‘Endeleeni Kurekebishwa Upya’
“JE! UNA uhakika hatutaikosa?” Yule abiria wa kike akaelekeza swali lake kwa ofisa wa kwanza wa meli. Wakati ile meli ndogo sana ilipoyumba-yumba na kushikwa sana na mawimbi makali ya Atlantiki Kusini, ilionekana kwa mwanamke huyo kwamba ni kama kwa mwujiza tu kwamba wangefika mahali padogo sana katika ramani ambapo walikuwa wakienda.
Hivyo basi ofisa wa kwanza alimkaribisha kwenye jukwaa la meli akamweleza utendaji wa vifaa vya ubaharia—dira mviringo, reda, vipokea ishara vya satilaiti, na hata kipima-umbali cha kawaida. Ingawa maelezo yale ya ustadi yaliuzidi kidogo ufahamivu wake, alikuja kuelewa kanuni moja ya msingi ya ubaharia: kurekebisha mwendo. Kwa kusaidiwa na vifaa vyake vya ubaharia, kapteni angeweza kusawazisha uvutano wa mipeperusho ya mikondo ya bahari na upepo kwa kufanya marekebisho ya daima. Bila marekebisho hayo, wangekengeuka wapakose mahali waendako kwa kilometa nyingi sana.
Wakristo ni kama meli katika bahari kuu ya jamii ya kibinadamu. Mradi wetu ni ‘kupatikana na Yehova mwishowe tukiwa hatuna doa na kasoro na katika amani.’ (2 Petro 3:14, NW) Lakini kama vile kwa habari ya meli, kuna kani—za ndani na za nje—ambazo zaelekea kutuondosha kwenye mwendo wetu. Basi, yafaa kama nini maneno ya mtume Paulo kwa Wakorintho: “Kwa ajili ya hili sisi tunasali, kurekebishwa kwenu upya. . . . Endeleeni . . . kurekebishwa upya.”—2 Wakorintho 13:9, 11, NW.
Yahusikayo Katika Kurekebishwa Upya
Neno la Kigiriki lililotafsiriwa hapa “kurekebishwa upya” larejezea kuleta kitu “katika mpangilio wa laini ifaayo.” (Ona kielezi-chini cha Reference Bible.) Katika maandiko fulani ya Biblia, hilo hutumiwa kueleza kurudisha kitu kwenye hali ifaayo. Mathalani, kwenye Mathayo 4:21, neno kama hilo latumiwa kueleza “kutengeneza” nyavu. (Kingdom Interlinear) Basi, yamaanisha nini kwa Wakristo kurekebishwa upya?
Basi, fikiria Wakristo kule Korintho ambao Paulo alikuwa akiandikia. Katika barua moja aliyotangulia kuwaandikia, Paulo alikuwa ameonyesha hali kadhaa zisizofaa zilizokuwa katika kundi: ufarakano, kuachilia ukosefu wa adili katika ngono, kushtakiana mahakamani miongoni mwa akina ndugu, kutostahi Mlo wa Jioni wa Bwana, na hata mikutano isiyo na utaratibu. (1 Wakorintho 1:10-13; 5:1; 6:1; 11:20, 21; 14:26-33) Hivyo Wakorintho walihitaji ‘kutengeneza’ hali huko, yaani, kuyaleta “katika mpangilio wa laini ifaayo” wakiwa na kanuni za kimungu.
Barua ya pili ambayo Paulo alielekeza kwao yaonyesha walifanya hivyo hasa. (2 Wakorintho 7:11) Hata hivyo, Paulo alijua kwamba misongo kutoka kwenye ulimwengu, kutoka kwa Shetani, na kutoka mibetuko yao wenyewe ya kimnofu ingeendelea kuwasukuma mara kwa mara waende kando ya mwendo wao mara kwa mara. Kwa sababu hiyo, kwa kufaa aliwashauri ‘waendelee kurekebishwa upya.’
Uhitaji wa Kurekebishwa Upya Leo
Ni lazima Mashahidi wa Yehova vilevile waendelee kurekebishwa upya leo. Shetani Ibilisi ‘anafanya vita’ na sisi, akifanya kazi kwa juhudi nyingi ili avunje uaminifu wetu wa maadili. (Ufunuo 12:17; Waefeso 6:12) Pia tumezungukwa na mfumo wa mambo wa ulimwenguni pote ambao huendesha kazi “kwa kumfuata mfalme wa uwezo wa anga.” Wanakazi na wanashule wenzetu huenda wakawa ni watu ‘waenendao katika tamaa za mwili wao, wakiyatimiza mapenzi ya mwili na ya nia.’ (Waefeso 2:2, 3) Pia tuna pigano la daima pamoja na maeleko yetu yenye dhambi tuliyorithi. (Warumi 7:18-25) Bila kurekebishwa upya daima, tungeweza kwa urahisi kusukumwa kando ya mwendo.
Tukio moja lililopata mtume Petro latoa vema kielezi cha jambo hili. Baada ya kumtambua Yesu kwa usahihi kuwa “Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai,” Petro alipongezwa kwa maneno haya: “Heri wewe Simoni Bar-yona; kwa kuwa mwili na damu havikukufunulia hili, bali Baba yangu aliye mbinguni.” (Mathayo 16:16, 17) Kwa wazi, kufikiri kwa Petro kulinyooka vizuri. Hata hivyo, katika pengo la muda wa mistari sita iliyofuata, alilazimika kukemewa vikali na Yesu! Alipojua kwamba Kristo ‘angepata mateso mengi na kuuawa,’ Petro alimhimiza Yesu hivi: “Hasha, Bwana, hayo hayatakupata.” Yesu alijibu kwa haraka hivi: “Nenda nyuma yangu, Shetani; u kikwazo kwangu; maana huyawazi yaliyo ya Mungu, bali ya wanadamu.”—Mathayo 16:21-23.
Petro alikuwa akifikiri kwa maoni ya kimnofu. Mawazo na mtazamo wake vilihitaji kurekebishwa upya. Je! hivyo sivyo huwa mara kwa mara juu yetu sote? Je! hatuwi na mbetuko wa kuona mambo kwa maoni yetu wenyewe badala ya maoni ya Mungu? Hivyo basi, pindi kwa pindi twahitaji kurekebishwa upya. Kama meli baharini, huenda nyakati fulani marekebisho hayo yakawa madogo, karibu kuwa duni. Lakini yaweza kumaanisha tofauti kati ya kufika kwetu mahali tuendako na kuvunjikiwa na meli kiroho. Kwa kweli, rekebisho dogo sasa huenda likazuia kulazimika kufanya marekebisho makubwa—labda yenye maumivu—baadaye.
Viwango vya Kimungu
Vifaa vya meli vya kupima viwango vya ubaharia visiporekebishwa kwa usahihi, masahihisho yafaayo hayawezi kufanywa. Vivyo hivyo, ili tuweke maisha zetu mwendoni, twahitaji mwongozo sahihi wa Neno la Mungu, Biblia. “Kila andiko limepewa kwa maongozi ya Mungu [limevuviwa, NW], na linafaa kwa mafundisho, na kwa kuonya watu juu ya makosa yao, na kwa kuwaongoza.” (2 Timotheo 3:16, ZSB) Neno hilo lililovuviwa huweka wazi viwango vya mwenendo na kufikiri. Kulisoma kwa ukawaida kwahitajiwa sana ili kufuata “njia za haki [uadilifu, NW].”—Zaburi 23:3.
Mwelekezo zaidi hutoka kwa jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ya Wakristo wapakwa-mafuta. Hawa wamesaidiwa na roho ya Yehova kuelewa makusudi yake kwa uendelevu. (Mathayo 24:45-47; Mithali 4:18) Hivyo, mwelekezo ujapo kutoka tengenezo la Yehova, kwa hekima twaweza kuunyenyekea, tukijua vema kabisa kwamba Yehova atatuongoza kwa njia ambayo tu itakuwa kwa manufaa yetu ya milele.—Isaya 48:17.
Ingawa hivyo, nyakati fulani twahitaji msaada wa kibinafsi ili tubaki mwendoni. Paulo alihimiza hivi kwenye Wagalatia 6:1, NW: “Akina ndugu, hata ingawa binadamu achukua hatua fulani isiyo sahihi kabla ya yeye kutanabahi juu yayo, ninyi ambao mna sifa za kufaa kiroho jaribuni kurekebisha upya mtu huyo katika roho ya upole.” Wazee na watumishi wa huduma ni miongoni mwa wale walio na sifa za kustahili kiroho. Mara nyingi wao wataonyesha moja kwa moja eneo fulani ambamo sisi twahitaji kufanya marekebisho.
Jitihada Yatakwa
Si rahisi sikuzote kufanya mabadiliko yahitajiwayo kabisa katika maisha zetu. Tena, mfikirie Petro. Kwa kuzaliwa akiwa Myahudi, Petro alikua akiyashiriki maoni hasi yenye kuwapo sana juu ya watu wa jamii nyinginezo. Kama vile alivyomwambia Kornelio Asiye Myahudi: “Ninyi mnajua ya kuwa si halali mtu aliye Myahudi ashikamane na mtu aliye wa taifa lingine wala kumwendea.” Hata hivyo, baada ya kung’amua kwamba yalikuwa mapenzi ya Mungu kwamba aushiriki ukweli wa Kikristo pamoja na mwanamume huyu na familia yake, Petro alikata shauri hivi: “Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki [uadilifu, NW] hukubaliwa na yeye.”—Matendo 10:28, 34, 35.
Petro alikuwa amefanya badiliko la kugutusha katika kufikiri na mtazamo wake kuelekea jamii nyingine za watu! Lakini yaonekana kulikuwa na uhitaji wa yeye kuendelea kurekebishwa upya katika jambo hili, kwa maana miaka michache baadaye, Petro alijiacha ashindwe na msongo wa marika na kuanza kupuuza waamini Wasio Wayahudi. Mtume Paulo alilazimika kumkaripia, akitumia maneno thabiti sana ili kumsaidia arekebishe upya kufikiri kwake hata zaidi!—Wagalatia 2:11-14.
Vivyo hivyo leo, huenda ikawa Mkristo alikulia kwenye mazingira yenye ubaguzi wa rangi. Baada ya kuja katika ukweli, huenda kiakili akakiri kwamba Mungu hana upendeleo lakini bado ashikamane na hisia za kupendelea rangi. Ingawa si mwenye uhasama kuelekea wale wa jamii nyingine, huenda akachukua moja kwa moja tu kwamba wao wana sifa zisizotamanika kwa sababu ya urithi wao wa rangi. Huenda akatatiza subira yao kwa mizaha kuhusu rangi au maneno yavutayo uangalifu daima kwenye tofauti za jamii au rangi. Huenda hata akakataa onyo la upole la kiroho kutoka kwa Mkristo mwenzake ambaye, kwa sababu ya uhaba wa hadhi ya kielimu au ya kijamii, ashindwa kujieleza kwa njia fulani. Kwa wazi, jitihada halisi huhitajiwa ili mtu wa jinsi hiyo arekebishe upya kufikiri kwake kupatana na ya Yehova!a
Lakini kama suala lihusikalo ni ubaguzi wa rangi, ufuatiaji wa vitu vya kimwili, mihusiko ya kijamii shuleni na kazini, au uhitaji wa kuhudhuria mikutano ya Kikristo, ni lazima tuwe waitikivu kwa mwelekezo wenye kuandaliwa kupitia Neno la Mungu na tengenezo lake. Haitupasi kamwe kuhisi kwamba shauri halali la Kimaandiko halitumiki kwetu na kulipuuza. Kumbuka kwamba Waisraeli wasio waaminifu walisema hivi: “Njia ya Bwana [Yehova, NW] si sawa [haikurekebishwa ifaavyo, NW].” Je! sio sisi ambao ni lazima tujirekebishe kulingana na njia za Yehova?—Ezekieli 18:25.
Twashangilia kwamba Yehova hupendezwa kwa uchangamfu na jinsi tutembeavyo mbele yake, akiandalia watu wake sahihisho la daima. Ni kama vile Isaya alivyotoa unabii: “Na masikio yako yatasikia neno nyuma yako, likisema, Njia ni hii, ifuateni; mgeukapo kwenda mkono wa kulia, na mgeukapo kwenda mkono wa kushoto.” Sisi, kwa upande wetu, na tuwe wepesi kufuata mwelekezo huo wenye upendo kutoka kwa Yehova na ‘tuwe tayari kutii.’ (Isaya 30:21; Yakobo 3:17) Ndiyo, acheni tuendelee kurekebishwa upya ili mwendo wetu utuongoze kwenye mradi wa umilele katika upendeleo wa Mungu!
[Maelezo ya Chini]
a Ona makala kuhusu ubaguzi zilizotokea katika toleo la Septemba 1985 la jarida andamani letu, Amkeni! Ona pia Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 1988, kurasa 10-20.