“Wakati wa Kunena”—Lini?
MARY anafanya kazi akiwa msaidizi-tiba kwenye hospitali moja. Takwa moja analopaswa kufuata katika kazi yake ni kutunza siri. Ni lazima azuie hati na habari zinazohusu kazi yake zisifikie watu wasioruhusiwa. Vifungu vya sheria katika mkoa wa kwao vinakataza pia kufunulia wagonjwa habari za siri.
Siku moja Mary alikabili tatizo la kuchagua kati ya mambo mawili. Katika kushughulika-shughulika na maandishi ya kitiba, aliona habari zenye kuonyesha kwamba mgonjwa mmoja, aliye Mkristo mwenzake, alikuwa amekubali kutoa mimba. Je! yeye alikuwa na daraka la Kimaandiko kufunulia wazee katika kundi habari hiyo, hata ingawa kufanya hivyo kungeweza kufanya apoteze kazi yake, ashtakiwe, au kufanya mwajiri wake apate matatizo ya kisheria? Au je! andiko la Mithali 11:13 (NW) lingetetea haki ya kuendelea kuficha jambo hilo? Linasema hivi: “Mtu anayetembea-tembea akiwa mchongezi anafunua maongezi ya siri, lakini mtu aliye mwaminifu katika roho anafunikia jambo.”—Linganisha Mithali 25:9, 10.
Hali kama hiyo zinaelekewa na Mashahidi wa Yehova mara kwa mara. Kama Mary, wao wanakuwa wakijua kwa uwazi sana lile ambalo Mfalme Sulemani aliona: “Kwa kila jambo kuna majira yake, na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu. . . . wakati wa kunyamaza, na wakati wa kunena.” (Mhubiri 3:1, 7) Je! huo ulikuwa wakati wa Mary kunyamaza, au ulikuwa wakati wa kunena juu ya jambo alilokuwa amepata habari zalo?a
Hali zinaweza kutofautiana sana. Kwa hiyo, haingewezekana kuweka utaratibu ulio kiwango cha kufuatwa katika kila kisa, kama kwamba kila mtu anapaswa kushughulikia mambo kama Mary alivyofanya. Kwa kweli, kila Mkristo akielekeana na hali kama hii wakati wo wote lazima awe amejitayarisha kupima uzito wa mambo yote yanayohusika na afikie uamuzi unaofikiria kanuni za Biblia na unaopima pia uzito wa matokeo yo yote ambayo sheria inadokeza yanaweza kutokea, uamuzi ambao utamwacha yeye akiwa na dhamiri safi mbele za Yehova. (1 Timotheo 1:5, 19) Wakati madhambi ni madogo na yenye kusababishwa na kutokamilika kwa kibinadamu, kanuni hii inatumika: “Upendo unafunika wingi wa dhambi.” (1 Petro 4:8, NW) Lakini wakati inapoelekea kuwa kuna kosa zito, je! Mkristo mshikamanifu anapaswa kufunua analojua kwa sababu ya kupenda Mungu na Mkristo mwenzake, ili kwamba anayeonekana kuwa mtenda dhambi aweze kupokea msaada na utakato wa kundi uhifadhiwe?
Kutumia Kanuni za Biblia
Ni baadhi ya kanuni gani za msingi za Biblia zinazotumika? Kwanza, mtu ye yote anayetenda kosa zito hapaswi kujaribu kulificha. “Afichaye dhambi zake hatafanikiwa; bali yeye aziungamaye na kuziacha atapata rehema.” (Mithali 28:13) Hakuna jambo lo lote linalokosa kuonwa na Yehova. Lazima hatimaye makosa yetu yaliyofichwa yafanyiwe hesabu. (Mithali 15:3; 1 Timotheo 5:24, 25) Nyakati nyingine Yehova anafanya kosa lililofichwa lionekane na mshiriki wa kundi ili liweze kukaziwa fikira zinazofaa.—Yoshua 7:1-26.
Mwongozo mwingine wa Biblia unaonekana kwenye Walawi 5:1, NW: “Basi ikitukia kwamba nafsi anafanya dhambi kwa kuwa amesikia kulaani kwa peupe naye ni shahidi au ameliona hilo au amejua habari zalo, kama haripoti hilo, hapo ni lazima ajibu kwa kosa lake.” Huku “kulaani kwa peupe” hakukuwa kusema machafu juu ya mambo matakatifu wala hakukuwa kukufuru. Bali, mara nyingi kulitukia wakati mtu fulani aliyekuwa amekosewa alipodai kwamba watu wo wote wanaoweza kuwa mashahidi wamsaidie kupata haki, na wakati huo yeye akiwa anatoa-toa laana—inaelekea kutoka kwa Yehova—juu ya mtu yule aliyekuwa amemkosea, ambaye labda hakuwa ametambulika. Hiyo ilikuwa namna ya kuweka wengine chini ya kiapo. Mashahidi wo wote wa kosa lile wangejua ni nani alikuwa ametendwa jambo lisilo la haki na wangekuwa na daraka la kujitokeza kuthibitisha hatia hiyo. Ama sivyo, wao wangelazimika ‘kujibu kwa kosa lao’ mbele za Yehova.b
Amri hiyo kutoka kwa Kiwango Kikubwa Zaidi cha mamlaka katika ulimwengu wote iliweka daraka juu ya kila Mwisraeli la kuripoti kwa waamuzi kosa lo lote zito aliloona ili jambo hilo liweze kushughulikiwa. Ingawa Wakristo hawana wajibu unaowashurutisha kabisa kuwa chini ya Sheria ya Musa, kanuni zayo zingali zikitumika katika kundi la Kikristo. Kwa sababu hiyo, huenda zikawako nyakati ambapo Mkristo ana wajibu wa kupeleka jambo likafikiriwe na wazee. Ni kweli, katika nchi nyingi ni kinyume cha sheria kufunulia watu wasioruhusiwa na mamlaka jambo lililopatikana katika maandishi ya faragha. Lakini baada ya kufikiria jambo lile kwa sala, ikiwa Mkristo anahisi kwamba anaelekeana na hali ambapo sheria ya Mungu inamtaka aripoti jambo analojua yajapokuwako madai ya mamlaka zilizo ndogo zaidi, basi hilo ni daraka analolikubali mbele za Yehova. Kuna nyakati ambapo Mkristo ‘lazima atii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.’—Matendo 5:29, NW.
Ingawa viapo au ahadi nzito-nzito hazipasi kamwe kuchukuliwa ki-hivi-hivi tu, huenda zikawako nyakati ambapo ahadi zinazotakwa na wanadamu zinapopingana na takwa la kwamba tujitolee kwa Mungu wetu peke yake tu. Wakati mtu anapotenda dhambi nzito, anakuwa kama matokeo, ni kama amekuja chini ya ‘laana ya peupe’ kutoka kwa Yule aliyekosewa, Yehova Mungu. (Kumbukumbu 27:26; Mithali 3:33) Wote wanaokuwa sehemu ya kundi la Kikristo wanajiweka wenyewe chini ya “kiapo” cha kutunza kundi likiwa safi, kwa yale wanayotenda kibinafsi na pia kwa jinsi wanavyosaidia wengine wabaki wakiwa safi.
Daraka la Kibinafsi
Hizi ni baadhi ya kanuni za Biblia ambazo inaelekea Mary alifikiria katika kufanya uamuzi wake wa kibinafsi. Hekima ilimwamuru asitende kwa haraka, bila kupima uzito wa mambo kwa uangalifu sana. Biblia inashauri hivi: “Usiwe shahidi dhidi ya mtu mwenzako bila misingi. Ndipo wewe ungelazimika kuwa mpumbavu kwa midomo yako.” (Mithali 24:28, NW) Ili kuthibitisha jambo kwa neno mkataa, ushuhuda wa angalau mashahidi wawili walioliona wenyewe unahitajiwa. (Kumbukumbu 19:15) Kama Mary angalikuwa ameona mtajo mfupi tu juu ya kutoa mimba, huenda ikawa angaliamua kwa dhamiri kwamba ushuhuda wa kuonyesha hatia yo yote ulipungukiwa sana kuwa neno mkataa hata asichukue hatua nyingine zaidi ya hapo. Kungaliweza kuwa na kosa katika kuandika hati ya fedha anazodaiwa mgonjwa, au kwa njia nyingine fulani huenda ikawa maandishi hayakuionyesha hali hiyo kama ilivyofaa.
Hata hivyo, katika kisa hiki, Mary alikuwa na habari nyingine za maana. Kwa mfano, yeye alijua kwamba dada yule alikuwa amezilipa pesa alizodaiwa, ikionyesha alikubali kwamba alikuwa amepokea utumishi ule uliotajwa wazi. Pia, alijua kibinafsi kwamba dada huyo alikuwa mseja, hivyo jambo hilo likatokeza uwezekano wa kwamba alifanya uasherati. Mary alihisi akiwa na tamaa ya kumsaidia kwa upendo mtu ambaye huenda akawa alikosa kisha auhami usafi wa tengenezo la Yehova, akikumbuka Mithali 14:25: “Shahidi wa kweli huponya nafsi za watu; bali atoaye uongo hudanganya.”
Mary aliogopa-ogopa kidogo mambo yale ya kisheria lakini akahisi kwamba katika hali hii kanuni za Biblia zinapasa kuchukua uzito mwingi kuliko takwa la kwamba ahami faragha ya maandishi ya kitiba. Kwa uhakika dada yule hangetaka kuona uchungu moyoni na kujaribu kulipa kisasi kwa kumwingiza matatani, ndivyo Mary alivyowaza. Kwa hiyo Mary alipoyachanganua mambo yote ya uhakika aliyokuwa nayo, aliamua kwa dhamiri kwamba huo ulikuwa wakati wa “kunena,” si wa “kunyamaza.”
Sasa Mary alielekeana na swali jingine zaidi: Anapaswa kusema na nani, na angeweza kufanyaje hivyo kwa akili? Angeweza kwenda moja kwa moja kwa wazee, lakini aliamua kwanza kuendea dada yule kwa faragha. Hiyo ilikuwa njia yenye upendo. Mary aliwaza kwamba dada huyo aliyekuwa chini ya shuku fulani angeweza labda kuikubali nafasi hiyo ya kueleza mambo wazi au, ikiwa ni mwenye hatia, aihakikishe shuku hiyo. Ikiwa huyo alikuwa tayari amesema na wazee juu ya jambo hilo, inaelekea angemwaambia Mary, na Mary hangehitaji kuzidi kufuatia mambo hayo. Mary aliwaza kwamba ikiwa dada huyo alikuwa amekubali kutolewa mimba na hakuwa ameungama kosa hilo la kuvunja sheria ya Mungu, yeye angemtia moyo afanye hivyo. Ndipo wazee wangeweza kumsaidia kulingana na Yakobo 5:13-20. Jambo la kufurahisha ni kwamba, hivyo ndivyo mambo yalivyokuwa. Mary alikuta kwamba dada yule alikuwa amekubali kutolewa mimba chini ya mkazo mwingi na kwa sababu ya kuwa dhaifu kiroho. Aibu na woga ulimsukuma kuficha dhambi yake, lakini alikuwa mwenye furaha kupata msaada kutoka kwa wazee ili apate nafuu ya kiroho.
Kama Mary angaliripoti kwanza kwa baraza la wazee, wao wangalielekewa na uamuzi kama uo huo. Wao wangeshughulikiaje habari za siri ambazo zingewajia? Wangalipaswa kufanya uamuzi wenye kutegemea jambo ambalo wao walihisi Yehova na Neno lake aliwataka wafanye wakiwa wachungaji wa kundi. Ikiwa ripoti ile ilihusu Mkristo aliyebatizwa aliyekuwa mshirika mtendaji wa kundi, wangalipaswa kuupima uzito wa ushuhuda ule kama alivyofanya Mary ili kuamua kama walipaswa kuchukua hatua nyingine zaidi ya hapo. Kama wangaliamua kwamba kulikuwa na uwezekano mwingi wa kwamba hali fulani ya “chachu” ilikuwa kundini, huenda ikawa wangaliipa halmashauri fulani ya hukumu mgawo wa kuchunguza jambo lile. (Wagalatia 5:9, 10) Ikiwa mwenye kushukiwa angalikuwa amejiuzulu kuwa mshiriki, awe hakuwa akihudhuria mikutano yo yote kwa muda fulani na hajitambui kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, huenda ikawa wangalichagua kuacha jambo hilo lipumzike mpaka wakati ambao angeanza kujitambua tena kuwa Shahidi.
Kufikiria Mapema Matokeo ya Baadaye
Waajiri-kazi wana haki ya kutazamia kwamba waajiriwa wao walio Wakristo ‘wataonyesha uaminifu mwema kwa ukamili,’ kutia na kushika amri zinazohusu kutunza siri. (Tito 2:9, 10, NW) Wakikubali kufanya kiapo, kisichukuliwe ki-hivi-hivi tu. Kiapo kinafanya ahadi iwe nzito zaidi na yenye kufunga mtu katika wajibu. (Zaburi 24:4) Na mahali ambapo sheria inakaza sana takwa linalohusu kutunza siri, jambo hilo linakuwa zito hata zaidi. Kwa sababu hiyo, kabla Mkristo hajafanya kiapo au kujiweka mwenyewe chini ya kizuizi cha kutunza siri, iwe ni kuhusiana na kazi ya kuajiriwa au jambo jinginelo, ingekuwa hekima kufikiria kwa kadiri iwezekanayo ni matatizo gani huenda yakatokezwa na jambo hilo kwa sababu ya hitilafiano lo lote na matakwa ya Biblia. Mtu atashughulikiaje mambo ikiwa ndugu au dada anakuwa mteja? Kwa kawaida kazi kama zile za kufanya kazi pamoja na madaktari, hospitali, mahakama, na wanasheria ni namna ya uajiriwa ambamo tatizo lingeweza kusitawi. Hatuwezi kupuuza sheria ya Kaisari au uzito wa kiapo, lakini sheria ya Yehova ndiyo kubwa kupita zote.
Kwa kutazamia tatizo hilo, ndugu wengine walio wanasheria, madaktari, wahasibu, na kadhalika, wametayarisha miongozo iliyoandikwa na wakawaomba ndugu ambao huenda wakawaendea kwa mashauri waisome miongozo hiyo kabla hawajafunua jambo lo lote la siri. Hivyo ufahamiano unatakiwa ufanywe mapema ili kwamba kosa zito likija kujulikana, mwenye kukosa angetiwa moyo kuendea wazee katika kundi lake kuhusiana na jambo hilo. Ingefahamiwa kwamba asipofanya hivyo, mshauri angehisi akiwa na wajibu wa kuendea wazee yeye mwenyewe.
Huenda kukawa na pindi ambapo mambo ambayo mtumishi mwaminifu wa Mungu anasadiki yeye binafsi, yenye msingi wa maarifa yake juu ya Neno la Mungu, yanamsukuma ayaruke au hata ayavunje kidogo matakwa ya kutunza siri kwa sababu ya madai makubwa zaidi ya sheria ya kimungu. Ushujaa na akili ya uangalifu yangehitajiwa. Shabaha haingekuwa kupeleleza uhuru wa mwingine bali kusaidia wenye kukosa na kutunza kundi la Kikristo likiwa safi. Makosa madogo-madogo yenye kusababishwa na dhambi yanapasa kuachiliwa. Hapa, “upendo unafunika wingi wa dhambi,” na inatupasa tusamehe “mpaka kufika mara sabini na saba.” (Mathayo 18:21, 22, NW) Huo ndio “wakati wa kunyamaza.” Lakini kunapokuwa na jaribio la kuficha dhambi kubwa-kubwa, huenda huo ukawa ndio “wakati wa kunena.”
[Maelezo ya Chini]
a Mary ni mtu wa kuwaziwa tu anayeelekeana na hali ambayo Wakristo fulani wamekwisha kuelekeana nayo. Jinsi anavyoishughulikia hali hiyo inawakilisha jinsi watu fulani wametumia kanuni za Biblia katika hali zinazofanana na hizo.
b Katika kichapo chao Commentary on the Old Testament, Keil na Delitzsch wanasema kwamba mtu angekuwa mwenye hatia ya kosa au dhambi ikiwa ‘alijua uhalifu wa mwingine, awe alikuwa ameuona, au alikuwa amekuja kuujua kwa uhakika kwa njia nyingine yo yote, na hivyo akastahili kuonekana mahakamani akiwa shahidi wa kushtakiwa kwa mhalifu, lakini hakujali kufanya hivyo, na hakusema jambo alilokuwa ameona au kujua, wakati alipokisikia kiapisho kizito cha mwamuzi kwenye uchunguzi wa hadharani juu ya uhalifu ule, ambao kupitia huo watu wote waliopo, waliojua habari yo yote juu ya jambo hilo, walihimizwa wajitokeze kuwa mashahidi.”
[Picha katika ukurasa wa 15]
Mwendo unaofaa na wenye upendo ni kumtia moyo Shahidi mwenye kukosa aseme kwa wazee, akiwa na uhakika kwamba wao watashughulikia tatizo lile kwa njia yenye fadhili na ufahamu