Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 11/15 kur. 13-18
  • Kusitawisha Tunda La Kujidhibiti

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kusitawisha Tunda La Kujidhibiti
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuhofu Mungu na Kuchukia Lililo Baya
  • Kujidhibiti, Mwendo wa Hekima
  • Upendo Usio Wenye Ubinafsi Husaidia
  • Imani na Unyenyekevu Zikiwa Wasaidizi
  • Kujidhibiti Ndani ya Familia
  • Kutumia Msaada Ambao Mungu Huandaa
  • Kujidhibiti —Kwa Nini Ni Kwa Maana Sana?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Iweni Wenye Kujidhibiti Ili Mshinde Tuzo!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Jazeni Kwenye Ujuzi Wenu Kujidhibiti
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Sitawisha Sifa ya Kujizuia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2017
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 11/15 kur. 13-18

Kusitawisha Tunda La Kujidhibiti

“Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi [kujidhibiti, NW]; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria.”—WAGALATIA 5:22, 23.

1. Ni nani wametupa sisi mifano mizuri kabisa ya kujidhibiti, kama ionwavyo kupatana na maandiko gani?

YEHOVA MUNGU na Yesu Kristo wametutolea mifano iliyo mizuri kabisa ya kujidhibiti. Tangu wakati wa kutotii kwa mwanadamu katika shamba la Edeni, Yehova ameendelea kuzoea sifa hiyo. (Linganisha Isaya 42:14.) Mara tisa katika Maandiko ya Kiebrania tunasoma kwamba yeye “si mwepesi wa hasira.” (Kutoka 34:6) Hilo linahitaji kujidhibiti. Na kwa hakika Mwana wa Mungu alijidhibiti sana, kwani “alipotukanwa, hakurudisha matukano.” (1 Petro 2:23) Hata hivyo, Yesu angeweza kumwomba Baba yake wa kimbingu ampe utegemezo wa “zaidi ya majeshi kumi na mawili ya malaika.”—Mathayo 26:53.

2. Tuna mifano gani mizuri ya Kimaandiko juu ya kujidhibiti kulikozoewa na wanadamu wasio wakamilifu?

2 Tunayo pia mifano mizuri ya Kimaandiko juu ya kujidhibiti kulikozoewa na wanadamu wasio wakamilifu. Kwa mfano, sifa hiyo ilionyeshwa wakati wa tukio lenye maana maishani mwa Yusufu, mwana wa mzee wa ukoo Yakobo. Lo, Yusufu alijidhibiti jinsi gani wakati mke wa Potifa alipojaribu kumtongoza! (Mwanzo 39:7-9) Kulikuwako pia ile mifano mizuri ya vijana Waebrania wanne waliozoea kujidhibiti kwa kukataa kula vyakula vitamu vya mfalme wa Babuloni kwa sababu ya vizuizi vya Sheria ya Musa.—Danieli 1:8-17.

3. Ni nani wanaojulikana kwa mwenendo wao mzuri, kama ionwavyo na ushuhuda gani?

3 Kupata mifano ya ki-siku-hizi ya kujidhibiti, twaweza kuelekeza fikira kwa Mashahidi wa Yehova kwa ujumla. Wanastahili sifa wanayopewa na kichapo New Catholic Encyclopedia—kwamba wao ndilo “mojawapo la makundi yenye tabia nzuri sana ulimwenguni.” Mfunzi wa chuo kikuu cha Ufilipino alitaarifu kwamba “Mashahidi hutumia kwa uangalifu sana yale wanayojifunza katika Maandiko.” Kuhusu mkusanyiko wa Mashahidi huko Warsaw katika 1989, mwandikaji-habari mmoja wa Polandi aliandika hivi: “Watu 55,000 hawakuvuta hata sigareti moja kwa siku tatu! . . . Wonyesho huo wa nidhamu inayozidi uwezo wa kibinadamu ulinivutia kwa mshangao wenye kuchanganyika na hofu.”

Kuhofu Mungu na Kuchukia Lililo Baya

4. Ni nini mojawapo ya misaada mikubwa zaidi katika kuzoea kujidhibiti?

4 Mojawapo ya misaada mikubwa zaidi katika kusitawisha kujidhibiti ni hofu ya Mungu, ile hofu ifaayo ya kutompendeza Baba wetu wa kimbingu mwenye upendo. Kadiri hofu ya Mungu yenye kicho yapasa kuwa na maana kwetu yaweza kuonwa katika uhakika wa kwamba Maandiko huitaja mara nyingi. Abrahamu alipokaribia kumtoa mwana wake Isaka, Mungu alisema hivi: “Usimnyoshee kijana mkono wako, wala usimtendee neno; kwa maana sasa ninajua ya kuwa unamcha Mungu, iwapo hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee.” (Mwanzo 22:12) Bila shaka kulikuwako mkazo mwingi wa kihisiamoyo wakati huo, kwa hiyo ni lazima kiasi kikubwa cha kujidhibiti kilitakiwa kwa upande wa Abrahamu ili aendelee na amri ya Mungu hadi hatua ya kukiinua kisu chake kumchinja mwana wake mpendwa Isaka. Naam, hofu ya Mungu itatusaidia kuzoea kujidhibiti.

5. Kuchukia lililo baya kuna sehemu gani katika kuzoea kwetu kujidhibiti?

5 Jambo linalohusiana kwa ukaribu na hofu ya Yehova ni kuchukia ubaya. Twasoma katika Mithali 8:13: “Kumcha BWANA [Yehova, NW] ni kuchukia uovu.” Kisha, kuchukia lililo baya kwatusaidia pia kuzoea kujidhibiti. Mara kwa mara, Maandiko hutuambia tuchukie—naam, tukirihi—lililo baya. (Zaburi 97:10; Amosi 5:14, 15; Warumi 12:9) Lile lililo baya mara nyingi ni lenye kupendeza sana, lenye kushawishi sana, lenye kuvutia sana hivi kwamba ni lazima tulichukie tu ili tuweze kujiimarisha dhidi yalo. Chuki yote ya jinsi hiyo kwa lile lililo baya ina tokeo la kuimarisha azimio letu la kuzoea kujidhibiti na hivyo inatumika kama ulinzi kwetu.

Kujidhibiti, Mwendo wa Hekima

6. Kwa nini ni mwendo wa hekima kuzuia mielekeo yetu ya ubinafsi kwa kuzoea kujidhibiti?

6 Msaada mwingine mkubwa katika kuzoea kujidhibiti ni kuthamini hekima ya kuzoea sifa hiyo. Yehova atuomba tuzoee kujidhibiti kwa faida yetu wenyewe. (Linganisha Isaya 48:17, 18.) Neno lake lina mashauri mengi yanayoonyesha jinsi lilivyo jambo la hekima kuzuia mielekeo yetu ya ubinafsi kwa kuzoea kujidhibiti! Hatuwezi kuepuka tu sheria za Mungu zisizobadilika. Neno lake latuambia hivi: “Cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna. Maana yeye apandaye kwa mwili wake, katika mwili wake atavuna uharibifu; bali yeye apandaye kwa Roho, katika Roho atavuna uzima wa milele.” (Wagalatia 6:7, 8) Mfano wa wazi ni ule wa kula na kunywa. Kuna matokeo mengi mabaya kwa sababu watu wanakula au kunywa kwa kupita kiasi. Hali yote hiyo ya kujiachilia kwa ubinafsi humfanya mtu akose kujistahi. Zaidi ya hayo, mtu hawezi kujiachilia kwa ubinafsi bila kuharibu pia uhusiano wake pamoja na wengine. Lililo na uzito zaidi ya yote ni kwamba, ukosefu wa kujidhibiti huharibu uhusiano wetu pamoja na Baba yetu wa kimbingu.

7. Ni nini kichwa kikuu cha kitabu cha Mithali, kama ionyeshwavyo na maandiko gani ya Biblia?

7 Kwa hiyo, ni lazima tuendelee kujiambia wenyewe kwamba ubinafsi una matokeo ya kinyume kwetu. Kichwa chenye kutokeza cha kitabu cha Mithali, kinachokazia kujitia nidhamu, ni kwamba ubinafsi hauna faida yoyote na kuna hekima katika kuzoea kujidhibiti. (Mithali 14:29; 16:32) Na ifahamiwe kwamba kujitia nidhamu kunahusisha mengi kuliko kuepuka tu lililo baya. Kujitia nidhamu, au kujidhibiti, kunahitajiwa pia ili kufanya lililo zuri, ambalo huenda likawa gumu kufanya kwa sababu hilo linapinga mielekeo yetu yenye dhambi.

8. Ni ono gani linalokazia hekima ya kuzoea kujidhibiti?

8 Kisa kinachotoa mfano wa jinsi lilivyo jambo la hekima kuzoea kujidhibiti ni kile cha mmoja wa Mashahidi wa Yehova aliyekuwa amesimama kwenye mstari wa watu katika benki wakati mwanamume mmoja alipojiingiza mbele yake kwa nguvu. Ingawa Shahidi huyo aliudhika kidogo, yeye alijidhibiti. Siku hiyo hiyo alihitaji kumwona mhandisi fulani ili apate sahihi kwa ajili ya mipango fulani ya Jumba la Ufalme. Kumbe mhandisi huyo akawa ni nani? Mtu yule yule aliyekuwa amejiingiza mbele yake kwa nguvu kwenye benki! Mhandisi huyo hakuthibitika kuwa mwenye urafiki sana tu bali alimtoza Shahidi huyo kiasi kinachopungua sehemu moja ya kumi ya bei ya kawaida. Shahidi huyo alifurahi jinsi gani kwamba alijidhibiti mapema siku hiyo, akijizuia asichokozeke!

9. Mwendo wa hekima ni upi tunapokutana na maitikio ya matukano katika huduma?

9 Mara kwa mara tunapoenda nyumba kwa nyumba tukihubiri habari njema za Ufalme wa Mungu au tunaposimama kwenye kona ya barabara tukijaribu kupendeza wapita njia na ujumbe wetu, sisi hukabili usemi wa matukano. Mwendo wa hekima ni upi? Taarifa hii ya hekima inatolewa kwenye Mithali 15:1: “Jawabu la upole hugeuza hasira.” Maana yake ni, tunahitaji kuzoea kujidhibiti. Na si Mashahidi wa Yehova peke yao ambao wameona hilo kuwa kweli lakini wengine pia wameiona hivyo. Thamani ya kuponya ya kujidhibiti inathaminiwa zaidi na zaidi na wenye kufanya kazi ya kitiba.

Upendo Usio Wenye Ubinafsi Husaidia

10, 11. Kwa nini upendo ni msaada wa kweli katika kuzoea kujidhibiti?

10 Ufafanuzi wa Paulo wa upendo katika 1 Wakorintho 13:4-8 unaonyesha kwamba nguvu yao yaweza kutusaidia kuzoea kujidhibiti. “Upendo huvumilia [ni mstahimilivu, NW].” Kuwa mstahimilivu kunahitaji kujidhibiti. “Upendo hauhusudu [si wenye wivu, NW]; upendo hautakabari [haujigambi, NW]; haujivuni [haujitutumui, NW].” Sifa ya upendo hutusaidia kudhibiti mawazo na hisia zetu za moyoni, kuzuia mwelekeo wowote wa kuwa wenye wivu, kujigamba, au kujitutumua. Upendo hutuchochea tuwe tofauti kabisa na hivyo, ukitufanya tuwe wanyenyekevu, wanyenyekevu wa akili, kama Yesu alivyokuwa.—Mathayo 11:28-30.

11 Paulo aendelea kusema kwamba upendo “haukosi kuwa na adabu.” Kujidhibiti kunatakiwa pia ili kutenda kwa adabu nyakati zote. Sifa ya upendo hutuzuia tusiwe na pupa, ‘kujitafutia mambo yetu’ tu. “Upendo hauoni uchungu [hauchokozeki, NW].” Ni rahisi kama nini kuchokozeka kwa sababu ya mambo ambayo wengine husema au hufanya! Lakini upendo utatusaidia kuzoea kujidhibiti na kutuzuia tusiseme au tusifanye mambo ambayo tungejuta baadaye. Upendo “hauhesabu mabaya.” Asili ya kibinadamu huelekea kuweka kinyongo au kulea udhia moyoni. Bali upendo utatusaidia kuondolea mbali mawazo kama hayo katika akili zetu. Upendo “haufurahii udhalimu.” Kujidhibiti kunatakiwa ili kutofurahia mambo yasiyo ya uadilifu, kama pornografia au mifululizo ya programu za televisheni zenye kushusha tabia. Upendo pia “huvumilia yote” na “hustahimili yote.” Kujidhibiti kunatakiwa ili kuchukuliana na mambo, kuvumilia mambo yenye kujaribu au yenye kulemeza na kutoyaacha yatuvunje moyo, yatufanye tulipe kisasi, au kutuelekeza tuache kumtumikia Yehova.

12. Ni gani njia moja ya kuuonyesha uthamini wetu kwa yote ambayo Yehova Mungu na Yesu Kristo wametufanyia?

12 Ikiwa tunampenda Baba yetu wa kimbingu kweli kweli na kuthamini sifa zake nzuri ajabu na yote ambayo ametufanyia, tutataka kumpendeza kwa kuzoea kujidhibiti nyakati zote. Pia, ikiwa tunampenda Bwana wetu, Yesu Kristo, na kuthamini yote ambayo ametufanyia, tutatii amri yake ‘kuokota mti wa mateso wetu, na kumfuata kwa kuendelea.’ (Marko 8:34, NW) Hilo bila shaka hutaka kwamba tuzoee kujidhibiti. Upendo kwa ndugu na dada zetu Wakristo utatusaidia pia tusiwaumize kwa kuchukua mwendo fulani wa ubinafsi.

Imani na Unyenyekevu Zikiwa Wasaidizi

13. Kwa nini imani yaweza kutusaidia kuzoea kujidhibiti?

13 Msaada mwingine mkubwa katika kuzoea kujidhibiti ni imani katika Mungu na ahadi zake. Imani itatusaidia tumtumaini Yehova na kungojea wakati wake wa kunyosha mambo. Mtume Paulo aeleza jambo kama hilo anaposema hivi katika Warumi 12:19: “Wapenzi, msijilipize kisasi, . . . maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena Bwana [Yehova, NW].” Kwa habari hiyo, unyenyekevu waweza kutusaidia pia. Ikiwa sisi ni wanyenyekevu, hatutaudhika upesi kwa sababu ya madhara yenye kuwaziwa au ya kweli. Hatutajaribu kujilipia kisasi kwa njia yetu wenyewe bali tujidhibiti na kuwa na nia ya kumngojea Yehova.—Linganisha Zaburi 37:1, 8.

14. Ni ono gani linaloonyesha kwamba kujidhibiti kwaweza kupatikana hata na wale wanaopungukiwa sana nako?

14 Ono linalohusu mwanamume mwenye hasira yenye jeuri lakazia sana kwamba tunaweza kujifunza kuzoea kujidhibiti. Alikuwa akipanda hamaki sana hivi kwamba polisi walipoitwa kwa sababu ya ghasia ambayo yeye na baba yake walikuwa wakisababisha, aliwapiga polisi watatu wakawa hoi kabla ya wengine kumweza! Hata hivyo, baadaye, alikutana na Mashahidi wa Yehova akajifunza kuzoea kujidhibiti, ambalo ni moja la matunda ya roho ya Mungu. (Wagalatia 5:22, 23) Leo, miaka 30 baadaye, mwanamume huyo angali akimtumikia Yehova kwa uaminifu.

Kujidhibiti Ndani ya Familia

15, 16. (a) Ni nini kitakachomsaidia mume aonyeshe kujidhibiti? (b) Kujidhibiti kunahitajiwa katika hali gani hasa, kama ionwavyo kutokana na ono gani? (c) Ni kwa nini kujidhibiti kunahitajiwa na mke?

15 Hakika kujidhibiti kunahitajiwa ndani ya familia. Ili mume ampende mke wake kama anavyojipenda mwenyewe ni lazima adhibiti sana mawazo, maneno, na vitendo vyake. (Waefeso 5:28, 29) Naam, kujidhibiti kunatakiwa kwa waume ili watii maneno ya mtume Petro katika 1 Petro 3:7: “Ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili.” Mume mwamini atahitaji kuzoea kujidhibiti hasa ikiwa mke wake si mwamini.

16 Kwa kutoa mfano: Kulikuwako mzee aliyekuwa na mke asiyeamini mwenye ugomvi sana. Hata hivyo, yeye alizoea kujidhibiti, na hilo lilimnufaisha sana hivi kwamba daktari wake alimwambia hivi: “John, ama wewe kwa asili ni mtu mwenye saburi nyingi ama una dini yenye nguvu nyingi.” Kwa kweli sisi tuna dini yenye nguvu nyingi, kwani “Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi,” inayotuwezesha kuzoea kujidhibiti. (2 Timotheo 1:7) Kuongezea hayo, kujidhibiti kunatakiwa kwa upande wa mke ili awe mtiifu, hasa wakati mume wake si mwamini.—1 Petro 3:1-4.

17. Kwa nini kujidhibiti ni kwa maana sana katika uhusiano kati ya mzazi na mtoto?

17 Kujidhibiti kunahitajiwa pia katika uhusiano kati ya mzazi na mtoto. Ili wawe na watoto ambao ni wenye kujidhibiti, ni lazima kwanza wazazi wenyewe waweke mfano mwema. Na wakati watoto wanapohitaji kutiwa nidhamu ya aina moja au nyingine, inapasa sikuzote itolewe kwa utulivu na upendo, jambo linalohitaji kujidhibiti kweli kweli. (Waefeso 6:4; Wakolosai 3:21) Kisha pia, utii watakiwa ili watoto waonyeshe kwamba wanawapenda wazazi wao kweli kweli, na bila shaka kutii kunahitaji kujidhibiti.—Waefeso 6:1-3; linganisha 1 Yohana 5:3.

Kutumia Msaada Ambao Mungu Huandaa

18-20. Ni maandalizi gani matatu ya kiroho ambayo ni lazima tujifaidi nayo ili kusitawisha sifa zitakazotusaidia kuzoea kujidhibiti?

18 Tunahitaji kujifaidi na msaada wote ambao Yehova Mungu ameandaa ili tukue katika hofu ya Mungu, katika upendo usio na ubinafsi, katika imani, katika kuchukia lililo baya, na katika kujidhibiti. Acheni tuzungumzie maandalizi matatu ya kiroho yawezayo kutusaidia kuzoea kujidhibiti. Kwanza, kuna lile pendeleo lenye thamani kubwa la sala. Hatutaki kamwe kuwa wenye shughuli sana tusiweze kusali. Naam, twapaswa kutamani ‘kuomba bila kukoma,’ ‘kudumu katika kusali.’ (1 Wathesalonike 5:17; Warumi 12:12) Acheni tufanye kusitawisha kujidhibiti kuwe jambo la sala. Lakini tunapopungukiwa katika kuzoea kujidhibiti, acheni tumsihi Baba yetu wa kimbingu kwa sikitiko ili tupate msamaha.

19 Eneo la pili la kusaidia katika kuzoea kujidhibiti ni kupata msaada unaotokana na kujilisha Neno la Mungu na vichapo vinavyotuwezesha tuelewe na kutumia Maandiko. Ni rahisi sana kupuuza sehemu hii ya utumishi wetu mtakatifu! Ni lazima tuzoee kujidhibiti na kuendelea kujiambia wenyewe kwamba hakuna habari ya kusoma iliyo na maana zaidi ya Biblia na habari inayoandaliwa na “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” na hivyo twapaswa kuitanguliza. (Mathayo 24:45-47) Imesemwa kwa kufaa kwamba maishani sisi huwa hatuna hiari ya kuchagua vyote, bali chaguo ni moja tu. Je! sisi kwa kweli ni wanaume na wanawake wa kiroho? Tukiona uhitaji wetu wa kiroho, tutazoea kujidhibiti kunakohitajiwa ili kuzima televisheni na kutayarisha mikutano yetu au kusoma Mnara wa Mlinzi ambalo huenda likawa limewasili sasa hivi kwa njia ya posta.

20 La tatu, kuna lile jambo la kuipa mikutano yetu ya kundi na yale makusanyiko na mikusanyiko mikubwa zaidi ustahili unaoipasa. Je! mikutano yote ya jinsi hiyo ni ya lazima kabisa kwetu? Je! tunakuja tukiwa tayari kushiriki na kufanya hivyo kwa kadiri tunavyokuwa na nafasi? Kwa kadiri tutambuavyo thamani ya kweli ya mikutano yetu, ni kwa kadiri hiyo hiyo tutakavyoimarishwa katika azimio letu kuzoea kujidhibiti chini ya hali zote.

21. Ni baadhi gani ya thawabu ambazo twaweza kufurahia kwa ajili ya kusitawisha tunda la roho la kujidhibiti?

21 Ni thawabu zipi tuwezazo kutazamia kwa kujitahidi sana kuzoea kujidhibiti nyakati zote? Kwanza, hatutavuna kamwe matunda ya ubinafsi yenye uchungu. Tutajistahi na kuwa na dhamiri safi. Tutajiokoa wenyewe tusipatwe na matatizo mengi sana na tutabaki kwenye barabara ya uhai. Isitoshe, tutaweza kuwafanyia wengine wema ulio mkubwa zaidi. Zaidi ya yote, tutakuwa tukitii Mithali 27:11: “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; ili nipate kumjibu anilaumuye.” Na hiyo ndiyo zawadi kubwa zaidi ambayo tungeweza kupata—pendeleo la kuufurahisha moyo wa Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo, Yehova!

Je! Unakumbuka?

◻ Hofu ya Mungu inatusaidiaje kuzoea kujidhibiti?

◻ Kwa nini upendo hutusaidia kuzoea kujidhibiti?

◻ Kujidhibiti kunasaidiaje katika uhusiano mbalimbali wa familia?

◻ Ikiwa tutasitawisha kujidhibiti ni lazima tutumie vizuri maandalizi gani?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Yusufu alizoea kujidhibiti aliposhawishwa

[Picha katika ukurasa wa 17]

Nidhamu inayotolewa kwa mtoto kwa utulivu na upendo huhitaji kujidhibiti kweli kweli

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki