Ubishi Juu Ya Kifo Cha Yesu
SIKU ya Kupitwa ya 33 W. K., mauaji matatu yalitukia. Wanaume watatu waliohukumiwa kuwa na hatia walisukumwa hadi mahali fulani nje ya ukuta za Yerusalemu na kuuawa kwa njia yenye kuteseka, yenye kushusha sana: kutundikwa juu ya miti iliyosimamishwa. Kuuawa hivyo kulikuwa kawaida katika nyakati za Waroma, basi yaweza kudhaniwa kwamba kufikia sasa mauaji hayo katika Sikukuu Kupitwa yangesahauliwa kitambo. Hata hivyo, mmoja wa wale wanaume waliouawa, alikuwa Yesu Kristo. Kifo chake kilitokeza badilisho la kidini lililo na maana sana na ubishi.
Karibu miaka elfu mbili imepita tangu jambo hilo litokee, basi ungeelekea kuliona kuwa historia ya kale tu. Hata hivyo, je, unatambua kwamba ubishi huo uliotokea hauko hata karibu kujibiwa?
Kama unavyojua, mamilioni huamini kwamba Yesu alikufa kwa ajili yao. Wao huamini kwa nguvu kwamba kifo cha Kristo ni ufunguo kwa fidia na msamaha wa dhambi, kwamba imani katika kifo chake ni njia ya wokovu. Ingawaje, kwa kushangaza, makala moja katika Anglican Theological Review yaripoti kwamba fundisho hili lenye kupendwa sana limo “katika taabu.” Na “taabu” hiyo yatoka kwa viongozi wa kidini.
Anglican Theological Review laeleza hivi: “Fundisho la malipio katika wazo la Kikristo limo katika taabu kwa sababu misingi yayo ya Kibiblia inatiliwa shaka, maelezo yayo yamebanwa dhana za kupita upesi . . . , na wonyesho walo katika hali ya kiroho yenye kupendwa na wengi umekuwa namna ya msisimuko wa kibinafsi na kujihesabia haki bila kujichunguza.” Kwa kweli, wanatheolojia Waprotestanti na Wakatoliki wameshindwa kufikia mapatano yoyote juu ya ni nini maana ya kifo cha Yesu Kristo, ikiwa ipo.
Waweza kufikiri kwamba hilo ni ugomvi kati ya wanatheolojia maalum wachache tu, kwamba hilo halihusiki na uhai wako. Lakini hebu fikiria hili: Ikiwa kifo cha Yesu kwa kweli kinalingani na msimamo wako mbele ya Mungu na matazamio yako ya kuwako milele (mbinguni au mahali popote pengine), basi ubishi huu wadai ufikirio wako.
Kwa nini wanatheolojia wangali wakibishana juu ya jambo hilo? Fikiria kwa mfano, Kanisa la Katoliki ya Kiroma. Lina fundisho la kanuni lililoelezwa vizuri juu ya kutokufa kwa nafsi na juu ya Utatu. Walakini, kwa ajabu Kanisa halijakata maneno kuhusu fidia kupitia kifo cha Kristo. New Catholic Encyclopedia chakiri hivi: “Taratibu nyingi na zilizo za namna mbalimbali zimestawishwa kueleza jinsi binadamu anakombolewa kutoka uovu wa dhambi na kurudishwa kwenye neema . . . lakini hakuna mmoja wa taratibu hizi ambao umefanikiwa kabisa. . . . Utheolojia wa Fidia haujafaulu katika sehemu fulani na unaendelea kujiweka kuwa tatizo katika utheolojia.”
Basi, haipasi kuwa mshangao kwako kwamba kwa wale mamilioni ambao hutamka kwa nguvu kwamba ‘Yesu alikufa kwa ajili yetu,’ ni wachache wenye ufahamu zaidi kidogo juu ya hilo humaanisha nini hasa. Ni kama vile Anglican Theological Review laeleza: “Akibanwa . . . mara nyingi Mkristo anayeamini hawezi kutaja chanzo cha kibiblia cha fundisho hilo, au kueleza jinsi linafanya kazi.” Wakilemewa na fundisho ambalo hawawezi ama kulielewa wala kulieleza, waabudu kanisani wamekazwa sana kuona jinsi kifo cha Kristo kina maana katika maisha zao.
Kushindwa kwa Jumuiya ya Wakristo kueleza vyema fundisho la wazi juu ya fidia kumevunja jitihada zayo za kuwafikia Wayahudi, Wahindu, Wabuddha, na wengine na ujumbe wa Kikristo. Ingawa wengi kama hao wanapenda na wanaheshimu mafundisho mengi ya Yesu, mchafuko unaozunguka kifo cha Kristo na kinachomaanishwa nacho ni kama vizuizi vya imani.
Je! maana ya kifo cha Kristo ni fumbo tu—ambalo lapita uelewevu wa binadamu? Au, je! kuna elezo la akili, lililo na msingi wa Biblia? Maswali hayo yanastahili ufikirio wako, kwa ajili Biblia inafanya dai hili la kugutusha kuhusu Yesu: ‘Kila mtu amwaminiye hatapotea, bali atakuwa na uzima wa milele.’—Yohana 3:16.