Twahitaji Mtu Mwenye Kusikiliza
TUKIWA wanadamu, sisi hujaribu kupata shangwe na uradhi maishani. Lakini matatizo ya kibinafsi yanapotokea, huwa inasaidia na kufariji kama nini kuwa na mtu ambaye twaweza kuongea naye juu ya taabu zetu.
Dakt. George S. Stevenson asema: “Kuzungumza juu ya tatizo husaidia kuuondoa mkazo wako, hukusaidia uone hangaiko lako kwa udhahiri zaidi, mara nyingi hukusaidia uone jambo uwezalo kufanya juu yalo.” Dakt. Rose Hiferding alionelea hivi: “Sisi sote twahitaji kushiriki taabu zetu. Twahitaji kushiriki mahangaiko. Twahitaji kuhisi kuna mtu ulimwenguni aliye na nia ya kusikiliza na awezaye kuelewa.
Pasipo shaka, hakuna mwanadamu yeyote awezaye kutosheleza uhitaji huo kikamili. Kwa sababu ya vizuizi vya wakati na mambo mengine, wanadamu ambao sisi hutolea siri zetu huenda wasiweze kupatikana tunapowahitaji zaidi, au huenda tukasita kuzungumza mambo fulani hata na marafiki wetu wa karibu zaidi.
Hata hivyo, Wakristo wa kweli, hawakosi kabisa kamwe mtu wa kuwasikiliza, kwani njia ya sala hupatikana sikuzote. Biblia hututia moyo tena na tena tusali kwa Mungu, Muumba wetu, ambaye jina lake ni Yehova. Tunaelekezwa tusali kwa moyo mweupe, katika jina la Yesu, na kwa kupatana na mapenzi ya Mungu. Hata mambo ya kibinafsi na ya faragha ni habari zifaazo kwa sala. “Katika kila neno . . . haja zenu na zijulikane na Mungu,” twaambiwa kwenye Wafilipi 4:6. Hiyo ni zawadi yenye kutokeza kama nini! Mtawala Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wetu wote mzima yu tayari sikuzote kukaribisha na kupokea sala za watumishi wake wanyenyekevu wakati wowote wanapotaka kumkaribia.—Zaburi 83:18; Mathayo 6:9-15; Yohana 14:13, 14; 1 Yohana 5:14.
Hata hivyo, je, Mungu husikiliza kweli kweli? Wengine huenda wakaona ni kama matokeo ya sala hutegemea uwezo wa kibinadamu tu: Mtu asali, akipanga mawazo yake na kuyatoa kwa maneno. Akiwa amefafanua tatizo lake jinsi hiyo, atafuta suluhisho linalofaa na aangalia kila jambo liwezalo kuchangia kulipata. Tatizo lake linaposuluhishwa, aweza kumpa Mungu sifa, lakini kwa kweli ni akili na jitihada zake mwenyewe zilizoleta matokeo hayo yaliyotamaniwa.
Wengi leo hufikiri kwamba kwa kweli hilo tu ndilo linalohusika katika sala. Je! wewe hufikiri hivyo? Je! uwezo wa sala huwekewa mpaka jinsi hiyo? Ni kweli, akili na jitihada za kimwili za mtu kwa kupatana na sala zake huwa na daraka la maana katika kupokea majibu. Hata hivyo, vipi juu ya daraka la Mungu mwenyewe katika jambo hilo? Je! Mungu husikiliza usalipo kwake? Je! yeye huona sala zako kuwa za maana, akitoa ufikirio juu ya yale yaliyomo na kuziitikia?
Majibu ya maswali hayo ni ya maana. Ikiwa Mungu hatolei sala zetu uangalifu wake, basi sala ina thamani ya kisaikolojia (inayotegemea kutumia akili) tu. Kwa upande ule mwingine, ikiwa Mungu hupokea na kusikiliza kila moja ya sala zetu akiwa na upendezi, twapaswa kuwa na shukrani kama nini kwa ajili ya uandalizi kama huo! Wapasa utusukume kuutumia uandalizi huo kila siku.
Twakualika, basi, uendelee kusoma, kwa kuwa masuala hayo yanazungumzwa katika makala ifuatayo.