Je! kwa Kweli Mungu Anasema Leo?
MHUTUBU wa chuo alitembea kwenda mbele ya darasa, akiwa tayari kuanza somo lake. Kisha akaona kwamba mwanafunzi mmoja alikuwa ameandika kitu fulani juu ya ubao: “ULIZA MAMLAKA!” Bila kusema neno hata moja, mhutubu huyo akaandika chini ya maandishi hayo hivi: ‘‘Mamlaka ikijibu, je! utasikiliza?”
Hilo ni ulizo zuri. Nalo linahusu kwa habari ya mwenye mamlaka aliye juu zaidi ya wote, Yehova Mungu. Wengi wetu tutakubali kwamba, leo, wanadamu wanahitaji msaada. Mambo mengi sana yamekwenda kombo na hayaongozeki—uchafuzi wa hewa na maji, kuzidi kwa idadi ya watu, maafa ya njaa ambayo yameenea sehemu kubwa, infuleshoni na tisho baya sana la vita ya nyukilia, hewa au viini vya magonjwa. Huenda ukaona hivi: ‘Hakika, ikiwa Mungu ana jambo la kuwaambia wanadamu, sasa ndio wakati bora wa kulisema!’
Hiyo ni kweli. Walakini lazima ulizo hili liulizwe: Ikiwa Mungu angesema, ni nani angesikiliza? Ingawa kwa wazi wanadamu wanahitaji uongozi, je! wangeukubali kama ungetolewa?
MUNGU ANASEMA
Hata hivyo, kwanza fikiria ulizo hili, Je! Mungu anasema nasi leo? Ikiwa sivyo, wakati wetu ujao hauna matumaini. Kwa furaha, ushahidi ni kwamba anasema. Namna gani?
Ikiwa kwa kweli Mungu ana ujumbe wa maana wa kuwaambia wanadamu, njia bora zaidi ya kuwapasha ingekuwa nini? ‘Kwa sauti kutoka mbinguni,’ huenda ukasema. Hiyo ingekuwa njia ya wazi, bila shaka. Walakini je! ndiyo ingekuwa njia yenye kufaa zaidi?
Mwanamume mmoja mwenye ujuzi wa muda mrefu katika kazi ya usimamizi alieleza hivi: “Ninapokuwa na habari ya maana ya kupasha, sipashi kamwe kwa kusema kwa mdomo. Sikuzote ninaiandika. Kwa njia hiyo hakutokei mvurugo baadaye.”
Jambo hilo linafahamika. Kama Mungu angesema kutoka mbinguni, hakika jambo hilo lingekuwa lenye kutokeza sana. Walakini kama watu 1,000,000 wangemsikia, karibuni kungekuwa maana tofauti 1,000,000 za yale aliyosema. Kwa upande mwingine, kama angehakikisha maagizo yake yameandikwa, baadaye hakungekuwa shaka juu ya ujumbe wake ulivyokuwa.
Hata hivyo, ujumbe kutoka kwa Mungu ulioandikwa ungehitaji hati ya pekee sana. Ungepasa kuwa na hekima ya kimungu iliyo wazi, na ungepasa kupatikana kwa wingi, ili kwamba kila mtu ambaye angetaka aweze kuusoma. Zaidi ya hayo, ungepasa kushinda vizuizi vingi vya lugha za ulimwengu.
Je! kuna hati iliyopo inayodai kuwa imetoka kwa Mungu na inayotimiza matakwa hayo? Ndiyo, kuna moja, na ndiyo pekee iliyopo. Ndicho kitabu kilichoenezwa kwa wingi zaidi katika historia yote, kikiwa na nakala bilioni nyingi zilizoenezwa. Na sasa kinapatikana, chote au katika visehemu-sehemu, katika lugha 1,710, hata kwamba karibu mtu ye yote anayeweza kusoma, anayetaka kusoma, anaweza kusoma angaa sehemu yacho katika lugha yake mwenyewe. Hati hiyo ni nini? Ndiyo Biblia.
JE! KWA KWELI NI MUNGU ALIYESEMA?
Unaiitikiaje habari hiyo? Je! unaona hivi: ‘Aa, hapana, si Biblia! Ingewezekanaje leo Mungu awe akisema kupitia kitabu ambacho ni cha kizamani hivyo?’
Bila shaka Biblia ni ya kale, kwa sababu jamii ya kibinadamu ni ya kale, na Mungu amekuwa akisema na wanadamu kwa muda mrefu. Walakini je! kwa kweli ni ya kizamani? Hata!
Je! ungeweza kusema kitabu ni cha kizamani kama kilitabiri maelfu mengi ya miaka iliyopita juu ya hali ya wanadamu leo, wanadamu kuogopa wakati ujao, hatari ya wao kuiharibu dunia yote, na hata vitisho vilivyomo ndani-ndani ya bahari na katika anga ya juu? Na Biblia inatabiri hayo.—-Luka 21:25-28; 2 Tim. 3:1-5; Ufu. 6:3-8; 11:18.
Katika siku ambazo talaka na kuvunjika kwa ndoa ni mambo yaliyoenea sana, je! ungeweza kusema kitabu ni cha kizamani kama ndani yacho mnapatikana shauri la ndoa amblo limepata kuwa lenye kufanikiwa zaidi ya yote yaliyopata kutolewa? Huenda hilo lisiwe shauri lenye kupendwa na watu wengi kwa sababu ya kizazi cha leo chenye kufuata wazo la kichoyo la “mimi,” walakini lina matokeo. Nalo limeandikwa katika Biblia.—Efe. 5:21-33.
Ni kweli kwamba leo ni jambo la kielimu lenye kuheshimika katika sehemu fulani kuifikiria Biblia kuwa mkusanyo wa hadithi tu na hekima ya kitamaduni. Lakini je! mambo hayo ndiyo yaliyofanyiza tokeo ambalo ni Biblia? Maelfu mengi ya miaka iliyopita, wakati ilipokuwa ikikusanywa, kulikuwa vitabu vya hadithi tu na hekima ya kitamaduni. Hata hivyo, vyote vilisahauliwa kwa kadiri wakati ulivyopita. Vingine vimepatikana hivi karibuni tu na wabukuzi wa mambo ya kale. Kwa sababu gani Biblia ikahifadhiwa ijapokuwa hivyo havikuhifadhiwa?
Wakati wa historia yake ndefu Biblia imeshinda upinzani usio wa kawaida. Nakala zisizohesabika zimeteketezwa moto. Watu waliojaribu kufanya ipatikane kwa watu wa kawaida waliteswa hata kufa. Kwa karibu miaka 200, imeendelea kushambuliwa na wachambuzi wa Biblia wenye elimu nyingi, wenye kufuata wazo !a mageuzi na wenye kufuata maongozi ya kufanya mambo yawe ya kisasa. Hakuna kitabu kinginecho kilichotendwa hivyo kwa uadui. Hata hivyo kwa ushindi Biblia imeokoka na inaendelea kuongoza maisha za mamilioni mengi ya watu. Kwa sababu gani? Kwa sababu yenyewe si kitabu cha hadithi tu na hekima ya kitamaduni. Kwa kweli ni ujumbe ambao Mungu ametupa sisi.
Kijana mmoja asiyeamini kuna Mungu alisema hivi: “Mimi nilikuwa na maoni ya kwamba si kitu kama kuna Mungu au hakuna kwa kuwa sikuona anawafanyia wanadamu jambo lo lote.” Kisha alitolewa mwito aisome Biblia na vitabu fulani ili asaidiwe kufahamu ujumbe wayo. Matokeo yalikuwa nini? “Nilivutiwa sana, kwamba kila kitu . . . kilileta maana.” Ndiyo, alimsikiliza Mungu alipokuwa akisema, na anayosema yanatoa maana.
Kuelekea mwishoni mwa karne ya 19 mchunguzi wa Biblia anayejulikana sana aliandika hivi: “Wakati Columbus alipovumbua mto Orinoco, mtu fulani alisema hicho ni kisiwa alichokuwa amevumbua. Yeye alijibu hivi, ‘Hakuna mto kama huo unaotiririka kutoka katika kisiwa. Lazima mbubujiko huo mkubwa uwe unachukua maji ya kontinenti.’ Kwa hiyo kina na nguvu na uwezo na wingi wa ushahidi wa Biblia unatusadikisha kwamba si mwanadamu, bali Mungu Mwenye Nguvu Zote, ndiye mbuni wa mipango na mafunuo yayo.”
Tunakualika ujifunze Biblia wewe mwenyewe. Uone kama hukubali kwamba hapa, hakika, pana mawazo ya Mungu mwenyewe.