Je! Kuna Njia ya Kutoka Katika Hali ya Dhambi ya Binadamu?
AKIWA na watoto wake wanne matineja, Chisako alikuwa akisafisha vyoo vya watu wote katika jiji lililokuwa umbali wa kilometa 600 kutoka nyumbani kwake. Alipokuwa akifanya hivyo, aliimba usimulizi wa Kibuddha, ambao hakuelewa maana yao. Ulikuwa mmoja wa mazoea ya kikundi cha kidini kilichokuwa kikitafuta kile kilichoko katika shina lenyewe la dini zote.
“Nijapoendelea na mazoea ya kujiepusha na anasa,” Chisako akumbuka, “Nilishindwa kubadilisha utu wangu. Mle ndani sana ya moyo wangu, nilishindwa kuwasamehe wengine na nilishindwa kuonyesha upendo nikiwa na kusudio la moyo mweupe.”
Hata katika mabara ya Mashariki, ambapo watu wengi hawatambui dhambi kama inavyofundishwa katika Biblia, wengi huwa na mashaka ya kidhamiri kuhusu mielekeo yao ya dhambi, kama vile Chisako. (Warumi 2:14, 15) Ni nani hajapata kuhisi vibaya kwa kukosa kuonyesha fadhili kwa mtu aliye katika hali ya kusikitisha au ni nani hajapata kuhisi majuto yenye kuhuzunisha kwa ajili ya maneno ambayo hayakupaswa kusemwa? (Yakobo 4:17) Na je! wivu mbaya haumo ndani ya vijana na wazee pia?
Kwa nini watu huwa na hisi hizo zenye kusumbua? Ni kwa sababu, iwe wanajua au la, wana hisi ya ndani ya kutambua kosa, na dhambi. Kwa kweli, iwe watu wanajua mafundisho ya Biblia ya dhambi au la, wote wanaathiriwa na mielekeo ya dhambi. Mstadi mmoja wa jambo hilo alifanya mkataa huu wakati mmoja: “Wote wamefanya dhambi, na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.”—Warumi 3:23.
Je! Dhambi Yaweza Kufutwa?
Watu wengi leo, hasa katika Jumuiya ya Wakristo, wanajaribu sana kufuta hisi za dhambi na hatia katika dhamiri zao. “Neno lenyewe ‘dhambi’ . . . limekuwa karibu kutoweka,” akasema Dakt. Karl Menninger katika kitabu chake Whatever Became of Sin? Hata hivyo, kuepuka neno “dhambi” huwa hakusaidii kwa vyovyote sawa na vile mtu mzee-mzee kutaka kuepuka neno “uzee.” Tunapaswa tukubali uhakika wa kwamba tuna mielekeo ya dhambi na tunahitaji kuokolewa katika hali hiyo mbaya. Lakini tuokolewe na nani?
Mtume Mkristo Paulo aliuliza swali hilo baada ya kuungama mielekeo yake ya kufanya dhambi ajapotaka kufanya tofauti na hivyo: “Ole wangu, maskini mimi! ni nani atakayeniokoa na mwili huu wa mauti?” Ndipo Paulo akaendelea na kujibu: “Namshukuru Mungu, kwa Yesu Kristo Bwana wetu.” Kwa nini? Kwa sababu Mungu alikuwa amepangia msamaha wa dhambi kupitia dhabihu ya fidia ya Yesu.—Warumi 7:14-25.
Hata hivyo, wengi wa wasio-Wakristo wapatao 3,500,000,000 ulimwenguni (mara mbili ya idadi ya waitwao eti Wakristo) huona wazo la fidia kuwa gumu sana kuelewa. Kwa mfano, fundisho la fidia lilikuwa kikwazo kikubwa zaidi kwa Mwislamu anayeishi Japani aliyejifunza Biblia kwa muda fulani. Kwa watu wengi wa Mashariki, wazo la kwamba mtu mmoja angeweza kufa kwa ajili ya wote si la kawaida.
Hilo linaeleweka, kwa vile hata baadhi ya wale walio katika Jumuiya ya Wakristo hupata fundisho hilo la msingi kuwa gumu kuelewa. “Fundisho la Ukombozi,” ikakiri New Catholic Encyclopedia, “halijafaulu katika sehemu fulani na huendelea kuwa tatizo katika theolojia.”
Kadiri ya mvurugo kuhusu fundisho hilo imeonyeshwa vyema na maneno ya mwandikaji wa kidini N. H. Barbour: “Kifo cha Kristo hakingeweza kulipia adhabu ya dhambi ya mwanadamu kama vile kuchomelea pini katika mwili wa inzi na kufanya ihisi uchungu na kifo kusingefikiriwa na mzazi wa kidunia kuwa malipo yanayostahili kwa kosa la mwanaye.” Wakati huo Charles T. Russell alikuwa akishirikiana na Barbour, naye aliona uhitaji wa haraka wa kutetea fundisho la fidia. Aliacha kushirikiana na Barbour na katika 1879 akaanza kuchapisha gazeti jipya, ambalo baadaye likaja kuwa jarida unalosoma. Tangu mwanzo walo, Mnara wa Mlinzi limekuwa mtetezi wa dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo.
Lakini je! fundisho hilo linaweza kukubalika kwa wale wasio na malezi ya “Kikristo”? Ili kupata jibu, acha tuchunguze kwa makini zaidi fundisho hili la mtu mmoja kufa kwa ajili ya wote.