Je! Wewe Hukana Mielekeo Yenye Dhambi?
BASI nimeona sheria hii, ya kuwa kwangu mimi nitakaye kutenda lililo jema, lipo lililo baya. Kwa maana naifurahia sheria ya Mungu kwa utu wa ndani; lakini katika viungo vyangu naona sheria iliyo mbali, inapiga vita na ile sheria ya akili zangu, na kunifanya mateka ya ile sheria ya dhambi iliyo katika viungo vyangu.”—Warumi 7:21-23.
Unyenyekevu ulihitajiwa ili mtume Paulo akubali yaliyo juu. Hata hivyo, kwa kufanya hivyo, alisaidia kuzuia mielekeo yake isiyo mikamilifu imshinde.
Ni vivyo hivyo na Wakristo wa kweli leo. Tulipopata maarifa sahihi ya kweli ya Biblia, tulifanya mabadiliko yaliyokuwa ya lazima katika mtindo-maisha wetu, kupatana na viwango vya Yehova. Lakini mielekeo yenye dhambi hubaki, “maana mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu ujana wake.” (Mwanzo 8:21) Je! sisi twaweza kukiri kweli kweli kwamba tunayo mielekeo hususa inayosonga sana? Au je, tunakana kwamba hatuna, labda tukikata maneno kwamba, ‘Huenda hayo yakawa ni matatizo ya wengine lakini si yangu’?
Kujidanganya huko kwaweza kuwa kwenye hatari. Kielezi chenye msingi wa Biblia huenda kikatusaidia tuthamini uhitaji wa kukiri mielekeo yetu yenye dhambi na kuidhibiti.
Kwa Sababu Gani Kukana Kwaweza Kuwa Hatari
Katika nyakati za Biblia majiji mengi yalilindwa kwa kuta. Malango—yenye kufanyizwa kwa mbao mara nyingi—yalikuwa sehemu ya ukuta wa ndani wa jiji iliyokuwa rahisi zaidi kuvunjwa; kwa hiyo, yalilindwa kwa nguvu sana. Wenyeji walijenga kadiri malango yalivyohitajiwa tu kwa kupita watu wakati wa kipindi cha amani. Mara nyingi malango ya mbao yalifunikwa chuma, ili kuzuia kuharibiwa na moto. Minara ilijengwa ndani ya kuta hivi kwamba walinzi waliowekwa kwenye minara hiyo wangeweza kuona adui waliokuwa wakikaribia kutoka mbali.
Sasa ebu fikiria: Kungetukia nini ikiwa wenyeji wa jiji wangekana waseme kwamba malango ya jiji hayawezi kuvunjwa kwa urahisi hivyo wasiandae ulinzi wa kutosha? Askari adui wangeingia jiji hilo kwa urahisi, iongoze kwenye ushinde walo.
Hivyo ndivyo ilivyo na sisi pia. Yehova ajua sehemu zetu mmoja mmoja zilizo rahisi kuvunjwa. “Wala hakuna kiumbe kisichokuwa wazi mbele zake, lakini vitu vyote vi utupu na kufunuliwa machoni pake yeye aliye na mambo yetu.” (Waebrania 4:13) Shetani pia huenda akaona mwelekeo fulani wenye dhambi katika sisi, mwelekeo wetu uwe ama kupotoa kweli, uharaka wa kukasirika, kupendezwa na ngono haramu, kupenda vitu vya kimwili, kiburi, ama jambo jingine lolote. Tukikana kwamba hatuna mielekeo yenye dhambi, tunafanya iwe rahisi hata zaidi imani yetu ishambuliwe na Shetani. (1 Petro 5:8) Twaweza kushindwa wakati tamaa zisizofaa zinapoendelea kuwa zaidi ya mielekeo tu kisha zizae dhambi. (Yakobo 1:14, 15) Tunahitaji kuwa kama Paulo, tukikiri kikweli kwamba huenda yakawako ‘malango yoyote ya mbao.’
Jiimarishe Mwenyewe!
Ingekuwa kazi bure kutambua miegemeo yoyote mibaya lakini kutofanya lolote juu yayo. Hiyo ingekuwa kama mtu anayejiangalia katika kioo, aona sehemu zinazohitaji uangalifu, naye aenda zake bila kufanya marekebisho yanayohitajika. (Yakobo 1:23-25) Naam, tunahitaji kuchukua hatua tujilinde wenyewe tusivutwe na mielekeo yenye dhambi. Twaweza kufanyaje hivyo?
Mara nyingi, katika nyakati za Biblia, miji midogo, au “miji” fulani fulani, haikuwa na kuta. (Hesabu 21:25, 32; Waamuzi 1:7; 1 Nyakati 18:1; Yeremia 49:2) Wenyeji wa miji hiyo waliweza kukimbia kwenda kwenye jiji lenye kuta shambulio lilipotukia. Hivyo majiji yaliyoimarishwa yalitumikia kuwa kimbilio kwa watu katika eneo la karibu.
Biblia inamsema Yehova Mungu kuwa mnara (ngome), kimbilio, ukuta ambao twaweza kukimbilia ili tupate himaya. (Mithali 18:10; Zekaria 2:4, 5) Kwa hiyo Yehova ni ulinzi mkuu wa watumishi wake. Kumpelekea sala bila kukoma kunahitajiwa sana. (1 Thesalonike 5:17) Msaada mwingine ni Biblia. Kwa kutumia Neno la Mungu, tunafanya vizuri kuzichunguza kwa njia ya pekee zile sehemu ambazo tuna udhaifu. Huenda pia tukazitunza zile makala zenye msingi wa Biblia zinazoshughulika na ‘malango yetu ya mbao’ moja moja, ili tuzichunguze kwa kurudia-rudia.
Pia, kama vile walinzi katika mnara, sisi twaweza kumwona adui kutoka mbali, na kutenda kwa kulingana. Kwa jinsi gani? Kwa kuepukana na hali ambazo katika hizo huenda tukashawishwa au kusongwa. Kwa mfano, mtu anayejitahidi kuwa mwenye kiasi katika kunywa vileo atachagua kwa hekima kuepuka mahali ambapo uwezekano wa ku-nywa vinywaji hivyo ni rahisi au ambapo hata kunatiwa moyo.
Hayo yote yanahitaji jitihada. Hata hivyo, ikiwa mtume Paulo alipaswa ‘kuutesa mwili wake’ ili kupinga miegemeo isiyo mikamilifu, je, sisi hatuhitaji pia kujitahidi? Uangalifu huo wa kufahamu kwamba tuna mielekeo yenye dhambi utaonyesha kwamba tunafuata mwelekezo huu wa mtume Petro: “Fanyeni bidii ili mwonekane katika amani kuwa hamna mawaa wala aibu mbele yake.”—1 Wakorintho 9:27; 2 Petro 3:14.
Kiri na Kutenda
Usivunjike moyo ikiwa mielekeo yako yote isiyo mikamilifu haiondoki, zijapokuwa jitihada zako. Maadamu sisi ni wasio wakamilifu, miegemeo mibaya itakuwapo kwa kadiri fulani, kama ilivyokuwa kwa habari ya Paulo. Lakini tunahitaji kuendelea kujitahidi tuikandamize, tuizuie isizae dhambi.
Hata hivyo, uwe na ufahamu wa tofauti kati ya kukubali kwamba kuna kutokamilika na kule kukuvumilia. Hilo laweza kutolewa kielezi cha mtu aliye na moyo dhaifu kifuani mwake. Apaswa akubali hilo kwa kujaribu kudumisha moyo wake katika hali njema kadiri atumainivyo. Yeye hatoi sababu kwamba kwa kuwa moyo wake wa kihalisi ni dhaifu, hana haja ya kujizuia kwa njia yoyote na aweza kuishi jinsi yoyote apendavyo.
Basi, jua kwamba nguvu yetu haimo katika kukana kwa ujinga kwamba hakuna mielekeo yenye dhambi bali imo katika kukiri kwamba ipo kisha kuchukua hatua kuipinga. Kwa hiyo usiogope kujiambia mwenyewe na pia Yehova kwamba una maeneo ambayo katika hayo unashawishwa na kusongwa kwa urahisi. Kwa kufanya hivyo si lazima iwe na maana ya kwamba hujipendi sana, wala upendo wa Yehova kwako hautapunguka. Kwa hakika, ukaribiapo zaidi kwa Mungu ukitamani sana kupata kibali chake, yeye atakukaribia hata zaidi.—Yakobo 4:8.
[Picha katika ukurasa wa 31]
Kiolezo hiki cha Megiddo hutoa kielezi cha malango yaliyoimarishwa na kuta zenye ulinzi za majiji ya kale
[Hisani]
Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.