Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 9/1 kur. 28-30
  • Je! ni Lazima Uwe Mashuhuri?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! ni Lazima Uwe Mashuhuri?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ‘Wote Watakuwa na Fungu Lao’
  • Utumishi Wenye Kiasi, wa Nafsi Yote
  • Matokeo kwa Wale Wanaotumikia kwa Unyenyekevu
  • Kuchagua Mitume Wake
    Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi
  • Kuchagua Mitume Wake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Yesu Achagua Mitume Kumi na Wawili
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
  • Yehova Hupendezwa Sana na Utumishi Wako wa Nafsi Yote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 9/1 kur. 28-30

Je! ni Lazima Uwe Mashuhuri?

KIWAMBO cha TV chaanza kazi wakati kamera zinapoelekezwa juu ya mchezaji yule yule mashuhuri. Akianza kwa tabasamu ya kuzoelea kazi yake, anaanza kucheza. Tunafurahia kusikiliza muziki wake. Kamera inamkaribia, ikituwezesha tutazame ishara zake za usoni na vidole vyake vyenye ufundi mwingi anapopiga muziki kutokana na chombo chake.

Ndiyo, mwenye kucheza ndiye anayefurahia umashuhuri. Lakini wonyesho ule ukiisha, ebu angalia ile orodha ndefu ya pongezi inayokuwa katika kiwambo​—wanamuziki wenzake, kiongozi wao, mafundi wa mitambo ya sauti, wapiga picha, wakurugenzi, watengenezaji wa kipindi, wastadi wa kupamba jukwaa, na wengine wengi sana. Wote wanahitajiwa sana ili wonyesho ule ufanikiwe. Wote wanauunga mkono.

Hali kama hiyo imo katika kundi la Kikristo. Watu fulani wanatumiwa kwa njia ya umashuhuri sana. Lakini, wengine wanashiriki sehemu ambazo kidogo ni kama hazionekani sana wakiwa wahubiri wa kikawaida tu wa ujumbe wa Ufalme. Lakini, je! watu wa namna hiyo wajione kwamba si wa maana sana kwa sababu ‘si watu mashuhuri? Je! wasumbuke isivyofaa wasipopata umashuhuri?

‘Wote Watakuwa na Fungu Lao’

Masimulizi mamoja yanayohusu Mfalme Daudi yanafunua mambo mengi. Biblia inaonyesha kwamba yeye aliongoza kikosi cha wanaume 400 katika shughuli ya uokoaji yenye kutazamisha. Walienda wakakomboe jamaa na mali zao mikononi mwa kikosi cha watekaji. Ingawa hivyo, mia mbili waliachwa nyuma walinde mizigo. Wakati kile kikundi cha uokoaji kiliporudi kikiwa kimeshinda na kuja pamoja na wanawake, watoto, na bidhaa, kuongeza na nyara nyingi, tatizo lilitokea: Ni nani ambao wangeshiriki nyara zilizotekwa piganoni? Je! ni wale tu walioshiriki hasa kupigana ndio wangehesabiwa wamestahili kushiriki mapato hayo? Daudi alitoa jibu lililokuja kuonwa kuwa mfano halali wa kufuatwa, “amri na agizo la Israeli.” Alisema: “kwa kuwa kama lilivyo fungu lake yeye ashukaye vitani, ndivyo litakavyokuwa na fungu lake huyo akaaye karibu na vyombo; watagawiwa sawasawa.” (1 Samweli 30:24, 25) Yehova ndiye aliyemwelekeza Daudi afanye uamuzi huo wa hukumu. Nao ulionyesha jinsi Yehova anavyothamini sana wale wanaotumikia katika vyeo vya kuunga mkono.

Lakini je! kanuni hiyo ingali hivyo katika kundi la Kikristo? Mtume Paulo anajibu kwa kutoa mfano. Akilinganisha kundi na mwili wa kibinadamu, yeye anasema: “Jicho haliwezi kuambia mkono: ‘Mimi sikuhitaji wewe’; au, tena, kichwa hakiwezi kuziambia nyayo: ‘Mimi siwahitaji ninyi.’” Ndiyo, katika mwili wa kibinadamu kila sehemu​—hata kile kidole kidogo cha mguu​—ina kazi ya maana. Mungu anaonyesha hekima ile ile katika kulipanga kundi lake kitengenezo. “Mungu ameweka wale watu mbalimbali katika kundi,” akagawia watu tofauti-tofauti madaraka mbalimbali.​—1 Wakorintho 12:21, 28, NW.

Katika karne ya kwanza, kwa sababu hiyo Wakristo fulani walifurahia kiasi fulani cha umashuhuri. Kwa mfano, Petro alikuwa mashuhuri sana. Yeye ndiye aliyekuwa mnenaji kwa ajili ya mitume siku ile inayojulikana sana ya Pentekoste. (Matendo 2:14) Ndiye aliyekuwa na pendeleo la kusaidia waongofu wa kwanza wa Mataifa wawe Wakristo. (Matendo 10:44-48) Kwa kweli, vitabu viwili vya Biblia vina jina lake! Hata hivyo baadhi ya mitume wale wengine hata hawatajwi sana. Mathayo, Nathanaeli (Bartholomayo) Thadayo (Yuda, mwana wa Yakobo), Simoni yule zelote (mwenye bidii), na Yakobo, mwana wa Alfayo (aliyeitwa Yakobo yule Mdogo), wanatajwa kwa ufupi tu. Hata hivyo, wao walimwunga mkono kwa uaminifu Bwana wao katika shughuli yake ya kuhubiri na kufundisha.

Utumishi Wenye Kiasi, wa Nafsi Yote

Hali kama hiyo ipo leo. Katika kundi la Kikristo, bado Yehova ‘anaweka washiriki kama vile yeye apendavyo.’ Jambo hilo linafanya wengine mashuhuri zaidi ya wengine. Lakini mwelekeo wetu unapaswa kuwa nini juu ya mapendeleo yetu ya utumishi, vyo vyote yalivyo? Wakolosai 3:23, 24 inaeleza hivi: “Lo lote mfanyalo, lifanyeni kwa moyo, kama kwa [Yehova], wala si kwa wanadamu, mkijua ya kuwa mtapokea kwa [Yehova] ujira.”

Mashahidi wengi leo wanapata furaha ya kweli kwa kutumikia wakiwa katika vyeo vya kiasi, vya kuunga mkono tu wale wengine. Kwa mfano, fikiria Edmundsen, Shahidi anayetumikia katika Pietermaritzburg, Afrika ya Kusini. Yeye alibatizwa mwaka 1946 na akaingia utumishi wa wakati wote mwaka wa 1950. Kwa kweli yeye hajapata kamwe kuwa mashuhuri. Lakini, amekuwa na furaha ya kuona 15 kati ya watoto na wajukuu wake wakiwa Mashahidi walio wakfu na kubatizwa, na wengine 27 wa wajukuu na vijukuu vyake wakihudhuria mikutano ya kundi! Na leo, ingawa ana kizuizi cha kutosikia na kutoona vizuri, anatumikia kwa uaminifu akiwa mhubiri msaidizi wa wakati wote. Akiwa na umri wa miaka 84 angali akitumikia akiwa mzee katika kundi na anatoa hotuba za watu wote! Hata hivyo, sana-sana kiasi kikubwa cha utumishi wa Edmundsen kimekuwa kikifanywa katika nafasi zisizo za umashuhuri sana. Lakini kama maelfu mengi ya watumishi waaminifu wa Yehova, yeye ametolea Yehova utumishi wenye thamani kubwa na wenye maana.

Ndiyo, inahitaji unyenyekevu ili kutumikia katika nafasi zisizo za umashuhuri sana. Lakini kufanya hivyo kunaturuhusu pia wakati wa kusitawisha nyutu zetu na ustadi wa kufanya mambo mbalimbali kabla ya kutupiwa madaraka mazito. Mfalme Yosia akawa mfalme wa Yuda akiwa na umri wa miaka minane. (2 Wafalme 22:1) Lakini yeye angaliwezaje kuwa alikuwa tayari kwa cheo hicho? Kwa upande mwingine, Musa alipasishwa kukaa miaka 40 bila kuwa mashuhuri akiwa mchungaji katika Midiani kabla ya kuwa mkombozi. Wakati wa kipindi hicho yeye alisitawisha sifa kama vile upole. (Hesabu 12:3) Alijifunza kumngojea Yehova. Na wakati mwishowe Yehova alipomwita aongoze Israeli kwa miaka 40 iliyofuata, yeye alikuwa tayari kwa daraka hilo!

Kwa hiyo mtu anayehisi kwamba uwezo wake hautumiwi kikamili katika kundi hahitaji kufa moyo. Labda Yehova anaona kwamba ni lazima mtu huyo asitawishe subira au unyenyekevu zaidi kabla hajapewa mapendeleo zaidi. Kumbuka, pia, kwamba hesabu iliyo kubwa zaidi ya watumishi wa Yehova wanatumikia katika vyeo visivyo vya umashuhuri sana. Mnara wa Mlinzi umekuwa sehemu mashuhuri ya programu ya funzo la Mashahidi wa Yehova kwa zaidi ya karne moja. Hata hivyo wenye kuliandika gazeti hilo hawatajwi majina. Fikiria, pia, yale maelfu mengi ya wenye kutumikia katika makao ya Betheli au wakiwa mapainia na wamisionari. Ni mara chache sana wanapokuwa mashuhuri. Hata hivyo wao wanafurahia maisha zenye shughuli nyingi na za kuthawabisha, tena wanapata uradhi mwingi sana unaotokana na kujitoa wasaidie wengine.​—Matendo 20:35.

Matokeo kwa Wale Wanaotumikia kwa Unyenyekevu

Kati ya wale mitume wa kwanza 12, ni mmoja tu aliyeshindwa​—yule msaliti Yuda Iskariote. Wengine walifurahia thawabu tukufu. Kwenye Ufunuo 21:10, 14 Biblia inaueleza ule “mji mtakatifu” kuwa umejengwa juu ya mawe ya msingi 12. Juu ya kila jiwe, limeandikwa jina la mtume mmoja wa Mwana-Kondoo. Kwa kupendeza, wawili wa mitume hao waaminifu waliitwa Simoni. Yule mmoja mwenye kuitwa Simoni Petro alikuwa mashuhuri sana; yule mwenye kuitwa Simoni zelote (mwenye bidii) hakuwa mashuhuri sana. (Matendo 1:13) Kwa kweli, ni machache sana yanayosemwa juu ya Simoni huyo. Lakini Simoni wote wawili walipokea thawabu ile ile moja​—pendeleo la kuwa washiriki wa msingi wa serikali ya kimbingu iliyo chini ya Mfalme Yesu Kristo!

Bila shaka, si wapakwa-mafuta wote waliofufuliwa watakaotumikia kwa umashuhuri wakiwa ‘mawe ya msingi.’ Yehova atatumia wafanya kazi wa serikali yake kwa nafasi yo yote atakayowafikiria kuwa wanaifaa zaidi. Wale kati yetu tulio na matumaini ya kuishi milele katika Paradiso duniani tunaweza vivyo hivyo kuwa na uhakika kwamba chini ya mpango huo, Mfalme wetu atatutumia kwa njia bora zaidi iwezekanavyo. Tukiwa na mazingira ya kupendeza, wenzi washikamanifu, namna-namna za kazi ya kufurahika, na bila kizuizi na uchovu, nyutu na ustadi wetu utasitawishwa ukafikie kiwango kamili!

Kwa hiyo kama tumeitiwa thawabu ya kimbingu au tunatazamia uzima katika dunia iliyorembeshwa, na turidhike na mgawo katika tengenezo la Yehova kisha tuutimize kwa nafsi yote. Huo ndio mwendo wa hekima na furaha. Badala ya kutafuta makuu kwa kutaka umashuhuri sana, sitawisha mwelekeo wa unyenyekevu aliokuwa nao Mfalme Daudi aliyesema hivi: “Neno moja nimelitaka kwa [Yehova], nalo ndilo nitakalolitafuta, nikae nyumbani mwa [Yehova] siku zote za maisha yangu. Niutazame uzuri wa [Yehova], na kutafakari hekaluni mwake.”​—Zaburi 27:4.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki