Kujua Yaliyo Katika Habari
“Wazo Baya”
Hangaiko linaloongezeka juu ya damu iliyochafuliwa linalazimisha wataalamu wa kitiba wafikirie tena kama inafaa kutia damu katika mishipa ya watu. Henry B. Soloway, M.D., mhariri wa jarida Pathologist, alisema kwamba tangu utiaji damu mishipani uanzishwe umekumbwa na matatizo. “Mapema kidogo,” yeye anaeleza, “utiaji mishipani wa damu iliyochafuliwa wakati wa kuitoa katika watu na kuiweka akibani . . . ulisababisha vifo vingi sana kutokana na sepsisi [ambukizo] na mshtuko unaotokana na endotoksiki [sumu]. Kupitishwa kwa ugonjwa wa mfuro-ini B kwa kuingiza mwilini damu na vitu vilivyotengenezwa kwa damu kulisababisha ugonjwa mwingi sana wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili.” Hata baada ya kutokezwa njia za kiufundi zilizokusudiwa kuhakikisha damu yenye kuingizwa mwilini ilikuwa “salama,” bado magonjwa kama UKIMWI yanaendelea kuingizwa mwilini kwa kutia damu mishipani.
Mahangaiko mapya sasa yametokea juu ya muda mrefu wa kuendelea kuwa hai kwa wagonjwa wa kansa baada ya kupasuliwa kwa kuingizwa damu mishipani. Soloway anasema: “Kuna hasara kubwa ya muda wa kuendelea kuwa hai wakati . . . damu inaingizwa katika mishipa ya wagonjwa wanaopasuliwa kwa sababu ya kansa ya mapafu, matiti, na chini ya utumbo mkubwa.” Basi, ni njia gani zinazoweza kutumiwa badala ya hizo? Soloway anakubali hivi: “Mashahidi wa Yehova wamesisitiza . . . kwamba kutia damu mishipani ni wazo baya. Labda siku moja hivi karibuni watathibitishwa kuwa wanakosea. Lakini kwa sasa kuna ushahidi mkubwa wa wazi kuunga mkono jambo wanaloshikilia, yajapokuwa mateto ya wenye kuhifadhi damu kukataa jambo hilo.”
Kwa kweli, kutii sheria ya kimungu ndiko kumekinga Mashahidi wa Yehova wasipatwe na matokeo mabaya mengi ya kutia damu mishipani. Andiko la Walawi 17:14 (NW) linasema hivi: “Ni lazima ninyi msile damu ya mwili wa aina yo yote, kwa sababu nafsi ya kila aina ya mwili ni damu yao.” Na Wakristo waliambiwa ‘wajiepushe na damu.’ (Matendo 15:28, 29) Kwa wazi, Mungu anaona kutwaa damu ikiwa katika namna yo yote kuwa “wazo baya.”
“Pengo Katika Mageuzi”
“Mabawa ya wadudu hayakugeuka-geuka kutokana na viungo vyo vyote vya mwili wala kutokana na kitu kinginecho chote. Yalianza kama viungo vidogo zaidi sana vyenye kutokeza mgongoni.” Ndivyo linavyosema gazeti la Kiswedi Svenska Dagbladet, likiripoti juu ya uchunguzi wa hivi majuzi kuhusu jinsi wadudu walivyopata mabawa yao. “Kulingana na nadharia moja,” ripoti hiyo inasema, “wao wangaliweza kuwa walitumia mabawa hayo waliyotazamia kuwa nayo kama namna fulani ya kichungi cha kunasia wadudu, mpaka siku moja, wakakuta kwamba wangeweza pia kuruka na kujiinua wenyewe kutoka chini kupitia hewani au kuruka kwenda chini kutoka katika miti.”
Ripoti hiyo inaonyesha pia kwamba wanabayolojia wanazungumza lile wazo la kwamba ingawa hayo “mabawa waliyotazamia kuwa nayo” yalikuwa madogo mno yasiweze kuwarusha, yangaliweza kuwa yalitumika yakiwa vipokea-joto la jua ili kuupasha mwili joto na nishati. Ni nini kilichoyawezesha mabawa hayo kukua yaache kuwa madogo yafikie ukubwa kamili? “Hilo ni pengo katika mageuzi ambalo ni vigumu kulieleza,” inakiri ripoti hiyo.
Ijapokuwa hivyo, Biblia inaonyesha kwa wazi jinsi wadudu walivyopata mabawa yao. “Mungu akaendelea kuumba . . . kila kiumbe chenye mabawa kinachoruka kulingana na aina yacho,” linasema andiko la Mwanzo 1:21 (NW). Ingawa miaka ya uchunguzi wa kisayansi imetokeza tu nadharia za kukisia-kisia na “pengo . . . ambalo ni vigumu kulieza,” usimulizi wa Biblia unafaana na mambo ya hakika yanayojulikana. Ubuni mzuri ajabu na kazi ya mabawa ya wadudu vinaleta sifa si kwa mageuzi yenye upofu bali kwa Muumba mwenye akili.
Kuwatumia Vibaya Watu Wenye Umri Mkubwa
Watu wenye umri mkubwa wanaendelea zaidi na zaidi kutumiwa vibaya na kuachiliwa tu. Ni kawaida siku hizi kusikia ripoti juu ya watu wenye umri mkubwa wakitendwa vibaya, wakinyang’anywa vitu vyao, wakipigwa na kuuawa—hata katika nchi ambamo watu wenye umri mkubwa wamekuwa wakipewa heshima kubwa kulingana na mapokeo. Katika nchi moja ya Mashariki, “mfanya kazi wa mitaani anaeleza juu ya mwanamke mmoja mzee aliyefungwa minyororo na jamaa yake kwa miaka kumi na minne na kuruhusiwa aoge mara moja tu kila majuma mawili,” kinaripoti kichapo Asiaweek. Kichapo hicho kinaongeza kwamba mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 60 katika nchi nyingine ya Esia “alikufa hivi majuzi katika makao ya watu wazee. Mwanaye na binti-mkwe wake hata hawakuja kumwona alipokuwa katika kitanda cha kifo chake.” Hali si tofauti katika nchi za Magharibi. “Karibu 1 katika Waamerika 25 wazee-wazee anaachiliwa tu au kutumiwa vibaya, ama nyumbani ama katika makao ya utunzaji wa wazee,” kinasema kichapo U.S.News & World Report. “Kuachiliwa bila utunzaji ndiyo namna iliyo ya kawaida zaidi ya kutendwa vibaya . . . Lakini namna zote mbili za kutumiwa vibaya kimwili na kutumiwa vibaya katika ngono zinaendelea kuongezeka.”
Wakaaji wa Israeli ya kale na pia washiriki wa kundi la Kikristo la kwanza-kwanza walionywa kwa upole wawaonyeshe heshima, mafikirio, na staha walio na umri mkubwa zaidi. (Kutoka 20:12; Walawi 19:32; Waefeso 6:1, 2; 1 Timotheo 5:1, 2) Ijapokuwa hivyo, mtume Paulo alitabiri kwamba katika siku za mwisho tungekuja kuingia ndani ya “nyakati za hatari” ambapo watu wangesonga mbali zaidi na zaidi kutoka kwenye mwelekezo wa Mungu. (2 Timotheo 3:1) Moja ya tabia ambazo Paulo alitaja wazi ni kwamba watu wangekuwa “wenye ukosefu kabisa katika . . . shauku za upendo zilizo kawaida ya kibinadamu.” (2 Timotheo 3:2, 3 The New Testament in Modern English, iliyofanywa na J. B. Phillips) Ni nani anayeweza kutilia shaka ukweli wa maneno yake?