Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Je! Biblia huunga mkono kuwapo kwa farasi wenye pembe moja, wanaotajwa katika tafsiri fulani?
Tafsiri ya King James, ya Douay, na nyinginezo, hutaja farasi wenye pembe moja. Lakini sivyo ilivyo katika tafsiri za ki-siku-hizi zinazotafsiri lugha ya Kiebrania kwa usahihi.—Zaburi 22:21; 29:6; 92:10 (21:22; 28:6; 91:11, Douay).
Muda wote wa karne zilizopita ngano zimesitawi juu ya mnyama aliye na mwili na kichwa cha farasi lakini mwenye miguu ya paa na mkia wa simba. Labda sura yenye kutokeza zaidi ya kiumbe huyo wa kihekaya ni ile pembe moja yenye kupindamana iliyo juu ya kichwa chake.a
“Wakati mmoja watu waliamini kwamba pembe ya farasi mwenye pembe moja ilikuwa na dawa ya kuzuia madhara ya sumu, na katika Enzi za Katikati, unga-unga uliodhaniwa kuwa ulifanyizwa kwa pembe hizo uliuzwa kwa bei za juu sana. Wanachuo wengi huamini kwamba taswira ya farasi mwenye pembe moja ilitokana na masimulizi ya Ulaya ya habari isiyothibitishwa kuhusu kifaru.” (The World Book Encyclopedia) Nguzo fulani za Ashuru na za Kibabuloni zilionyesha wanyama wenye pembe moja. Hizo hutambuliwa sasa kuwa paa-dume, mbuzi mwitu, ng’ombe, na mafahali walioonyeshwa kutoka upande mmoja tu, kwa njia isiyoonyesha pembe zote mbili.
Hiyo ni habari yenye kupendeza wanafunzi wa Biblia kwa kadiri fulani kwa sababu Maandiko hurejezea mnyama mmoja mara tisa kwa neno la Kiebrania re’emʹ. (Hesabu 23:22; 24:8; Kumbukumbu la Torati 33:17; Ayubu 39:9, 10; Zaburi 22:21; 29:6; 92:10; Isaya 34:7) Kwa muda mrefu watafsiri hawakujua kwa hakika ni mnyama yupi aliyemaanishwa. Septuagint ya Kigiriki ilifasiri re’emʹ likiwa na maana ya ‘pembe moja’ au farasi mwenye pembe moja. Vulgate ya Kilatini hulitafsiri mara nyingi kuwa “kifaru.” Tafsiri nyinginezo hutumia ‘ng’ombe dume mwitu,’ ‘hayawani mwitu,’ au ‘nyati.’ Robert Young hulitafsiri kwa kutumia neno lile lile la Kiebrania katika Kiingereza kuwa “Reem,” kwa msingi akiacha msomaji bila kujua maana yalo.
Lakini, wanachuo wa ki-siku-hizi wameondoa mvurugo mwingi juu ya neno re’emʹ. Watunga kamusi Ludwig Koehler na Walter Baumgartner huonyesha kwamba linamaanisha “ng’ombe dume mwitu,” wanaotambulishwa kisayani kwa maneno Bos primigenius. Hilo ni “familia ndogo kutoka kwa ile familia kubwa yenye wanyama wenye pembe na kwato.” The New Encyclopœdia Britannica hueleza hivi:
“Mafungu fulani ya kishairi ya Agano la Kale hurejezea mnyama mzuri mwenye nguvu aliye na pembe aitwaye re’emʹ. Neno hilo linatafsiriwa ‘farasi mwenye pembe moja’ au ‘kifaru’ katika tafsiri nyinginezo, lakini tafsiri nyingi za ki-siku-hizi hupendelea ‘auroki’ (ng’ombe dume mwitu mwenye pembe ndefu) ambayo ndiyo maana sahihi ya neno la Kiebrania re’emʹ.”
Kwa kuwa katika Kiingereza cha kisasa maneno “ng’ombe dume” yana maana ya ng’ombe maksai, New World Translation of the Holy Scriptures hufasiri neno re’emʹ kwa upatani na kwa usahihi kuwa “fahali mwitu.” Wale auroki (ng’ombe dume mwitu, au mafahali) yaonekana walikufa na kutokuwako tena kufikia karne ya 17, lakini wanasayansi wamepata kuona kwamba hao walikuwa tofauti sana na farasi mwenye pembe moja wa hekaya. Auroki wa kale walikuwa na kimo cha mwili cha karibu meta 1.8, na urefu wa meta tatu hivi. Huenda ikawa walikuwa na uzito wa kilo 900, na kila moja ya pembe zao mbili ingeweza kuwa na urefu wa centimeta 75.
Hilo kwa hakika hupatana na mtajo wa Kibiblia wa re’emʹ, au fahali mwitu. Alijulikana kwa sababu ya nguvu na mwelekeo wake wa ukaidi (Ayubu 39:10, 11) pamoja na wepesi wake. (Hesabu 23:22; 24:8) Kwa wazi alikuwa na pembe mbili, si moja tu kama yule farasi mwenye pembe moja wa kihekaya. Musa alirejezea pembe zake mbili alipokuwa akitoa kielezi cha yale makabila mawili yenye nguvu ambayo yangetoka kwa wana wawili wa Yusufu.—Kumbukumbu la Torati 33:17.
Kwa hiyo Biblia haiungi mkono wazo la farasi wenye pembe moja walio mashuhuri katika hekaya. Inaonyesha picha sahihi, lakini yenye mipaka, ya auroki wenye kuhofisha, waliokuwako katika nyakati za Biblia na hadi kufikia wakati uliopita usio mbali sana.
[Maelezo ya Chini]
a Profesa Paul Haupt aeleza hivi: ‘Kati ya vitu vya enzi ya katikati vilivyokusanywa, pembe za virafu au pembe za nyangumi wadogo (waliotiwa pia samaki wenye pembe moja au nyangumi wenye pembe moja) zilionwa kuwa pembe za farasi mwenye pembe moja.’
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 31]
Treasury of Fantastic na Mythological Creatures: 1,087 Renderings from Historic Sources, cha Richard Huber/Dover Publications, Inc.