Ni Nini Kinachotendeka Shuleni Leo?
“SHULE Zetu Ziko Matatani: Leteni Polisi Sasa” kilikuwa kichwa cha hivi majuzi kwenye ukurasa wa kwanza katika gazeti la habari la New York City. Baraza la Elimu la New York City lina walinzi walo lenyewe wa kulinda usalama shuleni—kikundi cha 3,200— ambao hushika doria katika shule za jijini zaidi ya 1,000. Sasa watu wengi wataka polisi wa kawaida wa jiji waletwe shuleni ili kusaidia kudumisha usalama. Je, wanahitajika kweli?
Kichwa kikuu cha New York Times kilisema hivi: “Ripoti Zaonyesha asilimia 20 ya Wanafunzi katika New York City Hubeba Silaha.” Mkuu wa shule za New York City tangu 1990 hadi 1992, Joseph Fernandez, alikiri hivi: “Sijapata kuona jeuri kama tuliyo nayo sasa katika shule zetu za jiji kuu. . . . Singeweza kuwazia wakati nilikubali usimamizi katika New York mnamo 1990 kwamba hali ingekuwa mbaya hivyo. Si mabadiliko fulani, ni uovu.”
Hali Ni Mbaya Kadiri Gani?
Fernandez aliripoti hivi: “Wakati wa miezi yangu ya kwanza kumi nikiwa msimamizi, kwa wastani mtoto wa shule mmoja aliuawa kimakusudi kila siku mbili—kudungwa kisu kwenye reli za chini ya ardhi, kupigwa risasi katika uwanja wa shule au kwenye pembe za barabara . . . Shule nyingine zina [walinda usalama] kumi na watano au kumi na sita wanaoshika doria ukumbini na nyanjani.” Yeye aliongezea hivi: “Jeuri katika shule zetu imeenea, na hatua zisizo za kawaida zimehitaji kuchukuliwa. Shule katika Chicago, Los Angeles, Detroit—majiji yote makubwa—sasa zafanana zikiwa zimejaa ukatili wa kimsiba wa kuogofya.
“Ile aibu iliyoko katika jambo hili iko wazi kwa njia ya kushangaza. Kwa muda wa miongo miwili ya miaka iliyopita tumekuja kukubali yale yasiyokubalika: Kwamba shule za Marekani ni nyanja za vita. Majumba ya hofu na kitisho badala ya makao ya kuelimisha.”
Kuna maofisa wa usalama katika mifumo ya shule 245 katika Marekani, na katika 102 ya hii, hao maofisa wamejihami. Lakini si wao peke yao ambao wamejihami. Kulingana na uchunguzi wa Chuo Kikuu cha Michigan, yakadiriwa kwamba wanafunzi katika Marekani hubeba shuleni bunduki zipatazo 270,000, bila kuhesabu silaha nyinginezo, kila siku!
Badala ya hali kuwa nafuu, imeendelea kuwa mbaya zaidi. Vifaa vya kuchunguza silaha vitumiwavyo katika shule nyingi vimeshindwa kusimamisha mmiminiko wa silaha. Wakati wa vuli ya 1994, visa vilivyoripotiwa vya jeuri katika shule za New York City vilipanda kwa asilimia 28 vikilinganishwa na kipindi hichohicho mwaka mmoja mapema! “Kwa mara ya kwanza kabisa,” laeleza Phi Delta Kappan kuhusu uchunguzi uliofanywa katika Marekani, “ule mpangilio wa ‘kupigana, jeuri, na magenge’ huwania nambari moja huku ‘ukosefu wa nidhamu’ ukiwa tatizo kubwa kupita yote yanayokabili shule za umma za hapo.”
Jeuri ya shuleni imesababisha matatizo kwa shule katika nchi nyingi. Katika Kanada, Globe and Mail la Toronto lilikuwa na kichwa kikuu: “Shule Zabadilika Kuwa Nyanja Hatari.” Na uchunguzi fulani katika Melbourne, Australia, ulifunua kwamba karibu asilimia 60 ya watoto wa shule za msingi hupelekwa shuleni na kurudishwa na wazazi kwa kuhofu mashambulizi au utoroshwaji.
Hata hivyo, jeuri ni sehemu moja tu ya tatizo. Kuna mambo mengine yanayotukia katika shule zetu ambayo husababisha hangaiko kubwa.
Suala la Maadili
Hata ingawa Biblia husema kwamba uasherati—kuwa na uhusiano wa kingono nje ya ndoa—ni kosa, leo shule hazishikilii fundisho hilo la kimaadili lifaalo. (Waefeso 5:5; 1 Wathesalonike 4:3-5; Ufunuo 22:15) Kwa kweli hili limechangia hali iliyofafanuliwa na Fernandez aliposema hivi: “Matineja wengi kufikia asilimia 80 ni wenye kufanya ngono.” Katika shule moja ya sekondari katika Chicago, thuluthi moja ya wanafunzi wa kike walikuwa na mimba!
Shule nyingine zina makao ya kutunza watoto kwa ajili ya vitoto vya wanafunzi. Kwa kuongezea, kondomu hugawanywa kwa ukawaida katika jitihada isiyofua dafu ya kuzuia kipuku cha UKIMWI na ongezeko la kasi la watoto haramu. Ikiwa kondomu zinazogawanywa kwa hakika hazihimizi wanafunzi kufanya uasherati, hizo huwaruhusu kufanya hivyo. Inapohusu maadili, wanafunzi wanapaswa kufikiria nini?
Mwalimu wa siku nyingi wa chuo kikuu alisema kwamba kuna “idadi kubwa ya vijana wanaofikiri hakuna jambo lililo sawa wala baya, kwamba machaguzi ya maadili hutegemea unavyohisi.” Kwa nini vijana hufikiri kwa njia hii? Mwalimu alionelea: “Labda ni yaliyowapata katika shule ya sekondari ambayo yaliwafanya wawe wapuuza-maadili.” Ni nini matokeo ya kukosa uhakika kuhusu maadili kama huko?
Tahariri moja ya gazeti la habari la hivi majuzi lililalamika: “Nyakati nyingine yaonekana, hakuna yeyote aliye tayari kukubali lawama kwa chochote. Kwa wakati wowote.” Naam, ujumbe ni kwamba kila kitu ni sawa! Ebu fikiria kielelezo fulani cha yale matokeo yenye kudhuru ambayo maoni hayo yaweza kuwa nayo kwa wanafunzi. Katika somo la chuo kikuu kuhusu ile habari ya Vita ya Ulimwengu 2 na kukwea kwa Unazi, profesa mmoja alipata kwamba wengi wa wanafunzi wake hawakuamini yeyote alipaswa kulaumiwa kwa ajili ya Teketezo la Umati! “Akilini mwa wanafunzi,” huyo mwalimu akasema, “Teketezo la Umati lilikuwa kama msiba wa asili: Halingezuilika na kuepukika.”
Kosa ni la nani wanafunzi wanaposhindwa kutofautisha jambo lililo sawa kutoka kwa lisilo sawa?
Katikati ya Nyakati za Hatari
Katika kutetea shule, aliyekuwa mwalimu hapo awali alisema hivi: “Tatizo latokana na jumuiya, shule zaonyesha tu matatizo yaliyoko tayari katika jumuiya.” Kwa kweli, ni vigumu kufunza kwa kufanikiwa kile ambacho viongozi wa jamii wameshindwa kufanya.
Akitolea kielelezo jambo hili, katika wakati ambapo ukosefu wa adili wa maofisa wa serikali ya Marekani ulikuwa kwenye vichwa vya habari, mwanasafu maarufu aliandika hivi: “Sielewi jinsi walimu katika kizazi hiki cha uasi wanaweza kufundisha maadili. . . . ‘Ebu tazama ikulu ya Washington!’ hata wanafunzi wataandamana kupinga. Wao wajua . . . kwamba uwongo uliofisidika zaidi katika historia hufanywa katika hiyo ikulu.”
Biblia ilitabiri kwamba “siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari.” (2 Timotheo 3:1-5) Kwa kweli hizi ndizo nyakati hatari! Kutokana na hili, ni jambo lipi linalofanywa kukabili matatizo shuleni leo na kusaidia wanafunzi kupata elimu nzuri? Nyinyi mkiwa wazazi na wanafunzi mwaweza kufanya nini? Makala zinazofuata zitazungumzia hili.