Kujua Yaliyo Katika Habari
Ponyo la Peke Yake
Wakati wengi walio wastadi wa ulimwengu kuhusiana na kuzeeka walipokutana mwaka uliopita kwenye Kitovu cha Tiba cha Mount Sinai ya New York ili wazungumzie bayolojia ya kuzeeka, uhakika mmoja ulionekana wazi —hakuna mmoja angeweza kuafikiana juu ya kwa nini mwanadamu huzeeka na kufa. Wastadi fulani wanatoa nadharia ya kwamba “kuzeeka ‘kumepangiwa programu’ kwa njia ya chembe za urithi, kama vile hatua nyinginezo za maisha,” inaripoti Newsweek on Science & Technology. Hata hivyo, kichapo hicho kinaongezea kwamba “ni vigumu kudhania ni kwa nini asili ingetokeza mgeuko-geuko wa chembe ya urithi iliyo ya kuzeeka.” Nadharia moja iliyodokezwa na Leonard Hayflick, mchunguzi wa uzeekaji anayefanya kazi na Chuo Kikuu cha Florida, ilikuwa kwamba “huenda ikawa chembe fulani za urithi ziligeuka-geuka ili ziendelee kufanya watu wawe wenye afya na kuendelea kutenda kazi mpaka waweze kuzaa.” Hayflick anamalizia kwamba kufikia wakati ambapo mwanadamu anakuwa na umri wa miaka 30 hivi, chembe hizo za kurefusha maisha zingeanza kuchakaa. Uhakika ni kwamba, wastani wa tazamio la maisha kwa Mwamerika ni kidogo zaidi ya miaka 74 “kwa kawaida ya leo,” na hata “maponyo kwa magonjwa ya umri wa uzee—kansa, yabisi kavu, ugonjwa wa kudhoofika kwa nguvu za kufikiri vizuri kwa sababu ya uzee—hayatasaidia sana kuyarefusha,” kinasema kichapo hicho.
Ingawa wanasayansi wanashindwa kupata ponyo la kuzeeka kama vile wanavyoshindwa kupata kisababishi chake, wanafunzi waangalifu wa Neno la Mungu hawashindwi. Sababu ya mwanadamu kuzeeka na kufa inaelezwa kwenye Warumi 5:12: “Kwa mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote.” Ponyo la pekee kwa athari za dhambi iliyorithiwa litakuja kupitia dhabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo. “Mungu alituma Mwana wake mzaliwa pekee ndani ya ulimwengu ili kwamba sisi tupate uhai kupitia yeye.” (1 Yohana 4:9, NW) Chini ya utawala wa Ufalme wake, “mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufunuo 21:3, 4.
Jambo la Umaana kwa Ulimwengu Wote Mzima
Wakati viongozi wa zile serikali mbili zilizo kubwa ulimwenguni walipokutana siku ya Desemba 8, 1987, kutia sahihi mkataba wa kupunguza makombora ya kutupwa, hilo lilielezwa kuwa tukio lililo ‘la umaana sana’ kwa aina ya binadamu. Kwa nini? Kwa sababu “ndiyo mara ya kwanza tangu kupambazuka kwa Kizazi cha Atomi kwamba zile serikali zilizo kubwa zaidi zimeafikiana si kuzuia tu silaha za nyukilia bali kuondoa kabisa mifumo mizima,” inaripoti Daily News ya New York. Ikieleza juu ya mkataba wenyewe na hata hesabu iliyopunguzwa ya silaha, News iliongezea hivi: “Ikiwa uthibitifu na kanuni za mambo hayo zinaweza kuendelezwa kwa muda mrefu zaidi, huenda mwishowe historia ikaziandika katika kumbukumbu kuwa ndicho kitendo cha kwanza katika utafutaji wa Dunia ulio wa maana zaidi wa amani na usalama wa kimataifa.”
Ni kweli, madokezo ya sasa hivi kuelekea amani na usalama ni yenye umaana. Hata hivyo, ulio na umaana mkubwa zaidi katika ulimwengu wote mzima utakuwa wakati ambapo katika historia viongozi wa ulimwengu watapaaza tangazo la amani na usalama kwa njia ya kutokeza wazi kuliko wakati mwinginewo uliotangulia. Wakati utakuja ambapo mpaazo wa tangazo lao utathibitika kuwa tofauti na zile jitihada nyingi za kuleta amani ambazo zilikuwa zimefanywa mpaka wakati huo. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika? Kwa sababu zamani za kale mtume Paulo alitabiri kwamba “wakati wo wote wanaposema: ‘Amani na usalama!’ ndipo uharibifu wa ghafula utakapokuwa juu yao papo kwa hapo . . . nao hawataokoka kwa vyo vyote.” (1 Wathesalonike 5:3, NW) Ndipo amani na usalama wa kweli utakapofuata chini ya ule utawala mzuri sana wa Kristo Yesu, “Mwana-Mfalme wa Amani.”—Isaya 9:6, 7, NW.
“Ugonjwa Ulio Halisi”
“UKIMWI si aksidenti inayotukia kwa nasibu isiyofaa wala si afa la kiasili lisiloweza kuepukwa. Kuenea sana kwao ni zao la upumbavu wetu wenyewe. . . . Sisi hatuna mtu wa kulaumu isipokuwa sisi wenyewe,” anasema daktari mmoja wa Denver anayehusika na matibabu ya uzazi, W. M. Merrick Thomas. Akieleza sababu ya maoni yake katika karatasi-habari Rocky Mountain News, yeye anasema hivi: “UKIMWI si ugonjwa wa ugoni-jinsia-moja. Ni ugonjwa unaotokana na uhusiano wa mkaribiano na wa kufanya ngono za ovyo-ovyo. . . . Magonjwa yanayotokana na ngono za ovyo-ovyo yataathiri moja kwa moja wote wanaofanya ngono za ovyo-ovyo.” Hivyo, kama vile Thomas anavyoonelea, “mwenendo wetu ndio ugonjwa ulio halisi.”
Jinsi yalivyo ya wakati unaofaa maneno ya mtume Paulo, ambaye, alipokuwa akieleza juu ya mwenendo usioweza kupata udhuru wa watu wanaodai kuwa wanajua Mungu, alisema: “Kwa ajili ya hayo Mungu aliwaacha katika tamaa za mioyo yao, waufuate uchafu, . . . tamaa zao za aibu, . . . wakiyatenda yasiyopasa, wakapata nafsini mwao malipo ya upotevu wao yaliyo haki yao”! (Warumi 1:24-27) Mara nyingi maisha safi kwa kupatana na viwango vya Biblia yanatumikia kama himaya dhidi ya masumbufu yanayokumba aina ya binadamu leo.—Zaburi 19:7-11.