‘Kuihubiri Injili’ Kupitia Kazi ya Kusaidia Watu Kimwili
KUO TUNG, mwanamume kijana mfuasi wa Buddha kutoka Hong Kong, alipokea elimu ya chuoni. Hsiu Ying, mama mmoja katika Taiwani, alipata matibabu yaliyohitajiwa sana kwa ajili ya ugonjwa hatari wa mwanaye. Matokeo haya yanayoonekana kuwa yasiyohusiana yana lengo gani moja?
Katika hali ya kikawaida Kuo Tung hangaliweza kabisa kupata elimu ya chuoni. Lakini kupitia kanisa ambalo yeye ni mshiriki, alifunguliwa milango ya kupata elimu hiyo. Vivyo hivyo, utaratibu wa tiba wenye magumu mengi uliohitajiwa na mwana wa Hsiu Ying uliweza kupatikana kwenye hospitali ya kanisa tu katika eneo la mama huyo. Tena, matatizo ya mama huyo yalitatuliwa kupitia mawasiliano pamoja na kanisa hilo.
Mambo yaliyowapata Kuo Tung na Hsiu Ying si matukio ya ajabu. Maelfu ya watu katika nchi zinazositawi wamevutwa waende kwenye shule, hospitali, makao ya kutunzia watoto yatima, na mashirika mengine ya kusaidia wenye shida yanayoendeshwa na makanisa. Kwa njia hiyo, wao wamejipatia manufaa nyingi ya vitu vya kimwili. Na katika kufanya hivyo, kwa kujiunga na kanisa, wengi wao wamesaidia kufurisha hesabu za washiriki wa kanisa.
Zoea Lenye Historia Ndefu
Bila shaka, shule na hospitali za kikanisa si jambo jipya. Kwa kweli, tangu zile siku za mwanzo-mwanzo wakati wamisionari walipotumwa kwenye zile nchi ambazo wengine wameziita za kipagani na zenye uadui, shule na hospitali zimetegemewa kuwa njia iliyo na matokeo makubwa zaidi ya kufungua maeneo mapya na kupata matumaini na urafiki wa watu wa kule.
Kwa mfano, kinapoeleza hali iliyokuwa katika India mwanzoni-mwanzoni mwa karne ya 19, kitabu Nineteen Centuries of Missions (1899) kinasema: “Wamisionari hawa wanahusika kwa bidii si katika kazi ya kueneza evanjeli tu, bali wanajitahidi pia kwa njia yenye mafanikio makubwa katika kazi ya kielimu, kitiba na ya zenana.” Matokeo yamekuwa nini? “Kila misheni ina shule zayo za mchana, shule za viwandani na shule za bweni, shule ya sekondari au chuo, na karibu katika kila kisa, seminari ya ualimu wa kidini.”
Kikitoa maelezo juu ya sehemu inayotimizwa na kazi ya kitiba katika “shughuli ya umisionari,” kitabu hicho kinaendelea kusema: “Sikuzote tabibu anapokewa na watu, na kitulizo kinachotolewa ili kupunguza taabu ya mwili hakifanyi tu watu waweke uhakika wao katika tabibu, bali mara nyingi jambo hilo linawafanya pia watu hao waiamini dini ambayo tabibu huyo anafundisha. Kwa sababu ya matibabu, mara nyingi vijiji vizima-vizima vinaongozwa viache ibada ya sanamu na kupokea mafundisho ya Kikristo.”
Ilivyokuwa katika India ndivyo pia ikawa katika nchi nyingine katika Mashariki ya Mbali, Amerika ya Kusini, na Afrika. Lile wazo la kuihubiri injili kwa kuwapa watu misaada ya kimwili likawa limekolea. Sosaiti za umisionari za Ulaya na Amerika, za Wakatoliki na Waprotestanti pia, zilituma wafanya kazi wakaingie katika maeneo hayo nao wakaanzisha misheni zao pamoja na shule zao, hospitali, na mashirika mengine. Sehemu kubwa ya kazi hiyo ikawa na mafanikio makubwa katika kuvuta watu wa maeneo hayo hivi kwamba baada ya muda mfupi kazi ya kusaidia watu kimwili ikawa sehemu kuu ya kazi ya umisionari yenye kudhaminiwa na makanisa katika nchi za ng’ambo.
Katika muda wa miaka iliyopita, mashirika hayo yenye kuendeshwa na kanisa yamesitawi yakachukua mahali pa maana sana katika jamii za mahali-mahali. Mara nyingi shule na vyuo vikuu vyao ndiyo mashirika yenye sifa kubwa zaidi na yenye kutafutwa sana na watu kwa masomo ya juu. Kwa ujumla, hospitali zao ndizo zenye vifaa vizuri zaidi na zenye hali za kisasa zaidi. Na, katika maeneo mengi, ambako serikali zimelemewa sana na matatizo mengi ya kijamii, mashirika hayo yanapokewa kwa furaha, na hata kuheshimiwa.
Hakuna shaka kwamba huduma zenye kuandaliwa kupitia programu kama hiyo zimeleta faida kubwa kwa jamii zilizotumikiwa hivyo. Shule na vyuo vikuu vyenye kuendeshwa na kanisa vimeandalia kihalisi maelfu ya wanafunzi elimu ambayo wangalinyimwa kama haingalikuwa hivyo. Hospitali na huduma hizo za kiafya zimezipa kitulizo idadi kubwa sana za watu katika maeneo yaliyo mbali sana na yasiyo na maendeleo sana. Kwa mfano, kazi za kufadhili wanadamu za Albert Schweitzer na “Mama” Teresa, zinajulikana sana katika mataifa na zimefanya wote hao wawili watuzwe zawadi ya Nobeli ya amani.
Kwa upande mwingine, ni lazima mtu aulize hivi: “Je! kweli injili ya kusaidia watu kimwili: imetimiza shabaha yayo? Je! imefanya wale ambao wamenufaika na kazi hizo za fadhili: wawe Wakristo wa kweli? Je! imewapa watu imani ya kweli na tumaini la kweli? Na ulizo lililo la maana hata zaidi ambalo lazima tuulize ni hili: Je! hilo ndilo jambo alilokuwa akifikiria Yesu alipoagiza wafuasi wake waende ‘wakaihubiri injili katika ulimwengu wote’?—Mathayo 24:14, King James Version.