Kutwa Moja Katika Kalikata Kufikia “Watu wa Namna Zote” kwa Habari Njema
KALIKATA ni mji wenye umayamaya mwingi wa “watu wa namna zote.” Miongoni mwa wakaaji wao zaidi ya milioni 10, Mashahidi wa Yehova wana shughuli nyingi wakizihubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Inahitaji mtu ajichukue kikawaida tu na kuwa na uvumilivu ili kuweza kufikia watu hao wote wenye malezi yanayotofautiana sana ya kikabila, kijamii, kitamaduni, kidini, na kiuchumi. Lakini kama vile mtume Mkristo Paulo, ambaye safari zake za umisionari zilimpeleka kwenye pembe za mbali za ulimwengu wa wakati huo, Mashahidi wa Yehova katika Kalikata pia ‘wamekuwa mambo yote kwa watu wa namna zote’ ili kwamba waweze “kwa njia zote kuokoa wengine.”—1 Wakorintho 9:22, NW; Wakolosai 1:23.
Mashahidi wanafanya-fanyaje kazi yao ya kuhubiri, na wanakuta watu na hali za aina gani katika huduma yao? Hivi majuzi, mimi nikiwa mgeni, nilishinda kutwa moja katika Kalikata pamoja na painia mmoja, au mhubiri wa wakati wote. Je! ungependa kutupa jieho ndani ya tukio hilo lisilo na kifani?
Shamba Kubwa Sana Lenye Hali Zinazotofautiana
Mwishoni-mwishoni mwa kutwa hiyo yenye shughuli nyingi na ya kusisimua ya kuhubiri nyumba kwa nyumba, mwandamani wangu na mimi tulikuwa tayari kwenda nyumbani. Tulipokuwa tukingojea basi, tulianza kusema juu ya matatizo ambayo yeye na mapainia wengine wanakabili katika mji huo mkubwa.
“Basi,” yeye akajibu, “uliza mtu ye yote aliye katika kazi ya kuhubiri wakati wote hapa kama angependa kuhamia mgawo ulio rahisi zaidi. Mimi sifikiri atapenda sana kufikiria jambo hilo.”
Alikuwa akisema kweli. Mapainia katika Kalikata wanaiona kazi yao kuwa moja ya shughuli za maisha yote iliyo ya kupendeza zaidi ulimwenguni. Wao wana shamba lililoenea sana na lenye hali zilizotofautiana sana katika mji huu wenye tofauti kubwa-kubwa.
Ingawa dini ya Kihindu inatawala mji huu, makanisa na misikiti ya Kiislamu ni mingi sana, na mmoja anapata mahekalu machache ya Kibudha hapa na hapa. Katika mitaa fulani, majumba makubwa-makubwa na yenye fahari yanakaliwa na baadhi ya watu walio matajiri zaidi sana ulimwenguni. Mwendo usio mbali sana kutoka hapo kuna vibanda vibovu-vibovu vya kuishi wafanya kazi waliohamia nchini wanaoweza kutazamia chumo dogo la rupia 150 (karibu Kshs. 192/-) kwa mwezi. Kama vile dini zao na hali zao za maisha zinavyotofautiana sana, ndivyo na desturi zao, lugha zao na sura zao.
Katikati ya yote hayo linasitawi kundi moja la Mashahidi wa Yehova lenye watangazaji wa Ufalme walio watendaji karibu mia moja. Ingawa hilo ni tatizo gumu sana, Mashahidi wanapata furaha ya pekee na uradhi kwa kuweza kubadilikana wenyewe ili wayaitikie mahitaji ya watu.
Wakati huo huo, Basi Na. 45 ikanguruma ikisimama mbele yetu. Ilikuwa imejaa kemkemu hata nikawaza hivi mara moja: “Siwezi kabisa kuipanda!” Nikasukumwa kwa urafiki nyuma yangu, na upesi sisi wote wawili tukapanda basi kwa kusukumwa-sukumwa na mikono hata miili ya watu wengi. Angalau watu kumi zaidi walipanda baada ya sisi. Wao walisimama penye ngazi za kuingilia, wakiwa wamening’inia mlangoni kama nyuki. Ndani ya gari hilo, lililotengenezwa likiwa na viti vya kuketi watu 46, nilihesabu vichwa zaidi ya mia moja ndipo nikachoka kuhesabu watu nami nikarudia maongezi yangu na rafiki yangu.
“Basi zinakuwa hivi sikuzote?”
“Mara nyingi zinakuwa zimesongamana kidogo,” akaeleza, “lakini hazitozi bei kubwa, na hiyo inamaanisha tunaweza kwa urahisi kuwa na pesa za kusafiri hata kilometa 10 mpaka 15 hivi kila siku kwenda sehemu zilizo mbali zaidi za mji tukahubiri.”
“Je! haingekuwa vizuri zaidi kufanya kazi katika mitaa iliyo karibu na nyumbani mara nyingi zaidi?”
“Ndiyo, lakini wengine wetu tulio wafanya kazi wa wakati wote tumeamua kuifanya jitihada ya kuwafikia watu katika maeneo mengine. Maandishi yetu yanaonyesha kwamba mitaa mingi ya ujirani wa Kalikata haijatembelewa kwa habari njema katika miaka 50 iliyopita!”
Hata hivyo kufikia kila mtu katika eneo fulani ni tatizo kweli kweli kwa sababu tu ya ule wingi wa watu. Uchunguzi mmoja wakati mmoja ulionyesha kwamba msongamano wa watu katika Kalikata ni mara tatu ya ule wa Mjini New York, na hesabu hiyo imeongezeka katika miaka ya juzi.
Angalau theluthi moja ya watu wa Kalikata wanaishi katika vitongoji vilivyosongamana mno vinavyoitwa hapa nchini mabasti. Mabasti halisi ni milolongo mingi sana ya vibanda vidogo-vidogo, ambavyo kwa kawaida vimekaribiana sana kimoja na kingine kiasi cha urefu wa mkono. Kila kibanda kina sakafu na kuta zilizofanyizwa kwa matope na samadi ya ng’ombe iliyopakwa katika fremu za mbao, vyote hivyo vikiwa chini ya paa iliyotengenezwa kwa vigae vya udongo. Kila kibanda, ambacho kina nafasi ndogo sana ya kuingilia hewa na vingine havina yo yote, ndiyo makao ya kulala watu saba au wanane. Kwa kawaida kunakuwa na bomba moja la maji wanapochota kila watu karibu 150, na katika mabasti ambayo yamekuwapo kwa muda mrefu, serikali inaandaa vyoo vichache vya matumizi ya ujumla mitaani.
Mmoja anapoanza kufanya ziara katika basti, ni jambo la kawaida kusindikizwa na umati wa watazamaji wadadisi kufika hata mia moja, sana-sana watoto. Shahidi mmoja, akiwa ameudhiwa kidogo na kijana mmoja aliyeendelea-endelea kutangaza ziara yake kwenye kila nyumba, alimwuliza kijana yule mwanamume kama angependa basi awaeleze wenye nyumba mambo yale mengine yote yaliyobaki. Kwa huo ulioonekana kama mwaliko, kijana huyo mwenye tabia nzuri alichukua trakti kutoka kwa Shahidi akatoa mahubiri neno kwa neno, mpaka kwenye toleo lenyewe la magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni!
Kupambana na Malezi ya Kidini Yanayotofautiana
Karibu nusu ya mabasti ya mji huo yanakaliwa na wafuasi wa Uislamu. Ijapokuwa hivyo mwelekeo wa kuvumilia hali ulio katika mji unafanya iwezekane kuhubiri nyumba kwa nyumba katika maeneo kama hayo, pendeleo lisilofurahiwa sikuzote katika nchi nyingi zenye mitaa mikubwa ya Kiislamu. Niliuliza kama mapainia katika Kalikata wana njia ya pekee ya kufikia watu wenye malezi hayo.
“Wengine wanatumia matatizo ya nchini kukazia kutokuweza kwa wanadamu kutatua ole wao mwingi,” akajibu rafiki yangu, “huku wengine wakijaribu kushinda chuki ya kidini isiyo na msingi kwa kuzungumza mambo yanayokubaliwa na wote kwa ujumla, kama vile imani ya kwamba kuna Mungu mmoja (si utatu) au imani tuliyo nayo kwa ujumla kwamba Biblia ile ya kwanza kabisa iliandikwa kwa uongozi wa Mungu.”
“Na matokeo yanakuwa nini?” mimi nikataka kujua.
“Ni wachache sana wanaopendezwa vya kutosha hata watake funzo la Biblia. Mambo pekee yanayoelekea kuwa akilini mwao ni kujipatia riziki na kuinua hadhi yao maishani. Jambo hilo, pamoja na elimu ndogo, ikiwapo, linafanya iwe vigumu sana wao kukubali habari njema.”
Maoni ya Kihindu yanakabiliwa sana katika mji huu. Wabengali, hasa, wanapenda sana kutaja-taja msemo mmoja wa Ramakrishna, aliyeishi na kuhubiri katikati ya karne ya 19. “Jotto moth, totto poth,” ni usemi unaomaanisha, ukitafsiriwa kwa ulegevu, kwamba dini zote ni barabara tofauti tu zinazoongoza kwenye mradi ule ule mmoja.
“Je! ni vigumu kushinda maoni hayo?” nikauliza.
“Si vigumu ikiwa mtu anataka kusikia sababu zinazotolewa. Sisi tunaweza kueleza kwa busara tofauti fulani za wazi, kama vile tumaini letu lenye msingi wa Biblia la kuishi milele katika ukamilifu wa kibinadamu duniani. Au tunaweza kuonyesha kwamba haiwezekani maoni yanayohitilafiana kuwa ya kweli yote pamoja wakati ule ule. Kwa mfano, ama kuna nafsi inayoweza kufa ama hakuna.”
“Hiyo ni njia timamu ya kusababu.”
“Ndiyo, lakini mara nyingi mno watu wanakataa kuchukua kwa uzito yale tunayosema. Wao wana uhakika kwamba wanajua tunayoamini na kwamba wao wanaamini jambo lile lile tu. Mwelekeo huo unaelekea kubatilisha mazungumzo yo yote yenye kujenga. Kwa hiyo sisi tunajaribu kuwaachia vitabu fulani na kusonga mbele kwenye mtu yule mwingine.”
“Je! kumekuwako watu wo wote kutoka jamii ya Kihindu wanaotafuta maarifa yenye kina kirefu zaidi juu ya Mungu na makusudi yake?”
“Ndiyo, mapainia walifikia kijana mwanamume aliyekuwa amefunguka macho akaona kutofaa kwa ushirika wake pamoja na wafuasi wa Ramakrishna,” rafiki yangu akasimulia. “Yeye alichukua magazeti na akawa ameyasoma kufikia wakati alipotembelewa tena siku mbili baadaye. Baada ya mazungumzo kadha, alianza kujifunza kijitabu The Path of Divine Truth Leading to Liberation. Angeandika majibu na maelezo yake kuhusu maulizo ya funzo katika kitabu cha habari. Katika muda wa miezi mitano, mwanamume huyo alibatizwa na kutumikia akiwa painia msaidizi ili kwamba aweze kushiriki maarifa yake pamoja na wengine wengi.”
“Hilo ni tukio zuri ajabu! Lakini itikio la jamaa yao lilikuwaje?”
“Yeye alikuwa akiishi pamoja na mamaye mjane na nyanya yake, wote wawili wakiwa ni Wahindu wenye kujitoa sana. Wao, pia, walianza kuonyesha kupendezwa na wakaanza kujifunza Biblia. Upesi, majirani wakaona mabadiliko katika wanawake hao, na wengine watatu wakapendezwa kwa sababu hiyo. Mama yake sasa amekwisha kubatizwa, na nyanya yake, ambaye anafanya polepole kwa sababu ana umri wa miaka 70, anatumainia kubatizwa karibuni.”
Kutokana na msisimuko wa rafiki yangu katika kusimulia hadithi hii, niliweza kuona kwamba mambo hayo yenye kuonwa ni kichocheo kweli kweli kwa mapainia. Nyakati nyingine huenda ikaonekana kama maendeleo ni kidogo, lakini ndipo mtu fulani anapoanza kupendezwa kwa njia ya pekee; hivyo mapainia wanatiwa moyo kusonga mbele katika utafutaji wao wa watu zaidi ambao huenda wakawa wanapendezwa.
Kuviruka Vizuizi vya Lugha
Ule umati wa watu katika basi ulikuwa umeanza kupungua kidogo, nami nikatambua Kiingereza fulani kilichotumiwa. “Ticket, apnar ticket,” akapaaza sauti mwanamume mmoja mfupi asiye na mavazi rasmi ya kikazi, aliyekuwa ameshika katika mkono wake wa kuume noti zenye rangi nzuri. Kifuko cha ngozi chenye chenji kilikuwa karibu na kiuno chake kuonyesha kwamba ndiye kondakta. Mimi nilijitolea kulipa, lakini rafiki yangu alifuata ukaribishaji wa Kihindi asitake kamwe kusikia hivyo. Aliangusha mkoba wake mikononi mwangu na kuingiza mkono katika shati lake achukue sarafu za pesa.
“Wewe umetia nini humu?” nikasema kwa mshangao. “Hii ni kama tani moja uzito!”
“Eh, chapa za Biblia za lugha ya Kihindi ni kubwa sana. Ili tuwe na vifaa vya kutosha katika Kalikata, tunahitaji kweli kweli kwenda tukiwa na Biblia katika lugha tatu—Kibengali, Kihindi, na Kiingereza—kuongezea vitabu vya Kibiblia, bila shaka.”
“Hakika ungeweza kuchukua Biblia ya Kiingereza tu ukatafsiri mistari unayosoma, sivyo?”
“Nadhani ningeweza. Ijapokuwa hivyo, watu wengi wanaosoma Kibengali tu au Kihindi hawajapata kamwe kuona Biblia kamili katika lugha yao wenyewe. Sisi tunahisi vizuri sana tunapoweza kuwaonyesha nakala moja na kuwasomea kutokana nayo. Kufanya hivyo kunaistahili ile jitihada ya ziada na uzito tunaochukua.”
Kujirekebisha kulingana na mahitaji ya vikundi tofauti-tofauti vya lugha za hapa kunafanya mapainia waendelee kuwa na shughuli nyingi. Walio wengi kati yao wanajizoeza kuweza kutoa ushahidi kwa matokeo mazuri katika lugha tatu kubwa-kubwa. Wengine walio na ustadi wa namna ya pekee wamejifunza kusema lugha tano au sita. Watu wa hapa wanathamini jitihada za wageni kujaribu kusema lugha ya jamii ile, na itikio lao la kusikiliza sana linaweza kuwa thawabu inayotosha kwa zile saa nyingi za kujifunza lugha.
Kupata Furaha Katika Eneo Gumu
Wakati huo huo basi yetu ikalilisha mlio wa kukwaruza ikisimamisha kwa breki zilizokuwa zimeisha tangu hapo, nami nikasogezwa nje.
“Mbona hapa?” nikauliza. “Wewe huishi hapa?”
“Hapana, hili ni eneo la Kipunjabi. Watu hawa ndio wanaotengeneza chai iliyo bora kabisa. Nilifikiri ungependa kuonja kikombe kimoja.”
Chai ile ilikuwa nzuri kabisa.
“Ulipajuaje mahali hapa?” mimi nikauliza.
“Tunapofanya kazi kuzunguka kila eneo, sisi mapainia tunapata kujua vitu bora vinavyotengenezwa mahali fulani na tunajua ni wapi maduka yaliyo bora kabisa na ya bei za chini zaidi yanakopatikana. Ikiwa tumbo lako lina nguvu za kutosha, tunaweza kwenda na kuonja-onja vyakula fulani vya kupendeza jioni ya leo.”
Kwa kukumbuka shauri nililokuwa nimepewa na wengine wa rafiki zangu wenye tahadhari zaidi, mimi nikakataa mwaliko huo. Lakini niliifurahia chai. Niliweza kuona kwamba mapainia wana usawaziko mzuri na wamejifunza kutumia hali zao kujipatia manufaa yaliyo makubwa zaidi. Hata mambo ambayo kwanza yanaonekana kama kwamba ni vipingamizi yanaweza kushindwa na kufurahiwa.
“Je! kuna lo lote usilofurahia juu ya kazi yako?” nikauliza mwishowe.
Rafiki yangu alifikiria sana ulizo hilo kwa muda. “Nafikiri hali ya hewa ya kiangazi na ya pepo za msimu ni jambo amhalo hatutapata kamwe kulizoea. Hata hivyo hilo ni tatizo ulilo nalo, uwe painia usiwe. Joto na fukuto vinaongezeka sana hata mara nyingi jasho linadondoka kutoka ncha ya pua na kuangukia Biblia yako unapoisoma. Na bado, sisi tunajifunza kuchukuliana na jambo hilo. Ndiyo, hapa katika Mei, ambao labda ndio mwezi ulio na joto jingi zaidi mwakani, tunaona hesabu iliyo juu ya mapainia wasaidizi wakijiunga nasi katika kazi ya kuhubiri.”
Nikitazama nyuma kuhusu siku yangu na maongezi yangu pamoja na rafiki yangu painia, nimevutiwa na uwezo wa mapainia wa Kalikata kubadilikana walingane na hali nyingi sana na jamii za watu zinazotofautiana ili waweze kuwafikia wakiwa na habari njema. Bila shaka, mimi natambua kwamba mapainia katika sehemu zote za ulimwengu wanafanya jambo ilo hilo. Wao ni wenye furaha kikweli ‘kuwa hali zote na kwa watu wa namna zote.’—Imechangwa.
[Map/Picture katika ukurasa wa 26]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
BARA HINDI
Kalikata