Kwa Nini Utahini Usahihi wa Biblia?
Wewe huionaje Biblia? Wengine huamini kwa uthabiti kwamba ni ufunuo wa Mungu kwa mwanadamu. Wengine huamini kwamba ni kitabu cha kawaida tu. Wengine bado husita kuamua. Ikiwa una shaka yoyote kuhusu chanzo cha Biblia, kuna sababu za lazima kwa nini unapaswa kuichunguza na kusuluhisha suala hilo.
MPAKA karne ya 18, Biblia ilistahiwa sana kuwa Neno la Mungu katika mabara ya Jumuiya ya Wakristo. Lakini tangu karne ya 19 na kuendelea, idadi yenye kuongezeka ya walimu, wanasayansi, na hata wanatheolojia na viongozi wa kanisa walianza kutilia shaka peupe usahihi wa Biblia.
Tokeo ni kwamba, uchambuzi wa Biblia umeenea sana hivi kwamba wengi huamua kimbele bila hata kujua yaliyomo ndani ya Biblia. Sasa watu wengi katika Jumuiya ya Wakristo huendea falsafa za watu badala ya Biblia. Bado, falsafa ya kisasa haijatokeza ulimwengu ulio salama zaidi au wenye furaha zaidi. Ndiyo sababu moja nzuri ya kuichunguza Biblia na kuona kama mwongozo wayo huelekeza kwenye furaha na mafanikio.
Sababu nyingine ya kutahini usahihi wa Biblia ni lile taraja zuri ajabu inalotolea ainabinadamu. Kwa kielelezo, Zaburi 37:29 husema hivi: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” (Ufunuo 21:3-5) Ahadi hizo zinakuathiri namna gani? Kwa hakika zinatoa sababu za kutosha za kuichunguza Biblia na kuona ikiwa inaweza kutumainiwa.
Sikuzote gazeti hili limeunga mkono ukweli wa Biblia na mara nyingi limetoa uthibitisho wa usahihi wayo. Kuna sehemu kadhaa ambazo kwazo usahihi wa Biblia waweza kutahiniwa. Matoleo mbalimbali ya Mnara wa Mlinzi yatakusaidia kuyajibu maswali haya: Je! mambo ya hakika ya historia ya kale yanapatana na Biblia? Je! matabiri yayo ni sahihi? Je! shauri layo lafaa, au walimu na wanafalsafa wa kisasa wamethibitisha kwamba Biblia haifai wakati huu?
Jiografia ni sehemu nyingi ambayo kwayo waweza kutahini usahihi wa Biblia. Ngano za kipagani mara nyingi hupingana na mambo ya hakika ya kijiografia. Kwa mfano, watu wengi wa kale walisimulia hadithi za safari za kwenda hadi mahali palipoitwa eti ulimwengu wa wafu. Kuhusu Wagiriki wa kale, kitabu A Guide to the Gods chaeleza hivi: “Dunia ilionwa kuwa uso tambarare uliozingirwa kwa maji mengi yaliyoitwa Bahari. Mbali zaidi ya hapo kulikuwako Ulimwengu wa Baadaye, bara-tupu la huzuni lenye mimea meusi-meusi bila matunda iliyotapakaa.” Hilo lilipothibitika kuwa ngano, wanafalsafa wapagani walilazimika kutafutia mahali papya ule walioita eti ulimwengu wa baadaye. “Mahali pafaapo palipatikana, chini ya dunia, palipounganishwa na ulimwengu huu kwa mapito mbalimbali,” aeleza mtungaji vitabu Richard Carlyon. Leo, twajua kwamba hiyo ilikuwa ngano pia. Hakuna ulimwengu wa chini wala mapito ya kwenda huko.
Tofauti na ngano za watu wa kale, Biblia haina yale maoni ya makosa kwamba dunia ni tambarare. Badala ya hivyo, inasema ile kweli ya kisayansi kwamba dunia ni kitu cha duara ambacho hakikalii chochote. (Ayubu 26:7; Isaya 40:22) Namna gani yale masimulizi mengine ya kijiografia yanayotajwa katika Biblia? Je! hayo ni ya kingano, au inawezekana kuona akilini kwa usahihi matukio ya Kibiblia unapotembelea Misri ya leo, kutia na Peninsula ya Sinai, na Israeli ya ki-siku-hizi?
[Picha katika ukurasa wa 3]
“Yeye ndiye anayeketi juu ya duara ya dunia.”—Isaya 40:22
“Akiining’iniza dunia pasipo na kitu.”—Ayubu 26:7, NW.