Muono-Ndani Juu ya Habari
Wakatoliki na Ubatizo
Hesabu ya watu wazima wanaobatizwa na Kanisa la Katoliki ya Kiroma katika Ufaransa inaongezeka, yaripoti Le Monde, karatasi-habari moja ya Kifaransa. Kwa uhakika, karatasi-habari hiyo inadai kwamba “tarakimu zenyewe zimekuwa maradufu katika muda wa miaka minne iliyopita.” Mitaala ya masomo yafunzwayo kabla ya ubatizo inafuatwa na watu wazima Wafaransa zaidi ya 4,000 wanaotafuta kuwa Wakatoliki waliobatizwa. Theluthi mbili kati yao ni wanawake wa kati ya umri wa 20 na 40. Robo moja hawana asili ya Kifaransa.
Hata hivyo, matayarisho ya kubatizwa kwa mtu mzima yaweza kuendelea kwa miaka miwili au mitatu. Padri Guy Cordonnier, mwenye daraka la kusimamia masomo hayo yanayotangulia ubatizo katika eneo la Versailles, alitaarifu hivi: “Ili kubatizwa, haitoshi mtu kusema kwamba anaamini katika Mungu. Anahitajiwa kabisa ajifunze jinsi ya kuishi ndani ya jumuiya.”
Bila shaka, ubatizo wa watu wazima si jambo jipya hata kidogo. Yesu mwenyewe alibatizwa kwenye umri wa miaka 30. Wala si jambo jipya kwamba mengi kuliko kuamini katika Mungu tu yanatakwa kwa mtu ili abatizwe. Amri ambayo Yesu aliwapa wafuasi wake ilikuwa ‘kufanya wanafunzi, kuwabatiza’ na “kuwafundisha” kushika amri zake. — Mathayo 28:19, 20.
Hata hivyo, kwa kuwa Kanisa Katoliki limezoea kubatiza vitoto vichanga kwa karne nyingi, msimamo wa kanisa kuelekea kubatiza watu wazima ni jambo lisilo na upatano. Wanamamlaka wa Kanisa wasema huchukua miaka miwili au zaidi kumtayarisha mtu mzima kwa ajili ya ubatizo, hata hivyo wao washikilia kwamba ubatizo wa vitoto vichanga wafaa. Wao wadai kwamba ubatizo hutakasa vitoto vichanga visiwe na dhambi ya kurithi, lakini mtume Yohana aliandika hivi: “Damu yake Yesu . . . yatusafisha dhambi yote.” (1 Yohana 1:7) Kwa kuwa watoto wachanga hawawezi kujizoeza imani katika Mungu na katika damu iliyomwagwa ya Kristo, mbona wabatizwe?
Maneno Yasiyopata Kusikiwa Kamwe
Karibu nusu ya wake 3,800 waliochunguzwa maoni na shirika la bima la Kijapani “hawajasikia waume wao wakiwaambia yale maneno ya kwamba ‘Mimi nakupenda’ katika muda wa miaka kadhaa,” yaripoti The Daily Yomiuri. Asilimia ya wake wasioyasikia maneno haya huongezeka kwa kadiri umri wao uendeleavyo, na kati ya wale walio katika miaka yao ya 50, ilistaajabisha kwamba ni asilimia 82 wasiopata kamwe kuyasikia maneno haya kutoka kwa waume zao. Hata miongoni mwa wake walio katika miaka yao ya 20, ni asilimia 10 tu ambao husikia waume zao wakiyatamka maneno haya kila siku.
Katika hadithi ya Mfalme Sulemani inayohusu mapenzi kati ya mvulana mchungaji na msichana mzuri wa mashambani aliyekuwa wa kutoka jiji la kale la Shunemu, ilikuwa ni kupitia “semi za upenzi mwingi” kwamba mvulana huyo akaweza kuuvuta moyo wa msichana yule. (Wimbo Ulio Bora 1:2) Waume wakiisha kuivuta mioyo ya wake zao, je! bado yahitajiwa kabisa kuwaonyesha shauku yao? Ndiyo! Biblia yahimiza hivi: “Waume endeleeni kuwa mnapenda wake zenu, sawa na vile Kristo pia alivyolipenda kundi akajitoa mwenyewe kwa ajili yalo.” —Waefeso 5:25, NW.
Katika usiku wa kusalitiwa kwake, Yesu Kristo alirudia-rudia kuwaonyesha upendo wanafunzi wake. (Yohana 13:34; 14:19-21; 15:9, 10, 12) Ni lazima mume afikirie kwamba mke wake anamhitaji yeye amhakikishie kwamba ampenda. Pia ni lazima waume wakumbuke kwamba Kristo ‘alijitoa mwenyewe kwa ajili ya kundi.’ Hivyo, yeye alionyesha upendo kwa maneno na vitendo pia. Ni wazi kwamba ingefaa waume waige kielelezo cha Kristo.