Tujapokuwa Wakimbizi, Twafurahi Kumtumikia Mungu
VITA, ukame, misiba, na msukosuko. Kwa watu wengine hizi ni habari zilizo kuu tu. Kwa wengine wengi mambo hayo ni sehemu ya maisha ya kila siku. Tukiwa ushirika wa ulimwenguni pote wa Wakristo, Mashahidi wa Yehova wanatambua vizuri sana kwamba wakati wowote vita vitokeapo au msiba utokeapo, sehemu ya udugu wao wa ulimwenguni pote hutaabika. Na wakati watu wanalazimika kukimbia kwa ajili ya uhai wao, ndugu zetu hulazimika kufanya vivyo hivyo.
Kwa miaka mingi Mashahidi katika nchi nyingi katika Afrika wamekuwa wakilazimika kuvumilia maono kama haya. Wengi wao wamekuwa wakilazimika kufunganya vitu vyovyote ambavyo wangeweza kubeba na kutafuta usalama kwingineko. Ingawa wachache wamekuwa na njia fulani za usafiri, labda baiskeli, iliwabidi walio wengi kutembea na kutembea na kutembea—kwa siku nyingi, hata majuma—kufika wanakokwenda.
Mojapo sehemu walizokuwa wakienda ulikuwa mji mmoja mdogo ulioitwa Mboki, katika nchi ya Jamhuri ya Afrika ya Kati. Kwa miaka mingi, wanaume kwa wanawake, wachanga kwa wazee, wamekuja kwa maelfu. Miongoni mwao walikuwamo idadi fulani ya ndugu na dada zetu Wakristo, wakiandamana na wenye kupendezwa. Bila shaka, Wakristo wenzi katika ofisi ya tawi ya Watch Tower Society katika Bangui, mji mkuu wa Jamhuri ya Afrika ya Kati, walipendezwa sana kukutana na wakimbizi hawa ili kuwapa msaada. Mara tano, mwakilishi wa Sosaiti alitumwa akiwa na pesa, chakula, mavazi, na dawa, zilizotolewa kwa ukarimu na Mashahidi katika Bangui, karibu umbali wa kilometa 1,130. Ingawa wote waliotoa huu msaada wa ukarimu walikuwa na machache kifedha, walifurahi kufanya waliyoweza.
Kwenda Mboki
Ndugu katika ofisi ya tawi walitaka kuona ni nini jingine lingefanywa na jinsi wakimbizi wangesaidiwa kiroho. Kwa hiyo mke wangu na mimi tukaondoka kwa gari aina ya Land Cruiser ya four-wheel-drive, tukiandamana na Symphorien, painia wa pekee na mke wake. Symphorien alijua barabara vizuri, naye anajua Kizande, lugha walioijua wakimbizi katika Mboki. Ilituchukua siku nne ndefu kufika huko.
Kilometa 400 za mwisho zilipita sehemu za mashambani zenye miteremko yenye kupendeza na mibuyu mikubwa mno. Tulipita vijiji vidogo hapa na pale. Kwenye sehemu hii ya barabara, mke wangu alihesabu madaraja 50 hasa—mengi yakiwa kwa hali mbaya sana, mengine yasiyopitika. Tulitengeneza madaraja mengine kwa miti na maboriti yaliyooza, tukaweka gari hiyo ya four-wheel-drive kwenye kijia, tukasali, na kuendesha kwa uangalifu sana. Mahali palipokuwa na kijiji karibu, wachanga wangekuja mbio kutusaidia—kwa malipo kidogo. Tuliona ajabu kwamba waliweza kupata vipande vya magogo na vibao kutoka darajani ndani sana ya nyasi na katika vichaka vilivyokuwa karibu. Ilitushangaza kama vilitolewa na kuwekwa hapo kwa ajili ya wateja wenye uhitaji.
Kwa pindi tatu tulikataa msaada wa wachanga hao, maana madaraja yalionekana hatari sana kupitika. Hivyo tukaondoa gari barabarani, tukateremka katika bonde, tukapita juu ya miamba, juu ya miinuko tena, na kurudi barabarani. Tulifurahi kama nini kwamba yalikuwa majira ya kiangazi, la sivyo hakungelikuwa na njia yoyote kwetu kufunga safari, isipokuwa labda kwa helikopta!
Mboki kungalikuwaje? Hili lilikuja kwa akili zetu mara kwa mara tuliposafiri kwenye piste hii isiyo na kikomo, neno hilo la Kifaransa linatumiwa katika Jamhuri ya Afrika ya Kati kumaanisha barabara au kijia cha mchanga, miamba, na mawe-mawe—na maelfu ya mashimo.
Baada tu ya alasiri, siku ya nne, Symphorien alionyesha kwa kidole vibanda fulani vya nyasi vilivyozungukwa na mipapai na mashamba ya mihogo. “Voilà! Mboki inaanza hapa,” alisema kwa sauti. Tulistaajabu sana kwa yale tuliyoyaona. “Hapa ni Mboki? Kambi iko wapi?” Tukauliza, maana tulichoona haikuwa kambi, ni nyumba tu zilizotapakaa. Vilikuwa vibanda vidogo vilivyoezekwa nyasi lakini vilivyo safi. Kulikuwa miti na vichaka pia kila mahali. Watu hupanda mimea kando ya nyumba zao. Mboki haikuwa aina ya kambi tuliyotazamia kuona; kilikuwa kijiji kikubwa sana, chenye urefu wa kilometa 35.
Kukutana na Ndugu
Ndugu katika Mboki walijua tulikuwa tukija, ingawa walidhani kuwa safari yetu ingechukua siku tano. Waliposikia gari letu, walikuja mbio. Wanaume, wanawake, na watoto walitoka haraka nje ya vibanda vyao na makwao kuja kutusalimu. Kila mmoja alitabasamu, kucheka, na kutusalimu, mara kadhaa ikiwezekana. Waliinyosha mikono ya watoto wao watusalimu. Wote walitaka kutusalimu, nao walitukaribisha kwa moyo mkunjufu.
Mimi na mke wangu hatukuwa na mengi ya kufanya kwa wakati ule kwa sababu ya kutojua lugha. Tulijaribu kusema Kifaransa kidogo, Kisango kidogo, Kiingereza kidogo, na Kiarabu. Wengi wa ndugu zetu huongea, husoma, na huandika Kizande. Ilimbidi Symphorien kutafsiri, akieleza programu ya kutembea kwetu.
Tuliendelea mbele maili nyinginezo zaidi na kufika kwenye Jumba la Ufalme. Lilikuwa “kanisa” la kwanza la dini yoyote kujengwa na wakimbizi katika Mboki. Ndugu wengine zaidi na watoto wao na wenye kupendezwa walikuja kutusalimu. Hata watoto wengi wa ujirani walikuja pamoja na ndugu kutusalimu.
Ndugu zetu walikuwa wametutayarishia sisi, tuliokuwa wageni wao, vyumba vidogo viwili vya huko. Vilikuwa safi. Ndoo za maji safi zilikuwa tayari zinatungoja. Tulikuwa tumekuja na chakula chetu na maji ya kunywa, tukidhani tutapata hali mbaya zaidi ya upungufu wa maji na chakula na ili tusiwatwike mzigo ndugu zetu. Tulipokuwa tukipakua gari, msichana mdogo alikuja na kutuuliza jinsi tungependa kuku apikwe usiku huo, aokwe au apikwe kwa mchuzi? Hatukutazamia hilo kamwe na tukauliza walichokuwa wamepanga kula nayo. Jibu: muhogo. Hivyo tukachagua kuku wa mchuzi uliokolezwa. Njaa yetu kubwa ilishibishwa vizuri usiku huo. Lakini waliendelea kutulisha kila siku—alasiri na jioni. Hatungeweza kuamini hata kidogo—wakimbizi kutulisha na kututunza, ingawa walikuwa na vichache tu.
Kutaniko Dogo Lenye Furaha
Tulikuwa hapa, katika sehemu hii ya mashambani lakini miongoni mwa ndugu zetu 21. Ni wawili tu wa hawa walikuja hapa wakiwa tayari wamebatizwa. Wengine walikuwa wenye kupendezwa walipokuja. Waliendelea kujifunza na wakabatizwa kwa miaka miwili iliyopita. Wengine wanne zaidi walibatizwa katika mto uliokuwa karibu tulipotembea.
Mmoja aliye kielelezo chenye kutokeza ni Faustino. Kabla ya kwenda Mboki, alijifunza kweli za msingi za Biblia kutoka kwa rafikiye. Faustino akathamini aliyokuwa akijifunza. Muda si muda yeye na rafikiye wakaanza kuwahubiri wengine, lakini wakakabiliwa na upinzani na kuwekwa gerezani kwa ajili ya “kuwataharakisha watu” kwa dini yao. Wakiwa gerezani, rafikiye Faustino akashindwa na woga naye aliachiliwa. Miezi miwili baadaye Faustino alijaribiwa mahakamani. Hata hivyo, ilionekana wazi kwamba mashtaka dhidi yake hayakuwa na msingi, kwa hiyo aliachiliwa. Vita ilipoanza katika eneo lake, Faustino alikimbilia Jamhuri ya Afrika ya Kati, alikokutana na ndugu na kuendelea na funzo lake la Biblia. Alibatizwa katika Julai 1991, na katika 1992 akaingia katika huduma ya wakati wote akiwa painia wa kawaida.
Kutaniko dogo lenye furaha na urafiki katika Mboki sasa lina painia wa pekee mmoja na wahubiri 21. Ndugu wawili wenye kusema Kiingereza watumikia wakiwa wazee na waweza kuendeleza uwasiliano mzuri pamoja na ofisi ya tawi katika Bangui. Tulidhani ndugu zetu wakimbizi walikuwa katika hali mbaya sana, yenye kukatisha tamaa, lakini haikuwa hivyo. Ingawa walikuwa maskini kimwili, hakuna yeyote aliyekuwa analalamika, kufadhaika, au kunung’unika. Tangu wafike ndugu wamejenga vibanda vyao na nyumba zao na wameanza kukuza chakula na kufuga kuku. Wana vichache kuliko walivyokuwa navyo mbeleni, lakini wako hai na wako pamoja na Wakristo wenzao.
Kwa kuwa kuna kati ya wakimbizi 17,000 na 20,000 katika Mboki, na wengine zaidi wakija kila mwezi, ndugu zetu wana shamba kubwa kwa ajili ya huduma yao. Tulienda kuhubiri pamoja nao, jambo lililotupendeza sana. Wao hutumia Biblia ya Kizande, na tafsiri hii ina jina la Mungu katika Maandiko ya Kiebrania na sehemu mbalimbali katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kwa watu hawa, Mungu si “Mboli” (“Mungu” wa Kizande) tu bali “Yekova,” njia ambayo wao hutamka jina la kibinafsi la Mungu. “Mboli Yekova” ni usemi wa kawaida. Tafsiri za Kiprotestanti katika lugha nyinginezo za Kiafrika hazifuati tafsiri hiyo iliyo sahihi, badala ya hivyo hizo huondoa “Yehova” na kuweka “Nzapa,” “Nzambe,” au majina mengine ya Kiafrika yamaanishayo Mungu.
Kwa kupatana kabisa na unabii wa Yesu, habari njema za Ufalme zinahubiriwa ulimwenguni pote, hata katika Mboki. (Mathayo 24:14) Kutaniko sasa linapata vizuri Biblia, vitabu, magazeti, vijitabu, na trakti za kutosha kwa lugha zote wanazohitaji. Labda katika siku zijazo, vichapo zaidi vitapatikana katika Kizande.
Wangoja Makao ya Kudumu
Katika jioni ya kwanza, tulionyesha programu ya Sosaiti ya slaidi ya “Wakusanyikaji Wenye Furaha Katika Ulaya ya Mashariki Wamsifu Yehova.” Usiku uliofuata programu ilikuwa “Kuwaleta Wengi Kwenye Uadilifu Wakati wa Mwisho.” Slaidi zilionyeshwa nje, kando ya Jumba la Ufalme, chini ya mbingu na mwezi mwangavu. Mazingira mazuri ajabu! Mamia walikuja kuona slaidi hizi zikionyeshwa, na ndugu zetu walifurahi na kujivunia kutoa kitu cha pekee kwa watu.
Jumatatu ilipofika, tulijitayarisha kwa ajili ya safari yetu ya kurudi. Ingalikuwa safari nyingine ya siku nne kupitia barabara zilezile na kuvuka zilezile daraja 50. Dada mmoja alisisitiza kutayarisha chakula kwa ajili ya safari—kuku wengine wawili, waliookwa na kukolezwa kwa kitunguu-saumu. Walinukia vizuri sana wakati wa zile saa za asubuhi ndani ya Land Cruiser. Alasiri tulisimama msituni kufurahia kuku aliyeokwa tukiwafikiria ndugu zetu katika Mboki. Wajapolazimika kuwa wakimbizi, wanaendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu, wakingoja makao ya kudumu ya amani katika dunia mpya iliyoahidiwa na Mungu. (2 Petro 3:13)—Imechangwa.