini lazima tuwe na saburi. Wakati unakaribia Yehova atakapotetea Jina lake na kuthibitishia viumbe vyote kwamba yeye ndiye Mungu wa pekee wa kweli. Sasa nataka kutoa saa zangu chache za mwisho kwake, kwa hiyo nitamaliza barua yangu na kusema kwa heri mpaka tutakapokutana tena hivi karibuni. Sifa na iwe kwa Mungu wetu Yehova! Pamoja na upendo wangu mchangamfu na salamu,
Mwana wenu mpendwa na ndugu,
Marcel”
AKINA DADA VILEVILE WATUPWA KATIKA KAMBI HIZO
Katika mwaka 1943 akina dada katika Alsace-Lorraine walianza kukamatwa na wengi walipelekwa kwenye kambi ya mateso ya Schirmeck-Vorbruck katika Alsace. Dada Arnold aliweza kupitisha Biblia kisiri, kama anavyosimulia:
“Kwa kuwa nilikuwa natazamia kukamatwa, nilikuwa na nguo ya pekee iliyotengenezwa ishikilie tumbo lenye kuning’inia ambayo ilikuwa na kifuko cha kujazwa kwa hewa. Nilikuwa na Biblia ndogo sana katika kifuko hicho. Waliponipeleka gerezani niliambiwa nivue nguo, walakini mkaguzi alipoona nguo hiyo yenye sehemu nyingi alisema hivi: ‘Ole wangu! hatuna wakati wa kuvua vyote hivyo.’ Kwa hiyo, shukrani kwa Yehova niliweza kuingiza katika kambi ya mateso ya Schirmeck chakula pekee cha kiroho ambacho kwa miezi mingi tungekuwa nacho. Niligawanya Biblia hiyo ndogo kuwa vipande vingi kulingana na hesabu ya dada waliokuwa katika kambi hiyo.”
Hesabu fulani ya akina dada hao walisafirishwa mpaka kwenye kambi za mateso katika Ujeremani, kutia ndani kambi ya mateso yenye kuogopewa sana ya Ravensbruck. Kwa hiyo ndugu na dada wengi, vijana na wazee, walionyesha ukamilifu wao chini ya majaribu makali, wengine wakiutimiliza uaminifu wao kwa maisha yao. Hakika, inaweza kusemwa kwamba historia ya kisasa ya Mashahidi wa Yehova katika Alsace-Lorraine ni kumbukumbu lenye kutukuza jina la Yehova.
KUJIKUSANYA TENA BAADA YA VITA
Utawala wa Nazi ulianguka katika mwaka 1945 navyo vita vikaisha. Hali za maisha katika Ufaransa zilikuwa ngumu kweli kweli, vitu vya lazima maishani vikiwa vichache sana kwa bei rasmi ambazo ziliuzwa, nazo zikiwa zenye gharama kubwa sana katika uuzaji wa magendo. Adui alikuwa amenyang’anya nchi hiyo utajiri wake, akaharibu barabara na reli zake, na kuharibu njia zake za kusafiria. Ilikuwa chini ya hali kama hizo ambazo ndugu na dada waliodhoofika kimwili, walakini wenye nguvu kiroho, walianza kurudi kutoka kambi za mateso.
UPUNGUFU WAKATI WA MIAKA YA VITA?
Huenda ukakumbuka kwamba nyuma katika mwaka 1939, wakati vita ilipoanza, kilele cha wahubiri wa Ufalme 1,004 kilikuwa kimefikiwa katika Ufaransa. Hakika lazima iwe kwamba palikuwapo upungufu wakati wa miaka hiyo migumu ya vita. Sivyo kabisa! Hesabu ya wahubiri iliongezeka maradufu kufikia 2,003 katika Oktoba 1945! Na kama unavyojua, wahubiri hao wapya walianza kuhubiri wakiwa wanahatirisha uhuru wao, na hata maisha yao!
Vilevile hudhurio la Ukumbusho lilipanda juu, kutoka 1,510 katika mwaka 1939 mpaka 3,644 katika mwaka 1945. Hivyo, ingawa ilikuwa imechukua muda wa miaka karibu 40 ya utendaji ili kufikia jumla ya wahubiri 1,004 katika mwaka 1939, ilichukua miaka sita peke yake—miaka yenye magumu ya vita ya ulimwengu ya pili—ili kufanya hesabu iwe maradufu. Hilo ni jambo lenye kutokeza katika historia ya kisasa ya Mashahidi wa Yehova katika Ufaransa, jambo la hakika amblo linashuhudia kwamba Yehova alilinda na kubariki watu wake.
Katika mwaka 1947, Adolphe Weber alikuwa amemaliza mwendo wake wa kidunia akiwa mwaminifu kwa Yehova. Mtakumbuka kwamba alikuwa ndiye yule ndugu Mswisi aliyekuwa ameanzisha kazi katika Ufaransa karibu nusu karne kabla. Katika pindi kadha alikuwa amesaidia ndugu Wafaransa kuzuia tufani za majaribu ambazo zilikuwa zimetikisa shamba lenye kuzungumza Kifaransa. Ndugu wote katika Ufaransa waliomjua Ndugu Weber huzungumza juu yake kwa uchangamfu nao wanajua sehemu yenye maana aliyofanya katika kusitawisha kazi hiyo huko Ufaransa.
LAWA JAMBO LA LAZIMA BETHELI IPANULIWE
Kufikia mwaka 1972 Betheli ya Ufaransa katika magharibi ya kiunga cha mji ya Paris wa Boulogne-Billancourt ilikuwa imekuwa ndogo sana, ikawa lazima ipanuliwe. Sana sana nafasi ilihitajiwa katika idara ya kuweka na kutuma vitabu. Katika mwaka 1959, wakati Betheli ya Boulogne ilipomalizwa, vitabu 85,000 kila mwaka vilitumwa, hali kufikia mwaka 1972 hesabu hiyo ilikuwa imeongezeka kuwa 1,094,231, licha ya vijitabu, fomu na vifaa vingine vilivyochapwa.
Lilielekea kuwa jambo la busara kujenga jumba hilo la upanuzi mahali fulani katikati ya Paris na Le Havre, bandari fulani katika upande wa magharibi wa Ufaransa mahali ambapo vitabu vilifika kutoka Amerika. Katika Novemba 1970, kisehemu cha ardhi chenye urefu wa metres 73 (futi 240) na upana wa metres 33 (futi 108) kilipatikana kwenye mji mdogo katika Normandy unaoitwa Louviers, karibu kilometres 105 (maili 65) mwendo unaolingana ukiwa unatoka Paris au ukiwa unatoka Le Havre. Ilichukua karibu miezi 18 kushinda matatizo ya wasimamizi, na kwa hiyo haki za kisehemu hicho cha ardhi hazikutiwa sahihi mpaka Aprili 28, 1972. Jengo lenyewe lilianzishwa mwezi uliofuata nalo likamalizwa katika Desemba ya mwaka uo huo.
UPANUZI WA PILI WAONGEZWA
Katika mwaka 1973, wakati mpanuko wa jengo katika Louviers ulipozinduliwa, ilidhaniwa ungeangalia mahitaji katika Ufaransa kufikia “dhiki kubwa.” Hata wakati kisehemu cha nchi kiliponunuliwa katika Incarville (kijiji kilicho kando tu ya Louviers) katika mwaka 1974, hakukuwako wazo la kujenga mpanuko wa jengo, ila Jumba la Ufalme tu. Walakini ukuzi wa haraka wa kazi ya Ufalme karibuni ulibadili mawazo yetu. Mwishowe, katika Aprili 2, 1976, kibali kilipatikana cha kujenga jengo lenye orofa mbili lenye nafasi ya sakafu ya metres za mraba 2,483 (futi za mraba 26,727).
Mwishowe mpanuko huo mpya wa jengo ulimalizwa, na siku ya Jumamosi, Mei 13, 1978, Ndugu Raymond Franz alitoa hotuba ya mzinduo katika Kifaransa. Mpanuko wa jengo wa Incarville sasa unatia ndani yake idara ya kuweka na kutuma vitabu na vilevile una makao ya ndugu wa Betheli wanaofanya kazi katika Louviers. Karibu vyumba vyote vya kulala 34 vilivyo katika orofa ya pili na ya tatu vina watu. Kwa wakati huu jumla ya washiriki wa jamaa ya Betheli ni 136, 46 wao wako Boulogne na 90 katika Louviers-lncarville.
MATARAJA YA UKUZI ZAIDI
Watu wangali wanaitikia ujumbe wa Ufalme. Jambo hilo linaonyeshwa na uhakika wa kwamba katika hudhurio la Ukumbusho wa mwaka 1979 katika Ufaransa kulikuwako watu 133,584. Hao ni watu 9,810 zaidi ya wale waliokuwako miaka miwili tu iliyotangulia. Nao uhakika wa kwamba hudhurio hilo la Ukumbusho ni maradufu ya wahubiri wa Ufalme kama 67,000 walioko Ufaransa unaonyesha taraja kubwa sana la ukuzi wenye kuendelea wa kazi ya Ufalme.
Tayari kufikia mwishoni mwa mwaka 1978 kulikuwako makundi 1,188, mizunguko 60 na wilaya sita katika Ufaransa. Kuna makundi 28 katika Paris peke yake, na 116 katika eneo lililo karibu karibu na Paris, hiyo ikifanya jumla iwe 144. Kuna makundi 17 katika Marseilles, 11 katika Lyons, 10 katika Nice, 8 katika Nantes, 8 katika Toulouse, 7 katika Grenoble, 7 katika Mulhouse, 5 katika Caen, na miji mingine mingi ya Ufaransa ina makundi mawili au matatu.
Tunapowaza namna kazi imekua kuanzia na Wakristo wachache tu waliokuwa wajasiri na waliokuwa wameazimia mwanzoni mwa karne hii, twaweza kuona kweli kweli kwamba Yehova amebariki watu wake. Twatumaini kwamba masimulizi hayo yatawatia moyo wote wale wanaoyasoma waendelee kusonga mbele katika utumishi wa Yehova, wakikumbuka kwamba matukio ambayo yametajwa humu yote yanathibitisha ukweli wa maneno ya mtume Paulo: “Kwa maana hatuwezi kutenda jambo lo lote kupinga kweli, bali la kuunga mkono kweli.’’—2 Kor. 13:8, NW.—Kutoka Kitabu cha Mwaka cha 1980.