Obadia Anatoa Onyo na Faraja Kutoka kwa Mungu
“MAONO yake Obadia.” Hayo ndiyo maneno ya kwanza ya kitabu kilicho kifupi zaidi cha Maandiko ya Kiebrania yaliyoongozwa na Mungu. Kina onyo la msiba kwa nchi na watu wa Edomu (upande wa mashariki ya kusini mwa Bahari ya Chumvi) na ujumbe wa faraja kwa watumishi wa Mungu. Yanayofuata ni kati ya maneno yacho ya utangulizi:
“Ndivyo asemavyo Bwana [Yehova] juu ya Edomu; tumepata habari kwa [Yehova], na mjumbe ametumwa kati ya mataifa, akisema, Haya, inukeni ninyi; na tuinuke tupigane naye.”—Obadia 1.
Jina “Obadia” lina maana ya “mtumishi wa Yah [Yehova]”; na hayo tu ndiyo tunayoyajua juu ya mwandikaji wa kitabu hiki cha unabii. Walakini, kitabu cha Obadia ni chenye faida kubwa kwa waabudu wa Mungu leo. Shughuli za Yehova kwa Edomu, kama zinavyoonyeshwa na Obadia, ni mfano unaotoa onyo la namna siku moja Muumba atakavyoiondolea dunia kabisa watu wote wanaomchukia Mungu na watu wake. Kwa upande mwingine, zaidi ya Obadia kuchangamsha waabudu wa Mungu kwa kutumia ahadi ya kwamba wangewekwa huru wasionewe tena, yeye anatumia pia ahadi ya kupata ufanisi usio na mwisho ili kuwachangamsha.
Kwa kufaa, ujumbe wa Obadia unaitwa “maono” (njozi) (Obadia 1) Mara nyingi Maandiko yanawaita manabii ‘waonaji.’ (1 Samweli 9:9; 2 Samweli 15:27; 1 Mambo ya Nyakati 9:22) Hata ikiwa nabii hakuona kitu cho chote chenye kuonekana, wakati alipopashwa habari za unabii, mara nyingi habari hizo ziliitwa maono (njozi). —Danieli 9:24; Nahumu 1:1.
EDOMU YENYE KIBURI YASHUSHWA CHINI
Kulingana na Obadia, Mungu alikuwa akichochea mataifa yapige vita vyenye kuwaharibu Waedomi. Kwa kuwa habari ambazo Obadia anataja kuhusu jambo hili zilitokana na “yule Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova” (NW), pasipo shaka jambo hilo lingetimizwa.
Inaweza kuwa kwamba Waedomi walikuwa na maelekeo ya kudhihaki matabiri hayo ya msiba yaliyotolewa kuhusu taifa lao. Eneo la Edomu lilikuwa la milima-milima. Wakaaji wa kwanza-kwanza katika eneo hilo walikuwa “Wahori,” jina hilo likiwa na maana ya wakaaji wa mapangoni. (Mwanzo 14:6; Kumbukumbu la Torati,2:12, 22) Waedomi walijisikia mno wakiwa salama wasiweze kushambuliwa na adui kwa sababu makao yao yalikuwa juu sana milimani.
Kwa sababu hiyo, Mungu alitangaza hivi kwa kumtumia Obadia: “Tazama, nimekufanya mdogo kati ya mataifa; umedharauliwa sana. Kiburi cha moyo wako kimekudanganya, wewe ukaaye katika pango za majabali, mwenye makao yako juu sana; asemaye moyoni, Ni nani atakayenishusha mimi? Ujapopanda juu kama tai, ijapokuwa kioto chako kimewekwa kati ya nyota, nitakushusha kutoka huko; asema [Yehova].”—Obadia 2-4.
Waedomi wenye kujitanguliza wangefanywa ‘wadogo’ katika wingi wao na fahari yao. Mungu angewaharibisha wajapoyapandisha juu sana makao yao, hata kama yangekuwa mbali namna gani.
‘WANATAFUTWA-TAFUTWA’ KABISA
Sasa ndipo Yehova anapoonyesha kadiri ambayo adui za Edomu wangeliharibu taifa hilo liwe utupu: “Kama wevi wangekujilia, kama wanyang’anyi wangekujilia usiku, (jinsi ulivyokatiliwa mbali!) je! wasingeiba kiasi cha kuwatosha? Kama wachumao zabibu wangekujilia, je! wasingeacha baadhi ya zabibu, ziokotwe?”—Obadia 5.
Kwa ujumla wevi wanaiba “kiasi cha kuwatosha” (‘kiasi wanachotaka,’ NW) badala ya kufagia vitu vyote ndani ya nyumba na kuiacha utupu. Vivyo hivyo, wenye kukusanya zabibu walikuwa na kawaida ya kuacha zabibu nyingine nyuma. Lakini sivyo mambo yangekuwa kwa upande wa Edomu.
Obadia anaeleza hivi: ‘Jinsi watu wa Esau walivyotafutwa-tafutwa! jinsi hazina zake zilizofichwa zilivyoulizwa-ulizwa!” (Obadia 6) Adui za Waedomi walipaswa kupekua-pekua kila pango na kutafuta-tafuta vitu vyo vyote vilivyoachwa na wenye kutoroka (kukimbia). Wao wasingeacha nyuma hazina zo zote zilizokuwa zimefichwa.
HAKUNA MSAADA KWA EDOMU
Wakati ambao mataifa ya adui yangeanza matayarisho ya kupigana na Edomu, ni wazi kwamba taifa hilo lingetafuta msaada kutoka kwa watu wenye kujisingizia kuwa rafiki wenye mwungano na taifa hilo. Walakini, wakati Waedomi wangetuma wajumbe wakatafute msaada na ulinzi wa kujikinga na majeshi yenye kuwaingilia, wajumbe hao ‘wangefukuzwa hata kwenye mipaka’ ya nchi zile walikokwenda kuomba msaada. Wangesindikizwa waondoke ndani ya nchi hizo bila ahadi ya kupewa usaidizi. Hivyo hivyo ndivyo Waedomi wenye kupita kwenye mipaka ya nchi jirani-jirani wakitoroka wasiuawe wangetazamia kutendwa. Ama wangekatazwa kuingia katika nchi hizo ama wangefukuzwa watoke ndani. (Obadia 7) Hata kati ya Waedomi wenyewe hakuna wowote wangekuwa na hekima ya kutosha wala nguvu za kuwawezesha kuondoshea mbali msiba.—Obadia 8, 9.
SABABU
Sababu ya Edomu kupatwa na msiba huo imeonyeshwa katika maneno haya: “Kwa sababu ya udhalimu aliotendwa ndugu yako Yakobo, aibu itakufunika, nawe utakatiliwa mbali hata milele. Siku ile uliposimama upande, siku ile wageni walipochukua mali zake, na watu wa kabila nyingine walipoingia katika malango yake, na kutupa kura juu ya Yerusalemu, wewe nawe ulikuwa kama mmoja wao.”—Obadia 10, 11.
Waisraeli walikuwa wazao wa Yakobo na Waedomi wazao wa Esau, ndugu-pacha naye. Esau alianza kukuza chuki ya uuaji kumwelekea Yakobo kwa sababu Yakobo alijipatia hali ya mzaliwa wa kwanza kutoka kwa huyo ndugu yake. (Mwanzo 25:27-34; 27:30-45) Muda wote wa historia yao, Waedomi waliendelea kuonyesha wazi chuki ya namna hiyo kuelekea Israeli. (Hesabu 20:14-21; 2 Wafalme 8:20-22; 2 Mambo ya Nyakati 21:8-10; 28:16-20; Zaburi 83:4-8) Wakati wa karne ya tisa K.W.K., Yehova alimtumia nabii Amosi kuilaumu vikali Edomu “kwa sababu alimfuatia ndugu yake kwa upanga, akatupilia mbali huruma zake zote; hasira yake ikararua-rarua daima, akaishika ghadhabu yake milele.”—Amosi 1:11.
Karne zaidi ya mbili baadaye chuki hiyo ilionyeshwa kwa uovu mwingi sana wakati Wababeli walipoliharibu jiji la Yerusalemu na hekalu lake wakiongozwa na Mfalme Nebukadreza. Akitazama nyuma kwenye tukio hilo, mtunga zaburi aliyeongozwa na Mungu aliandika hivi: “Ee [Yehova], uwakumbuke wana wa Edomu, siku ya Yerusalemu. Waliosema, Bomoeni’ Bomoeni hata misingini!”—Zaburi 137:7.
Mungu alimtumia Obadia kulaumu Edomu vikali kwa sababu ya roho hiyo ya ukatili, akisema: “Usiitazame siku ya ndugu yako, siku ya mashaka yake, wala usisimange juu ya wana wa Yuda siku ya kuangamizwa kwao; . . . Wala usisimame penye njia panda, ili kuwakatilia mbali watu wake wakimbiao; wala usiwatoe watu wake waliosalia, katika siku ya dhiki.” (Obadia 12-14) Ujanja wa Edomu kwa Israeli ulifikia hatua ya kuwafuatia watu wenye kutoroka wakaponyoe uhai wao kisha kuwarudisha mikononi mwa adui zao. Lakini kwa kutenda hivyo Waedomi walionyesha hawakujua jambo fulani la maana sana. Namna gani?
‘SIKU YA YEHOVA I KARIBU’
Yehova aliendelea kusema hivi: “Kwa maana hiyo siku ya [Yehova] i karibu juu ya mataifa yote; kama ulivyotenda, ndivyo utakavyotendwa; malipo yako yatakurudia juu ya kichwa chako mwenyewe. Kwa maana kama vile mlivyokunywa juu ya mlima wangu mtakatifu, ndivyo mataifa yote watakavyokunywa daima; naam, watakunywa na kubabaika, nao watakuwa kana kwamba hawakuwa kamwe.”—Obadia 15, 16.
Edomu walijiunga na adui za watu wa Mungu kulewa na kula kwa kelele nyingi wakisherehekea ushinde na kutekwa nyara kwa Israeli. Sasa ilikuwa zamu yao ‘kunywa’ kikombe cha hasira ya Mungu. Si Waedomi tu, bali na mataifa yote pia yenye ukatili kwa taifa la Mungu alilolichagua ‘wangekuwa siku moja kana kwamba hawakuwa kamwe.’
EDOMU WANAKUWA KAMA “MABUA MAKAVU”
Yehova aliahidi kwamba uzao wa Ibrahimu, Isaka na Yakobo ungeimiliki nchi ambayo baadaye ilikuja kuitwa Palestina. (Mwanzo 15:7, 17-21) Uliimiliki, lakini wakahamishwa na Wababeli, wakaiacha nchi hiyo ikiwa utupu.
Yehova alimtumia Obadia kutoa uhakikisho kamili kwamba Waisraeli wangeimiliki tena, kwa maana Mungu alisema hivi kupitia nabii huyo: “Katika mlima Sayuni watakuwako wenye kuokoka, nao utakuwa mtakatifu; na nyumba ya Yakobo watamiliki milki zao. Na nyumba ya Yakobo itakuwa moto, na nyumba ya Yusufu itakuwa mwali wa moto, na nyumba ya Esau itakuwa mabua makavu, nao watawaka kati yao, na kuwateketeza; wala hatasalia mtu awaye yote katika nyumba ya Esau; kwa kuwa [Yehova] amesema hayo.”—Obadia 17, 18.
Israeli wasingegawanyika tena wakiwa ufalme wa makabila mawili ya Yuda na Benyamini (ambao nyakati nyingine uliitwa “Yakobo” katika Biblia) na ule ufalme wa kaskazini wenye makabila 10 (ambao nyakati nyingine uliitwa “nyumba ya Yusufu”). Maneno hayo yanatabiri kurudishwa katika umoja kwa makabila yote 12 ya Israeli. Tofauti na jambo hilo, Edomu wangepotelea mbali. Waisraeli walipaswa kuwamaliza wazao hao wa Esau kama vile moto unavyoyatafuna mabua (vijiti vya mimea) makavu na kuyamaliza.
Je! Edomu waliharibiwa hivyo kweli kweli? Ndiyo, na katika utimizo wa tangazo la adhabu ambalo Mungu alitoa kupitia Obadia, watu wa mataifa yasiyo ya Kiyahudi (mstari wa 1) na Waisraeli (mstari wa 18) walishiriki ndani. Tafadhali angalia ushuhuda wa kadiri fulani unaohakikisha kwamba matabiri yaliyokuwa yametolewa yalitimizwa.
Maandishi yaliyoandikwa katika mawe ya kale yanaeleza habari za kuangushwa kivita kwa Edomu wakati wa karne ya sita K.W.K. na majeshi ya Kibabeli yakiongozwa na Mfalme Nabonido. Kulingana na C. J. Gadd, aliye mwanachuo wa historia ya Kibabeli na mambo ya vitabu, askari wa Nabonido walioshinda Edomu na Tema walikuwa wamechanganyika na askari Wayahudi. Akieleza juu ya jambo hilo, John Lindsay anaandika hivi katika makala yenye kichwa “Wafalme wa Kibabeli na Edomu”: “Hivyo, maneno ya nabii yalitimizwa angaa kwa kiasi fulani, maneno aliyoyaandika akitaja kwamba Yahweh alisema ‘Nami nitaweka kisasi changu juu ya Edomu, kwa mkono wa watu wangu Israei’ (Ezekieli 25:14). Vilevile kulikuwa na utimizo mdogo wa maneno ya Obadia aliyesema kwamba ‘wenye mwungano’ na Edomu, ‘wenye mkataba mmoja’ naye, ‘rafiki wenye kutumainiwa’ ndio ‘wangemdanganya,’ ‘wamshinde nguvu’ na ‘kumtega mtego’. Hapa tunaona wakitajwa Wababeli ambao waliongozwa na Nabonido kuzikomesha kabisa kabisa tamaa za Edomu za kujipatia makuu upande wa kibiashara na wa ubepari, ingawa siku za Nebukadreza walikuwa na nia ya kuwaruhusu washirikiane nao kuitia Yuda katika hasara (linganisha Obed. 1 na 7).”—Kitabu Palestine Exploration Quarterly, Januari mpaka Juni 1976, ukurasa wa 39.
Maelezo hayo yanalingana vizuri na ushuhuda wa Biblia kuhusu wakati wa kuanguka kwa Edomu katika ushinde. Kama ilivyokwisha kuonwa, Edomu ni taifa lililokuwa likijitegemea wakati jiji la Yerusalemu liliposhindwa na majeshi ya Nebukadreza. Walakini, kitabu cha Malaki, kilichoandikwa karibu na katikati ya karne ya tano K.W.K. (yapata miaka 100 baada ya shughuli kali ya kuwaingilia Waedomi chini ya uongozi wa Nabonido), kinasimulia kwamba Mungu alikuwa tayari amekwisha kuifanya ‘milima ya Edomu kuwa ukiwa, na urithi wake akawapa mbweha wa nyikani.’—Malaki 1:3.
‘HUO UFALME UTAKUWA NI MALI YA YEHOVA’
Waisraeli wangeimiliki tena nchi ambako walifukuzwa wakati wa kuhamishiwa kwao Babeli. Zaidi ya hilo, kitabu cha Obadia kinaeleza kwamba eneo la Israeli lingepanuliwa pande zote. Wao wangesambaa kusini mpaka waingie Negebu, waende mashariki waingie katika iliyokuwa nchi ya Waedomi kisha waende magharibi waiingie Shefela na nchi ya Filistia. Wangesambaa kuelekea magharibi ya kaskazini waifikie pwani yote ya Ufoinike mpaka kaskazini huko Zarefathi (Sarepta) kati ya Tiro na Sidoni. Kuelekea mashariki ya kaskazini wangesambaa waliingie eneo lote lililokuwa likikaliwa na ufalme wa Israeli wenye makabila 10, kutia na Efraimu, Samaria na eneo la Gileadi lililoko mashariki ya Mto Yordani. Badala ya kufungiwa katika nchi ya mbali ugenini, wahamishwa wa Yerusalemu waliotoka hata kule mbali Sefaradi (panapoaminiwa kuwa ni Asia Ndogo) wangerudi wamiliki urithi wa eneo lenye kupanuka kuelekea kusini kufika Negebu ambako zamani Waedomi walikuwa wamejinyakulia nchi.—Obadia 19, 20.
Kitabu cha Obadia kinafikia mwisho kwa njia yenye kutia moyo, kikitangaza hivi: “Tena waokozi watakwea juu ya mlima Sayuni ili kuuhukumu mlima wa Esau; na huo ufalme utakuwa ni mali ya [Yehova].” (Obadia 21) Katika siku zilizofuata baada ya kifo cha Yoshua, Mungu aliinua waamuzi ‘kuokoa’ Israeli katika uonezi na kulipata tena eneo la nchi walilonyang’anywa na adui zao, naye Obadia anawaonyesha Waisraeli waliorudishwa kwenye nchi yao wakichukua hatua inayolingana na hiyo.—Waamuzi 2:16.
Linalofuraisha ni kwamba, unabii huu ukitumiwa katika maana iliyopanuliwa unatoa uhakikisho kamili kwamba siku moja adui wote wa Mungu wataangamizwa kisha utawala wa kimungu usambae duniani pote. (Zaburi 22:27, 28) Ujumbe huo wenye onyo na faraja kutoka kwa Mungu wa kweli unastahili uenezwe kote kote uwezako kuenezwa. Je! wewe unashiriki kwa ukawaida kuwaeleza wengine ujumbe huo?
[Picha katika ukurasa wa 17]
EDOMU
Ujumbe wa Obadia—onyo la uharibifu kwa Edomu na ahadi ya kurudishwa kwa watu wa Mungu