Utatu Hufafanuliwaje?
KANISA Katoliki la Kiroma hutaarifu hivi: “Utatu ndio mtajo ambao hutumiwa kumaanisha fundisho kuu la dini ya Kikristo . . . Hivyo, kwa kutumia maneno ya Imani ya Athanasio: ‘Baba ni Mungu, Mwana ni Mungu, na Roho Mtakatifu ni Mungu, na bado hakuna Miungu watatu bali Mungu mmoja.’ Katika Utatu huu . . . Watu [Nafsi] hao wana umilele-sawa na cheo-sawa: wote hali moja hawakuumbwa na wana uweza wote.”—The Catholic Encyclopedia.
Karibu makanisa yote katika Jumuiya ya Wakristo huafikiana. Kwa kielelezo, Kanisa Orthodoksi la Kigiriki huita Utatu pia “fundisho la msingi la Ukristo,” hata kusema hivi: “Wakristo ni wale wenye kukubali kwamba Kristo ni Mungu.” Katika kitabu Our Orthodox Christian Faith, kanisa ilo hilo hujulisha wazi hivi: “Mungu ni mwungano wa watatu. . . . Baba ni Mungu kabisa. Mwana ni Mungu kabisa. Roho Mtakatifu ni Mungu kabisa.”
Hivyo, Utatu huonwa kuwa “Mungu mmoja katika Watu [Nafsi] watatu.” Kila mmoja husemwa kuwa hana mwanzo, akiwa amekuwako kwa umilele. Kila mmoja husemwa kuwa mweza yote, huku kila mmoja akiwa si mkubwa zaidi wala si mdogo zaidi ya wengine.
Je! kusababu huko ni kugumu kueleweka? Waamini wengi wenye mioyo myeupe wamekuona kuwa kwenye kuvuruga, kuwa kinyume cha akili ya kusababu mambo kikawaida, tofauti na chochote walichopata kujua. Wao wauliza, Baba awezaje kuwa Mungu, Yesu awe Mungu, na roho mtakatifu awe Mungu, na bado kusiwe Miungu watatu bali Mungu mmoja tu?
“Limezidi Uwezo wa Kufahamu wa Akili ya Kibinadamu”
MVURUGO huu umeenea kwa mapana. The Encyclopedia Americana husema kwamba fundisho la Utatu hufikiriwa kuwa “limezidi uwezo wa kufahamu wa akili ya kibinadamu.”
Wengi ambao hukubali Utatu huuona kwa njia iyo hiyo. Monsinya Eugene Clark asema hivi: “Mungu ni mmoja, na Mungu ni watatu. Kwa kuwa hakuna kitu kama hicho katika uumbaji, sisi hatuwezi kukielewa, ila kukikubali tu.” Kardinali John O’Connor hutaarifu hivi: “Sisi twajua kwamba ni fumbo lenye kina sana, ambalo hatuanzi kulielewa.” Na Papa John Paul 2 hunena juu ya “lile fumbo lisilochunguzika la Mungu Utatu.”
Hivyo, A Dictionary of Religious Knowledge husema hivi: “Wanautatu hawaafikiani miongoni mwao wenyewe juu ya fundisho hilo ni nini hasa, au tuseme jinsi hasa lipasavyo kufafanuliwa.”
Basi, twaweza kuelewa kwa nini New Catholic Encyclopedia hutoa maoni haya: “Ni walimu wachache wa theolojia ya Utatu katika seminari za Katoliki ya Kiroma ambao hawajasumbuliwa wakati mmoja au mwingine na swali hili, ‘Lakini mtu aweza kuuhubirije Utatu?’ Na ikiwa swali hilo ni dalili ya mvurugiko kwa upande wa wanafunzi, labda kwa jinsi iyo hiyo ni dalili ya mvurugiko kwa upande wa maprofesa wao.”
Ukweli wa maoni hayo waweza kuthibitishwa kwa kwenda kwenye maktaba na kuchunguza vitabu ambavyo huunga mkono Utatu. Kurasa zisizohesabika zimeandikwa kujaribu kuufafanua. Hata hivyo, baada ya kutatizika sana kuelewa mvurugo mwingi wa mitajo na mafafanuo mbalimbali ya kitheolojia, bado wachunguzi huacha jitihada hiyo bila kutosheka.
Katika habari hii, Myeswiti Joseph Bracken atoa maoni haya katika kitabu chake What Are They Saying About the Trinity?: “Mapadri ambao kwa jitihada nyingi walijifunza . . . Utatu wakati wa miaka yao ya seminari husita kiasili kuutokeza kwa watu wakiwa kwenye mimbari, hata katika Jumapili ya Utatu. . . . Kwa nini mtu achoshe watu kwa kitu ambacho hata mwishowe hawangekielewa vizuri?” Pia asema hivi: “Utatu huaminiwa katika desturi rasmi tu, lakini una [matokeo] kidogo au hauna yoyote katika maisha na ibada ya Kikristo ya siku kwa siku.” Na bado, hilo ndilo “fundisho kuu” la makanisa!
Katika kitabu chake Christianity and the World Religions mwanatheolojia Mkatoliki Hans Küng atoa maoni ya kwamba Utatu ni sababu moja kwa nini makanisa hayakuweza kufanya maendeleo makubwa kati ya jamii zisizo za Kikristo. Ataarifu hivi: “Hata Waislamu wenye maarifa ya kutosha hawawezi kabisa kuelewa, kama vile Wayahudi wameshindwa mpaka sasa kufahamu, wazo la Utatu. . . . Tofauti ambazo hufanywa na fundisho la Utatu kati ya Mungu mmoja na nafsi tatu hazitoshelezi Waislamu, ambao huvurugika, kuliko kuangaziwa maarifa, na mitajo ya kitheolojia iliyotokana na Kisiria, Kigiriki, na Kilatini. Waislamu huuona wote huu kuwa mchezo wa maneno. . . . Kwa nini mtu yeyote atake kuongeza kitu chochote kwenye wazo la umoja na upekee wa Mungu ambacho chaweza tu kupunguza au kutangua umoja na upekee huo?”
“Si Mungu wa Mvurugo”
FUNDISHO lenye kuvuruga jinsi hiyo lingeweza kuanzaje? The Catholic Encyclopedia hudai hivi: “Kanuni ya imani iliyo ya kifumbo jinsi hiyo ingedokeza tu ufunuo wa Kimungu.” Wanachuo Wakatoliki Karl Rahner na Herbert Vorgrimler wataarifu hivi katika Theological Dictionary yao: “Utatu ni fumbo . . . katika maana halisi . . . , ambalo halingeweza kujulikana bila ufunuo, na hata baada ya ufunuo haliwezi kufahamika kabisa.”
Hata hivyo, kushindania kwamba kwa kuwa Utatu ni fumbo lenye kuvuruga sana, ni lazima uwe ulitokana na ufunuo wa kimungu hufanyiza tatizo jingine kubwa. Kwa nini? Kwa sababu ufunuo wa kimungu wenyewe hauruhusu kuwe na maoni kama hayo juu ya Mungu: “Mungu si Mungu wa mvurugo.”—1 Wakorintho 14:33, Revised Standard Version (RS).
Kulingana na taarifa hiyo, je! Mungu angekuwa na daraka la kutokeza fundisho la kumhusu yeye mwenyewe ambalo linavuruga sana hivi kwamba kwa kweli hata wanachuo Waebrania, Wagiriki, na wa Kilatini hawawezi kulifafanua?
Zaidi ya hilo, je! ni lazima watu wawe wanatheolojia ili ‘wajue Mungu aliye wa kweli peke yake na Yesu Kristo ambaye ametuma’? (Yohana 17:3, JB) Kama ingalikuwa hivyo, kwa nini ni wachache sana kati ya viongozi wa kidini Wayahudi wenye elimu waliomkubali Yesu kuwa Mesiya? Badala ya hivyo, wanafunzi wake waaminifu walikuwa wakulima, wavua-samaki, wakusanya-kodi, wake za kinyumbani walio wanyenyekevu. Watu hao wa kawaida walikuwa na uhakika sana kuhusu mambo aliyofundisha Yesu juu ya Mungu hivi kwamba wangeweza kufundisha wengine na hata walikuwa na nia ya kufia imani yao.—Mathayo 15:1-9; 21:23-32, 43; 23:13-36; Yohana 7:45-49; Matendo 4:13.
[Picha katika ukurasa wa 4]
Wanafunzi wa Yesu walikuwa watu wa kawaida walio wanyenyekevu, si viongozi wa kidini