Mavuno Tele Yaleta Shangwe Katika Taiwan
TAIWAN ni kisiwa chenye urefu wa kilometa 390 kwa upana wa kilometa 140. Kikiwa na idadi ya watu zaidi ya 20,000,000, ni kimoja cha maeneo yenye idadi kubwa zaidi ya watu ulimwenguni. Walio wengi wa wakaaji wayo husema Kichina, au Kichina cha Mandarini kama vile kiitwavyo na watu wa Magharibi. Lakini lahaja kadhaa na karibu lugha 13 za kikabila husemwa hapa pia.
Ikiwa katika Tropiki ya Kansa, Taiwan ni kisiwa chenye rutuba sana, chenye kuzaa mavuno tele sana ya mchele na mazao mengine hivi kwamba kimekuwa mpelekaji wa chakula kwenye nchi za nje. Hata hivyo, mavuno ya aina nyingine yanaleta shangwe kubwa kwa wale wanaohusika katika hayo. Haya ni mavuno ya kiroho ya wale wanaoitikia “habari njema za ufalme” kwa upendelevu.—Mathayo 24:14, NW.
Upandaji Mdogo wa Kwanza
Kazi ya kupanda mbegu za ukweli wa Biblia katika Taiwan ilianza karibu miaka 60 iliyopita, wakati mwakilishi wa Watch Tower Society alipotoka Japani na kutoa hotuba kadhaa za Biblia katika Taipei, mji mkuu. Mwanamume kijana mmoja Mjapani aitwaye Saburo Ochiai aliuitikia kwa upendelevu ujumbe wa Ufalme na muda si muda akaanza kuongea na wengine juu ya huo. Baadaye, wahudumu wawili wa wakati wote kutoka Japani walizunguka-zunguka kisiwa hicho, wakipanda mbegu za habari njema. Mwishowe walitiwa gerezani na mabwana wa vita Wajapani na kutoa maisha zao kwa ajili ya Ufalme wa Mungu. Nyingi za mbegu walizopanda zilichipuka kwa haraka miongoni mwa kabila la Amis, lakini ni upendezi kidogo uliopatikana miongoni mwa Wachina wengi wanaoishi katika pwani ya magharibi ya kisiwa. Wao sana-sana ni Wabuddha au Watao.
Kazi ya mavuno ya kiroho katika Taiwan imesonga mbele kutoka mwanzo mdogo huo, hivi kwamba leo kisiwa hiki kimekuwa shamba lenye mazao. Kwa kielelezo, katika miaka mitano iliyopita, watu 529 walibatizwa, sana-sana wakitoka miongoni mwa wakaaji Wachina. Hii ilileta hesabu ya wapiga mbiu ya Ufalme kisiwani kwenye kilele cha 1,552 katika 1989. Ndiyo, Watao, Wabuddha, na Wakristo wa jina tu wanaziitikia habari njema na wanajifunza juu ya Yehova Mungu! Lakini ikoje kuongea juu ya Biblia na watu wenye malezi yenye kutofautiana jinsi hiyo? Na matokeo yamekuwa nini?
Itikio la Moyo Mkunjufu Dhidi ya Upendezi wa Kweli
Kazi ya Kuhubiri katika Taiwan ni yenye kuthawabisha na yenye kutokeza wito wa ushindani pia kwa sababu kwa asili Wachina ni watu wenye moyo mkunjufu. Kwa ujumla, wao husikiliza wageni kwa uungwana. Fasihi za Biblia zitolewapo, mara nyingi hukubaliwa ili kuonyesha adabu. Hivyo, wahudumu fulani wa wakati wote wameangusha kufikia magazeti 300 au wamepata maandikisho 100 ya majarida yetu katika mwezi mmoja. Muda wa miaka iliyopita, Biblia, vitabu, magazeti, na trakti zimeachwa pamoja na watu hawa. Basi, kwa nini ongezeko la wahubiri wa Ufalme limekuwa la polepole kwa kulinganisha?
Sababu moja yahusu mawazo ya Kikonfyushashi ambao yamefinyanga kufikiri kwa watu muda wa karne nyingi. Kulingana na Konfyushashi, yeye ambaye “kwa kuwastahi Roho hukaa mbali nao, aweza kuitwa mwenye hekima.”a Wazo ni kwamba mtu mwenye hekima hajihusishi mno na ibada ya roho au miungu. Hivyo, huenda wengi wakaulizia ha-bari za ujumbe wa Ufalme, lakini ni wachache watakao kuhusika katika funzo la Biblia. Halafu, pia, ingawa Wachina huamini katika roho na miungu, ile dhana ya kwamba kuna Muumba mkuu kupita wote ni ya kigeni sana kwa walio wengi kati yao. Zaidi ya hilo, hata watu wa Biblia wajulikanao sana kama Abrahamu na Daudi huenda wasiwe wa maana kwao. Kwa hiyo, si vigumu kuona ni kwa nini wakati na subira nyingi vyahitajiwa ili kusaidia watu hapa wakubali Biblia kuwa Neno la Mungu lililovuviwa na kusitawisha uhusiano wa kibinafsi pamoja na Muumba, Yehova Mungu. Hata hivyo, kwa baraka ya Yehova jitihada hizo zinathawabishwa.
Kichochezi cha Ukuzi
Kwa miaka mingi, makundi ya watu wa Yehova katika Taiwan yalitumia majumba ya kukodi kwa ajili ya mikutano yao. Uhitaji wa mahali pafaapo zaidi pa mikutano ulivutwa kwenye uangalifu wa wazee katika kundi moja wakati mtu mwenye kupendezwa aliposema hivi: “Ikiwa nyinyi ndio wenye ukweli, mnafanya nini katika mahali pa jinsi hii? Mbona nyinyi hamna mahali pa kudumu pa mikutano?” Hivyo basi kwa kumtegemea Yehova, kundi hilo lilianza kutafuta mahali pafaapo kuwa na Jumba la Ufalme. Mwishowe, walinunua nyumba mbili zenye kuungana katika jengo moja kubwa, na sasa wana Jumba la Ufalme zuri.
Katika miaka sita iliyopita, Majumba ya Ufalme 11 yamejengwa au yakanunuliwa katika Taiwan. Katika kila kisa, hiyo imetokeza mavuno yenye kuongezeka na hudhurio kubwa la mikutano. Kielelezo kimoja kilikuwa lile kundi katika jiji la kusini la Tainan. Katika 1981 jiji kubwa hili lenye watu 600,000 lilikuwa na kundi dogo moja tu lenye wahubiri 44 wa Ufalme. Kwa sababu ya uhitaji, kikundi hiki kiliamua kujenga Jumba la Ufalme lao wenyewe. Wakiwa na imani kwamba Yehova angewabariki, akina ndugu na dada walisonga mbele na mradi huo hata ingawa jumba lingegharimu karibu dola 200,000. Baadhi yao walichanga dhahabu yao ya mahari; wengine waliahirisha safari zao za kwenda ng’ambo. Kila mmoja katika kundi aliunga mkono kwa ukamili. Akina ndugu kwenye ofisi ya tawi ya Watch Tower Society walipopata habari juu ya mradi huu, waliamua kujenga kao la wamisionari juu ya Jumba la Ufalme, hivyo wakishiriki nusu ya gharama. Jumba lilimalizwa katika muda wa miaka miwili. Tokeo? Kufikia wakati ambapo Jumba la Ufalme lilimalizwa, jumla ya hesabu ya wahubiri ilikuwa imefikia 74! Wakati uliopo, makundi mawili, yenye jumla ya wahubiri 160, yanatumia jumba hilo, na hudhurio la mikutano kila juma lina wastani wa karibu 250. Makundi hayo mawili sasa yanapanga kujenga Jumba la Ufalme la pili.
Mavuno Miongoni mwa Vikundi vya Kikabila
Mavuno miongoni mwa vikundi vya kikabila katika pwani ya mashariki ya Taiwan yamekuwa yakiendelea tangu mwanzo wenyewe wa kazi ya Ufalme katika kisiwa hicho. Baadhi ya Waamisi waliojifunza ukweli mara ya kwanza miaka zaidi ya 50 iliyopita wangali ni watendaji. Muda wa miaka hiyo, wamekuta miito mingi ya ushindani. Wakati ule wa kumilikiwa na Wajapani katika Vita ya Ulimwengu ya 2, walilazimika kujifunza Kijapani. China iliporudishiwa kisiwa hiki baada ya vita, walilazimika kujifunza lugha ya Wachina. Katika miaka ya mapema ya 1960, walikabili mtihani wa aina nyingine. Wakati huo watu wengi mashuhuri wa kabila la Amis waliacha tengenezo safi la Yehova au wakathibitika kuwa wasiofaa kushirikiana nalo. Katika yote haya, kiini cha Mashahidi waaminifu kiliendelea kumtumikia Yehova. Wengi wa wajukuu wa ndugu na dada hawa waaminifu-washikamanifu walio na umri mkubwa zaidi wanaongoza sasa katika kazi ya kuhubiri.
Watu wa kutoka vikundi vya makabila mengine pia wamefanya maendeleo kiroho. Kwa kielelezo, kuna kikundi kimoja kiaminifu cha wahubiri wa Ufalme miongoni mwa kabila la Bunun. Baadhi ya babu zao wa hivi majuzi walikuwa wakata vichwa vya maadui. Sasa watu hawa wanahubiri ujumbe wenye amani wa Ufalme wa Mungu. Makabila ya Lukai na Paiwan yamepokea pia ushahidi mzuri, na wengi miongoni mwao wamefanya mabadiliko makubwa katika maisha zao. Ba Chu Fu asimulia ono lake, akisema:
“Mimi nilizaliwa katika eneo lenye milima-milima la Pingtung. Kwa kuwa baba yangu alikuwa chifu wa kabila la Lukai, watu walikuwa wakileta zawadi za chakula, hivyo basi hatukulazimika kufanya kazi yoyote nzito. Kwa sababu ya mazingira haya, nilisitawisha roho ya kiburi sana. Mimi nikawa ‘chifu’ wa genge la wakora vijana, tukitisha watu na kuwapokonya pesa. Nilihofiwa katika kijiji chetu. Katika umri wa miaka 22, nilichukua mmoja wa wasichana rafiki zangu wengi awe mke. Lakini maisha ya kukosa adili na kunywa kupindukia yalikuwa yametia mizizi kwa kina kirefu ndani yangu hivi kwamba nikapata maisha ya ndoa yakiwa magumu kukubali. Muda si muda ndoa yetu ikavunjika, nami nikarudia mtindo-maisha wangu wa zamani.
“Karibu na wakati huu, mke wangu alianza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Mimi sikupendezwa na nilijichukua kuwa mtu asiyeamini kuwako kwa Mungu. Kutokana na jitihada za mke wangu za bidii ya moyo mweupe, katika 1973 niliafiki kuandamana naye kwenye mkusanyiko mmoja wa kimataifa katika Taipei. Tulikaa pamoja na familia moja Mashahidi. Fadhili na adabu zisizo na ubaguzi za yule dada Mchina zilikaza kwangu mawazo yasiyofutika. Niliporudi nyumbani, nilianza kujifunza Biblia na nikafanya jitihada ya moyo mweupe nibadilike. Nilibatizwa katika 1974.
“Tangu wakati huo, kumekuwa na mitihani mingi. Mmoja ulikuwa kujifunza kusoma Kichina. Mwingine ulikuwa kukaa mbali na wengine. Kwa sababu hakukuwa na ndugu wakomavu wa kushirikiana nao wala wa kutafuta msaada kwao, nilitiwa moyo kumtegemea Yehova. Nilijifunza kuwa mnyenyekevu na kushikamana na tengenezo la Yehova. Tokeo likawa nini? Leo, wote katika familia yangu ni watendaji katika ukweli. Mimi nina pendeleo la kuwa mtumishi wa huduma katika kundi, ambalo sasa lina wahubiri 60 wenye bidii. Hata ingawa sina majaliwa yoyote maalumu, Yehova amebariki na kuunga mkono jitihada zangu katika kazi ya mavuno.”
Mavuno Yaendelea
Taiwan ni sehemu ndogo tu ya shamba la ulimwenguni pote. Hata hivyo, maneno ya Yesu, “Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache,” ni ya kweli hapa pia. (Mathayo 9:37) Mwaka uliopita, watu 4,534 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Na kadiri mavuno yasongapo yakafikie upeo, wafanya kazi ambao wamekuwa wakitoa jasho katika Taiwan wanavuna kwa kilio chenye shangwe.—Linganisha Zaburi 126:5, 6.
[Maelezo ya Chini]
a The Analects, vii 20, kama kilivyotafsiriwa na Arthur Waley, katika The Analects of Confucius, 1938, Vitabu vya Vintage, New York.
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 31]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
JAPANI
CHINA
TAIWAN
UFILIPINO
[Picha]
Jumba la Ufalme lililojengwa hivi majuzi katika pwani ya mashariki ya Taiwan
Wapiga mbiu ya Ufalme waleta shangwe kwa wengi katika bara hili lenye ubichi