Huduma ya Kusaidia Watu Kimwili—Jinsi Inavyohusu Watu
KWA kuanza akiwa na mikate mitano tu ya shayiri na visamaki viwili, Yesu Kristo alilisha kimuujiza wanaume, wanawake, na watoto zaidi ya 5,000 karibu na wakati wa sikukuu ya Kupitwa (Machi-Aprili) katika 32 W.K. (Mathayo 14:14-21; Yohana 6:1-13) Kwa kutambua kwamba Yesu alikuwa na uwezo wa kufanya mambo mengi ya ajabu, watu walitaka kumfanya awe mfalme wao. Inaweza kuwa kwamba wao walihisi yeye angewakomboa watoke katika nira ya Waroma na kuleta maendeleo katika hali za maisha yao. Itikio la Yesu lilikuwa nini?
Badala ya kujiacha afuate dai lililotakwa na wengi, Yesu ‘alijitenga akaenda tena mlimani yeye peke yake.’ (Yohana 6:15) Lakini umati wa watu haukuchoka kwa urahisi. Walimjia tena kesho yake. Akigundua kusudio lao la chini-chini, Yesu aliwaambia: “Nawaambieni, Ninyi mnanitafuta, si kwa sababu mliona ishara, bali kwa sababu mlikula ile mikate mkashiba.” Ndipo alipoongeza hivi: “Msikitendee kazi chakula chenye kuharibika, bali chakula kidumucho hata uzima wa milele.”—Yohana 6:25-27.
Tunaweza kujifunza nini kutokana na usimulizi huo? Miongoni mwa mambo mengine, unaonyesha waziwazi kwamba kwa kutumia manufaa ya kimwili ni rahisi kwa kiasi fulani kuvuta watu. Ijapokuwa hivyo, kujenga uthamini wa kweli kwa ajili ya mambo ya kiroho—mambo yenye thamani ya kudumu—ni jambo tofauti kabisa. Leo, watu wana maelekeo makubwa hata zaidi ya kutazama mambo kutokana na maoni ya kimwili kabisa.
Uvutano Wenye Nguvu wa Huduma ya Kusaidia Watu kimwili
Machoni pa watu wa nchi zinazositawi, mataifa za Magharibi yaliyofanya maendeleo yana nafasi zote na manufaa ya kimwili ambazo mtu angeweza kutaka kuwa nazo—lakini zisizopatikana katika nchi yao wenyewe. Ufanisi ule unaonewa kijicho, na mtindo wa maisha ya kule unafuatishwa sana. Nafasi ya kupata elimu ya juu inawekwa mbele ya karibu kila mwanafunzi kuwa paspoti ya kupata maendeleo na mafanikio. Watu wakiwa wamekuzwa kwa kutegemea msingi huo, si vigumu kufahamu ni kwa nini programu za kusaidia watu kimwili za makanisa ya kigeni zimevuta sana watu katika nchi hizo. Lakini matokeo ni nini?
Kwa mfano, katika nchi za Mashariki nia ya watu ya kutaka kufanya lo lote lile ambalo makanisa yanataka ili wastahili kupewa zawadi za bure au misaada imetokeza wale ambao wamebandikwa kwa madharau jina la “Wakristo wa mchele.” Bila shaka, sehemu iliyo ya kuhuzunisha zaidi ni kwamba, wakati kitulizo au msaada huo unapokoma, ndivyo pia kupendezwa kwa watu kunavyokoma. Wengi wa wale watu ambao ni Wakristo wa mchele wanapotea kabisa wasionekane. Hivyo, kati ya Wakantoni, kuna usemi unaopendwa na wengi ambao tafsiri yao ni kama hivi: “Mungu anaupenda ulimwengu, lakini kinachopendwa na ulimwengu ni kule kupewa maziwa-unga.”
Ingawa vikundi vilivyo vingi vya makanisa vimeacha kuendesha programu za kusaidia watu kimwili, isipokuwa labda nyakati za maafa, mambo yaliyotendwa na makanisa hayo zamani yameacha alama nyuma. Kwa watu wengi wa Mashariki, makanisa ni kama tu matengenezo ya kufadhili watu kwa kuwapa vitu, na sababu moja tu ya kwenda kanisani ni kupata, wala si kutoa. Wao hawaoni uhitaji wa kufanya dhabihu yo yote ya kibinafsi kwa ajili ya kanisa. Kwa mfano, mwelekeo huo unaonyeshwa katika kutokutaka kwao kuchangia vitabu vya Kibiblia kwa sababu, katika akili zao, kitu kilichotengenezwa na kanisa kinapasa kutolewa bure.
Kulitumia kanisa kama njia ya kufikia kusudi fulani kunaonekana kwa urahisi zaidi katika upande wa elimu. Katika nchi nyingi zinazositawi, kupata elimu iliyo mtindo wa nchi ya Magharibi kunaonwa kuwa njia hakika ya kupata sifa na mafanikio. Kulingana na chanzo kimoja, wakati India ilipokuwa ikipata uhuru wa kujitegemea mbali na Uingereza, asilimia 85 ya wabunge wa taifa hilo walikuwa wamehudhuria “shule za Kikristo.” Na kulingana na mawazo ya Confucius katika Mashariki ya Mbali, kuelimishwa vizuri ni mmoja wa miradi iliyo ya juu zaidi maishani. Kwa kawaida watu wengi wanategemea shule za makanisa, ambazo kwa ujumla zinatumia njia na viwango vya nchi za Magharibi kuwa ndizo njia za kujipatia maendeleo ya binafsi. Na, wakitumainia kuingiza watoto wao katika moja ya shule hizo zinazoendeshwa na makanisa na labda baadaye watoto hao waende ng’ambo, wazazi wengi wa nchi za Mashariki ambao kwa kawaida wanazifuata dini za kimapokeo wanafurahi kwenda kanisani wao wenyewe na kuhimiza watoto wao wafanye ivyo hivyo.
Matunda Ni Nini?
Kwa kulinganisha na makanisa ya kule nyumbani kwao, kwa kawaida makanisa ya misheni yanahudhuriwa vizuri. Hivyo watu wengi wanajulishwa mafundisho ya kanisa na wazo fulani juu ya Ukristo. Lakini je! kujulishwa kwao mambo hayo kumewasaidia waifahamu Biblia na ujumbe wayo? Je! kweli jambo hilo limewafanya wakawa Wakristo, yaani, wafuasi wa Yesu Kristo?
Kwa mfano, mchukue Kuo Tung, yule mwanamume kijana aliyetangulia kutajwa. Alipoulizwa kama yeye sasa anaamini kuna Mungu baada ya kuhudhuria kanisa kwa muda fulani, yeye alijibu: “La. Uthibitisho wa kwamba Mungu yuko haukuzungumzwa kamwe.” Kwa kweli, yeye alikiri kwamba hakuwa na uhakika kama ye yote wa rafiki zake aliamini Mungu fulani mwenye utu, ingawa wao walikuwa wamekuwa wakihudhuria kanisa pamoja naye. Wao walifuatana na kanisa ili wapate tu nafasi ya kujifunza lugha ya Kiingereza, akasema.
Mwanamume mwingine kijana alikuja nyumbani akiwa likizoni kutoka chuoni katika United States. Wakati mmoja wa Mashahidi wa Yehova alipomtembelea, yeye aliuliza kama Mashahidi wanafanya mikutano yao katika lugha ya Kiingereza. Kwa sababu gani? “Ili mimi niweze kuendelea vizuri kusema Kiingereza bila kuachwa nyuma,” akasema. Alipoambiwa kwamba mikutano inafanywa katika lugha ya mahali pale ili wote waweze kunufaika kiroho, mwanamume yule kijana alisema yeye angeenda mahali ambako mikutano ya Kiingereza ilifanywa mara mbili kwa juma.
Hata wale ambao wamekuwa washiriki wa kanisa na wamebatizwa wanaonyesha badiliko dogo tu katika maoni yao. Bado wengi wao wanashikilia itikadi au mazoea waliyokuwa nayo hapo kwanza, mara nyingi yakikubaliwa, ikiwa si kubarikiwa pia, na kanisa lao. Kwa mfano, katika China Wakatoliki Waroma wanaruhusiwa waendelee na ibada yao ya kuabudu wazazi wa kale waliokufa, ingawa jambo hilo limekatazwa mahali kwingineko. Vibao vyenye maneno yanayosihi mungu wa milangoni alete baraka vinaonwa mara nyingi kando-kando ya kumbi za milango ya kuingia katika nyumba za “Kikristo.” Na katika Okinawa, mifano ya wanyama walio miungu yao ya kienyeji inawekwa katika pembe za paa za nyumba ili kuilinda jamaa.
Namna gani wale ambao wamenufaika m programu za kanisa? Katika usalama wao mpya wa kifedha na kimwili, si jambo lisilo la kawaida kuwasikia wakisema kwamba utatuzi wa matatizo ya leo ni mtu kujitegemea mwenyewe. Matokeo ni kwamba wengi wao ama wamejitenga kabisa wasihusike hata kidogo m kanisa au, ikiwa wamefanya vizuri zaidi ya hivyo, wamejiweka mbali na kanisa kwa kiasi cha kutosha.
Wamisionari wa makanisa wamepata nafasi nyingi nzuri sana za kufundisha watu mambo yanayofundishwa na Biblia. Lakini badala y kuwafundisha wafuate onyo la upole la Yesu linalosema “basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, na hivi vitu vingine vyote vitaongezwa kwenu ninyi,” wao wameweka mkazo juu ya “vitu vingine.” (Mathayo 6:33, NW) Kupitia programu zao za kusaidia watu, wao wamefanya mengi kuwasaidia ki mwili, kitiba, na kielimu. Lakini manufaa hizo hasa ni za muda tu. Bila kuwapa matumaini y kiroho, mara kwa mara programu hizo zinakuwa kihimizo cha kufanya watu wajitahidi kupata faida zaidi zilizo za muda tu au za kilimwengu.
Makanisa yalijitokeza yakaanze kuihubiri injili. Lakini matokeo katika visa vingi yamekuwa kuendeleza njia ya maisha ya nchi za Magharibi, ya kufuatia vitu vya kimwili. Ndiyo, yamepata waongofu wengi. Lakini kama vile ambavyo tumeona, wengi wa hao wamekuwa na fikira za kilimwengu na kufuatia vitu vya kimwili zaidi ya wakati mwinginewo wote. Katika siku za Yesu, yeye alisema hivi juu ya viongozi wa kidini: “Mnazunguka katika bahari na nchi kavu ili kumfanya mtu mmoja kuwa mwongofu; na akiisha kufanyika mnamfanya kuwa mwana wa jehanum mara mbili zaidi kuliko ninyi wenyewe.” (Mathayo 23:15) Katika maana hiyo, jitihada ya Jumuiya ya Wakristo katika kuihubiri injili kwa kutumia njia ya kusaidia watu kimwili imewageuka kinyume. Imepungukiwa sana isitimize lile agizo kuu alilotoa Yesu Kristo: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru ninyi.”—Mathayo 28:19, 20, NW.