Kijia Kisicho na Mwisho
Kama ilivyosimuliwa na Eva Carol Abbott
NILIZALIWA mwaka 1908, katika mwezi wa Desemba siku ya 21. Nilizaliwa nikiwa mtoto wa Grace Pearl na William Reuben Vaughan. Mahali pa kuzaliwa palikuwa shamba moja lililo karibu na Emporia, Kansas, United States (Amerika). Tulitoka Emporia tukahamia nyika za Colorado, ambako maisha yalikuwa magumu na ya upweke. Tulikuwa na ghala ya nafaka, kinu kilichojengwa kuendeshwa na upepo, na nyumba ambayo Mama alinieleza kuwa ilifanana kidogo na behewa la gari-moshi. Kulikuwa na eneo kubwa sana la kupikia chakula na chumba kingine kikubwa kilichokuwa muungano wa sebule na chumba cha kulala.
Ingawa hivyo, wengine wa majirani wachache sana waliokuwako waliishi katika mahandaki. Makao hayo yalikuwa yameinuka nusu juu ya udongo na nusu ile nyingine ikiwa chini ya udongo. Wakati wa sehemu fulani za majira yale marefu ya baridi, vijumba vyao vilikuwa vikifunikwa kabisa na theluji. Katika pindi hizo wazazi wangu walipigiwa-pigiwa simu na majirani hao waliofungiwa na theluji (yaani, wao walikuwa na simu ingawa walikuwa maskini sana) kumwuliza ni saa ngapi na baada ya kuambiwa, ulizo lililofuata lilikuwa, ‘Unamaanisha saa za usiku au za mchana?’
Mara kadhaa kwa mwaka wakaa-vijumbani, kama sisi tulivyoitwa, walikuwa wakienda kwenye “Mierezi” muda wa siku nyingi kwa safari moja ili kukata vigingi. Vigingi hivyo vilikuwa vikirundikwa mpaka vinafika juu katika mikokoteni ya farasi wenye maungo yenye nguvu na kupelekwa mjini ili kuvibadilishana kwa chakula, kwa vifaa vya kutumia katika majira ya baridi, na kwa mbegu za wakati wa kiangazi za kupandwa ili tupate mavuno. Wakati wa vipindi hivyo Mama alikuwa akikaa peke yake na mimi, na nyakati za jioni hizo ndefu alikuwa akiendelea kuwasha taa ya mafuta mpaka usiku wa manane, huku akisoma Biblia yake na kurudia kuisoma. Yeye aliamini kwa uthabiti kwamba Mungu ana kundi fulani la watu wake, naye akawa akitafuta kijia chenye kuelekeza waliko.
Nilipokuwa na umri wa miaka mitatu, wazazi wangu walihamia shamba moja katika Kansas karibu na mji mdogo wa Kiowa. Walifunga sehemu moja ya safari hiyo kwa kutumia mkokoteni wa farasi. Baba aliifunika sehemu ya juu ya mkokoteni kwa kutumia kitambaa kizito. Mimi nikawa mgonjwa sana kwa kupatwa na homa kali sana ya wakati huo, nami nakumbuka nililalia godoro ya majani makavu kwenye sakafu ya mkokoteni wa farasi, mahali pazuri na penye joto, huku nikiitazama ile taa ya mafuta ya makaa-mawe iliyokuwa ikicheza-cheza kwa kuangikwa katika kitambaa kizito cha mkokoteni kilichokuwa juu yangu. Mama alikuwa akinisugua kwa mchanganyiko wa mafuta ya nguruwe, mafuta ya miti, na mafuta ya makaa-mawe. Bado mimi nakumbuka jinsi nilivyofurahia kutendewa hivyo, nikahisi joto na upendo uliohusika.
Mwanzo wa Kijia
Kati ya mambo ninayokumbuka juu ya utoto wangu, moja ni kwamba tulihamia Alva, Oklahoma. Bado Mama alikuwa akikitafuta kijia kinachoelekeza kwa “watu wa Mungu.” Siku moja Mama akapata trakti fulani za Biblia juu ya kiingilio cha nyumba yetu. Muda mfupi baada ya hapo Baba yangu alifikiwa na kolpota (mhudumu wa wakati wote) katika duka alimokuwa akifanya kazi, akaonyeshwa kimoja cha vitabu vya mfululizo wa Studies in the Scriptures, kilichotungwa na C. T. Russell, msimamizi wa kwanza wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi. Ingawa Baba alikinunua kitabu hicho, Mama ndiye aliyekisoma na kutambua kwamba ujumbe uliokuwamo ulitokana na chanzo kile kile kama zile trakti zilizoachwa juu ya kiingilio cha nyumba.
Baba alialikwa na kolpota kwenye mkutano wa kujifunza Biblia jioni hiyo. Yeye hakuamua kuenda, lakini Mama alienda, mimi nikaambatana naye. Siwezi kukumbuka vizuri sana juu ya jinsi nilivyohudhuria mkutano huo, lakini nimesikia mara nyingi Mama akieleza kwa urefu jinsi ulivyokuwa. Walikuwako watu kama 10 au 12, na ulizo liliulizwa, “Sisi tunakufaje?” Dada mmoja aliyekuwapo akajibu, “Kama mnyama asiyejua kitu.” Mama alishtuka. Akakatiza akisema: “Pole kwa kukatiza, lakini Je! mmesema mnaamini kwamba sisi tunakufa kama mnyama asiyejua kitu?” Ndugu mwenye kuongoza mkutano huo akajibu: “Tafadhali fungua Mhubiri 3:19-21 ujisomee mwenyewe.”
“Waliniacha nikauvunja mkutano wote huo kwa maulizo yangu yenye kufuatana-fuatana, wakatumia jioni yote kuyajibu,” Mama akawa akifurahia sana kunieleza. Nakumbuka kwamba Mama alikuwa na msisimuko mwingi aliporudi nyumbani. Hakika yeye alikuwa amepata watu wa Mungu na mwendo wa maisha aliotaka kufuata. Huo ulikuwa ndio mwanzo wa kile kijia!
Huo ulikuwa mwaka 1913. Baada ya muda usio mrefu ile sinema ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi yenye slaidi pia ilionyeshwa, yenye kuitwa “Mchezo wa Kuigiza Wenye Picha za Uumbaji.” Mama alifurahi sana kuwa mmoja wa wakaribishaji wakati ilipokuwa ikionyeshwa katika jumba la mawonyesho la mjini. Miaka hiyo tuliokuwa katika Alva ilichangamsha moyo wa Mama. Mimi nikawa nikimwambia, “Mama, siku hizi wewe unatabasamu, na zamani hukuwa ukifanya sana hivyo.”
Kufikia sasa Mama alikuwa amechukua msimamo imara kwa ajili ya ukweli. Huo ni wakati ambao Wanafunzi wa Biblia wengine waliamini kwamba wangepelekwa mbinguni siku yo yote ile ya muda huo, kwa hiyo wakawa na maoni ya kwamba wangepata maisha ya starehe baada ya muda mfupi. Lakini Mama hakuwa na maoni hayo. Yeye hakuvutwa sana fikira na matazamio ya kupelekwa mbinguni mara hiyo hiyo. Mama ‘alikuwa mwenye shughuli mno,’ kama yeye alivyosema: “akipata habari za mambo asiyokuwa amejua, akijifunza, akienda mikutanoni, na kushiriki kuzihubiri habari njema za Ufalme.’
Baada ya muda mfupi Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilivuma kweli kweli, basi mateso yakaletwa na watu wa mjini. Nakumbuka nilienda na Mama mlango kwa mlango kupata sahihi za watu, zikiomba serikali ya United States ifungue Ndugu Rutherford na washirika saba wenzake kutoka gereza la serikali la Atlanta, Georgia, ambako walikuwa wamefungwa bila haki. Lakini jambo jingine likatukia ambalo lilitulazimisha kuhama.
Vita ilikwisha, na ambukizo la ile homa kali likaenea kweli kweli. Homa hiyo ilifanya Mama akaisha sana kimwili. Daktari akamshauri Baba amhamishe kumpeleka kusini mwa California ambako majira yangekuwa mazuri zaidi. Tulifika katika Los Angeles na kutulia katika Alhambra, kimoja cha viunga vya jiji hilo. Huko ndiko nilikoelekeana na uamuzi ulio mkubwa zaidi wa maisha yangu.
Mwaka 1924 msichana rafiki yangu na mimi tulipanda gari-moshi kwenda Los Angeles kuhudhuria maziko ya dada mmoja Mkristo tuliyependezwa sana naye. Wakati wa safari ya kurudi, tulizungumza habari ya uteule (ambayo sasa unajulikana kuwa wakfu). Mimi nilianza kufikiria maisha yangu mwenyewe kwa uzito na kuzungumza jambo hilo na Mama. Kwa sababu hiyo nilichunguza-chunguza habari hiyo nikitumia nakala zilizorudiwa kuchapwa za Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), nikasoma kila jambo lililohusu uteule kurudi nyuma mpaka mwaka 1908. Muda mfupi baada ya hapo niliweka maisha yangu wakfu kwa Yehova, na katika Oktoba 1925 nikabatizwa.
Wenzi Katika Kijia
Siku moja katika mwaka 1927, niliambiwa kwamba ndugu mmoja jina lake Herbert Abbott alitaka kuniona. Mimi niligutuka, kwa kuwa hata sikumjua yeye. Lakini haikunichukua muda mrefu kujua alikuwa nani. Kujua kwamba mimi nilikuwa na umri wa miaka 18 na kwamba nilikuwa nimeteuliwa kwa miaka miwili, kulimpendeza yeye. Tulijulishwa kwa mmoja na mwenzake, tukachumbiana muda wa miezi mitatu, na kufunga ndoa katika Julai 1927.
Herbert na mimi tulinunua nyumba katika vilima vizuri vya Pasadena. Siku moja katika masika ya mwaka 1928 mimi nilileta barua nyumbani, na ndani mlikuwa na habari zilizohusu utumishi wa painia. Jioni wakati Herbert alipokuja nyumbani kutoka kazini, nikamtolea wazo la kwamba tuuze nyumba yetu tuingie utumishi wa painia wa wakati wote. Yeye akasema kwamba kama mimi nilikuwa na nia ya kuacha vitu vyote, yeye hangeweza kukataa.
Tulipokea eneo katika Mji wa Charles, Iowa, ambalo tungelifanyia kazi baada ya kuhudhuria mkusanyiko katika Detroit, Michigan. Kufikia wakati wa kiangazi mipango yetu ya kupainia ilikuwa imekamilika, lakini tulishangaa kujua kwamba nilikuwa na mimba. Tungefanya nini? Kubadili mipango yetu sasa kungekuwa kama kusema: “Yehova, tunajua kwamba wewe ungeweza kututunza sisi wawili lakini si watu watatu.”
Baada ya mkusanyiko, Herbert na mimi tulienda kwenye mgawo wetu katika Mji wa Charles. Lakini kufikia karibu mwezi wa nane wa mimba yangu ilionekana ni hekima kurudi Los Angeles. Mapema katika mwezi Januari wa mwaka 1929, Perousia Carol binti yetu mwenye sura nzuri alizaliwa. Ingawa hivyo, furaha tuliyokuwa nayo pamoja naye iliendelea kwa miezi tisa tu; katika Oktoba yeye alikufa.
Ahadi ya Yehova ya ufufuo ndiyo hasa tuliyoweka akilini mwetu. Lakini, kifo ni adui, nasi tulijisikia tumeachwa ukiwa kumwona binti yetu mdogo sana aliyekufa! Lile wazo la kuumiza kwa kumfikiria mpendwa wetu mdogo akiwa amelala katika udongo baridi lilitulizwa na maarifa yetu ya kujua Neno la Mungu. Yeye alikuwa amelala tu; angebaki katika kumbukumbu la Yehova. (Yohana 11:11-14, 23-25) Kwa kweli, tangu alale ni muda mrefu umepita, lakini siku moja wakati ujao yeye ataamka athibitishe Neno la Mungu ni kweli. Tamaa yangu inaendelea kuwa kwamba yeye apate kuletea jina kuu la Yehova sifa milele.
Vijia na Magari ya Kupita Vijiani
Tulifanya tena mipango ya kupainia. Mwezi Machi uliofuata tukanunua gari la kukokotwa lililofunikwa kwa kitambaa kizito chenye kukunjika katika sehemu ya juu, kisha tukabadilishana gari letu Studebaker lenye nafasi ya abiria saba tukapata gari la “Ford Muundo A” la kuvuta ile sehemu nyingine ya kukokotwa. Hivyo ndivyo ilivyoanza miaka yetu 25 ya kufuata vijia na kuendesha magari yaliyopita vijiani.
Lile gari dogo la kukokotwa tulilofurahia sana kulitumia kuteremka barabarani liliendelea kututumikia kwa miaka zaidi ya minane. Eneo la sakafu lilikuwa meta 1.2 kwa meta 1.5, na nafasi ya kupikia ilikuwa ubao mmoja wa sentimeta 28 kwa 30, nao ulivutwa ukatokezea wakati wa kupika. Palikuwa na vitanda viwili vizuri, jiko la kutumia gasolini lenye mahali pawili pa kutokea moto. Pia tulikuwa na ndoo ya maji, taa yenye kutumia gasolini, mtungi wenye kupasha maji moto kwa kutumia mafuta ya makaa-mawe, birika kubwa la kuogea, ubao wa kufulia nguo, pasi yenye kutumia gasolini, na ubao wa kupigia pasi. Pia humo ndani ulikuwa na rafu yenye kubebeka kwa urahisi iliyokuwa juu ya mahali ambapo lile jiko lilikuwa. Hapo palikuwa na kabati ndogo pia ambamo mimi niliweka vikombe na visahani vyetu vya namna ya “Haviland China,” tulivyokuwa tumepewa kama zawadi ya arusi. Usiku mmoja vikomeo vilivyokuwa vimeishikilia rafu vilikatika, nayo rafu ikateremka chini na kuanguka pa. Ilianguka pia ile taa ya gasolini ikiwa juu chini, lakini haikuvunjika. Lakini vile vyombo vyetu vya kupendeza sana vilivunjika vipande vipande!
Mara chache tulilazamika kuondoa ile sehemu ya juu ya kitambaa kizito katika gari letu la kukokotwa na kuweka kingine. Ili kufanya hivyo tulikuwa tukinunua vitambaa vizito walivyokuwa wakivitumia wakuza-matunda ili kufunika michungwa yao wakati wa kupiga dawa. Tulikuwa tukivikata vitambaa hivyo viwe visehemu vyembamba virefu, kisha tunavishonelea katika kitambaa cha gari letu kwa kutumia sindano za mviringo mpaka hatimaye sehemu hiyo ya gari inafunikwa.
Jumatatu ilikuwa siku ya kufua nguo. Tulikuwa tukipasha maji moto katika moto tuliowasha nje na kusuza nguo hizo katika maji tuliyoteka katika kijito, mto, au katika kisima cha mjini. Tulikuwa pia na jiko dogo la kuokea ambalo lingeweza kukunjwa, nami nilikuwa nikilitumia kuoka keki za kuliwa saa za mchana katika juma ambalo lingefuata. Sasa tukawa tayari kukabiliana na hali za kutatiza katika eneo letu.
Katika miaka ya 1930 watu walihama sana wakatoka mashambani kwenda mijini. Nyakati nyingine tulikuwa tukifuata barabara fulani kisha inajipinda kuelekea nyumba fulani mwendo wa maili nyingi kupita katika milima na mabonde yenye mito, kumbe tunakuta nyumba hiyo imeachwa na wenyewe. Ili kutatua tatizo hilo, tulitumia vioo vya kuonea mbali tujue kama nguo zilikuwa zimeanikwa nje kwenye kamba au kama nyumba yenyewe ilikuwa ikitoa moshi, au labda kama walikuwako ng’ombe. Kufanya hivyo kulituokolea wakati na petroli. Bila shaka, si sikuzote tulipoweza kuona kama kulikuwa na nyumba barabarani, kwa hiyo tulikuwa tukiuliza majirani kama barabara yenyewe ilielekeza kwenye nyumba fulani.
Wakati mmoja hatukujua la kufanya. Kulikuwa na shamba kubwa lenye majani ya kulishia ng’ombe kilometa 24 ng’ambo ya milima, lakini majirani hawakuwa na uhakika kama nyumba hiyo ilikuwa na mtu. Ilikuwa lazima tufikirie kuepuka kupoteza petroli kwa ajili ya kesho yake. Tulikuwa karibu na kijito safi cha milimani chenye upana wa meta kama 1.2 au 1.5, naye Herbert aliona kiu. Alipiga magoti apate kunywa maji, halafu akaona kitu kikimeta-meta. Alinyosha mkono akaokota katika sakafu ya kijito hicho sarafu za pesa zilizokuwa za dola kadha. Kwa hiyo, bila shaka, hatukusita-sita tena bali tulisonga mbele. Ilikuwa safari ndefu na ngumu, naye bwana shamba hakupendezwa, lakini sisi tulijua kwamba tumelimaliza eneo, na kwamba bwana shamba huyo alikuwa ameupokea ushahidi.
Mambo Tuliyoona Kwenye Kijia Hiki
Muda wa miaka iliyopita tuliona mambo mengi ya kusisimua, na kuchekesha pia. Kwa mfano, kuna wakati tulipokabili jeuri ya watu wenye ghasia katika Corning, California. Mimi na dada wengine wanne tulienda kumsaidia Aleck Bangle (ambaye sasa ni mmisionari katika Jamaica) aliyekuwa akipigwa barabarani. Walikuwako watazamaji zaidi ya mia moja, wote wakimshangilia mwenye kumtesa. Sasa inachekesha ninapokumbuka kwamba nilivua kiatu changu chenye kisigino kilichochongoka nikamgonga yule mtesi kichwani alipokuwa akijikunja amwangushie Ndugu yetu Aleck dharuba kali!
Toleo la Mei 29, 1940 la Consolation (ambalo sasa ni Amkeni!) lilikuwa na picha ya rais wa tatu wa Amerika, Thomas Jefferson, na bendera ya Amerika katika jalada. Kwa kuwa siku hizo zilikuwa za matata na mateso, mimi niliona ingekuwa vizuri sikuzote kwenda nikiwa na nakala kadha za matoleo hayo katika mfuko wangu wa magazeti, iwapo ingetukia kwamba tungehitaji nakala ya kutumia. Na ndivyo ilivyokuwa. Jumamosi moja nilipokuwa nikitoa ushahidi kwa kutumia magazeti barabarani, nilifikia wanaume wawili kwenye pembe ya barabara. Mmoja, aliyekuwa mtu mwenye sura kali sana, alisema hivi kwa ugomvi: “Ewe bibi mchanga, kama ungekuwa na nakala moja yenye bendera ya Amerika ningeichukua, lakini ninyi Mashahidi wa Yeho—” Kabla yeye hajaweza kusema neno jingine, bila shaka jibu langu lilikuwa hili: “Mheshimiwa, nafurahi sana kwamba ninayo nakala ile ile unayotaka,” nami nikalitoa toleo hilo katika mfuko wangu wa magazeti. Aliacha kuchezesha-chezesha sarafu za pesa alizokuwa nazo mfukoni mwa suruali yake, rangi ya uso wake ikabadilika kwa kuona aibu, akasita-sita katika usemi, na kunipa mchango wa gazeti hilo—nami nikampa gazeti lenyewe!
Niliona jambo jingine la kuchekesha, wakati tulipokuwa tukigawia viongozi wa kidini kijitabu cha pekee—The Kingdom, the Hope of the World. Kwenye nyumba moja, kiongozi wa kidini aliitika nilipopiga hodi. Yeye hakupendezwa hata kidogo kukipokea, lakini maagizo tuliyokuwa tumepewa ni kwamba tukiache kijitabu hicho mlangoni ikiwa inawezekana, kwa hiyo mimi nikasema hivi kwa furaha: “Hii ni nakala yako, mheshimiwa, nami nitakuwekea hapa tu.” Nikageuka niende zangu, na nilipokuwa nikitembea katika njia iliyoteka kwenye nyumba hiyo, kile kijitabu kilirushwa kikanipita na kuanguka chini karibu na kisehemu chenye maji machafu ya mvua. Mimi nilikiokota, nisitake kukiache pale, lakini dakika hiyo mbwa mkubwa sana akanifuata akinigurumia, akakinyakua kijitabu hicho nilichokuwa nikishika, akarudi mbio kwa bwana yake, yule mhubiri. Kwa hiyo jambo lililonishinda kufanya likafanywa na mbwa!
Mwaka 1953, Mama, Herbert, na mimi tulienda kukaa Sacramento tukatulia kule. Kwa maana Herbert alikuwa akisumbuliwa na afya yake, sisi wote wawili tulilazimika kubadili mtindo wa maisha zetu. Mara nyingi nimempigia Yehova asante kwamba nilibarikiwa kuwa na Mama yangu mwaminifu na mume mshikamanifu. Sasa wote wawili wameenda zao, kwa maana wamekwisha kupokea thawabu yao ya kimbingu. Mama alikufa mwaka 1975; Herbert alimaliza mwendo wake wa kidunia Septemba 1980, akiwa na umri wa miaka 82. Upweke nilio nao ungali mkubwa, lakini ninapofikiria miaka ya utumishi tulioufanya pamoja, ninafarijiwa. Nami najua hakutakuwa kamwe na mwisho wa kijia hiki, kwa maana Yehova, kupitia Mwanaye Kristo Yesu, ndiye Mwongozi wangu katika kijia hiki kinachonyoka kikielekea kwenye umilele wote.