Kuwezana na Hali za Udhaifu Wangu
Kama ilivyosimuliwa na Thomas Addison
NILIPOKUWA mvulana, hata ndege ambaye si mwenye madhara angefanya nitimue mbio kwa hekaheka ya woga wa bure tu. Watu wa ukoo au marafiki walipokuja kuzuru, wangeniona kuwa mtoto asiyewasiliana na watu mwenye kujificha nyuma ya rinda la mama yake. Kwa kawaida nilipoona wageni nilikimbia upesi iwezekanavyo kwenye chumba cha kulala. Nilifyata ulimi kabisa nilipokuwa mbele ya mtu yeyote mwenye mamlaka, hasa walimu wa shule.
Ni nini kilichoniwezesha kubadilika? Kijana mwenye haya nyingi kadiri hiyo aliwezaje kuhutubia maelfu ya wasikilizaji kwenye mikusanyiko mikubwa katika miaka ya majuzi?
Kazi ya Wazazi ya ‘Kukunjua Kijiti Kingali Kibichi’
Wazazi wangu—hasa Baba, akiwa Mskochi mwenye umbo la kimbaombao na mwenye nishati—aliniona mimi kuwa mtoto mgumu kueleweka. Yeye alipata kuwa yatima akiwa na miaka 13, naye alikuwa mtu sugu kwa kuvumilia taabu. Alijifunza kujitafutia riziki kuanzia umri wa mapema. Kwa upande mwingine, Mama alikuwa binti ya mkulima na alikuwa kielelezo halisi cha upole. Mazoezi niliyopata tangu utoto mchanga yalikuwa yenye fadhili na imara, hata hivyo hayakuwa ya kunilinda kupita kiasi.
Nikiwa na miaka sita, katika 1945, niliingia kwa mara ya kwanza katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Nilitoa hotuba yangu ya kwanza kwa nuru ya taa ya mafuta katika kundi dogo la Kiaustralia lenye jamaa tatu tu. Baba alinisaidia kutayarisha mapema vya kutosha, akieleza faida za uneni wa bila kutazamia hali mapema. Pia alikazia kutoogopa vile watu wengine watasema au kufikiri. Kama alivyoweka wazo lenyewe: “Sisi sote wanadamu ni marundo ya mavumbi. Marundo fulani ni makubwa kidogo kuliko mengine, na basi.” Magoti yangu yakagongana, viganja vyangu vikaanza kutoa jasho, na kufikia nusu ya hotuba, nilifyata ulimi nisiweze kumaliza.
Ni lazima iwe nilikuwa na karibu miaka kumi wakati Baba aliponipeleka mimi na Robert ndugu yangu mchanga zaidi katika barabara kuu ya mji, pale pale nje ya sinema ya mji huo. Tukiwa hapo tukainua magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa kuonwa kabisa na wanafunzi wenzi wa shule yetu. Nilihisi magazeti hayo yakiwa mazito kama madini-risasi, na nyakati fulani yangeniangukia mgongoni! Kwa kuzidiwa na mambo ningejaribu kujikunyata kwa kurudi niwe mahali pasipoonekana waziwazi.
Hata hivyo, nilipokuwa nikitazama kielelezo kijasiri cha Baba, nilitiwa moyo ajabu. Sikuzote yeye alisema kwamba kujikunyata kwa kurudi nyuma kulikuwa kujiachilia kushindwa na Shetani na hofu kwa wanadamu. Mtihani mwingine ulikuja shuleni. Muda mrefu ulikuwa haujapita tangu kumalizika kwa Vita ya Ulimwengu 2, na utukuzo wa taifa katika Australia ulikuwa ungali imara. Ellerie dada yangu na mimi tungebaki tumeketi wakati wa kusanyiko la shule ambapo wimbo wa taifa ulipigwa. Mimi niliuona kuwa mtihani halisi kuonekana wazi nikiwa tofauti, lakini hapo tena kutegemezwa na kutiwa moyo daima na wazazi wangu kulinisaidia nisiridhiane msimamo.
Kielelezo Kizuri cha Baba
Kwa kufikiria malezi na nia ya Baba huko nyuma, kwa kweli alikuwa mwenye saburi sana kwangu. Alianza kufanya kazi katika migodi ya makaa-mawe katika Uingereza akiwa kivulana wa miaka 13 tu. Katika miaka yake ya 20, alihamia Australia atafute maisha mazuri zaidi. Lakini mshuko wa thamani ya fedha wa miaka ya 1930 ukawa umeingia, naye akakubali kazi chini ya hali zenye kuvunja moyo sana ili kuandalia jamaa yake.
Baba alizinduliwa macho na hali kwa ujumla na hasa siasa, kwa hiyo aliposoma vitabu vya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi na ufichuzi wavyo usio na hofu juu ya unafiki wa kisiasa, kibiashara, na kidini, vilimgusa mshipa wa itikio. Punde si punde akajiweka wakfu kutumikia Yehova, muda mfupi baada ya Mama kuwa amefanya hivyo. Ajapoteswa na pafu moja lililoacha kufanya kazi alipobomokewa na mgodi wa madini na akiwa hana ufundi hususa wa kazi, Baba alipeleka jamaa yetu kutumikia mahali-mahali kulikokuwa na uhitaji wa kiroho. Tegemeo lake juu ya Yehova liliniacha nikiwa nimevutiwa kwa kina kirefu.
Mathalani, nakumbuka kuhamia mji mdogo wa migodi ya makaa-mawe ambako Mashahidi wa pekee huko walikuwa dada wawili wazee-wazee, wote wakiwa na waume wasioamini. Ilikuwa vigumu kupata nyumba, lakini mwishowe tuliweza kukodi nyumba ya zamani kilometa nyingi nje ya mji. Njia yetu moja tu ya kusafiri ilikuwa kwa miguu au kwa baiskeli. Halafu, asubuhi moja mapema, wakati sisi watoto watatu tulipokuwa tumeenda kukaa pamoja na marafiki, nyumba iliteketea ikatandazika kabisa. Wazazi wetu waliponyosha maisha zao, lakini hakuna kilichookolewa. Hatukuwa na bima wala pesa.
Baba alikuwa akisimulia hayo punde tu kabla ya kifo chake katika 1982. Alisema: “Mwanangu, je! wakumbuka jinsi hali ilivyoonekana bila tumaini hapo kwanza, lakini Yehova akatutegemeza? Naam, baada ya moto ule, akina ndugu katika Perth walipeleka fanicha, mavazi, na pesa. Kwa sababu ya ukarimu wao, tukawa na hali nzuri kuliko ilivyokuwa kabla ya moto ule!” Kwanza nilifikiri Baba alijitanguliza kidogo aliponena juu ya msaada mwingi sana wa Yehova katika maisha zetu. Hata hivyo, visa vyenye kutukia mara nyingi vya kile alichokiita msaada wa kimungu viliongezeka mno vikawa havielezeki vingeweza kutukiaje kwa njia nyingine yoyote.
Ufikiri Chanya (wa Kutazamia Mema) wa Mama
Sikuzote moja la matatizo yangu makubwa limekuwa kufikiri kwa mwelekeo hasi (kutazamia mabaya tu). Mama aliuliza hivi mara nyingi: “Kwa nini sikuzote wewe huona tu upande ule wenye giza maishani?” Kielelezo chake mwenyewe cha kutazama upande ulio mwangavu kilikuwa kichocheo kwangu ili kufuliza kufanya jitihada ya kufikiri kwa mwelekeo chanya zaidi.
Hivi majuzi, Mama alinena juu ya kituko kimoja katika mji mdogo wa ukulima mara tu tulipohamia huko. Tamko moja lililofanywa na daktari wa huko lilimfurahisha. Daktari huyo alikuwa amechukua kwamba wazazi wetu ni wenye mali, kwa kuona mavazi yao maridadi na sura ya kujipamba vizuri. Ukweli ulikuwa kwamba nyumba yetu ilikuwa ghala kubwa, ikiwa na vyumba vilivyogawanywa-gawanywa kwa kujengwa na magunia mazito. Hakukuwa na nguvu za umeme, gesi, wala maji ya mifereji. Siku moja ng’ombe dume alijaribu kuvu-nja kupitia mlango wa mbele. Wewe kisia nilikuwa wapi: chini ya kitanda!
Mama alibeba maji yetu kutoka kisima kilichokuwa umbali wa meta 200, akitumia mapipa ya lita 15 yaliyofungwa kwenye nira yenye kupita pande zote za mabega yake. Yeye alikuwa na kipawa cha kutafuta vichekesho hata katika mambo yenye kutatiza na, kwa kuchochewa kidogo na Baba, aliona hali yoyote ngumu kuwa wito wa ushindani uliopasa kushindwa badala ya kuuona kuwa kipingamizi. Angeonyesha wazi kwamba hata ingawa hatukuwa na wingi wa vitu vya kimwili, tuliona shangwe ya mibaraka mingi iliyo chanya.
Kwa kielelezo, tulitumia siku nyingi zenye furaha tukisafiri maeneo ya mbali kuhubiri, tukipiga kambi chini ya nyota, tukipika nyamachumvi ya nguruwe na mayai juu ya moto wa peupe, na kuimba nyimbo za Ufalme wakati wa kusafiri. Baba angeandaa muziki kwa akodioni yake. Ndiyo, kwa njia hizi tulikuwa matajiri kweli kweli. Katika miji fulani ya mashambani, tulikodi majumba madogo na kutangaza hotuba za watu wote, ambazo tulizitoa alasiri za Jumapili.
Nyakati fulani, kwa sababu ya kutokea-tokea kwa matatizo katika afya ya Baba, Mama alihitaji kufanya kazi ya kimwili ili kuongezea mapato ya Baba. Kwa miaka kadhaa Mama aliuguza mama yake mwenyewe na babu na mwishowe baba yetu kabla hawajafa. Alifanya hivyo bila kulalamika. Ingawa mara kwa mara nilikuwa bado na vipindi vya mshuko wa moyo na mara nyingi nilikuwa na mwelekeo hasi, kielelezo na vichocheo vyanana vya Mama vilinipa tamaa ya kufuliza kujaribu.
Kuwezana na Mshuko wa Moyo
Katika miaka ya mwishoni mwa utineja wangu, hali zangu zote za udhaifu wa utotoni nilizofikiri zilikuwa zimetulia zilirudi kwa fujo nyingi. Maswali juu ya maisha yalinifadhaisha. Nikaanza kushangaa hivi, ‘Je! watu wote mmoja mmoja wana fursa sawa ya kumjua na kumtumikia Yehova?’ Kwa kielelezo, namna gani mtoto aliyezaliwa India au China? Hakika fursa yake ya kupata kumjua Yehova ingekuwa kidogo zaidi ya ile ya mtoto aliyependelewa kulelewa na wazazi Mashahidi. Ilionekana kuwa si haki hiyo! Pia, hali za urithi na mazingira, ambayo mtoto hawezi kuzidhibiti, huwa ni lazima zihusike kwa kadiri kubwa. Maisha yalionekana yakikosa haki kwa njia nyingi sana. Mimi nilizozana na wazazi wangu muda wa saa nyingi kuhusu maswali hayo. Pia nilikuwa mwenye wasiwasi juu ya sura yangu. Kuna mambo mengi niliyokuwa sipendi juu yangu mwenyewe.
Nilipokuwa nikifikiria mambo haya, yalinishusha moyo, nyakati fulani kwa mfululizo wa majuma. Sura yangu ya kibinafsi iliharibika. Mara kadhaa nikafikiria kwa siri kujiua. Kuna nyakati ambazo nilijitosheleza hisia kwa kujiachilia tena nikaekae nikijisikitikia. Nilijiona kuwa mfia-imani asiyeeleweka vizuri. Nikawa mtu wa kujikalia peke yangu na wakati mmoja, bila onyo, nikapatwa ghafula na hisia ya kuogopesha. Kila kitu chenye kunizunguka kilionekana kutokuwa halisi, kana kwamba nilikuwa nikitazama nje kupitia dirisha lenye ukungu.
Kituko hiki kilinishtua nikang’amua kwamba kujisikitikia kwaweza kuwa hatari. Katika sala kwa Yehova, niliazimia kufanya jitihada ya kupiga moyo konde nisijiache nishindwe tena na hali ya kujisikitikia. Nilianza kukaza fikira juu ya mawazo chanya ya Kimaandiko. Kuanzia hapo na kuendelea, kwa uangalifu unaozidi ulio wa kawaida nilisoma kila makala katika magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ambayo yalikazia tabia za utu halafu nikayaweka vizuri katika jalada. Pia niliandika kwa uangalifu mawazo yaliyotolewa katika Huduma ya Ufalme juu ya jinsi ya kuongea na wengine.
Mradi wangu wa kwanza ulikuwa kujaribu kuongea kwa muda mrefu iwezekanavyo na mtu mmoja kwenye kila mkutano wa Kikristo. Mwanzoni, kila moja la maongeo hayo liliendelea kwa karibu dakika moja tu. Tokeo ni kwamba, mara nyingi nilikuja nyumbani nikihisi nimepondeka moyo. Hata hivyo, pole kwa pole uwezo wangu wa kuongea ukapata nafuu kwa kudumisha jitihada.
Pia nilianza kufanya utafiti mwingi wa kibinafsi juu ya maswali ya kufadhaisha niliyokuwa nayo. Kwa kuongezea, nilijali ulaji wangu wa kimwili nikapata kwamba kwa kula vitu vyenye kuimarisha mwili zaidi, nia na ziha ya mwili wangu vilipata nafuu. Baadaye nilipata kujua kwamba visababishi vingine vingeweza kufyatua mshuko wa moyo. Kwa kielelezo, nyakati fulani nilijihusisha sana na upendezi fulani hususa hata nikawa nikisisimuka hisia kupita kiasi. Nyakati zote hiyo iliongoza kwenye mshuko wa hisia, ikitokeza potezo la nishati halafu mshuko wa moyo. Jibu lilikuwa kujifunza kuendeleza upendezi katika jambo lakini bila kusisimuka sana. Hata leo hii, huwa ni lazima nijichunge.
Hatua iliyofuata ilikuwa ni kushika sana miradi ambayo wazazi wangu walikuwa sikuzote wametuwekea mbele sisi watoto, yaani, huduma ya wakati wote. Kupiga moyo konde kwa dada yangu kushikilia pendeleo hili la kupainia kwa miaka zaidi ya 35 kungali ni kichocheo chanya kwangu.
Kuwezana na Tatizo la Mwana Wangu
Baada ya miaka fulani nikiwa painia mseja, nilifunga ndoa na painia mwenzi, Josefa. Amekuwa kikamilishio kizuri kwangu katika kila njia. Baada ya muda, tulizaa watoto watatu. Craig, mtoto wetu wa umri mkubwa zaidi, alizaliwa katika 1972 akiwa na upoozi mkali wa ubongoni. Hali yake imekuwa wito halisi wa ushindani, kwa kuwa hawezi kujifanyia lolote isipokuwa kushika kijiko cha chakula kwa uzembezembe. Bila shaka, sisi twampenda sana, kwa hiyo nilifuatia njia zote za kumsaidia awe mwenye kujitegemea zaidi. Nilimfanyia misaada mbalimbali ya kutembelea. Tulienda kuwaomba ushauri wastadi wengi tusifanikiwe sana. Hiyo imenielewesha kwamba hali fulani katika maisha haya ni lazima zikubaliwe.
Wakati wa miaka 12 ya kwanza ya maisha yake, kwa ghafula Craig angeacha kula na kunywa. Hiyo iliandamana na kichefuchefu cha kutojitakia. Kisababishi kilifikiriwa kuwa ni uharibifu wenye kuhusu mishipa ya fahamu. Yeye angeanza mnyong’onyeo wa kufa akiwa mbele ya macho yetu hasa. Sala ilitusaidia kuwezana na hali hiyo, na utibabu alioagiziwa umesaidia kudhibiti tatizo hilo. Kwa kufurahisha, Craig alionekana kuacha unyong’onyevu wake kabla tu hajamalizika, na kwa mara nyingine angetufurahisha kwa tabasamu yake yenye kunasa fikira na burudisho la nyimbo zisizo na mwisho.
Hapo kwanza Josefa aliona ikiwa vigumu sana kujipatanisha na hali hii. Lakini upendo na saburi yake katika kutunza kila uhitaji wa Craig ulifaulu hatimaye. Hii imemaanisha kwamba tumeweza kuendelea kuhamia mahali kokote ambako msaada wa Kikristo ni mkubwa zaidi. Kwa tegemezo na msaada wenye mafaa wa Josefa, mimi niliweza kufanya kazi ya nusu-wakati kwa miaka kadhaa, hiyo ikiniruhusu kufanya upainia msaidizi na pia kutegemeza jamaa yetu.
Uhitaji wa Kufikiri kwa Mwelekeo Chanya
Craig awapo ameshuka moyo kwa sababu ya ugonjwa wenye kurudi-rudi au kwa kuvurugwa na mapungukio yake, sisi humwimarisha kwa moja la maandiko yangu niyapendayo zaidi: “Sisi hatumo miongoni mwa wale wanaorudi nyuma.” (Waebrania 10:39) Yeye analijua kwa moyo, na sikuzote hilo huwa na tokeo la kumtia moyo.
Tangu Craig alipokuwa mchanga sana, amekuwa na upendo hususa kwa utumishi wa shambani. Kwa kutumia kiti-magurudumu maalumu, mara nyingi yeye huweza kujiunga nasi. Hususa yeye huona shangwe kuja pamoja nasi wakati ambapo, mara kwa mara, mimi hutumikia makundi mengine katika kazi ya mzunguko iliyo badala. Maelezo yake yenye upungufu kwenye funzo la kikundi na kuongea kwake daima juu ya hadithi za Biblia kwenye shule ya pekee aliyohudhuria, kulikuwa na matokeo makubwa tusiyokuwa nayo sisi ambao hatuna vizuizi. Hivyo Craig alinikumbusha kwamba hata tuwe tuna mapungukio gani, Yehova aweza kututumia kusogeza mbele mapenzi na kusudi lake.
Muda fulani uliopita nilipata pendeleo la kuwa mfunzi kwenye Shule ya Huduma ya Ufalme. Baada ya miaka yangu yote katika huduma, nilikuwa ningali mwenye wasiwasi hapo kwanza. Lakini muda si muda, kwa kutegemea Yehova, fahamu zangu zilitulia, na kwa mara nyingine tena nikahisi nguvu za Yehova zenye kutegemeza.
Ninapotazama nyuma kwenye miaka karibu 50 ya maisha yangu sasa, nasadiki kwamba ni Yehova peke yake ambaye angeweza kuzoeza mtu aliye kama mimi, akimfanya awe mwanamume wa kiroho.