Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w87 12/15 kur. 26-29
  • Yehova Ajenga Nyumba

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Ajenga Nyumba
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Vichwa vidogo
  • Kushinda Matatizo
  • Jengo Lenye Fahari Katika Mazingira Yenye Uzuri
  • Ile Programu ya Wakfu
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
w87 12/15 kur. 26-29

Yehova Ajenga Nyumba

JUMAMOSI, Machi 21, 1987, ilikuwa siku ambayo wafanyi kazi wa tawi la Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi la Afrika Kusini hawatasahau kamwe. Hii ilikuwa pindi ya kihistoria. Lile jengo-tata jipya kwenye Roodekrans liliwekwa wakfu—ukiwa upeo wa miaka sita ya kazi ngumu. Lakini heshima inaenda kwa Yehova. Ni kama vile Sulemani alivyoeleza: “BWANA [Yehova, NW] asipojenga nyumba wajengao wafanya kazi bure.”—Zaburi 127:1.

Acheni tufuatie kwa ufupi ule ukuzi wa Mashahidi wa Yehova katika Afrika Kusini. Katika 1902 watu wawili wa kwanza wa nchi hiyo walianza kujifunza vichapo vya Sosaiti na kuhubiria wengine. Katika 1910 Will Johnston alielekezwa na Ndugu Russell afungue afisi ya tawi yenye mtu mmoja katika Durban. Mwaka uliofuata moja la makundi ya kwanza ya Kiafrika lilipangwa kitengenezo katika Ndwedwe iliyo karibu. Wakati wa ule mwaka wa maana sana wa 1914, mkusanyiko wa kwanza ulifanywa katika Durban ukiwa na hudhurio la 50. Tawi lilihamishwa likapelekwa Cape Town katika 1923, na mwaka uliofuata mashine-chapa ya muundo rahisi tu ikaanza kutumiwa. Tawi lilihamishwa kwenye sehemu kubwa zaidi katika 1933, lakini hakukuwa na Kao la Betheli.

Bado hatua nyingine ya maana ilitukia katika 1952, kuhamia Elandsfontein—zapata kilometa 1,500 kaskazini mwa Cape Town na karibu kilometa 20 mashariki mwa Johannesburg. Hilo lilikuwa la kwanza la majengo katika Afrika Kusini ambalo kwa kweli lilipangiwa muundo walo na Sosaiti, kwa hiyo lilitia ndani nafasi ya kutosha ya uchapaji na pia Kao la Betheli, au mahali pa kukaa. Kwa sasa, kazi ya Ufalme ilikuwa ikifunguka katika nchi kadha zenye kutunzwa na tawi la Afrika Kusini. Kwa hiyo tawi lilihitaji kupanuliwa katika 1959, tena katika 1971, na bado tena katika 1978. Halafu hakukuwa na nafasi ya mpanuko zaidi kwenye uwanja huo.

Wale wahubiri wawili wa kwanza katika Afrika Kusini walikuwa wameongezeka kufika karibu 28,000. Ulikuwa wakati wa kutafuta mahali papya, jambo ambalo lilihusu utafutaji wa muda mrefu. Mwishowe shamba zuri la hektari 87 lilipatikana Roodekrans, ulio kilometa zapata 60 kutoka Elandsfontein. Mwongozo na msaada wa Yehova ulionekana wazi sana katika kupata na kununua mahali hapo pa kupendeza.

Kushinda Matatizo

Hata hivyo, matatizo mazito yalipasa kushindwa. Gharama ya pale mwanzoni-mwanzoni ilionekana kuwa kubwa sana, na idhini za pekee zilihitajiwa ili kujenga karakana, afisi, na mahali pa makao katika eneo la manispaa. Utatanishi wa ziada ulikuwa kule kutaminika kwa Mashahidi weusi ambao walikuwa watafsiri waishi huko. Lilionekana kama jambo la kimuujiza jinsi vipingamizi hivi vilivyoshindwa, hiyo ikitoa ushuhuda kwamba Yehova alikuwa akijenga nyumba ile. Tatizo jingine lilikuwa ukosefu mkubwa wa mafundi. Lakini wafanya kazi wa kujitolea walikuwa wepesi kujifunza zile kazi mbalimbali. Hiyo ilitia ndani akina dada. Mwangalizi mmoja alieleza hivi: “Wasichana wachanga wenye adabu sana ambao hawafai kuwa katika mahali pa ujenzi wakawa wapanga vigae walio stadi. Mimi sijaona wapanga vigae bora kuliko hao.”

Kazi ya ujenzi iliendelea polepole hapo kwanza. Ndipo wenye kujitolea wakamiminika Roodekrans—weusi, weupe, machotara na Wahindi. Akina ndugu hata walikuja kutoka nchi nyinginezo, kama vile New Zealand na United States. Jambo hilo lilikuwa lisilo la kikawaida sana katika Afrika Kusini. “Inapendeza kuona akina ndugu na dada wakifanya kazi pamoja, mataifa na rangi mbalimbali kutoka mandhari za nyuma zilizo tofauti,” akasema mmoja mwenye kujitolea. Wengi waliacha kabisa kazi nzuri-nzuri au wakachukua malikizo marefu kusaidia ujenzi kule Roodekrans. Wao walikuwa ni kutia ndani mekanika wenye ujuzi, wasanii ramani za ujenzi, mhandisi, watayarishi warasimu ramani za ujenzi, na waangalizi wa ujenzi. Vifaa vingi vya kimashine vilivyo vya gharama kubwa vilichangwa au vikatolewa kwa kuazimwa.

Namna gani ile gharama kubwa sana iliyohusika? Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova lilifanya uandalizi kwa ajili ya mkopo wa donge kubwa sana, na Mashahidi wa mahali hapo walio wa rangi zote na umri wote wakachanga kwa ukarimu. Msichana mmoja wa miaka sita aliandika. “Mimi nilikuwa nikiokoa pesa hizi kununua mtoto-bandia, lakini mimi nazipeleka kwenu ninyi. Mimi natumaini ninyi mnaweza kumaliza Roodekrans kwa pesa hizi. Wakati mimi nitakapokuwa mkubwa, mimi pia nataka kwenda Roodekrans na kufanya kazi huko.” Mvulana Mhindi wa miaka mitano alichanga pesa zake za matumizi ya kibinafsi za ile miezi sita iliyotangulia!

Katika miisho-juma mamia ya Mashahidi wa ziada walikuja kushiriki katika mradi huu muhimu. Wenye kujitolea wengine walikuja kila siku, mara nyingi wakifanya mambo ya kujidhabihu kweli kweli na kutokeza jitihada kubwa ya kufanya hivyo. Watu wenye kuzuru wasio Mashahidi walivitikisa vichwa vyao kwa kutokuwa na itikadi walipoona jinsi kazi ilivyoungwa mkono na watu wengi sana, kwa idili. Watu wanaoishi katika ujirani walivutiwa sana. Mashirika ya kibiashara ya mahali pale yalishindana ili kupata kazi ya kushughulikia katika Roodekrans, na wawakilishi wao mara nyingi walitoa maelezo juu ya ile hali ya amani na umoja.

Jengo Lenye Fahari Katika Mazingira Yenye Uzuri

Vilima vya miamba-miamba katika upande wa kusini wa ule uwanja wa ujenzi vinatazama upande wenye bonde na kijito cha kupendeza. Ingawa mali hiyo iko karibu na kitongoji cha kuvutia, bado hapo pana viumbe-mwitu wenye uhai, kama vile kware na sungura. Tai weusi na mabweha wanatembelea mahali hapa mara nyingi pia. Lile jengo lililo mahali pa kukaa, ambalo limeenezwa karibu-karibu ya ile miinamo ya chini zaidi ya vile vilima kwa meta zipatazo 360, ni la matufali mekundu. Hilo lina orofa tatu, zikiwa na mandhari zenye uzuri. Katikati pana eneo la utumishi lenye chumba cha kulia chakula, jiko, mahali pa kufulia nguo, na mahali pa kutibu wasio na afya nzuri. Karibu na hapo pana lile jengo lenye afisi nyingi na mahali pakubwa sana pa uchapaji, ambapo kwa kutaja kijuu-juu tu ni kama ukubwa wa safina ya Noa. Hapo ndipo penye nyumba ya kuwekea ile mashine-chapa ya offseti ya muundo wa TKS inayotumia rangi nne.

Upande wa magharibi wa jengo lile lililo mahali pa kukaa lipo eneo la ukulima na ghala kubwa, ambayo ilitumiwa kama chumba cha kulia chakula na jiko wakati wa ujenzi. Viwanja vya nyasi na alfalfa vinaandaa majani makavu kwa ajili ya kundi la ng’ombe wa maziwa. Kuna mamia ya vichaka vyenye majani yanayotokea-tokea kwa zamu katika vile vilima vilivyo nyuma ya mahali pa kukaa. Zaidi ya mitieukalipto mirefu iliyoko, miti mipya mingi, sakafu za udongo wa maua yenye rangi tofauti-tofauti, na viwanja vikubwa vilivyotandazwa majani mazuri vimepandwa.

Ile Programu ya Wakfu

Kutano la watu karibu 4,000 lilikusanyika katika nafasi wazi karibu na lile jengo la mahali pa kukaa kwa ajili ya wakfu Jumamosi alasiri, Machi 21,1987. Jukwaa la muda lilielekeana na vile vilima, likitoa hali ya watu kuhisi wamo katika wanja kubwa la michezo lililozingirwa kwa ukuta. Mwenye kiti, Ndugu R. F. Stow, alisoma ujumbe mbalimbali wa kuunga mkono kutoka nchi 17. Uliokuwa wa kugusa moyo zaidi kati ya ujumbe huo ulikuwa ule kutoka kwa Maud Johnston, mke wa yule mwangalizi wa tawi wa kwanza katika Durban. Akiwa na umri wa miaka 92, yeye bado anatumikia katika Betheli ya Australia.

P. J. Wentzel, mwangalizi wa Idara ya Utumishi, alikuwa ndiye msemaji wa kwanza, na yeye alitoa muhtasari mfupi wa historia ya kazi ya Ufalme katika Afrika Kusini. Yeye alilinganisha lile hudhurio la 50 kwenye kusanyiko la kwanza katika 1914 na lile hudhurio la 99,000 kwenye mikusanyiko ya 1986. Halafu, J. R. Kikot, mwangalizi wa karakana, akaeleza juu ya uchapaji vitabu katika lugha nyingi na ile kazi ya watafsiri zaidi ya 50. Yeye alitaja pia kwamba katika 1979 mashine-chapa kubwa ya muundo wa TKS ambayo ilikuwa zawadi kutoka tawi la Japani, ilisimamishwa mahali payo, lakini ilichapa katika rangi mbili tu. Hivi majuzi, visehemu viwili zaidi, ambavyo vilikuwa pia zawadi kutoka Japani, viliongezwa kwenye ile mashine-chapa. Kama tokeo, Mnara wa Mlinzi wa Aprili 1, 1987, ulichapwa ukiwa na rangi kamili, kwa mfurahio wa wote.

C. F. Muller, mratibu wa Halmashauri ya Tawi, alieleza jinsi Yehova alivyosaidia kuandaa ule uwanja, zile pesa, wale wastadi, na wale wafanya kazi wenye ujuzi mwingi. Roho ya Mungu pia ilitokeza upatano mzuri miongoni mwa zile jamii za rangi mbalimbali. Ingawa katika hatua moja ilionekana kama haiwezekani kujenga karakana katika eneo la kimakao lililo la hali ya juu, na kwa weusi kuishi humo, Yehova aliifungua njia, kwa hiyo yeye alikuwa ndiye yule Mjenzi Stadi wa kweli kweli!

Msemaji aliyefuata alikuwa Carey Barber, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Hotuba yake nzuri ilitegemea Isaya 65:17-19, NW, ambayo inatabiri jinsi watu wa Yehova ‘watachachawa na kuwa wenye shangwe milele.’ Msemaji alieleza kwamba ‘kuchachawa’ kunamaanisha “kurukaruka kwa furaha” na kwamba ndiyo namna ya furaha iliyo ya juu kupita zote. Kwa uhakika ilikuwa siku yenye furaha kwa wale waliokuwako. Ile hotuba ya wakfu ilitolewa na Milton Henschel, pia wa Baraza Linaloongoza. Yeye alitoa sala ya pekee kwa Yehova, akitoa shukrani kwa kuandaa lile jengo, ambalo sasa liliwekwa wakfu kwake Yeye.

Siku iliyofuata Mashahidi 28,250 na watu waliopendezwa walikusanyika katika Rand Stadium, Johannesburg, ambako wao walisikia muhtasari mfupi wa ile programu iliyokuwa kule Roodekrans. Katika hotuba moja ambayo ilitafsiriwa katika Kizulu, Henschel alionyesha jinsi Mashahidi wa Yehova, wakiongozwa na Yehova na Yesu, ni wenye shangwe ya ushindi kila mahali na wanaeneza “harufu tamu ya Kristo” na maarifa mengine ya Biblia. (2 Wakorintho 2:14-17, NW) Yeye alimalizia kwa mambo yaliyoonwa yenye kutia moyo ambayo yalifurahisha sana ile hadhirina kubwa.

Wakati wa zile siku chache zilizofuata, mikusanyo kama hiyo ilifanywa katika Durban na Cape Town. Hizo zilikuwa pindi ambazo hazitasahauliwa kamwe na Mashahidi wa Yehova katika Afrika Kusini. Jamaa ya Betheli kule Roodekrans kwa uhakika itakumbuka kwa muda mrefu ile siku ya kuwekwa wakfu kwa kao jipya lao. Kukiwa na Mashahidi zaidi ya 40,000 walio watendaji sasa katika Afrika Kusini badala ya wale 28,000 wakati kazi ilipoanza kule Roodekrans, ile ‘nyumba ambayo Yehova alijenga’ inajazia uhitaji wa haraka ulio wa muhimu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki