Mkusanyiko Ambao Uliongeza Itibari Yetu Katika Yehova
BABA yetu wa kimbingu, Yehova Mungu, anajua mambo yale hasa ambayo sisi tunahitaji. Na yeye anayatia katika akili za watumishi wake waliojitoa wakfu ambao wanaelekeza kazi yake duniani ili waridhishe uhitaji huo. Kwa uhakika jambo hilo linaweza kusemwa juu ya ile “Itibari Katika Yehova” (“Tumaini Katika Yehova”) Mikusanyiko ya Wilaya, iliyofanywa katika sehemu zote za dunia kutoka Juni, 1987 na kuendelea. Kwa kweli hiyo ilitumikia kuimarisha Wakristo dhidi ya mawazo ya kufikiriwa-fikiriwa tu, mashaka, na ukosefu wa itibari ulioenea sana katika ulimwengu.
Kile kichwa cha “Itibari Katika Yehova” (“Tumaini Katika Yehova”) kiliunganishwa-unganishwa kwa ustadi ndani ya programu. Hicho kilikaziwa na taarifa ambazo zilikuwa zenye mkazo na za kutoboa mambo wazi, ambazo zilisema mambo kinaga-ubaga na bila kuficha. Yote hayo yalitilia nguvu itibari ya wasikilizaji katika Yehova. Wao wangeweza kwenda nyumbani huku kile kichwa kikiwa kimekazwa kwa njia isiyofutika juu ya mioyo na akili zao, wakiwa wamepiga moyo konde kwamba kwa vitendo na maneno yao wao wangetangaza kwa wote kwamba wao wanaitibari kwa ukamili katika Yehova.
“Itibarini Katika Yehova, Ninyi Watu”
Maneno hayo yanayopatikana kwenye Isaya 26:4 yalieleza kile kichwa cha siku ya kwanza. Kwa kufaa sana, ile programu ilianza kwa hotuba “Elekeza Sikio Lako Kwenye Semi za Mungu.” Msemaji alionyesha kwamba usemi huo, ambao unatukia mara nyingi katika Neno la Mungu, unamaanisha kutoa fikira kamili kwa akili na moyo pia kwenye mambo ambayo yanasemwa, kwa kusudio la kutumia mambo ambayo yanasikiwa. Hiyo inamaanisha kujizoeza kujiweza na kukaza fikira juu ya mambo yanayosemwa, si kuacha akili itange-tange. Ni kwa kuinamisha sikio hivyo tu ili lisikie kwamba itibari yetu katika Yehova itaimarishwa na mambo ambayo sisi tunasikia na ndipo sisi tutakaposukumwa kutenda kulingana na mambo yanayosemwa. Na je! huo sio unaopaswa kuwa mwelekeo wetu wakati wo wote sisi tunaposikia Neno la Mungu likielezwa waziwazi, kama vile kwenye mikutano yetu ya kundi?
Mwenyekiti wa mkusanyiko alitoa habari iliyofuata, “Wale Wanaoitibari [Wanaotumaini] Katika Yehova Wana Furaha Kuwa Hapa.” Yeye alionyesha kwamba kwa kadiri ambavyo itibari yetu inazidi kuwa kubwa katika Yehova, ndivyo furaha yetu inavyozidi kuwa kubwa. Kuwa na itibari katika Yehova kunamaanisha kujiwekelea kabisa kabisa na kwa uhakikisho juu yake. Kadiri ambavyo maarifa yetu ya kujua Yehova yanavyokuwa makubwa zaidi na shauku yetu kwake yeye, ndivyo itibari yetu katika yeye itakavyokuwa imara zaidi. Kichwa cha mkusanyiko hakikuwa shime ya vivi hivi tu. Sisi tunadhihirisha itibari yetu katika Yehova katika njia nyingi sana, na njia moja isiyo ndogo ya kufanya hivyo ni kuonyesha ufikirio kwa wengine. Kwenye umalizio wa maelezo yake na kwa upendezo wa wote, mwenyekiti alitoa kitolewaji cha kwanza—chombo cha rangi za kupendeza, chenye mafaa kwa kutolea ushuhuda. Hicho kilikuwa ile trakti Sababu kwa Nini Wewe Unaweza Kuitumaini Biblia.
Baada ya kuzungumzia juu ya kielelezo kinachostahili kuangaliwa cha Daudi wakati alipoelekeana na lile jitu Goliathi, msemaji aliyefuata alitokeza ile sehemu “Jinsi Wengine Wameitibari [Wametumaini] Katika Yehova” katika nyakati za ki-siku-hizi. Mathalani, kulikuwa na dada yule ambaye mume wake asiyeitikadi, akiwa na bunduki mkononi, alitisha kumuua kama yeye angeendelea kwenda kwenye mikutano. Wengine wameonyesha itibari yao katika Yehova wakati walipoambiwa kwamba uhai wao ulitegemea kukubali kutiwa damu mishipani. Vijana wametoa uthibitisho wa itibari yao katika Yehova kwa kuzuia sana mikazo ya kuingilia michezo au kuchagua kufuatia elimu ya juu zaidi baada ya kumaliza shule ya sekondari.
Ile programu ya asubuhi ya Ijumaa ilimalizia kwa hotuba “Watu Waliowekwa Mbali na Ulimwengu.” Sisi tunaonyesha kwamba tuna itibari katika Yehova kwa kuendeleza mwenendo wetu pamoja na ile jinsia tofauti ukiwa usioweza kufanyiwa shtaka la aibu, kwa kuacha kanuni za Kikristo zisimamie tafrija zetu, na kwa kuepuka mavazi yote na mapambo ambayo yangeelekea kuzuia ule utofautiano wa wazi kabisa kati ya jinsia zile mbili zisionekane. Sisi tunapoendelea hivyo kuwekwa mbali na ulimwengu, kwa mara ushuhuda wenye nguvu nyingi unatolewa, hata ukifanya watu fulani waingie katika ukweli.
Alasiri ya Ijumaa, programu ilianza na ile hotuba “Kupainia Kunahimiza Ukuzi wa Kiroho.” Na hiyo ni kweli kama nini! Kupitia Neno la Yehova, roho takatifu yake, na tengenezo lake, Mungu anaandaa mambo ambayo sisi tunahitaji ili tusonge mbele kuwa “mtu mwenye ukuzi kamili,” lakini kupainia kunatutia katika hali ya kuweza kutumia vizuri zaidi na kwa ukamili zaidi maandalizi ya kiroho hayo yote. (Waefeso 4:13, NW) Kwa njia ya mahoji, mapainia walieleza jinsi huduma ya wakati wote iliwawezesha wao wasitawishe kwa ukamili zaidi lile tunda la roho ya Mungu, kuonyesha upendo mwingi zaidi kwa watu, kuwa hodari zaidi katika kufanya huduma, kumwitibari Yehova kwa kadiri kubwa zaidi, na hivyo kuwa na uhusiano wa karibu zaidi pamoja na yeye. Yote hayo yamehimiza ukuzi wao wa kiroho.
Ndipo ilipokuja ile hotuba ya msingi, “Watu Ambao Sikuzote Huitibari [Hutumaini] Katika Yehova.” Hotuba hiyo yenye kuchochea ilionyesha kwamba sisi tuko tofauti na ulimwengu kwa sababu sisi tunaitibari katika Yehova kwa ukamili. Kwa kutegemea msingi wa Maandiko mbalimbali kutoka kitabu cha Isaya, msemaji alionyesha jinsi sisi tumeona maunabii ayo hayo yenye kutia moyo yakitimizwa katika Mashahidi wa Yehova kwa sababu sisi tunaitibari katika Mungu. Tukiwa na uhakika, sisi tunaweza kutazama mbele kwenye muda katika wakati ujao ulio karibu ambapo Yehova ataonyesha ghadhabu yake kuelekea mataifa yote na ndipo aleteshe Paradiso.
Wanamkusanyiko walitiwa moyo kwamba “Eneza Habari Njema Katika Kila Nafasi.” Baada ya umaana wa kufanya jambo lilo hilo kukaziwa, mawonyesho kadha yalionyesha jinsi ile trakti mpya Sababu kwa Nini Wewe Unaweza Kuitumaini Biblia inaweza kutumiwa kwa matokeo mazuri katika ushuhuda wa vivi hivi na usio wa vivi hivi pia. Kwa uhakika, sikuzote sisi tunataka kuwa na trakti hizi pamoja nasi, kwa maana kueneza hizi habari njema katika kila nafasi kunapasa kuwa tabia ya kila shahidi wa Yehova na ni njia ya kuonyesha kwamba sisi tunaitibari katika Yeye.
Iliyothaminiwa sana ilikuwa ile hotuba “Wazazi—Fikieni Moyo wa Mtoto Wenu Tangu Uchanga.” Ili mtoto akue katika kuitibari katika Yehova, lazima mazoezi yake yaanze katika uchanga na lazima mazoezi hayo yapewe nafasi ya kwanza. Ni hapo tu inapowezekana kuyamaliza nguvu yale mavutano mabaya yote ya televisheni, ya shuleni na ya mitaani. Wewe ukitaka mtoto wako awe jambo fulani, acha yeye aone jambo hilo katika wewe,’ wazazi wakaambiwa. Ndiyo, kuweka kielelezo kizuri ndiyo njia bora zaidi ya kufikia moyo wa mtoto. Lazima pande zote za utumishi mtakatifu zije kiasili na ziwe zenye kufurahisha ndipo hali ya mazingira ya nyumbani yawe ya kiroho kweli kweli. Sisi hatutaki kamwe kunung’unika juu ya wakati na jitihada zinazohusika. Endelea kufikia moyo wa mtoto kwa mawasiliano mazuri pia. Jizoeze kutumia uthabiti pamoja na upendo, na uvute fikira kwenye sababu za mambo wakati unapotoa nidhamu. Toa sifa na thawabu wakati zinapostahiliwa, lakini usihonge kamwe mtoto wako.
Yenye kuhusiana sana na tatizo zito lililo miongoni mwa Mashahidi fulani vijana ilikuwa ile hotuba “Vijana—Lindeni Dhidi ya Kuishi Maisha Maradufu.” Kwa sababu gani vijana fulani wanajaribu kuendesha maisha maradufu? Kwa sababu wao wanataka kibali cha wazazi wao na ndugu zao na bado wanaogopa mzaha wa vijana walimwengu wa rika lao. Au, wao wanahisi kwamba wanakosa anasa fulani ikiwa wao hawavuti sigareti, hawatumii dawa za kulevya, au hawashiriki katika ngono zisizo halali. Lakini hakuna kabisa njia ya kuepuka uhakika wa kwamba kuishi ko kote huko kwa maisha maradufu kunaleta shtaka la aibu juu ya Yehova, kihoro kwa wazazi wa mtu, na shida kubwa kwa mtu mwenyewe. Mtu ye yote anayepanda mbegu kuelekea kwenye mwili anavuna uozi, hali kudumisha uhusiano mwema pamoja na Yehova, kuitibari katika yeye kwa ukamili, kunalinda mmoja asiishi maisha maradufu.—Wagalatia 6:8.
Yenye kukazia kwa nguvu nyingi kanuni zote hizo ilikuwa ile drama ambayo ilifuata mara baada ya hapo. Ikiwa na kichwa “Utii Mshikamanifu kwa Yehova na Tengenezo Lake,” ilikuwa na chakula kingi kwa mawazo ilipokuwa ikionyesha jinsi mzee mmoja alivyohisi akishurutika kujiuzulu kwa sababu binti yake alifunuliwa wazi kuwa mmoja mwenye kuishi maisha maradufu. Drama hiyo ilifanya wengi watokeze maneno ya uthamini wenye idili.
“ltibari [Tumaini Katika] Yehova na Ufanye Mema”
Kwa kutegemea msingi wa Zaburi 37:3, NW, hicho kilikuwa ndicho kichwa cha siku ya pili ya mkusanyiko. Baada ya ufikirio wa andiko la siku, ambao ulitia ndani kitia-moyo cha kufanya hivyo kila siku, programu ilitokeza wazi mfululizo wenye sehemu tatu wenye kichwa “Kudhihirisha Itibari Yetu [Utumainifu Wetuj Katika Yehova.” Msemaji wa kwanza alionyesha uhitaji wa kufanya hivyo “Kwa Kujifunza kwa Bidii Neno la Mungu.” Ni lazima sisi tufanye hivyo ili tuepuke ule mtego wa kinaya na vitanzi vya ufuatiaji wa vitu vya kimwili, ukosefu wa adili za ngono, na uasi-imani. Sosaiti imeandaa wingi wa maandalizi ya kujifunzia Biblia, kama ile Watch Tower Publications Index 1930-1985 mpya. Ni kwa kutumia kwa ukamili tu misaada hiyo kwamba sisi tunaweza kuwa na uhusiano mwema, wenye itibari pamoja na Baba yetu wa kimbingu na kuwa wenye matokeo tukiwa Mashahidi wake.
Msemaji aliyefuata alikazia uhakika wa kwamba itibari katika Yehova inadhihirishwa “Kwa Kuzoea Mambo Tunayojifunza.” Ndiyo, sisi tunataka kuwa watendaji wa lile Neno, sikuzote tukihangaikia kufanya maendeleo. Katika maeneo gani? Ala, ni katika mahusiano yetu pamoja na wengine, katika mavazi na mapambo yetu, katika kutafuta kwanza Ufalme wa Mungu, na katika kuendeleza amani na umoja miongoni mwa ndugu zetu! Ili tuepuke ile dhambi ya kujitanguliza, ni lazima sisi tuwe waangalifu kubaki katika mahali petu katika jamaa na kundi. Sisi tukitumia hivyo mambo ambayo tunajifunza, itakuwa dhahiri kwa wote kwamba sisi tunaitibari katika Yehova.
Mfululizo huo ulimalizia kwa mazungumzo juu ya ile habari “Kudhihirisha Itibari Yetu [Utumainifu Wetu] Katika Yehova—kwa Kujikakamia Wenyewe Shambani.” Kwa kufanya hivyo, sisi tunaonyesha upendo wetu kwa Mungu na jirani yetu na kujihami wenyewe. Huenda tukatosheka na utumishi wenye uvuguvugu, wa kuonyesha tu, lakini je! Yehova anatosheka? Je! Mwana wake hatuhimizi sisi tujikakamie wenyewe kisulubu? (Luka 13:24, NW) Maongezeko ambayo sisi tunaendelea kuona katika wahubiri, mapainia, na saa za wastani zinazotumiwa katika huduma ya shambani zapasa kutuchochea tujaribu kufanya mengi zaidi kibinafsi. Je! hivyo sivyo? Kwa utendaji wa juhudi, sisi tutaweka kielelezo kizuri, tuonyeshe itibari yetu katika Yehova, na kupata tabasamu yake ya kibali.
Ndipo lilipokuja ombi la kusihi dhamiri yetu katika ile hotuba “Kuzoea Kutoa kwa Kipimo Kilichojaa.” Ni kwa utele kama nini Yehova anatuandalia sisi kiroho na kimwili! Sisi tunaonyesha uthamini wetu kwa kufuata kielelezo chake kwa kutoa ushuhuda na pia kwa kuchanga kifedha kuelekea ile kazi ya kuhubiri. Je! sisi tungeweza kupunguza-punguza anasa zenye gharama nyingi ili tutoe kwa kipimo cha kujaa zaidi?
Ile hotuba ya ubatizo, “Wakfu na Ubatizo Wako Huonyesha Itibari [Kutumaini] Katika Yehova,” ilionyesha sababu kwa nini sisi tunaitibari katika Mungu na si katika wanadamu. Ubatizo wa maji unaonyesha kufa kuelekea mwenendo wetu wa zamani na kuinuliwa kuja kwenye njia ya maisha ambayo yanapatana na mapenzi ya kimungu. Baada ya hapo, lazima sisi tuendelee ‘kujizoeza haki, kupenda fadhili, na kuwa na kiasi katika kutembea pamoja na Mungu wetu.’ (Mika 6:8, NW) Miongoni mwa wale wenye kubatizwa walikuwamo msichana mmoja mwenye umri wa miaka 8 ambaye anaongoza mafunzo ya Biblia mawili kwa wanashule wenzake, mwanamume mwenye umri wa miaka 79, na mtu mmoja mwenye kupooza mikono yote miwili na miguu yote miwili mwenye umri wa miaka 44.
Programu ya alasiri ya Jumamosi ilianza kwa ile hotuba: “Kufanya ‘Mambo Yaliyo ya Lazima’ Ili Kumpendeza Mungu.” Ikitegemea msingi wa Matendo 15:28, 29, hiyo ilionyesha uhitaji wa kuzoeana mapema na madaktari wetu kuhusiana na msimamo wetu juu ya damu kabla ya jambo hatari la kitiba kutokea na ikatoa madokezo mazuri juu ya jinsi ya kufanya hivyo.
Hotuba ambayo ilitokeza kwa haraka maelezo mengi ya kuipendelea ilikuwa “Uzazi Unaojali Madaraka ya Kuzaa Katika Huo Wakati wa Mwisho.” Hiyo ilitokeza maoni yenye masawaziko, ikionyesha kwamba ingawa kuzaa watoto kunaweza kuleta shangwe za namna nyingi, kunaleta pia madaraka mengi na mara nyingi kunatokeza maumivu ya moyoni, kama vile wakati watoto wanapofanya kosa. Hasa akina mama wanaelekea kupata hasara kiroho kwa sababu ya himila za kuzaa watoto.
Ndipo ilipokuja ile hotuba “Wazee—Lindeni Itibari [Amana] Yenu.” Itibari hiyo ni kulichunga kundi la Mungu—kuwaongoza, kuwalisha, na kuwahami, kwa kupatana na Isaya 32:1, 2. Kutimiza wajibu mbalimbali ya kijamaa kama unavyostahili huku mtu akitunza majukumu ya kundi kunatokeza mwito wa ushindani kweli kweli. Ili wazee walinde itibari yao inamaanisha pia kuepuka vitanzi vya kufuatia vitu vya kimwili, tafrija za kupita kiasi, na anasa zisizo halali. Miongoni mwa wale waliohojiwa kwenye mkusanyiko wa wilaya wa Dortmund katika Jamhuri ya Muungano wa Ujeremani ya Magharibi alikuwamo mzee mmoja ambaye amekuwa akilinda itibari yake kwa miaka 60.
Ile hotuba “Tii Wale Wanaoongoza” kwa kufaa ikawa ndiyo iliyofuata. Upendo utatusaidia sisi tuwe wenye kujiweka chini na watiifu kwa waangalizi wa kundi na utatuzuia tusiwe wenye kukosa subira kwa sababu wao si wakamilifu, kwa maana wala sisi si wakamilifu. (Waebrania 13:17) Kwa kuonyesha staha kwa wazee katika mambo makubwa na madogo, sisi tunasaidia wao kuhimili himila zao badala ya kuziongezea.
Programu ya Jumamosi ilikuja kwenye kikomo kwa ule mfululizo wenye sehemu tatu “Neno la Mungu li Hai,” wenye kutegemea msingi wa Waebrania 4:12. Msemaji wa kwanza alionyesha kwamba hilo liko hali kwa sababu “Linatia Nguvu Zenye Kugeuza.” Leo, hata kama katika nyakati za Biblia, sisi tuna vielelezo vingi vinavyoonyesha jinsi itibari katika Neno la Mungu limesababisha watu kufanya mabadiliko makubwa katika maisha zao na imewatia nguvu kuhubiri pasipo woga.
Sehemu ya pili ya mfululizo huo ilionyesha kwamba Neno la Mungu “Ni Kali Zaidi ya Upanga wo Wote Wenye Makali Mawili.” Hilo linatuwezesha sisi kukata-kata vipande vipande mafundisho bandia ya Kibabuloni. Linatusaidia sisi pia ‘kugawa kati ya nafsi na roho’ katika maana ya kwamba linatuwezesha sisi tutofautishe wazi kati ya vitendo vyetu na makusudio yetu halisi. Kwa kutumia ule “upanga” katika njia hiyo, sisi tutakuwa wenye kupendeza zaidi Yehova Mungu na wenye amani zaidi pamoja na wengine na sisi wenyewe.
Ile sehemu ya kumalizia ilionyesha kwamba Neno la Mungu li hai kwa sababu “Linakaza na Kusukuma Moyo Wetu.” Katika Biblia, lile neno “moyo,” linatumiwa kwa ujumla kwa njia ya usemi wa mfano na linarejeza kwenye mtu wa ndani zaidi ambaye anadhihirishwa katika sifa zetu za kiakili na maoni ya kimoyo. Neno la Mungu linaimarisha moyo wetu kwa kufunua sifa zake za ajabu kupitia shughuli zake pamoja na aina ya wanadamu. Upendo wa Mungu usio na ubinafsi unatusukuma sisi kumwiga yeye. Katika maelezo yake ya kumalizia, msemaji alipitia-pitia kumbukumbu la hatua za Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi katika kuchapisha Biblia na akasisimua wasikilizaji kwa kutangaza kutolewa kwa chapa-dilaksi ya mfukoni iliyo na sura nzuri ya New World Translation.
“ltibari [Mtumaini] Katika Yehova kwa Moyo Wako Wote”
Kichwa hicho cha Jumapili, kilichochukuliwa kutoka Mithali 3:5, NW, kilipewa fikira na mzee ambaye alifungua programu na kuzungumzia andiko la siku. Ndipo ilipokuja ile hotuba yenye kutafuta-tafuta yaliyo katika nafsi “Je! Wewe Unachukua Vitu Vitakatifu Ki-Vivi-Hivi?” Ulimwengu unahisi kwamba hauna deni lo lote kwa Mungu, lakini tukiwa Mashahidi wa Yehova, sisi tunajua kwamba ili tuwe na kibali chake, ni lazima kuwaiga wale wanaume waaminifu wa zamani kwa kuonyesha uthamini kwa vitu vitakatifu. Msemaji alizungumza 13 kati ya hayo, miongoni mwa hayo likiwamo jina la Yehova, Neno lake, roho takatifu yake, sheria zake, tengenezo linaloonekana lake, uhusiano wetu pamoja na Mungu, mikutano yetu, na mapendeleo yetu ya utumishi. Ikiwa sisi tunathamini kweli kweli vitu vitakatifu hivi, sisi tutaviweka kwanza katika maisha zetu, tuitibari katika Yehova kwa ukamili, na tutathawabishwa na yeye.
Ndipo ilipokuja ile hotuba yenye mipigo mikali “Chukia Kabisa Kabisa Mwendo Wenye Aibu wa Ulimwengu.” Kwa sababu ya kutoboa mambo waziwazi, hiyo ilitokeza maelezo kama haya, “Ndicho kitu tulichohitaji hasa!” Kwa kuwa uovu umekolea, lazima Wakristo wajilinde dhidi ya kuona ukosefu wa adili na jeuri kana kwamba si kitu. (2 Timotheo 3:1-5) Basi, haitupasi sisi kutazama wala kusikiliza mambo kama hayo yanapotangazwa katika televisheni au redio, wala hatupaswi kusoma juu yayo katika vichapo vya pindi kwa pindi. Kwa kweli, sisi hatutaki hata kuwa tukifikiri juu ya mambo hayo. ‘Wakristo wa kweli ambao wanataka kudumisha uhusiano mwema pamoja na Yehova hawawezi kabisa kuwa na lo lote kuhusiana na poronografia,’ sivyo, hata kidogo!
Programu ya asubuhi ya Jumapili ilimalizia kwa ile drama ya Kibiblia yenye kuvuta fikira kwa mbano Yehova Huokoa Wale Wanaoita Juu ya Jina Lake. Hiyo ilishughulika na matukio kadha katika maisha ya Yoshua. Kulingana na hali za kihalisi, hiyo ilitia katika akili taswira ya jinsi wakaaji wa Yeriko lazima wawe waliona kule kupiga miguu kwa wanaume-vita wa Israeli kuzunguka mji huo siku baada ya siku. Iliyokaziwa pia ilikuwa imani kubwa ya Rahabu, ambayo ilitokeza kukombolewa kwake yeye na watu wa nyumba yake. Katika kumalizia, wote waliulizwa: ‘Je! wewe una imani thabiti na uhakika kama wa Yoshua na washiriki wake wenye ushujaa? Ikiwa ndivyo, sisi tunaweza kutumaini kushiriki katika ushindi wa mwisho kabisa wa Yehova juu ya adui zake.’
Ile sehemu kubwa yenye kuhusu watu wote ya “Itibari [Tumaini] Katika Yehova” Mkusanyiko wa Wilaya ilikuja kwa ile hotuba, yenye kichwa “Katika Nyakati Zetu Zenye Hofu, Ni Nani Unayeweza Kuitibari [Kutumaini] Kikweli?” Hiyo ilielewesha wazi sana ule uhakika wa kwamba aina ya wanadamu inahitaji sana sana chanzo cha itibari! Kwa uwazi, hiyo ilionyesha upumbavu wa kuitibari katika wanadamu. Kwa sababu hiyo, Neno la Mungu linatushauri sisi tuitibari katika Yehova na linatupa sababu zenye imara za kufanya hivyo. Inatupasa sisi tuitibari katika yeye kwa sababu ya sifa zake na kumbukumbu lake la matendo katika kukomboa wale ambao wamekuwa wakiitibari katika yeye, Mfalme Hezekia akiwa kielelezo kimoja chenye kuonekana wazi sana. Karibuni ukombozi kama huo utapatwa na wale ambao mwendo wa vitendo vyao unaonyesha itibari katika Yehova.
“Endeleeni ‘Kuishi Kiamani’ “ndicho kilichokuwa kichwa cha ile hotuba ambayo ilifuata mara hiyo. Kuishi kiamani kunamaanisha kuwa tukiishi kwa kuendeleza amani kwa utendaji. Kunamaanisha pia kuwa na amani pamoja na sisi wenyewe kwa sababu ya kushikilia dhamiri njema. Kwa kudhihirisha yale matunda ya roho ya Mungu, hasa upendo na kujiweza, sisi tutaweza kuishi kiamani pamoja na jamaa zetu wenyewe na pamoja na ndugu na dada zetu katika kundi.
Hakuna swali juu ya uhakika wa kwamba mkusanyiko huu ulitutayarisha sisi kwa vifaa vya “Kukabili Wakati Ujao kwa Itibari [Tumaini] Kamili Katika Yehova,” ambayo ilikuwa ndiyo habari ya hotuba ya kumalizia. Hiyo ilijumlisha pamoja programu ile kwa njia nzuri kama nini! Msemaji alikazia kwamba kila siku tunahitaji kuitibari katika Yehova kwa moyo wetu wote, tumwangalie sana kwa kujali mambo yake katika njia zetu zote, na kumwacha yeye aelelekeze vijia vyetu. (Mithali 3:5, 6) Wanamkusanyiko walithamini kwa njia kubwa kusikia kuhusu zile hotuba za watu wote 16, kaseti za Mnara wa Mlinzi, na kuchapwa upya kwa makala moja kuhusu damu ambayo ilitokea katika Amkeni! (la Kiingereza), na kwamba hiyo itapatikana kwa ajili ya sisi ili tuwape madaktari wetu. Ndivyo, na sisi tulisisimuliwa kujifunza juu ya kutolewa kwa drama nyingine ya Kibiblia ikiwa katika kaseti, kuchapwa upya kwa mabuku yaliyojaliwa ya Mnara wa Mlinzi (1960-1979, Kiingereza), na kuchapwa kwa trakti tatu zaidi.
Wote waliokuwapo kwa ajili ya ule “Itibari [Tumaini] Katika Yehova” Mkusanyiko wa Wilaya walijengwa kiroho kwa njia kubwa. Sasa wao wako tayari kuelekeana na wakati ujao wakiwa na uhakika kamili katika Baba yao wa kimbingu. Na kwa kufaa wote walitiwa moyo na lile himizo la kumalizia: “Tunapokabili wakati ujao, sisi sote kwa umoja na tuthibitishe kwa njia yetu ya maisha kwamba ‘tunaitibari katika Yehova.’”
[Chati katika ukurasa wa 26]
“Itibari [Tumaini] Katika Yehova” Mikusanyiko ya Wilaya mbalimbali
Hudhurio Waliobatizwa
Ailandi 4,326 61
Austria 24,686 360
Brazili 442,731 7,626
Denmark 23,029 200
Finland 26,144 284
Hispania 105,591 2,394
Hong Kong 2,661 49
Italia 221,227 5,496
Jamaika 18,540 184
Jamhuri ya Muunga
no ya Ujeremani 159,361 1,455
Japani 232,904 3,416
Kolumbia 82,321 1,852
Korea 82,296 2,013
Malaysia 1,154 15
Norowei 12,703 218
Puerto Riko 49,953 377
Sweden 30,099 312
Switzerland 19,459 261
Trinidad 10,649 132
Ufaransa 138,683 2,705
Uingereza 156,417 1,225
United States 1,288,313 13,562
Ureno 55,057 1,074
Venezuela 100,777 1,664
Zimbabwe 45,544 580
[Picha katika ukurasa wa 25]
Drama zenye kuamsha fikira ziiikazia uhitaji wa kuitibari katika Yehova
F. W. Franz, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, akihutubia wasikilizaji wi mkusanyiko ambao wanasikiliza kwa uangalifu mwingi
[Picha katika ukurasa wa 26]
Wengi walionyesha itibari katika Yehova kwa kubatizwa ili waonyeshe wakfu wao kwake