Ripoti ya Watangazaji Ufalme
Chile Yafanikiwa kwa Ongezeko la Nuru ya Elimu
KAMA vile nuru ya jua yenye kung’aa juu ya milima Andes wakati wa mapambazuko, nuru ya ukweli wa Biblia ilikuja Chile mara ya kwanza katika 1930. Mwaka huo, mmoja wa watumishi wa Yehova aliye wakfu alikuja kutoka Ajentina akiwa na habari njema. Leo, nuru ya Neno la Mungu imeangaza na kufikia pembe za mbali za nchi hii.
Ingawa afisi ya tawi ya kwanza katika Chile ilianzishwa katika 1945, jengo jipya, kubwa la tawi lilijengwa katika 1970, wakati hesabu ya watangazaji UfaIme ilikuwa imefika 7,000. Katika muda wa miaka kumi iliyofuata, nuru ya elimu iliyoongezeka kutoka Neno la Mungu iligusa mioyo mingi yenye kuitikia. Kufikia miaka ya kwanza-kwanza ya kuanzia na 1980, mpanuko zaidi wa afisi ya tawi ulihitajiwa kwa haraka sana. Hivyo katika Septemba 1982 kisehemu cha ardhi cha hekta 7 kilinunuliwa kwenye kiunga cha mji wa Santiago. Na baada ya kazi nyingi ya matayarisho, kazi ya kuchimbua ilianza kufikia Juni 1984.
Lilikuwa jambo lenye kuchangamsha moyo kuona jinsi ndugu wa Chile, wachanga na wazee, walivyounga mkono ujenzi huo kwa michango yao ya ukarimu. Maelfu ya wengine walitoa wakati na vipawa vyao. Baadhi yao waliokuwa na mazoezi ya ufundi walisaidia kwa kazi ya uhandisi. Wengine walifanya kazi ya seremala, kutambuza, kutengeneza mapazia, na mandhari, au walitoa kazi ya kawaida ya upendo kwa kung’oa magugu, kusukuma vigari vya kazi vya kukokotwa kwa mikono, na kuchimba mitaro. Kweli kweli, nuru ya Neno la Mungu yenye kuendelea hatua kwa hatua imegusa mioyo ya watu wake na kuwasukuma wajitolee wenyewe kwa moyo wa kupenda.—Zaburi 110:3.
Umoja huo na moyo wa kupenda haukukosa kuonwa na watu wa nje. Wauzaji bidhaa wengi na hata wanafunzi wa chuo kikuu na maprofesa walikuja kwenye mahali pa ujenzi ili wajionee na kujifunza. Mjenzi mmoja alitaka kuajiri kazi kikundi chote kilichofanyiza saruji ili kusaidia katika ujenzi wa duka kubwa alilokuwa akijenga. Muuza-bidhaa mmoja alitaja jinsi kikundi chote cha wafanya kazi kilivyokuwa tofauti— hakuna kusema matusi, hakuna kutanga-tanga. Alipoambiwa kwamba wote walikuwa Mashahidi wa Yehova na walikuwa hapo wakiwa wenye kujitolea, aliitikia hivi: “Mmoja hangeona hili katika mahali penginepo pote. Ninyi watu ni wa ulimwengu mwingine.”
Mwishowe, katika Agosti 1986 wafanya kazi wa tawi la Chile walihamia hilo jengo jipya katika Puente Alto. Na kwenye Oktoba 25, akiwapo A. D. Schroeder wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, umati wenye shauku wa watu 933 walionyesha kwa maneno uungaji mkono wao wa moyo wote katika kuyaweka wakfu majengo hayo mapya kwa ajili ya utumishi wa Yehova. Kesho yake, tukio la pekee lilifanyiwa kwenye uwanja wa michezo ulio karibu, na watu 18,012 waliongeza si [ndiyo] yao kwenye azimio hilo.
Je! kweli mpanuo huo ulihitajiwa? Acha mambo ya uhakika yatoe jibu. Wakati kisehemu hicho cha ardhi kiliponunuliwa katika 1982, kulikuwako wahubiri wa Ufalme 17,500 katika Chile. Sasa kuna zaidi ya 29,000! Na kukiwa na karibu mafunzo ya Biblia ya nyumbani 40,000 yanayoongozwa, hakuna mwisho unaoonekana. Kwa hiyo acheni nuru kutoka Neno la Mungu ing’ae kwa uangavu zaidi katika eneo hili lenye rutuba lililo chini ya vilima vya Andes, kwa sifa ya Yehova na baraka ya watu wake.—Danieli 12:3.