Je! Kwa Wazi Hilo Ni Fundisho la Biblia?
KAMA Utatu ungalikuwa wa kweli, ungalipasa kuonyeshwa wazi na kwa upatano katika Biblia. Kwa nini? Kwa sababu, kama vile mitume walivyosema kwa uthabiti, Biblia ni ufunuo wa Mungu juu yake mwenyewe kwa ainabinadamu. Na kwa kuwa twahitaji kujua Mungu ili tumwabudu kwa kukubalika, Biblia yapasa kuwa wazi katika kutuambia yeye ni nani hasa.
Waamini wa karne ya kwanza waliyakubali Maandiko kuwa ufunuo wa kweli wa Mungu. Yalikuwa ndio msingi wa imani zao, mamlaka ya mwisho. Kwa kielelezo, mtume Paulo alipowahubiri watu katika jiji la Beroya, “walilipokea lile neno kwa uelekevu wa moyo, wakayachunguza maandiko kila siku, waone kwamba mambo hayo ndivyo yalivyo.”—Matendo 17:10, 11.
Wakati huo watu mashuhuri wa Mungu walitumia nini kuwa mamlaka yao? Matendo 17:2, 3 hutuambia hivi: “Paulo, kama ilivyokuwa desturi yake . . . akahojiana [alisababu, NW] nao kwa maneno ya maandiko sabato tatu, akiyafunua na kuwaeleza [kutokana na Maandiko].”
Yesu mwenyewe aliweka kielelezo katika kutumia Maandiko kuwa msingi wa kufundisha kwake, akisema kwa kurudia-rudia hivi: “Imeandikwa.” “Akawafafanulia mambo yote yaliyomhusu yeye katika Maandiko.”—Mathayo 4:4, 7; Luka 24:27, Habari Njema kwa Watu Wote.
Hivyo Yesu, Paulo, na waamini wa karne ya kwanza walitumia Maandiko kuwa msingi wa fundisho lao. Walijua kwamba “Andiko lote limevuviwa na Mungu na lina manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, kwamba binadamu wa Mungu apate kuweza mambo kikamili, mwenye vifaa kamili kwa kila kazi njema.”—2 Timotheo 3:16, 17, NW; ona pia 1 Wakorintho 4:6; 1 Wathesalonike 2:13; 2 Petro 1:20, 21.
Kwa kuwa Biblia yaweza “kunyoosha mambo,” yapasa kufunua wazi habari za jambo lililo la msingi sana kama vile ambavyo Utatu hudaiwa kuwa. Lakini je! wanatheolojia na wanahistoria wenyewe wanasema kwamba hilo kwa wazi ni fundisho la Biblia?
Je! “Utatu” Umo Katika Biblia?
KICHAPO kimoja cha Kiprotestanti hutaarifu hivi: “Neno Utatu halipatikani katika Biblia . . . Hapo kwanza halikuwa katika theolojia ya kanisa mpaka karne ya 4.” (The Illustrated Bible Dictionary) Na mamlaka moja ya Kikatoliki husema kwamba Utatu “si . . . neno la Mungu kwa njia ya moja kwa moja na ya kihususa.”—New Catholic Encyclopedia.
The Catholic Encyclopedia pia hueleza hivi: “Katika Andiko hakujawa bado na mtajo wowote mmoja ambao kwao wale Watu [Nafsi] Watatu wa Kimungu hutajwa pamoja. Neno τρίας [triʹas] (ambalo trinitas ya Kilatini ni tafsiri yalo) hupatikana katika Theofilo wa Antiokia karibu A.D. 180. . . . Muda mfupi baada ya hapo huonekana katika namna yalo ya Kilatini ya trinitas katika Tertulliani.”
Hata hivyo, huu wenyewe si uthibitisho wa kwamba Tertulliani alifundisha Utatu. Kwa kielelezo, kitabu cha Kikatoliki Trinitas—A Theological Encyclopedia of the Holy Trinity husema kwamba baadhi ya maneno ya Tertulliani yalitumiwa baadaye na wengine kueleza Utatu. Halafu hutahadharisha hivi: “Lakini mambo hayawezi kukatwa haraka-haraka kutokana na utumizi, kwa maana yeye hatumii maneno hayo kuhusu theolojia ya Utatu.”
Ushuhuda wa Maandiko ya Kiebrania
INGAWA neno “Utatu” halipatikani katika Biblia, je! angalau wazo la Utatu hufundishwa wazi humo? Mathalani, Maandiko ya Kiebrania (“Agano la Kale”) hufunua nini?
The Encyclopedia of Religion hukiri hivi: “Leo wanatheolojia huafikiana kwamba Biblia ya Kiebrania haina fundisho la Utatu.” Na pia New Catholic Encyclopedia husema hivi: “Fundisho la Utatu Mtakatifu halifundishwi katika A[gano] la K[ale].”
Vivyo hivyo, katika kitabu chake The Triune God, Myeswiti Edmund Fortman hukiri hivi: “Agano la Kale . . . halituambii lolote kwa wazi kabisa wala kwa kudokeza fikira juu ya Mungu wa Mwungano wa Watatu aliye Baba, Mwana na Roho Mtakatifu. . . . Hakuna uthibitisho wa kwamba mwandikaji yeyote mtakatifu hata aliwazia kwamba ndani ya Uungu mna [Utatu]. . . . Hata kuchukua kwamba katika [“Agano la Kale”] mna madokezo au vivuli au ‘ishara zilizotiwa shela [zilizofichika]’ zenye kuonyesha utatu wa watu, ni kuruka mipaka ya maneno na kusudio la waandikaji watakatifu.”—Italiki ni zetu.
Uchunguzi wa Maandiko ya Kiebrania yenyewe utaonyesha kwamba maelezo haya ni ya kweli. Hivyo, hakuna fundisho la wazi juu ya Utatu katika vitabu 39 vya kwanza vya Biblia ambavyo hufanyiza kanoni ya kweli ya Maandiko ya Kiebrania yaliyovuviwa.
Ushuhuda wa Maandiko ya Kigiriki
BASI je! Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo (“Agano Jipya”) hunena wazi juu ya Utatu?
The Encyclopedia of Religion husema: “Wanatheolojia huafikiana kwamba Agano Jipya pia halina fundisho la wazi kabisa juu ya Utatu.”
Myeswiti Fortman hutaarifu hivi: “Waandikaji wa Agano Jipya . . . hawatupi sisi fundisho rasmi au lililofanywa rasmi juu ya Utatu, hawatupi fundisho la wazi kabisa kwamba katika Mungu mmoja mna watu [nafsi] watatu wa kimungu wenye cheo-sawa. . . . Hakuna mahali ambapo twapata fundisho lolote la utatu wa wahusika watatu tofauti wenye uhai na utendaji wa kimungu katika Uungu ule ule mmoja.”
The New Encyclopædia Britannica hutoa maoni haya: “Wala neno hili Utatu, wala fundisho la wazi kama hilo, halionekani katika Agano Jipya.”
Bernhard Lohse husema hivi katika A Short History of Christian Doctrine: “Kwa kadiri ambavyo Agano Jipya lahusika, mtu hapati ndani yalo fundisho halisi la Utatu.”
Vivyo hivyo The New International Dictionary of New Testament Theology hutaarifu hivi: A[gano] J[ipya] halina fundisho la Utatu lililositawishwa. ‘Biblia haina ujulisho wazi wa moja kwa moja kwamba Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu ni wenye asili sawa’ [akasema mwanatheolojia Mprotestanti Karl Barth].”
Profesa wa Chuo Kikuu cha Yale E. Washburn Hopkins alisema kwa uthabiti hivi: “Inaonekana fundisho la utatu halikujulikana kwa Yesu na Paulo; . . . wao hawasemi lolote juu ya huo.”—Origin and Evolution of Religion.
Mwanahistoria Arthur Weigall huarifu hivi: “Yesu Kristo hakutaja kamwe ajabu ya jinsi hiyo, na hakuna popote katika Agano Jipya ambapo neno ‘Utatu’ huonekana. Wazo hilo liliingizwa tu na Kanisa miaka mia tatu baada ya kifo cha Bwana wetu.”—The Paganism in Our Christianity.
Hivyo, wala vile vitabu 39 vya Maandiko ya Kiebrania wala kanoni ya vitabu 27 vilivyovuviwa vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo haviandai fundisho lolote la wazi juu ya Utatu.
Je! Ulifundishwa na Wakristo wa Mapema?
JE! WAKRISTO wa mapema walifundisha Utatu? Angalia maelezo yanayofuata yaliyotolewa na wanahistoria na wanatheolojia:
“Ukristo wa mwanzo-mwanzo haukuwa na fundisho la wazi kabisa juu ya Utatu kama lile lililofafanuliwa sana baadaye katika zile imani.”—The New International Dictionary of New Testament Theology.
“Hata hivyo, hapo kwanza Wakristo hawa wa mapema hawakufikiria kutumia wazo [la Utatu] kuhusu imani yao wenyewe. Walielekeza ujitoaji wao kwa Mungu aliye Baba na kwa Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, na walitambua . . . Roho Takatifu; lakini hakukuwa na wazo lolote juu ya watatu hawa kuwa Utatu halisi, ulio na cheo-sawa na wenye kuungamana katika Mmoja.”—The Paganism in Our Christianity.
“Hapo kwanza imani ya Kikristo haikuwa ya Utatu . . . Haikuwa hivyo katika vipindi vya mitume na vya mara tu baada ya mitume, kama ionyeshwavyo katika A[gano] J[ipya] na maandishi mengine ya mapema ya Kikristo.”—Encyclopædia of Religion and Ethics.
“Kabla ya kuelekea mwisho wa karne ya 4, tungo hili ‘Mungu mmoja katika Watu Watatu’ halikuthibitishwa kiimara, kwa hakika halikuingizwa kikamili katika maisha ya Kikristo na kudai kwayo kuwa na imani. . . . Miongoni mwa Mababa wa Kimitume, kulikuwa hakuna jambo lolote lenye kukaribia hata kwa mbali kuwaza huko wala oni hilo.”—New Catholic Encyclopedia.
Mambo Ambayo Mababa Waliotangulia Nisea Walifundisha
MABABA waliotangulia Nisea walikiriwa kuwa walikuwa wamekuwa walimu mashuhuri wa kidini katika karne za mapema baada ya kuzaliwa Kristo. Mambo ambayo walifundisha ni ya upendezi.
Justin Martyr, aliyekufa karibu 165 W.K., alimwita Yesu aliyekuwako kabla ya ubinadamu kuwa malaika aliyeumbwa ambaye ni “mwingine kuliko kuwa ndiye Mungu yule aliyefanya vitu vyote.” Alisema kwamba Yesu alikuwa na cheo kidogo kuliko Mungu na “hakufanya kamwe jambo lolote isipokuwa lile ambalo Muumba . . . alimkusudia afanye na kusema.”
Irenayo, aliyekufa karibu 200 W.K., alisema kwamba Yesu aliyekuwako kabla ya kuwa binadamu alikuwa na maisha yaliyo tofauti na ya Mungu na alikuwa na cheo kidogo kuhusiana naye. Alionyesha kwamba Yesu si sawa na yule “Mungu Mmoja wa kweli na wa pekee,” aliye “mkuu zaidi juu ya wote, na ambaye hakuna mwingine zaidi ya yeye.”
Clement wa Aleksandria, aliyekufa karibu 215 W.K., alimwita Mungu kuwa “Mungu mmoja aliye wa kweli peke yake asiyeumbwa na asiyeweza kuangamia.” Alisema kwamba Mwana “ndiye wa pili kwa Baba mweza yote wa pekee” lakini hayuko sawa na yeye.
Tertuliano, aliyekufa karibu 230 W.K., alifundisha ukuu wa Mungu uzidio wote. Alitoa maoni haya: “Baba ni tofauti na Mwana (mwingine), kwa maana yeye ni mkubwa zaidi; kama vile mzazi ni tofauti na mzaliwa; mtumi, tofauti na mtume.” Pia alisema: “Kulikuwako wakati ambapo Mwana hakuwako. . . . Kabla ya vitu vyote, Mungu alikuwa peke yake.”
Hippolytus, aliyekufa karibu 235 W.K., alisema kwamba Mungu ndiye “Mungu yule mmoja, yule wa kwanza na yule Mmoja wa pekee, Mfanyi na Bwana wa wote,” ambaye “hakuwa na chochote cha pindi-sawa [cha umri sawa] na yeye . . . Bali alikuwa Mmoja, akiwa peke yake kabisa; ambaye, kwa kupenda, aliumba vitu ambavyo havikuwako kabla ya hapo,” kama vile Yesu aliyeumbwa akawako kabla ya kuwa binadamu.
Origen, aliyekufa karibu 250 W.K., alisema kwamba “Baba na Mwana ni asili mbili . . . asili yao ni ya vitu viwili,” na kwamba “kwa kulinganishwa na Baba, [Mwana] ni nuru ndogo sana.”
Akitoa muhtasari wa uthibitisho wa kihistoria, Alvan Lamson husema hivi katika The Church of the First Three Centuries: “Lile fundisho maarufu la ki-siku-hizi la Utatu . . . halipati tegemezo lolote kutokana na usemi wa Justin [Martyr]: na maoni haya yaweza kupanuliwa yawahusu Mababa wote wa kabla ya Nisea; yaani, yawahusu waandikaji wote Wakristo kwa muda wa karne tatu baada ya kuzaliwa kwa Kristo. Ni kweli kwamba, wao hunena juu ya Baba, Mwana, na . . . Roho takatifu, lakini si wakiwa na cheo-sawa, si wakiwa asili moja kihesabu, si wakiwa Watatu katika Mmoja, katika maana yoyote ambayo hukubaliwa sasa na Wanautatu. Uhakika wenyewe ni kinyume cha hilo kabisa.”
Hivyo, ushuhuda wa Biblia na wa historia huonyesha wazi kwamba Utatu haukujulikana muda wote wa nyakati za Kibiblia na kwa karne kadhaa baada ya hapo.
[Blabu katika ukurasa wa 7]
“Hakuna uthibitisho wa kwamba mwandikaji yeyote mtakatifu hata aliwazia kwamba ndani ya Uungu mna [Utatu].”—The Triune God