Wakati Watu Waliokufa Watakapoishi Tena!
“Yesu akamwambia, Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele.”—YOHANA 11:25, 26.
1. (a) Ili mtu ye yote duniani adai kuwa yeye ndiye “huo ufufuo, na uzima,” angetakwa awe na nini? (b) Mwenye kudai kuwa hivyo anaweza kutumikia akiwa hivyo juu ya msingi gani?
KWA uhakika mwanadamu ye yote angetakwa awe na ujasiri mkubwa ndipo aweze kudai kwa mkazo hivi, “Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima.” Lakini maneno hayo hayo ndiyo yaliyosemwa na yule bwana wa zamani, Yesu Kristo, akijitaja mwenyewe zaidi ya karne 19 zilizopita. Mmoja wa mitume wake, jina lake Yohana, alimsikia akisema maneno hayo kisha akayaandika kwa faida yetu sisi leo. (Yohana 11:25) Yesu alimaanisha kwamba ndivyo yeye alivyokuwa kwa ajili ya waliokufa na wenye kufa pamoja na wanadamu waliokwisha kuzikwa. Bila shaka, yeye mwenyewe alikufa kwa kuuawa kikatili juu ya mti wa kuulia watu nje ya kuta za Yerusalemu. Kwa hiyo Baba yake mwenyewe, Yehova Mungu, sasa alipaswa kuwa “huo ufufuo, na uzima” kwa Yesu pia. Siku ya tatu ya kufa kwa Yesu, Mungu Mweza Yote alimfufua kutoka kwa wafu akamvika uzima usioweza kufa katika ulimwengu wa roho. Kwa kufanya mwujiza wa kujivika mwenyewe mwili wenye nyama kama ule aliokufa akiwa nao, Yesu alijifunua kwa wanafunzi wake wenye dhiki, na wakati mmoja alifanya hivyo kwa watu zaidi ya 500. (1 Wakorintho, sura ya 15) Hivyo yeye kweli angeweza kuwa ule ufufuo na uzima kwa wanadamu aliowafia.
2. Kwa sababu gani hakuna mtu hata mmoja leo anayeweza kuutupilia kando ufufuo wa Yesu Kristo kwa kusema hiyo ni hadithi ya bure tu ya karne ya kwanza W.K.?
2 Hakuna mwanadamu anayeishi leo anayeweza kucheka na kulitupilia kando tukio hilo lililohakikishwa kuwa kweli la kufufuliwa kwa Yesu Kristo mtundikwa kwa kusema ni hadithi ya bure tu iliyoenezwa sana katika karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida wetu. Isipokuwa daktari Luka peke yake, aliyeviandika vitabu vya Biblia vya Luka na Matendo ya Mitume, waandikaji wale wengine wote wa vile vitabu vingine 25 vya lile liitwalo Agano Jipya walimwona Mwana wa Mungu aliyefufuliwa kwa macho yao wenyewe. Mmoja wa mashahidi walioshuhudia zaidi ni mtu aliyekuwa mtesi wa Wakristo hapo zamani, Sauli wa mji wa Tarso, ambaye akawa mtume Mkristo Paulo, aliyeandika vitabu 14 vya “Agano Jipya” katika Kigiriki kilichotumiwa na watu wengi cha siku hizo.
3, 4. Akiwa Juu ya Kilima cha Mars, mtume Paulo aliwaambia Waathene nini juu ya siku ya hukumu ya Mungu na juu ya ufufuo?
3 Safari moja Paulo alikokotwa kwa nguvu akapelekwa mbele ya mahakimu wa Mahakama Kuu Zaidi waliokutana juu ya Kilima cha Mars, au Areopago. Wakati huo alikuwa katika ule mji wa Athene wa watu wenye ustaarabu mkubwa sana na akili nyingi sana.
4 Kwa kuwapa heshima iliyowastahili, Paulo alihutubia kikusanyiko hicho cha watu wenye akili juu ya Kilima cha Mars. Paulo alipokuwa akifikisha ushuhuda na utetezi wake kwenye kilele kizuri sana, yeye hakutumia madharau ya kuwaonyesha wasikilizaji wake wenye hekima ya kilimwengu kwamba yeye alikuwa na ubingwa wake. Yeye alisema:
“Basi, zamani zile za ujinga Mungu alijifanya kama hazioni; bali sasa anawaagiza watu wote wa kila mahali watubu. Kwa maana ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki, kwa mtu yule aliyemchagua; naye amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kwa kumfufua katika wafu.”—Matendo 17:30, 31.
5. Wasikilizaji hao Waathene waliitikiaje, na kwa hiyo ulizo linatokea kuhusu nani?
5 Fundisho hilo lililo zuri sana la ufufuo wa wafu liliwaingiaje Wagiriki hao wenye kuamini nafsi ya kibinadamu haiwezi kufa? “Basi waliposikia habari za ufufuo wa wafu wengine walifanya dhihaka; wengine wakasema, Tutakusikiliza tena katika habari hiyo.” Bado maoni yao yalikuwa kwamba yeye alikuwa “mtangaza habari za miungu migeni.” Lakini, Dionisio, aliyekuwa hakimu wa Areopago, aliweza kufahamu yaliyosemwa na Paulo juu ya siku inayokuja ya hukumu kwa wanadamu wote, basi akalithamini jambo hilo. Mwanamke jina lake Damari alilithamini pia. (Matendo 17:18, 32-34) Lakini namna gani sisi leo katika kizazi hiki cha kisayansi kilichokwisha kuendelea sana? Hili si jambo la kufanyiwa kicheko!
6. Je! ufufuo wa Yesu ulikuwa ndicho kisa cha kwanza cha kufufua wafu, na kutakuwa na uwezekano gani kwa wale ambao bado Yesu atawafufua wakati ujao?
6 Bila shaka, ufufuo wa Yesu Kristo haukuwa ndicho kisa cha kwanza cha kufufua wanadamu wafu wakiwa na fahamu zao. Biblia ina kumbukumbu la visa vilivyokitangulia hicho, kutia ndani ufufuo wa Lazaro, ambaye Yesu mwenyewe alimfufua siku ya nne ya kufa kwake na kuzikwa kaburini. (Yohana 11:1-44) Lakini kisa cha ufufuo wa Yesu mwenyewe ndicho kilichokuwa cha maana zaidi kwa wanadamu wote. Yeye hakufa tena kama wale wengine; lakini sasa akiwa katika hali yake ya kufufuliwa na ya kutoweza kufa, anaweza kuwa ‘ule ufufuo na uzima’ kwa wanadamu hata wapate uzima usio na mwisho wakiwa katika ukamilifu, bila laana ya kifo na wakiwa chini ya enzi kuu ya Mungu ya ulimwengu wote.
7, 8. (a) Urefu wa umri wa Adamu na Methusela unahakikishaje kwamba kuna uwezekano wa wanadamu waliokamilishwa kuishi milele? (b) Maisha ya Melkizedeki yanahesabiwa kuwa yalikuwa na urefu gani, na jambo hilo linahakikisha nini juu ya maisha ya yule aliyetangulia kumfananisha?
7 Uwezekano wa kuwa na uzima usiokwisha wa kibinadamu duniani wakati wanadamu watiifu watakapoinuliwa watoke katika dhambi na kifo (walivyovipata kupitia Adamu yule mtu wa kwanza) unahakikishwa na jambo la kwamba Adamu ajapomtenda Mungu dhambi, yeye aliishi miaka 930, na mwingi wa wakati huo aliutumia akiwa nje ya ile bustani kamilifu ya Edeni. Mmoja wa wazao wake, Methusela, aliishi akawa na umri wa miaka 969. (Mwanzo 5:5, 27) Mwaka wa 2370 K.W.K. ndipo Methusela alipokufa, na mwaka uo huo Gharika ya duniani pote ya siku za Noa ikafutilia mbali uhai wote wa kibinadamu na wa wanyama waliokuwa nje ya safina ambamo Noa na jamaa yake walikimbia wapate usalama. Karne nyingi baadaye, kufikia mwaka wa 1933 K.W.K. wala si baada ya hapo, ukuhani ulitokea duniani, ule wa Melkizedeki, ambaye alimbariki Abrahamu mzee wa ukoo na ambaye alikuwa na kibali ya Mungu. Tarehe za kuzaliwa na kufa kwake hazionyeshwi.
8 Kwa hiyo inaelekea kuwa kwamba ukuhani wake wa huko Salemu, ambako alikuwa mfalme na kuhani pia, haupimiki kwa wakati. (Mwanzo 14:18-20) Uwezekano wa kudumu kwa uhai wa Yesu Kristo aliyefufuliwa unafananishwa na ule wa Melkizedeki Kuhani-Mfalme, kwa maana Waebrania 7:15-17 inatuambia kwamba Yesu Kristo aliyetukuzwa sasa ana “nguvu za uzima usio na ukomo; maana ameshuhudiwa kwamba, Wewe u kuhani milele kwa mfano wa Melkizedeki.” (Ona pia Zaburi 110:1-4.) Kwa hiyo muda wote tangu apate utukuzo wa kimbingu katika mwaka wa 33 W.K., Yesu Kristo aliyepewa uwezo wa kutokufa amekuwa akifanya kazi ya Kuhani Mkuu kuelekea washiriki wa jamaa ya kibinadamu, ambao kwa ajili yao yeye alijitoa akiwa dhabihu kamilifu ya kibinadamu. Kwa hiyo, anaweza kufanya kazi akiwa Adamu wa pili kwa ajili ya jamaa ya kibinadamu yenye kutawalwa sana na kifo. Atakapowafufua wafu wa kibinadamu katika wakati unaofaa warudie uzima wa kidunia, watakuwa na nafasi ya kupata uzima wa milele katika ukamilifu wa kibinadamu katika Paradiso itakayopanuliwa ifikie sehemu zote za dunia. Yesu Kristo mwenye kujitoa nafsi yake hatashindwa kama Adamu wa kwanza kutimiza daraka lake kuelekea jamaa ya kibinadamu aliomwaga kwa ajili yao damu yake kamilifu yenye uhai.—1 Wakorintho 15:22-45.
Watu Waliokufa Watakutana Tena Duniani
9. Mungu alisawazisha mambo namna gani kwa ajili ya ufufuo wa wazao waliokufa wa Adamu na Hawa, kulingana na 1 Wakorintho 15:21 na Warumi 5:12?
9 Kwa umati ulio mkubwa zaidi wa wanadamu ambao wamepata kuikanyaga dunia hii, pendeleo la kuishi tena duniani chini ya Ufalme wa Mungu ulioahidiwa ambao uko mikononi mwa Kristo litategemea ufufuo wa wafu. Akitoa ushuhuda wa kwamba Mungu ana uwezo wa kusawazisha mambo kwa haki na ukamilifu, mtume Paulo aliyekuwa mmoja wa wenye kushuhudia kwamba Yesu Kristo alifufuliwa, aliandika hivi: “Kwa kuwa mauti ililetwa na mtu, kadhalika na kiyama ya wafu ililetwa na mtu.” (1 Wakorintho 15:21) Kwa kupatana na barua aliyoandikia Wakristo Wakorintho, Paulo aliandika hivi katika barua yake kwa Wakristo Waroma: “Kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.” (Warumi 5:12) Kwa sababu hiyo, Yehova Mungu angeweza kupanga ili wazao wa Adamu na Hawa wakombolewe na mtu mmoja ambaye yeye peke yake hakuhusika katika kanuni iliyoonyeshwa katika Warumi 5:12.
10. Ni juu ya msingi gani Yesu Kristo angeweza kutoa uhai wake wa kibinadamu uwe badala ya uhai mwingine kisha awe Baba wa Milele kwa wazao wa Adamu?
10 Mtu huyo wa pekee alikuwa Yesu, ambaye Mungu alimfanya azaliwe kimwujiza kutokana na Mariamu bikira Myahudi, binti ya Heli wa kabila la kifalme la Yuda. (Luka 3:23-38) Uhai wake wa kibinadamu ulio mkamilifu ambao ulikuwa dhabihu ungeweza kuwekwa mahali pa uhai mkamilifu wa kibinadamu ambao Adamu alipotezea wazao wake wote wa kimwili kwa kumtenda Muumba wake dhambi kwa makusudi katika bustani ya Edeni. Kwa hiyo, Yesu Kristo mfufuliwa angeweza kutumikia akiwa “Baba wa milele” kuelekea wale wote ambao Adamu alijifanya baba yao mwenye dhambi. Basi Mwana wa Mungu anaachiwa mikononi wajibu wa kuwa Baba wa Milele kwao.—Isaya 9:6.
11. Ikiwa Yesu Kristo na mitume wake walipokuwa wangali duniani wangeweza kufufua wafu, Yesu ana uwezo gani wa kufanya hivyo tangu wakati wa ufufuo wake mwenyewe?
11 “Wakati Yesu Kristo na mitume wake walipofufua watu kwa wafu, ufufuo huo haukuondolea watu hao matokeo ya laana ya kifo waliyokuwa wamerithi kwa Adamu yule wa kwanza. Kwa hiyo, hata Lazaro rafiki aliyependwa sana na Yesu alikufa tena akaingia katika uhitaji wa kupewa ufufuo wa mwisho chini ya Ufalme wa Mungu uliosimamishwa. Lakini hilo halitakuwa tatizo. Ikiwa Yesu alipokuwa duniani akiwa mwanadamu mkamilifu alipewa uwezo wa kufufua wanadamu wafu ili kuyafanya upya na kuyarefusha maisha yao ya kidunia angaa kwa muda mfupi chini ya huu mfumo wa mambo, je! sasa yeye hana uwezo mkubwa zaidi wa kufufua wanadamu waliokufa katika wakati wa Mungu, kwa kuwa kwa mara nyingine yeye ni Mwana wa kiroho wa Mungu? Bila shaka ana uwezo huo, kwa sababu amepewa mamlaka yote mbinguni na duniani tangu alipofufuliwa na akapaa amrudie Babaye wa kimbingu.
12. Je! uhusiano wa Yesu Kristo na jamaa ya kibinadamu ulikatizwa na namna alivyofufuliwa, naye atakamilishaje kusudi la dhabihu yake ya kibinadamu?
12 Wakati mmoja wa wanafunzi wa Kristo, yaani mtume Paulo, alipokuwa akizungumza habari ya ufufuo katika barua aliyowaandikia Wakristo Wakorintho, Paulo alisema: “Ndivyo ilivyoandikwa, Mtu wa kwanza, Adamu, akawa nafsi iliyo hai; Adamu wa mwisho ni roho yenye kuhuisha.” (1 Wakorintho 15:45) Kwa kuwa yeye anatajwa kuwa Adamu wa mwisho, hiyo inaonyesha kwamba bado ana uhusiano wa kijamaa wa kadiri fulani pamoja na wanadamu. Uhakika wa kwamba sasa yeye ni mtu wa kiroho mwenye nguvu zipitazo za kibinadamu haumzuii kuwa na uhusiano nao. (Zaburi 8:4, 5; Waebrania 2:5-9) Wakati wa siku ya hukumu inayokuja ya miaka elfu, yeye atakamilisha kusudi la dhabihu yake kamilifu ya kibinadamu kwa kuwarudisha wanadamu waliokufa wakiwa na nafasi ya kuinuliwa kwenye ukamilifu katika dunia-Paradiso na ya kuwa Baba wa Milele kwao na Mwana-Mfalme wa Amani. Kwa hiyo atawaondolea kile walicholetewa na Adamu.
13. Kabla Yesu hajamfufua Lazaro kutoka kwa wafu, Yeye alimwambia Martha nini juu ya watu waliokufa na wanaoishi wanaomwamini Yeye?
13 Kabla Yesu hajamfufua Lazaro wa Bethania, rafiki yake mpendwa, kutoka kwa wafu, yeye alimwambia Martha dada ya Lazaro hivi: “Ndugu yako atafufuka.” Martha alifikiri Yesu alimaanisha wakati ujao uliokuwa mbali na kwa hiyo akajibu: “Najua ya kuwa atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.” Wakati huo ndipo Yesu alipoipata nafasi ya kusema maneno haya yaliyo mazuri ajabu: “Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele.”—Yohana 11:23-26.
14. (a) Ili mwanadamu amwamini Yesu, kwanza anatakwa afanye nini? (b) Mungu akimchagua mtu huyo akapate urithi wa kimbingu, ni jambo gani litakalotukia karibuni ajapolazimika kufa?
14 Ili mwanadamu amwamini Yesu Kristo, ingempasa awe hai na kusikia au kujifunza habari zake. Ndipo mtu huyo angeweza kuweka maisha yake wakf kwa Mungu kupitia Kristo na kuonyesha amechukua hatua hiyo ya kukata maneno kwa kubatizwa katika maji. Ikiwa Baba wa kimbingu wa Yesu Kristo angeamua kumwita huyo mwanafunzi aliyejiweka wakf akabatizwa wa Mwanaye kwenye urithi wa kimbingu pamoja naye, yeye angemzaa huyo kwa roho yake. Hiyo ingemaanisha kwamba mwanafunzi huyo aliyezaliwa kwa roho angelazimika kufa mwishowe akiwa mwanadamu. Lakini Yesu alisema: “Ajapokufa, [huyo] atakuwa anaishi.” Kwa habari yake, uzima ambao angepata ni wa kufufuliwa akiwa kiumbe cha kiroho katika makao ya kimbingu awe pamoja na Yesu.
15. Mtu ambaye alionyesha imani inayofaa lakini hakuwa amezaliwa kwa roho ya Mungu akifa, hali ya mtu huyo itakuwa nini kwa habari ya ufufuo wake?
15 Leo mwanafunzi aliyejiweka wakf akabatizwa ambaye hakuwa amezaliwa na Yehova Mungu akapate urithi wa kimbingu pamoja na Kristo, akifa, kama vile wengi wamekufa tangu kukusanywa kwa “kondoo wengine” wa Kristo kulipoanza, hapo itakuwaje? (Yohana 10:16) Kwa sababu huyo alikuwa amemwamini Yule aliye “huo ufufuo, na uzima,” yeye angekuwa katika hali nzuri zaidi kwa kuhusiana na ule mfumo mpya wa mambo tangu wakati ule wa kufufuliwa kwake duniani na kuendelea. Inaelekea ingekuwa hivyo tangu mwanzo wa mfumo huo. (Waebrania 11:35) Ndipo angekuwapo mwanzoni-mwanzoni aweze kupata mapendeleo ya pekee ya utumishi akiwa chini ya Ufalme wa kimbingu. Kwa njia hiyo tumaini la ufufuo alilokufa akiwa nalo litatimizwa, kisha utukufu umwendee Mungu kwa tendo hilo!
16, 17. (a) Kwa habari ya ufufuo, ikoje kwa wale watu wa nyakati zilizoutangulia Ukristo ambao walitazamia tu kuja kwa “uzao” wa “mwanamke” wa Mungu? (b) Yesu alitumia maneno gani kutuhakikishia kwamba watafufuliwa?
16 Si wale tu ambao wamemwamini Yesu Kristo tangu kuja kwake mara ya kwanza walio na sehemu katika mipango ya ufufuo. Bali wale waliokuwako nyakati za kabla ya Ukristo ambao walimwamini Yehova Mungu wakatazamia kuja kwa “uzao” wa “mwanamke” wake wa mfano uliotabiriwa naye katika Mwanzo 3:15 watakuwa pia na sehemu katika mipango hiyo ya ufufuo. “Uzao” huo ulipata kuwa kitu kimoja na ule ulioitwa baadaye ‘uzao wa Abrahamu.’ (Mwanzo 12:1-3; Wagalatia 3:16) Watu wa namna hiyo waliotazamia kuja kwa “uzao” huo wa Abrahamu Mkubwa Zaidi, Yehova Mungu, bila shaka walikuwa ni pamoja na Abrahamu mzee wa ukoo na Mwanaye, Isaka, na mjukuu wake, Yakobo, au Israeli. Akithibitisha kwamba hao watafufuliwa pasipo shaka, Yesu Kristo, yule Mzao wa Abrahamu, alisema:
17 “Kwa habari ya kiyama [ufufuo] ya wafu, hamjalisoma neno lililonenwa na Mungu, akisema, Mimi ni Mungu wa [Abrahamu], na Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo? Mungu si Mungu wa wafu, bali wa walio hai.” (Mathayo 22:31, 32) “Na kwa habari ya wafu ya kwamba wafufuliwa, hamjasoma katika kitabu cha Musa, Sura ya Kijiti, jinsi Mungu alivyomwambia, akisema, Mimi ni Mungu wa [Abrahamu], na Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo? Yeye si Mungu wa wafu, bali wa walio hai.” (Marko 12:26, 27) “Kwa maana wote wako hai kwa maoni yake.” (Luka 20:37, 38, NW) Kwa njia hiyo isiyo ya moja kwa moja Yehova Mungu alituhakikishia sisi kwamba kuna ufufuo wa wanadamu waliokufa.
18. Kulingana na vile uzao ulioahidiwa ulivyo, Abrahamu rafiki ya Mungu alikuwa mfananishi wa nani?
18 Ahadi ambayo Mungu mwenyewe alimpa Abrahamu rafiki yake ilikuwa kwamba jamaa zote za dunia ‘zingejibariki’ kupitia “uzao” wake. (Yakobo 2:23; Mwanzo 12:1-3; 22:15-18) Kwa kuwa “uzao” huo umekuwa wa kiroho, Abrahamu binadamu alikuwa mfananishi wa Yehova Mungu, kwa maana Yeye peke yake ndiye angeweza kuwa Baba ya ule “uzao” wa kiroho, yaani Baba ya Yesu Kristo aliye mbinguni, ambaye sasa amekwisha kutukuzwa.
19. Katika Ufunuo 20:11-14, tunapewa wonyesho wa kiunabii wa kitu gani?
19 Sisi tunapewa wonyesho wa kiunabii wa ufufuo unaokuja wa hizo jamaa za dunia zilizokufa. Ufunuo 20:11-14 unasimulia ufufuo huo kwa kutumia maneno ya mfano na kusema: “Kisha [mimi Yohana] nikaona kiti cha enzi, cheupe, na yeye aketiye juu yake; ambaye nchi na mbingu zikakimbia uso wake, na mahali pao hapakuonekana. Nikawaona wafu, wakubwa kwa wadogo, wamesimama mbele ya hicho kiti cha enzi; na vitabu vikafunguliwa; na kitabu kingine kikafunguliwa, ambacho ni cha uzima; na hao wafu wakahukumiwa katika mambo hayo yaliyoandikwa katika vile vitabu, sawasawa na matendo yao. Bahari ikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake; na Mauti na Kuzimu zikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake. Wakahukumiwa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake. Mauti na Kuzimu zikatupwa katika lile ziwa la moto. Hii ndiyo mauti ya pili, yaani, hilo ziwa la moto.”
20. Mwishoni mwa siku ya hukumu ya miaka elfu, itakuwaje kwa wanadamu ambao majina yao yataandikwa katika kitabu cha uzima na kwa wale ambao majina yao hayataandikwa?
20 Wakati wa ile “siku” yenye urefu wa miaka elfu, ambayo Mungu “ameweka” na ambayo katika hiyo ‘atawahukumu walimwengu kwa haki, kwa mtu yule aliyemchagua,’ wanadamu wafu watakaofufuliwa watapaswa kujifaidi kutokana na mipango yote ya kimungu iliyofanywa kwa ajili ya wokovu wao wa milele. (Matendo 17:31) Katika maana hiyo itawapasa ‘wajibariki’ wenyewe. Kwa kulipita jaribu la mwisho la ukamilifu wao bila kuwa na kasoro, watapata thawabu ya uzima wa milele katika Paradiso ya duniani pote. Wasipoipata, basi watapata nini: “Mauti ya pili,” ambayo haitakuwa na ufufuo. (Ufunuo 20:14) Ni sawa na vile imeandikwa katika Ufunuo 20:15: “Na iwapo mtu ye yote hakuonekana ameandikwa katika kitabu cha uzima, alitupwa katika lile ziwa la moto.”
Je! Wewe Unaweza Kukumbuka?
□ Kwa sababu gani hakuna mtu leo anayeweza kuutupilia mbali ufufuo wa Yesu Kristo akisema ni hadithi ya bure tu?
□ Ni juu ya msingi gani Yesu angeweza kuwa Baba wa Milele kwa wazao wa Adamu?
□ Mtu mwaminifu asiyezaliwa kwa roho ya Mungu akifa, hali yake itakuwa nini atakapofufuliwa?
□ Ufunuo 20:11-14 unatupa sisi wonyesho wa kiunabii wa kitu gani?
[Picha katika ukurasa wa 8]
Furaha itakuwa tele wakati wale ambao sasa ni wafu watakapoishi tena