Biblia—Yatoka Kwa Mungu?
YEHOVA, Mungu wa uwezo na mamlaka yasiyozuiwa, kwa hakika ana haki ya kuwasiliana pamoja na uumbaji wake wa kibinadamu katika njia yoyote atakayo. Kama angechagua kuwasiliana kupitia neno lililoandikwa, angepaswa pia kuhifadhi ujumbe wake muda wa vipindi vyote. Je! ndivyo ilivyo na Biblia?
Miaka 1,500 hivi kabla ya Kristo, wakati kuandikwa kwa Biblia kulipoanza, kulikuwako maandishi mengineyo mengi ya kidini. Hata hivyo, yote hayo yaliachwa kutumiwa na hatimaye yakatokomea tu. Mengine yayo yamefukuliwa na wanaakiolojia nayo sasa ni vitu vya kale vinavyoonyeshwa katika nyumba za kuhifadhi. Kwa upande mwingine, sehemu za Biblia zilizoandikwa miaka zaidi ya elfu tatu iliyopita hazikusahauliwa kamwe, na nakala zimedumu hadi siku yetu. Hilo ni jambo la ajabu, hasa unapofikiria uadui uliotokea dhidi ya Biblia katika historia yote. Hakuna kitabu kingine ambacho kimekuwa shabaha ya upinzani na chuki kali kwa kadiri hiyo. Kusoma au kueneza Biblia kumeweza kuadhibiwa kwa faini, kutiwa gerezani, kuteswa, na mara nyingi kifo.
Kitabu tu kingeweza kuokokaje chini ya hali kama hizo? Biblia yenyewe yatuambia: “Neno la Bwana [Yehova, NW] hudumu hata milele.” (1 Petro 1:25) Uvumilivu na kutoharibika kwa Biblia kunatusaidia kuitambulisha kuwa Neno la Mungu takatifu.
Kuongezea hayo, kwa kusababu kiakili tunapaswa kutazamia kwamba ujumbe wa Mungu kwa ainabinadamu ungepatikana ulimwenguni pote. Je! ndivyo ilivyo na Biblia? Hakika ndivyo ilivyo! Hakuna kitabu kingine katika historia ambacho kimekaribia Biblia katika jambo hilo. Mwenezo wa Biblia umekadiriwa kuwa kwenye alama ya 3,000,000,000. Tena, hakuna kitabu kingine ambacho kimetafsiriwa katika lugha nyingi sana hivyo. Biblia sasa yaweza kusomwa, kwa ukamili au kwa sehemu, katika lugha tofauti-tofauti zaidi ya 1,900. Sosaiti ya Amerika ya Biblia inaripoti kwamba sasa inapatikana kwa asilimia 98 ya wakaaji wote wa ulimwengu. The New Encyclopœdia Britannica inaita Biblia “labda ndio mkusanyo wa vitabu vyenye uvutano zaidi katika historia ya kibinadamu.” Si kuwa na kiburi basi, kuieleza kuwa kitabu kikuu zaidi duniani.
Upatano wa kindani wa Biblia kutoka mwanzo hadi mwisho wenyewe ni uthibitisho wenye nguvu kwamba kwa kweli ilipuliziwa roho na Mungu. Je! lingekuwa jambo la halisi kutazamia kwamba maandishi yote ya watu tofauti-tofauti 40 hivi kupitia muda wa miaka 1,600 yangeweza yote kuthibitika kuwa yenye kupatana na yakiwa na kichwa kimoja cha msingi? Hilo lingekuwa jambo lisilowezekana ikiwa lingeachiliwa litendeke lenyewe tu au liongozwe na binadamu tu. Na bado, hali iko hivyo na vile vitabu 66 vinavyofanyiza Biblia. Ni akili inayopita asili ya kibinadamu, iliyoishi muda mrefu tu ambayo ingeweza kutokeza kazi ya ajabu kama hiyo.
Si Historia Tu
Mambo ya kihistoria yaliyomo katika Biblia ni yenye kutokeza. Lakini ujumbe kutoka kwa Mungu unaotia ndani mambo hakika ya kihistoria tu ungethibitika kuwa wenye thamani ya kiasi kwetu. Tunahitaji mwongozo na hekima yenye kutumika, navyo pia vyaweza kupatikana katika Biblia. Kwa mfano, Biblia hututia moyo tukuze “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti”—vichwa ambavyo habari nyingi juu yavyo imeandikwa kotekote katika kurasa zayo. (Wagalatia 5:22, 23, NW; Wakolosai 3:12-14) Biblia hupendekeza bidii ya kazi, usafi, ufuataji haki, uaminifu katika ndoa, staha na upendo kwa mwanadamu mwenzi; nayo inatia ndani wingi wa shauri juu ya mwenendo wa kibinadamu katika familia na jumuiya.
Linapotumiwa, shauri la Biblia latokeza kuwa lenye manufaa kikweli. Linatuweka huru kutokana na kutokujua na ushirikina. (Yohana 8:32) Hekima yayo yenye kutumika haina kifani. Kwa kweli, bila shaka ina hekima ya kimungu.
Dai la kwamba “Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu” lapatana kikamili na njia ambayo Biblia hasa hubadilisha watu. (Waebrania 4:12) Mamilioni leo wameshinda tabia za kiutu zenye kudhuru na kubadilisha mwendo wao wa zamani wa uharibifu kuwa bora kama tokeo la kuzingatia viwango vya Biblia.—Waefeso 4:22.
Ni jambo gani linalotukia wakati viwango vya Biblia vinapopuuzwa? Tokeo ni ukosefu wa furaha na huzuni nyingi, vita, umaskini, magonjwa yenye kuambukizwa kingono, na nyumba zilizovunjika. Mambo kama hayo ni yenye kutazamiwa tu kwa sababu kupuuza Biblia Takatifu kunamaanisha kukataa mwongozo wa Mungu, aliyeumba mwanadamu na ajuaye mahitaji yake.
Biblia pia hutabiri wakati ujao, jambo lisilowezekana kwa wanadamu kufanya. Kuinuka kwa mamlaka za ulimwengu kutoka Babuloni kupitia muda wa karne nyingi hadi siku yetu yenyewe kulitangazwa kiunabii katika Biblia. (Danieli, sura za 2, 7, 8) Kuongezea hayo, karibu miaka elfu mbili iliyopita, kulitiwa ndani ya Biblia maelezo sahihi ya hali za ulimwengu katika karne hii ya 20. (Mathayo, sura za 24, 25; Marko, sura ya 13; Luka, sura ya 21; 2 Timotheo 3:1-5; 2 Petro 3:3, 4; Ufunuo 6:1-8) Orodha ndefu ya unabii mbalimbali wa Biblia uliotimizwa inatuhakikishia kwamba matarajio kwa wakati ujao wenye furaha kama yalivyoelezwa katika kurasa zayo ni ya halisi.
Daraka Letu
Yote hayo ni ushuhuda mwingi sana kwamba Mungu kweli amewasiliana na wanadamu. Ni kweli, Mungu alipitisha ujumbe wake kwa mkono wa wanadamu wasio wakamilifu. Lakini hiyo si sababu ya kutoamini kwamba Biblia ni ya kweli kuliko vile ujumbe wa neno la mdomo kutoka kwa Mungu, au ulioletwa kupitia malaika, au ulioandikwa mbinguni kimuujiza na kuletewa wanadamu duniani kwa mkono ungekuwa.
Hata hivyo, kutambua chanzo kitakatifu, au cha kimungu cha Biblia kunatutwisha daraka. Yehova kwa haki hututazamia kusoma Neno lake kikawaida. (Zaburi 1:1, 2) Usomaji wa Biblia wenye matokeo mazuri unahitaji mtazamo unaofaa. Mtu anapaswa akumbuke kwamba Biblia haipasi isomwe kana kwamba ni kitabu kingine chochote. Ni lazima mtu aione “si kama neno la wanadamu, bali kama neno la Mungu.”—1 Wathesalonike 2:13.
Mambo mengine katika Biblia huenda yakawa magumu kufahamu. Lakini kupitia usomaji wa mara kwa mara, mtu aendelea kufahamu na kupata uelewevu ulio kamili zaidi wa mapenzi ya Mungu na wa kusudi zake. (Waebrania 5:14) Labda bado hujasadikishwa kikamili kwamba Biblia ni Neno la Mungu takatifu. Lakini, kwa kupatana, unaweza kuonyeshaje kuamini au kutoamini katika Biblia ikiwa hujaisoma kwa uangalifu?
Ijapokuwa utiaji shaka leo kuhusu chanzo chayo cha kimungu, uchunguzi wa uangalifu wa Biblia Takatifu umesababisha watu wengi wenye kufikiri wapaaze sauti kwa maneno ya mtume Paulo: “Mungu aonekane kuwa amini na kila mtu mwongo”!—Warumi 3:4.
[Grafu katika ukurasa wa 4]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Biblia inapatikana sasa kwa asilimia 98 ya
wakaaji wote wa ulimwengu
Hakuna kitabu kingine katika historia kilichokaribia mwenezo wa Biblia uliokadiriwa kuwa 3,000,000,000.
The New Encyclopœdia Britannica inaiita “labda ndio mkusanyo wa vitabu vyenye uvutano zaidi katika historia ya kibinadamu”
[Picha katika ukurasa wa 4]
Biblia imedumu, hali maandishi mengine ya kidini yakawa vitu vya kale vinavyoonyeshwa kwenye nyumba za kuhifadhi
Juu: Usimulizi wa Kiashuri wa Gharika
Kulia: Maombi kwa Ra mungu wa Kimisri
Zote Mbili: Hisani ya Trustees of The British Museum
[Hisani]
Both: Courtesy of the Trustees of The British Museum
[Picha katika ukurasa wa 5]
Ikiwa imeandikwa na watu tofauti-tofauti 40 hivi kupitia muda wa miaka 1,600, Biblia inafuata kichwa kimoja cha msingi kutoka mwanzo hadi mwisho. Ni akili inayopita asili ya kibinadamu, iliyoishi muda mrefu tu ambayo ingeweza kutokeza kazi ya ajabu kama hiyo
[Picha katika ukurasa wa 5]
Kuinuka kwa mamlaka za ulimwengu kutoka Babuloni kupitia muda wa karne nyingi hadi siku yetu yenyewe kulitangazwa kiunabii katika Biblia. (Danieli 2, 7, 8)
[Hisani]
Kulia: Kaisari Augusto
Museo della Civiltà Romana, Roma
[Picha katika ukurasa wa 6]
Karibu miaka elfu mbili iliyopita, Biblia ilitabiri kwa usahihi juu ya hali za ulimwengu leo. (Mathayo 24, 25; Marko 13; Luka 21; 2 Timotheo 3:1-5; 2 Petro 3:3, 4; Ufunuo 6:1-8) Usahihi wa unabii wa Biblia usiokosea unatuhakikishia kwamba ahadi ya Mungu ya dunia-paradiso haina budi kutimizwa
[Hisani]
Reuters/Bettmann Newsphotos