Ulimwengu Mpya U Karibu!
MADOKEZO ni tele kuhusu jinsi ya kutatua matatizo ya ulimwengu. Kwa ujumla, yahitaji hangaiko na ushirikiano, na pia jitihada kubwa sana ifanywe na mataifa yote ulimwenguni pote kwa kuratibiwa vizuri. Kuna hisia ya kwamba hali zizidipo kuwa mbaya, uhitaji wa kuhifadhiana wao kwa wao utalazimisha mataifa kukadiria upya mambo yaliyo muhimu zaidi kwayo na yafanye kazi pamoja kufanyiza ulimwengu mpya wenye kuendelezeka. Kuna mwono wa kimbele kwamba mipango ya matumizi ya kijeshi itapunguzwa sana kwa kupendelea kutumia mali ili kushughulikia matisho ya kimazingira na kwamba, kama ilivyosemwa katika State of the World 1990, “badala ya kutegemea majeshi yao wenyewe ya ulinzi yaliyo makubwa, huenda serikali zikaja kutegemea jeshi la kutunza amani lililopanuliwa na kuimarishwa sana la U.M., moja ambalo lingekuwa na uwezo na mamlaka ya kulinda nchi yoyote iliyo mshirika dhidi ya mchokozi.”
Lakini mipango ya jinsi hiyo hupungukiwa sana kuleta hali zitamaniwazo sana zilizoorodheshwa katika kurasa zetu za ufunguzi. Mbinu za kibinadamu tu haziwezi kwa vyovyote kuponya udhambi na pupa ya kibinadamu; haziondoi kabisa maoni ya ubaguzi na magomvi yahusuyo watu wa rangi mbalimbali. Hazileti upendo usio na ubinafsi miongoni mwa ainabinadamu yote; wala haziwezi kuhakikishia mwisho wa magonjwa na kifo. Uhalifu haushughulikiwi kwa matokeo mazuri, wala hakuna mtajo juu ya kushinda tofauti na chuki za kidini. Na kukomeshwa kwa misiba ya kiasili hakuwezi hata kufikiriwa. Utukuzo wa taifa, pamoja na uwezekano wao wa kusababisha matatizo, waruhusiwa ubakie. Basi, kwa njia isiyofurahisha, ni lazima tukate shauri kwamba wanadamu wameshindwa kutokeza utatuzi uwezao kufanya kazi.
Hata hivyo, kuna utatuzi! Kweli kweli, mambo yote haya yenye kutamaniwa sana na ainabinadamu yameahidiwa, na ahadi hiyo yatoka kwa Mungu “asiyeweza kusema uongo.” (Tito 1:2) Yeye ajua hasa ni mambo gani lazima yafanywe, naye ana hekima, nguvu, na uwezo wa kutimiza aliyokusudia.—Ufunuo 7:12; 19:1.
Mungu aahidi hivi: “Maana bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo, utapaangalia mahali pake wala hatakuwapo. Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zaburi 37:10, 11.
Hilo litatimizwaje? Isaya 11:9 hujibu hivi: “Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua BWANA [maarifa juu ya Yehova, NW], kama vile maji yanavyoifunika bahari.” Ndiyo, ainabinadamu yote itaagizwa katika ‘maarifa juu ya Yehova,’ na watu wowote mmoja mmoja watakaokataa kujipatanisha nayo hawataruhusiwa kubaki na kuchafua amani ya wengine. Dunia yetu yenye upendezi haitaangamizwa tena.
“Avikomesha vita hata mwisho wa dunia,” yaahidi Zaburi 46:8, 9. (Ona pia Mika 4:3, 4.) Jambo la maana katika kufanyiza amani ya tufe lote ni kumaliza tofauti za utukuzo wa taifa. Ushirikiano wahakikishwa kikamili, kwa maana ni serikali moja tu itakayokuwako ulimwenguni pote—ile ya Mungu. Na serikali yake ni Ufalme “ambao hautaangamizwa milele.” (Danieli 2:44) Zaidi ya hilo, Mfalme wayo ni Yesu Kristo mfufuliwa asiyeweza kufa, ambaye utawala wake utakuwa kwa njia ya haki na uadilifu.—Isaya 9:6, 7; 32:1, NW.
Lakini je! hiyo ingeharibiwa na kutokamilika ambako ni asili ya urithi wa binadamu na ivurugwe na maumivu, magonjwa, majonzi, na mauti yenye kuendelea? Sivyo, kwa maana haya pia yatakuwa mambo ya zamani. Ufunuo 21:4 watuhakikishia hivi: “Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.” Dhambi iliyorithiwa itasamehewa kwa msingi wa dhabihu ya ukombozi ya Yesu, na ainabinadamu itarudishwa kwenye hali kamilifu. (Warumi 6:23; Waefeso 1:7) Na ni nani awezaye kudhibiti kani za kiasili na kuzizuia zisidhuru ainabinadamu kwa njia bora kuliko Muumba wazo?—Zaburi 148:5-8; Isaya 30:30.
Mambo ambayo binadamu aweza kuyatumainia na kuyawazia kwa ndoto tu, Mungu atayaleta. Lakini lini? Unabii wa Biblia waonyesha kwamba mabadiliko hayo yatakuja wakati ambapo mataifa wangekuwa ‘wakiwaka hasira’ na ambapo binadamu angekuwa ‘akiangamiza dunia.’ (Ufunuo 11:18, HNWW) Siku za mwisho za ulimwengu wa zamani zingetiwa alama na “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo”—zikitokeza hali zinazozidi kuwa mbaya ambazo twaziona kutuzunguka sisi sasa hivi. (2 Timotheo 3:1-5, 13, NW) Na Yesu alitabiri kwamba kizazi chenye kuona mambo hayo kingekuwa ndicho kizazi ambacho kingeona utimizo wa ahadi za Mungu.—Mathayo 24:3-14, 32-34.
Chukua wakati wa kuchungua ahadi hizo zilizorekodiwa katika Biblia. Kwa maana kufikia hapo sasa, wanadamu wenye maarifa na pia Mungu waafiki hivi: Sasa ndio wakati wa ulimwengu mpya!