Kutangaza Habari Njema Katika Donegal
“Makubwa HAYO! ” “Imekuwa vizuri sana.” Maneno hayo yalisikiwa katika kikundi cha watu 120 waliokuwa wametoka Uingereza wakaenda Donegal, jimbo lililo katika kaskazini-magharibi ya Ailandi. Hapana, wao hawakuwa watalii wenye kueleza waliyoona. Walikuwa wanaume, wanawake, na watoto waliokuwa wameenda kule kwa kujigharimia wenyewe ili wakawaeleze watu wa Donegal ya Magharibi tumaini walilo nalo kwa wakati ujao.
Kwa kuwa kuna Mashahidi wa Yehova 19 tu kati ya wakaaji 120,000 wa Donegal, watu walio wengi katika eneo hilo hawakuwa wamepata kutembelewa na Mashahidi kwa miaka mingi. Kwa hiyo, kikundi hicho kikubwa cha wageni kilijitwika kwa kupenda daraka la kuzitangaza habari njema za Ufalme wa Mungu kandokando ya pwani inayopendeza macho ya bahari Antlantiki katika Donegal.
Mashahidi wa mahali hapo walikuwa wamefanya matayarisho mengi kwa ajili ya kikundi hicho. Wachache walikuwa wamesafiri mamia ya maili kuchora ramani za eneo lote, kurekebisha upya ramani zilizochorwa na wachoraji rasmi wa eneo hilo, na kuipa kila barabara namba fulani ya kuitambulisha kwa urahisi baadaye. Halafu, eneo liligawanywa katika visehemu vidogo zaidi, kila kimoja kikiwa na nyumba karibu 400. Wakati huo kule Uingereza, wale waliokusudia kufunga safari hiyo walikuwa wakijishughulisha na matayarisho yao wenyewe—wakihakikisha kwamba wangeweza kupata usafiri, mahali pa kulala, na vitabu vya Kibiblia vinavyotosha.
Siku ya kuondoka Uingereza ilikuwa Jumamosi, Juni 8, 1985. Alfajiri na mapema ya siku hiyo, wote walikusanyika wakaelekea kwenye uwanja wa ndege. Baada ya muda mfupi, wakawa wanatua katika Belfast, Ailandi Kaskazini. Halafu wakatawanyika kuingia basi ndogo kumi ambazo zingekuwa ndizo usafiri wao katika majuma mawili yenye kufuata. Walipokwisha kuipita Ailandi Kaskazini wakiwa ndani ya basi na kufurahia ukaribishaji wa Kundi la Londonderry, waliuvuka mpaka kisha wakatengana, wakaenda sehemu walizotangulia kugawiwa katika sehemu tatu tofauti za Donegal. Walipokewaje?
Watu wa Kule Wanaitikia
Watu wa Donegal ni wenye urafiki na ukaribishaji, na hivyo ikawa rahisi kusema nao. Hesabu fulani kati yao waliuliza maulizo, na ilifurahisha kufungua Biblia na kuwaonyesha majibu yaliyo wazi. Ilikuwa vizuri pia kuweza kuwaachia vitabu vya Kibiblia wenye kuuliza-uliza maulizo ili waweze kuongeza ufahamu wao wageni wakiisha kuondoka.
Bibi mmoja mwenye kuishi mbali katika nyumba ya shamba la mifugo alikaribisha Mashahidi wawili nyumbani mwake. Mwanamke huyo akakubali haraka kwamba hali za ulimwengu zinaendelea kuwa mbaya na kueleza kwamba huenda watu wengi katika eneo hilo wakasita-sita kukaribisha watu wasiowajua katika nyumba zao kwa sababu ya kuwako ongezeko kubwa la uhalifu katika kieneo hicho cha Ailandi kilichokuwa kitulivu na chenye amani. Watu wengi wenye umri mkubwa walikuwa wamepigwa na kunyang’anywa vitu vyao na vikundi vya wahalifu wenye kutangatanga huko. Basi mbona yeye akawakaribisha Mashahidi nyumbani mwake? Ni kwa sababu walionekana kuwa “watu wa kuaminika sana.”
Mwanamke huyo alipoona kwamba unabii wa Yesu juu ya siku za mwisho ulikuwa ukitimizwa, macho yake yaling’aa, halafu yakajawa na machozi alipopata habari juu ya tumaini la ufufuo. (Mathayo, sura 24; Luka, sura 21) Mume wake alikuwa amekufa miaka 20 kabla ya hapo. Akakubali kwa furaha nakala ya kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani na kutoa ombi la kwamba mtu fulani ajaribu kumtembelea tena.
Mambo ya aina hiyo yalionwa mara nyingi. Kijana mmoja mwanamume alieleza ana mashaka mengi juu ya kuwako kwa Mungu. “Ikiwa Mungu yuko kweli,” akasema, “mbona uovu ni mwingi sana? ” Mashahidi wenye kutembelea wakamwonyesha kwamba karibuni Mungu atajitia katika mambo ya wanadamu na kutatua mengi ya matatizo yanayosumbua kijana huyo mwanamume. Akawaomba wamtembelee tena wakutane na wazazi wake. Mashahidi walipofanya hivyo, wakaacha nakala ya kitabu Kuishi Milele ili jamaa hiyo iweze kupata majibu kwa mengi ya maulizo yao.
Kijana mmoja mwanamke alikuwa amefiwa na mwana wake mwenye umri wa miaka minne majuma kadha yaliyotangulia. Alitiwa moyo sana na habari zilizo katika kitabu Kuishi Milele, hasa na maelezo yacho kuhusu tumaini la ufufuo. Kwa sababu ya huzuni nyingi iliyosababishwa na kifo cha mwanaye, mwanamke huyo alikuwa ametia shaka kama kweli kuna Mungu. Lakini aliposomewa maandiko yanayoonyesha hali ya wafu na tumaini linalowahusu, sura yake ilibadilika. Kwa sababu gani? Kwa sababu alitambua kwamba mwanaye yu katika amani, amelala katika kifo akiwa na uwezekano wa kufufuliwa.—Mhubiri 9:5, 10; Yohana 5:28, 29.
Wawili kati ya Mashahidi wenye kutembelea walienda shule moja, na mwalimu akawakaribisha waingie katika darasa lililojawa na wanafunzi wachanga 30. Mwalimu huyo alikubali kwa furaha nakala ya kichapo Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia kisha akaliambia darasa: “Alasiri hii tutaelezwa hadithi katika kitabu hiki.” Baadaye, kikundi hicho cha Mashahidi kilipokuwa kikila chakula cha mchana pale karibu, wengine wa wanafunzi walikuja kuwasalimu. Walimu wengine wawili wakafika pale wajue kulikuwa na jambo gani, nao pia wakakubali kwa furaha kuchukua nakala za kitabu kile.
Baadaye siku hiyo, mmoja wa Mashahidi alikutana na mvulana wa miaka 11 na kumuuliza: “Wewe umepata kusikia juu ya Mashahidi wa Yehova? ” “Ndiyo,” mvulana akasema, “leo shuleni.” Halafu mvulana huyo akaomba nakala ya kitabu Hadithi za Biblia. Baadaye tena, kwenye nyumba ambayo mama wa kule hakukubali kukichukua kitabu Kuishi Milele, mtoto mdogo wa nyumba hiyo alisema aliona kitabu Hadithi za Biblia shuleni. Kwa hiyo mama akakubali kuchukua nakala ya kichapo hicho.
Kwa Watu wa Kila Namna
Kwenye nyumba moja, Mashahidi wenye kutembelea walionyesha mwanamke mwenye umri mkubwa picha zilizo katika kitabu Kuishi Milele. Bibi huyo akasema kitu alichohitaji hasa ni Biblia. Kwa hiyo Mashahidi wakafurahia kumtolea nakala ya New World Translation of the Holy Scriptures. Alipokwisha kuipata Biblia, bibi huyo akafurahi kuchukua nakala ya kichapo cha kujifunzia Biblia pia. Akawaambia wageni wake kwamba alikuwa amepata habari kwamba Mashahidi wamekuja katika eneo kisha akasali kwamba waweze kumtembelea na kumletea Biblia. Sasa alijisikia kwamba sala yake ilikuwa imejibiwa.
Kijana mwanamume mwenye umri wa miaka 30 na kitu alikaribisha Mashahidi wawili nyumbani mwake. Baada ya mazungumzo mafupi ya Kimaandiko, alisema: “Labda ninyi hamtafurahi mkijua mimi ni nani. Mimi ni padri.” Mashahidi wakasema wangefurahi kusema naye, naye padri akawauliza maulizo mengi juu ya imani zao. Alipouliza juu ya matumizi ya jina Yehova, wageni wale walifurahi kumtolea nakala ya broshua Jina la Mungu Litakaloendelea Milele. Yeye pia alikubali nakala ya kitabu Kuishi Milele, kichapo ambacho pasipo shaka kitamsaidia kupata majibu ya maulizo yake mengi.
Katika pindi nyingine, Shahidi mmoja mwanamke alifikiwa na kijana mwanamume aliyemsikia akizungumza na mfanya kazi wa mapokezi katika hoteli. Mtu yule akamuuliza maulizo kama, “Mbona ulimwengu una mvurugo mwingi sana? ” Shahidi alifurahi sana kumweleza mambo aliyokuwa amejifunza kutokana na Biblia juu ya jambo hilo na habari nyingine zinazohusiana. Naye kijana huyo alikuwa nani? Padri mwenye kulikiza katika eneo hilo.
Mbali na ile kazi ya kawaida ya kuhubiri nyumba kwa nyumba, nafasi nyingine zilitumiwa kusema na watu wa namna zote. Mahali pamoja pa milimani, moja ya basi zile ndogo ilisimama kando ya barabara kuwezesha baadhi ya abiria waliokuwamo watoe viatu vya mjini na kuvaa vya mpira kwa ajili ya safari ya kukanyaga majani kuni zenye majimaji ziliyoozea udongoni ili wakaseme na kikundi cha wanaume wenye kukata kuni hizo kwa matumizi ya majira ya baridi. Kikundi kingine kilisimama mahali pa kuvutia kando ya ziwa la mlimani katika msitu. Ndani ya gari lililokuwa karibu alikuwa amelala mfanya kazi wa kituo cha nguvu za umeme akifurahia upweke wa pumziko la mchana. Amani yake iliharibiwa, lakini akafurahia mazungumzo ya kusisimua sana naye akahudhuria mkutano kiliopangiwa kikundi jioni hiyo.
Mwanamume mwingine alikuwa akiendesha tingatinga barabarani wakati Shahidi alipomsimamisha akamuuliza kama ana dakika chache za kuongea. Alikuwa na hamu ya kuongea habari za Biblia, hasa kuhusu “nyakati za hatari” tunamoishi. (2 Timotheo 3:1-5) Alizidi kupendezwa sana alipoonyeshwa picha zilizo katika kitabu Kuishi Milele. Mwanamume huyo akafurahi sana kusikia kwamba kichapo hicho kingeweza kutumiwa kwa mazungumzo ya Kibiblia pamoja na jamaa na kusema kwamba angeanza mara hiyo kukitumia kufundishia watoto wake sita.
Wahudumu wale wenye nishati nyingi wa umri wote, pamoja na kikundi kile kidogo cha Mashahidi wa Donegal, wana sababu nzuri ya kufurahishwa na jitihada zao. Wakati wa majuma mawili ambayo wageni wale walikuwa kule, walitumia saa 5,767 wakiongea na wengine juu ya Biblia. Waligawa vitabu na Biblia 1,613, pamoja na nakala 2,611 za magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Kilichothaminiwa sana na wenye nyumba fulani ni fasiri ya Kiailandi ya kichapo Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia.
Wageni wale hawakwenda Donegal ili wakafundishe maoni yao binafsi kwa kiburi wala kwa kujiona kuwa waadilifu. Bali, wao walitaka kushiriki habari njema pamoja na watu ambao, kwa sababu ya kuishi katika eneo la mbali, huenda wakawa hawakupata nafasi nyingi za kuzisikia. Akieleza juu ya safari ya mapema zaidi ya namna hiyo, gazeti moja la kule lilikuwa limewaita wenye kuishiriki shughuli hiyo “mbayuwayu.” Inaonekana kusudi lilikuwa kudokeza kwamba walikuwa huko muda huo wa kiangazi tu na karibuni wangeruka waende zao. Lakini “mbayuwayu” hao, au wengine walio kama wao, watarudi kusaidia watu wenye mioyo minyoofu wapate maarifa sahihi juu ya ahadi nzuri ajabu za Biblia. Kwa kweli, wengine walioshiriki mapema zaidi katika safari za kutoa ushahidi wameenda kukaa daima katika Donegal.
“Imekuwa ndiyo safari iliyo bora zaidi kufikia sasa.” Hayo ni kati ya maneno ya uthamini na furaha yaliyosemwa na wengine walioishiriki shughuli hiyo ya kujaribia. Wao waliuona ukweli wa mithali hii ya Biblia: “Nafsi ya mwenye ukarimu itanenepa, naye anayenywesha, atanyweshwa mwenyewe.” (Mithali 11:25) Ndiyo, ilikuwa baraka kubwa kushiriki katika jitihada ya pekee kutangaza habari njema katika Donegal. Je, wewe unaweza kushiriki utumishi wa aina hiyo yenye kuthawabisha katika sehemu yenu ya shamba la ulimwengu ambalo sasa liko tayari kwa mavuno tele?
[Ramani/Picture katika ukurasa wa 29]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
DONEGAL
AILANDI KASKAZINI
Londonderry
Belfast
AILANDI
[Map]
ULAYA
BAHARI KUU ATLANTIKI
[Picture]
Walifurahi sana kutangaza habari njema katika Donegal
[Picha katika ukurasa wa 30]
Kutoa ushahidi nyumba kwa nyumba katika Ailandi ya kaskazini-magharibi